Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • lv sura 13 kur. 144-159
  • Sherehe Ambazo Zinamchukiza Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sherehe Ambazo Zinamchukiza Mungu
  • “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KRISMASI—JINA JIPYA LA IBADA YA JUA
  • MAONI YA BIBLIA KUHUSU SIKUKUU ZA KUZALIWA
  • ISTA—IBADA YA UWEZO WA KUZAA INAYOSINGIZIWA KUWA YA KIKRISTO
  • MKESHA WA SIKUKUU YA WATAKATIFU WOTE SI SIKU TAKATIFU HATA KIDOGO
  • NDOA YENU NA IWE SAFI
  • JE, KUMTAKIA MTU HERI KWA BILAURI YA KINYWAJI NI TENDO LA KIDINI?
  • “ENYI MNAOMPENDA YEHOVA, CHUKIENI YALIYO MABAYA”
  • MTUKUZE MUNGU KATIKA NENO NA TENDO
  • Je, Sherehe Zote Zinampendeza Mungu?
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Shughuli za Baada ya Masomo
    Shule na Mashahidi wa Yehova
  • Amua Kumwabudu Mungu
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Chukua Msimamo Upande wa Ibada ya Kweli
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Pata Habari Zaidi
“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
lv sura 13 kur. 144-159
Kijana wao akifungua zawadi aliyopewa na wazazi wake bila kutarajia

SURA YA 13

Sherehe Ambazo Zinamchukiza Mungu

“Endeleeni kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.”—WAEFESO 5:10.

1. Yehova anavuta watu wa aina gani kwake, na kwa nini wanapaswa kuendelea kuwa macho kiroho?

“WAABUDU wa kweli,” Yesu alisema, “watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:23) Yehova anapowapata watu kama hao—kama alivyokupata wewe—anawavuta kwake na kwa Mwana wake. (Yohana 6:44) Hilo ni pendeleo kubwa kama nini! Hata hivyo, wanaopenda kweli ya Biblia lazima ‘waendelee kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana,’ kwa kuwa Shetani ni stadi wa udanganyifu.—Waefeso 5:10; Ufunuo 12:9.

2. Eleza jinsi Yehova anavyowaona wale wanaojaribu kuchanganya dini ya kweli na ya uwongo.

2 Fikiria kilichotokea karibu na Mlima Sinai, Waisraeli walipomwomba Haruni awafanyie mungu. Haruni alikubali kwa moyo nusunusu, akatengeneza ndama wa dhahabu huku akisema kwamba ndama huyo anamwakilisha Yehova. “Kutakuwa na sherehe kwa ajili ya Yehova kesho,” akasema. Je, Yehova alipuuza tendo hilo la kuchanganya dini ya kweli na ya uwongo? Hapana. Aliwaangamiza waabudu-sanamu wapatao 3,000. (Kutoka 32:1-6, 10, 28) Tunajifunza nini? Ikiwa tunataka kukaa katika upendo wa Mungu, ‘tusiguse kamwe kitu chochote kilicho najisi,’ na lazima tutetee kweli kwa bidii ili isichafuliwe kwa njia yoyote.—Isaya 52:11; Ezekieli 44:23; Wagalatia 5:9.

3, 4. Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uzito kanuni za Biblia tunapochunguza desturi na sherehe zinazopendwa sana?

3 Inasikitisha kwamba baada ya kifo cha mitume, ambao walikuwa wamezuia uasi-imani usisitawi, Wakristo bandia ambao hawakuipenda kweli walianza kufuata desturi za kipagani, na kuadhimisha sherehe na siku “kuu” ambazo walidai kuwa ni za Kikristo. (2 Wathesalonike 2:7, 10) Unapochunguza baadhi ya sherehe hizo, ona jinsi zinavyoonyesha roho ya ulimwengu bali si roho ya Mungu. Kwa ujumla, kuna jambo moja linaloonekana wazi katika sherehe za kilimwengu: Zinachochea tamaa za mwili, na zinaunga mkono mafundisho ya dini za uwongo na mazoea ya kuwasiliana na pepo—mambo ambayo yanatambulisha “Babiloni Mkubwa.”a (Ufunuo 18:2-4, 23) Pia, kumbuka kwamba Yehova alijionea mwenyewe mazoea yenye kuchukiza ya dini za kipagani ambayo ndiyo chanzo cha desturi nyingi zinazofuatwa na wengi leo. Haikosi sherehe hizo zinamchukiza hata leo. Je, hatupaswi kutilia maanani maoni yake?—2 Yohana 6, 7.

4 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunajua kwamba sherehe fulani zinamchukiza Yehova. Hata hivyo, tunahitaji kuazimia kabisa moyoni mwetu kutohusishwa nazo hata kidogo. Kujikumbusha kwa nini Yehova anachukizwa na sherehe hizo kutaimarisha azimio letu la kuepuka chochote kinachoweza kutuzuia tusikae katika upendo wa Mungu.

KRISMASI—JINA JIPYA LA IBADA YA JUA

5. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu hakuzaliwa Desemba 25?

5 Biblia haitaji popote maadhimisho ya kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa Yesu. Kwa kweli, hata tarehe yenyewe ya kuzaliwa kwake haijulikani. Hata hivyo, tuna hakika kwamba hakuzaliwa Desemba 25, wakati ambapo kwa kawaida kunakuwa na baridi kali katika eneo alimozaliwa.b Sababu moja ni kwamba Luka aliandika kuwa Yesu alipozaliwa, “wachungaji [walikuwa] wakiishi nje,” wakichunga makundi yao. (Luka 2:8-11) Ikiwa wachungaji walikuwa “wakiishi nje” mwaka mzima, basi hakukuwa na haja ya kutaja jambo hilo. Hata hivyo, kwa kuwa Bethlehemu hupata mvua na theluji wakati wa majira ya baridi kali, makundi yalikuwa yakifungiwa ndani, nao wachungaji hawangekuwa “wakiishi nje.” Kwa kuongezea, Yosefu na Maria walienda Bethlehemu kwa kuwa Kaisari Augusto alikuwa ameagiza watu wahesabiwe. (Luka 2:1-7) Haielekei kwamba Kaisari angewaagiza watu ambao tayari walikuwa wakichukia utawala wa Roma, wasafiri kwenda majiji ya kwao kukiwa na baridi kali sana hivyo.

6, 7. (a) Desturi nyingi za Krismasi zilianzia wapi? (b) Kuna tofauti gani kati ya utoaji unaofanywa wakati wa Krismasi na utoaji wa Kikristo?

6 Krismasi haikutokana na Maandiko bali sherehe za kale za kipagani, kama vile sherehe ya Saturnalia ya Waroma, ambayo ilifanyiwa Saturn, mungu wa kilimo. Vivyo hivyo, waabudu wa mungu Mithra walisherehekea “kuzaliwa kwa jua lisiloshindika” mnamo Desemba 25. “Krismasi ilianza wakati madhehebu ya jua yalipositawi nchini Roma,” karne tatu hivi baada ya kifo cha Kristo.—New Catholic Encyclopedia.

Wakristo wa kweli hutoa kwa kuchochewa na upendo

7 Wakati wa sherehe zao, wapagani walipeana zawadi na kufanya karamu—mambo ambayo hufanyika hata leo wakati wa Krismasi. Lakini, kama ilivyo leo pia, mazoea ya kupeana zawadi wakati huo hayakupatana na kile kinachosemwa katika andiko la 2 Wakorintho 9:7, linalosema: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” Wakristo wa kweli hutoa kwa sababu ya upendo, hawawajibiki kutoa zawadi tarehe fulani tu, wala hawatoi zawadi wakitazamia kupokea zawadi pia. (Luka 14:12-14; Matendo 20:35) Zaidi ya hilo, wanafurahi sana kwamba wako huru kutokana na mahangaiko na madeni makubwa ambayo wengi hupata wakati wa Krismasi.—Mathayo 11:28-30; Yohana 8:32.

8. Je, wanajimu walimpa Yesu zawadi za siku ya kuzaliwa? Eleza.

8 Lakini, huenda watu fulani wakauliza, kwani wanajimu hawakumpa Yesu zawadi za siku ya kuzaliwa? Hapana. Zawadi walizotoa zilionyesha tu kwamba wanamtambua kuwa mtu wa maana, na hiyo ilikuwa desturi ya kawaida katika siku za Biblia. (1 Wafalme 10:1, 2, 10, 13; Mathayo 2:2, 11) Tena, hata hawakuja usiku ambao Yesu alizaliwa. Walipofika, Yesu hakuwa mtoto mchanga katika hori, bali alikuwa katika nyumba, akiwa na umri wa miezi kadhaa.

JE, NIJIUNGE NA WENGINE KATIKA MAADHIMISHO?

Mwanamke mkristo akikataa kusaidia kupamba eneo lake la kazi kwa ajili ya sherehe maarufu

Kanuni: “‘Tokeni katikati yao, na mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kilicho najisi’; ‘nami nitawakaribisha ndani.’”—2 Wakorintho 6:17.

Maswali fulani unayoweza kujiuliza kuhusu maadhimisho au desturi inayopendwa na wengi

  • Je, imetokana na mazoea au mafundisho ya dini za uwongo, kutia ndani kuwasiliana na pepo?—Isaya 52:11; 1 Wakorintho 4:6; 2 Wakorintho 6:14-18; Ufunuo 18:4.

  • Je, ni njia ya kuheshimu au kumtukuza mwanadamu, shirika, au taifa isivyofaa?—Yeremia 17:5-7; Matendo 10:25, 26; 1 Yohana 5:21.

  • Je, taifa moja au jamii moja inakwezwa kuliko mataifa au jamii nyingine?—Matendo 10:34, 35; 17:26.

  • Je, kuna “roho ya ulimwengu,” inayopinga roho takatifu ya Mungu?—1 Wakorintho 2:12; Waefeso 2:2.

  • Je, ninaweza kuwakwaza wengine kwa kushiriki?—Waroma 14:21.

  • Nikiamua kutoshiriki, ni kwa njia gani ninaweza kuwaeleza wengine kwa heshima sababu zangu za kufanya hivyo?—Waroma 12:1, 2; Wakolosai 4:6.

Maandiko yanayofuata yanaweza kutusaidia kufanya maamuzi kuhusu maadhimisho yanayopendwa na wengi:

  • “[Waisraeli wasio waaminifu] wakachangamana na hayo mataifa na kuanza kujifunza matendo yao.”—Zaburi 106:35.

  • “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo zaidi ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu ambaye si mwaminifu katika lililo dogo zaidi si mwaminifu katika lililo kubwa pia.”—Luka 16:10.

  • “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 15:19.

  • “Hamwezi kuwa mkishiriki ‘meza ya Yehova’ na meza ya roho waovu.”—1 Wakorintho 10:21.

  • “Wakati uliopita uliwatosha kufanya mapenzi ya mataifa wakati mlipotembea katika vitendo vya mwenendo mpotovu, uchu, divai kupita kiasi, karamu za kupindukia, mashindano ya kunywa, na ibada haramu za sanamu.”—1 Petro 4:3.

MAONI YA BIBLIA KUHUSU SIKUKUU ZA KUZALIWA

9. Ni mambo gani yaliyotokea wakati wa sikukuu za kuzaliwa zinazotajwa katika Biblia?

9 Ingawa sikuzote kuzaliwa kwa mtoto huwa pindi ya shangwe nyingi, Biblia haitaji popote sikukuu ya kuzaliwa ya mtumishi yeyote wa Mungu. (Zaburi 127:3) Zilisahaulika? Hapana, kwa sababu sikukuu mbili za kuzaliwa zinatajwa—siku ya kuzaliwa kwa Farao wa Misri na ile ya Herode Antipa. (Mwanzo 40:20-22; Marko 6:21-29) Hata hivyo, sikukuu zote mbili hazitajwi kwa uzuri—hasa sikukuu ya pili, wakati ambapo Yohana Mbatizaji alikatwa kichwa.

10, 11. Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na maoni gani kuhusu sikukuu za kuzaliwa, na kwa nini?

10 Kitabu kimoja kinasema: “Wakristo wa karne ya kwanza . . . waliona kusherehekea siku ya kuzaliwa ya mtu yeyote kuwa desturi ya kipagani.” (The World Book Encyclopedia) Kwa mfano, Wagiriki wa kale waliamini kwamba kila mtu ana roho fulani inayomlinda inayokuwapo anapozaliwa na huendelea kumlinda katika maisha yake yote. Roho hiyo “ilikuwa na uhusiano usioelezeka pamoja na mungu ambaye siku ya kuzaliwa kwake ililingana na siku ya kuzaliwa kwa mtu huyo.” (The Lore of Birthdays) Pia, kwa muda mrefu siku za kuzaliwa zimehusianishwa sana na unajimu na uaguzi.

SIKU “KUU” KATIKA DINI ZA KISHETANI

Inashangaza kwamba siku ya maana zaidi katika dini ya Kishetani ni siku ya kuzaliwa. Kwa nini? Kwa sababu wafuasi wa dini hiyo wanaamini kwamba kila mtu ni mungu maadamu anajiona hivyo. Kwa hiyo, kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa mtu ni sawa na kuadhimisha kuzaliwa kwa mungu. Bila shaka, watu wengi hawana maoni hayo yanayopita kiasi, ya kujiona kuwa miungu. Hata hivyo, kitabu kimoja kinasema: “Sikukuu nyingine husisimua moyo, lakini sikukuu za kuzaliwa huchochea kiburi.”—The Lore of Birthdays.

Siku “kuu” nyingine katika dini ya Kishetani ni Usiku wa Walburga na Halloween. Kamusi moja inafafanua sikukuu ya Usiku wa Walburga kuwa “mkesha wa Mei Mosi, usiku ambao inaaminika kwamba wachawi husafiri wakiwa juu ya ufagio hadi mahali fulani wanapokutana wote.”—Merriam-Webster’s Collegiate Dictionary.

11 Mbali na kukataa desturi za siku za kuzaliwa kwa sababu zilitokana na mazoea ya kipagani na ya kuwasiliana na pepo, inaonekana pia kwamba watumishi wa kale wa Mungu walizikataa kwa sababu hazikupatana na kanuni za Kimaandiko. Kwa nini? Walikuwa wanaume na wanawake wanyenyekevu na wenye kiasi ambao hawakuona kuzaliwa kwao kuwa tukio la maana sana linalopaswa kusherehekewa.c (Mika 6:8; Luka 9:48) Badala yake, walimtukuza Yehova na kumshukuru kwa sababu ya zawadi ya uhai yenye thamani.d—Zaburi 8:3, 4; 36:9; Ufunuo 4:11.

12. Ni kwa njia gani siku ya kufa inaweza kuwa bora kuliko siku ya kuzaliwa?

12 Wanapokufa, wote waliokuwa waaminifu wako salama katika kumbukumbu ya Mungu, na maisha yao ya wakati ujao ni hakika. (Ayubu 14:14, 15) Andiko la Mhubiri 7:1 linasema: “Jina ni bora kuliko mafuta mazuri, na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa kwa mtu.” “Jina” letu ni sifa nzuri ambayo tumejipatia mbele za Mungu kupitia utumishi wetu wenye uaminifu. Ni muhimu kukumbuka kwamba maadhimisho pekee ambayo Wakristo wameamriwa waadhimishe, hayahusiani na kuzaliwa bali kifo—kifo cha Yesu, ambaye wokovu wetu unategemea “jina” lake lililo bora.—Luka 22:17-20; Waebrania 1:3, 4.

ISTA—IBADA YA UWEZO WA KUZAA INAYOSINGIZIWA KUWA YA KIKRISTO

13, 14. Desturi za Ista zinazopendwa na wengi zilitoka wapi?

13 Ingawa inasemekana kwamba Ista ni maadhimisho ya ufufuo wa Kristo, ukweli ni kwamba inatokana na dini ya uwongo. Jina Ista limehusianishwa na Eostre, au Ostara, mungu wa mapambazuko na majira ya kuchipuka kwa majani aliyekuwa akiabudiwa na Wasaksoni wa kale wa Uingereza. Namna gani sungura na mayai yanayotumiwa wakati wa Ista? Kulingana na kitabu kimoja, mayai, “kwa muda mrefu yamekuwa yakiwakilisha uhai mpya na ufufuo,” naye sungura akiwakilisha uwezo wa kuzaa. Kwa hiyo, Ista ni maadhimisho ya kusherehekea uwezo wa kuzaa inayosingiziwa kuwa maadhimisho ya ufufuo wa Kristo.e

14 Je, Yehova angekubali sherehe yenye kuchukiza ya uwezo wa kuzaa itumiwe kuadhimisha ufufuo wa Mwana wake? Haiwezekani hata kidogo! (2 Wakorintho 6:17, 18) Maandiko hayaagizi wala kukubali ufufuo wa Yesu uadhimishwe. Kwa hiyo, kuadhimisha ufufuo wa Yesu na kuuita Ista ni kukosa ushikamanifu hata zaidi.

MKESHA WA SIKUKUU YA WATAKATIFU WOTE SI SIKU TAKATIFU HATA KIDOGO

15. Halloween ilitoka wapi, na ni nini kinachoonyeshwa na tarehe iliyoteuliwa kwa ajili ya sikukuu hiyo?

15 Mkesha wa Sikukuu ya Watakatifu Wote, sikukuu inayoitwa pia Halloween—ambayo wengi wanaihusianisha na wachawi, mizuka, na mavazi ya kutisha—ilitokana na Waselti wa kale wa Uingereza na Ireland. Siku iliyokuwa na mwezi mpevu karibu zaidi na Novemba 1, Waselti walikuwa wakiadhimisha sherehe ya Samhain, yaani, “Mwisho wa Kiangazi.” Waliamini kwamba wakati wa Samhain, kizuizi kilichokuwa kikiwatenganisha wanadamu na ulimwengu wa roho kiliondolewa na kwamba roho wema na waovu walizunguka kotekote duniani. Ilidhaniwa kwamba nafsi za wafu zilirudi kwa familia zao, nazo familia zilikuwa zikiandalia mizuka hiyo chakula na vinywaji ili kuituliza. Hivyo basi, leo watoto wanapovalia kama mizuka au wachawi na kwenda nyumba kwa nyumba wakiwatisha wenye nyumba kwamba watawafanyia mazingaombwe wasipopewa zawadi, wanaendeleza bila kujua desturi za Samhain.

NDOA YENU NA IWE SAFI

16, 17. (a) Kwa nini Wakristo wanaopanga kufunga ndoa wanapaswa kuchunguza desturi za kwao za arusi kwa kutumia kanuni za Biblia? (b) Kuhusiana na desturi za kutupa mchele au vitu vingine, Wakristo wanapaswa kufikiria nini kwa uzito?

16 Hivi karibuni “hakuna sauti ya bwana-arusi na bibi-arusi itakayosikiwa tena kamwe ndani” ya Babiloni Mkubwa. (Ufunuo 18:23) Kwa nini? Sababu moja ni mazoea ya Babiloni Mkubwa ya kuwasiliana na pepo ambayo yanaweza kuitia ndoa unajisi tangu siku ya arusi.—Marko 10:6-9.

17 Desturi zinatofautiana katika nchi mbalimbali. Huenda ikawa desturi fulani zinazoonekana kuwa sawa zilitokana na mazoea ya Kibabiloni ambayo yanakusudiwa kuletea ‘bahati njema’ bwana na bibi-arusi au wageni wao. (Isaya 65:11) Desturi moja ni ile ya kuwatupia mchele au vitu vingine. Huenda zoea hilo lilitokana na wazo la kwamba chakula hutuliza roho waovu na kuwazuia wasidhuru bwana na bibi-arusi. Pia, kwa muda mrefu mchele umehusianishwa na uwezo wa kuzaa, furaha, na maisha marefu. Bila shaka, wote wanaotaka kukaa katika upendo wa Mungu wataepuka desturi hizo zenye unajisi.—2 Wakorintho 6:14-18.

18. Ni kanuni gani za Biblia zinazopaswa kuwaongoza wale wanaopangia arusi na wale walioalikwa?

18 Pia, watumishi wa Yehova wanaepuka mazoea ya ulimwengu ambayo yanaweza kufanya arusi na karamu za arusi zikose heshima ya Kikristo au kusumbua dhamiri za wengine. Kwa mfano, wanaepuka kutoa hotuba zenye dhihaka inayoumiza au maneno na mizaha inayohusiana na ngono, na kutosema mambo yanayoweza kuwaaibisha wanaofanya arusi na wanaohudhuria. (Methali 26:18, 19; Luka 6:31; 10:27) Pia wanaepuka karamu za ndoa zenye madoido mengi ambazo, si zenye kiasi, bali ni njia ya “mtu kujionyesha mali yake maishani.” (1 Yohana 2:16) Ikiwa unapanga kufanya arusi, usisahau kamwe kwamba Yehova anataka uikumbuke kwa shangwe siku hiyo ya pekee maishani mwako, bali si kwa majuto.f

JE, KUMTAKIA MTU HERI KWA BILAURI YA KINYWAJI NI TENDO LA KIDINI?

19, 20. Kitabu kimoja kinasema nini kuhusu chanzo cha zoea la kuwatakia wengine heri kwa bilauri ya kinywaji, na kwa nini desturi hiyo haiwafai Wakristo?

19 Zoea moja ambalo limeenea sana katika arusi na karamu nyingi ni lile la kuwatakia wengine heri kwa bilauri ya kinywaji. Kitabu kimoja kinasema: “Kuwatakia wengine heri kwa bilauri ya kinywaji . . . huenda kunatokana na desturi ya zamani ya kufanya matambiko, ambapo kinywaji kitakatifu kilitolewa kwa miungu . . . ili kupata ombi fulani, au sala fupi yenye maneno, ‘maisha marefu!’ au ‘afya njema!’”—International Handbook on Alcohol and Culture cha mwaka wa 1995.

20 Ni kweli kwamba huenda watu wengi wasilione zoea la kuwatakia wengine heri kwa bilauri ya kinywaji kuwa zoea la kidini au lenye ushirikina. Hata hivyo, desturi ya kuinua bilauri zenye divai kuelekea mbinguni inaweza kuonwa kuwa ombi linaloelekezwa “mbinguni”—kwa nguvu fulani zinazopita zile za kibinadamu—ili kupata baraka kwa njia ambayo ni kinyume na Maandiko.—Yohana 14:6; 16:23.g

“ENYI MNAOMPENDA YEHOVA, CHUKIENI YALIYO MABAYA”

21. Ingawa huenda zisiwe za kidini, ni sherehe gani zinazopendwa na wengi ambazo Wakristo wanapaswa kuepuka, na kwa nini?

21 Leo, viwango vya ulimwengu vimezorota sana—jambo ambalo limechangiwa kwa njia moja au nyingine na Babiloni Mkubwa. Kwa mfano, nchi fulani huwa na sherehe mbalimbali zinazofanywa kila mwaka, kama vile carnival au Mardi Gras, ambazo zinahusisha dansi chafu na hutukuza maisha ya mashoga na wasagaji. Je, ingefaa ‘mtu anayempenda Yehova’ ahudhurie au kutazama sherehe kama hiyo? Ikiwa angefanya hivyo, kweli anachukia yaliyo mabaya? (Zaburi 1:1, 2; 97:10) Ni afadhali kama nini kuiga mtazamo wa mtunga-zaburi aliyesali hivi: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa”!—Zaburi 119:37.

22. Ni sherehe au desturi gani ambazo Mkristo anaweza kuamua kulingana na dhamiri yake ikiwa atashiriki au hatashiriki?

22 Siku za sherehe za kilimwengu, Mkristo anapaswa kuwa mwangalifu mwenendo wake usionyeshe kwamba anajiunga na wengine kusherehekea sherehe hizo. Paulo aliandika: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31; ona sanduku “Kufanya Maamuzi kwa Hekima.”) Kwa upande mwingine, ikiwa kwa wazi desturi au sherehe fulani haina mambo yoyote ya kidini, si ya kisiasa au ya kizalendo, na haivunji kanuni yoyote ya Biblia, basi kila Mkristo anaweza kufanya uamuzi wake mwenyewe, ikiwa atashiriki au hatashiriki. Pia, anapaswa kufikiria hisia za wengine ili asiwakwaze.

MTUKUZE MUNGU KATIKA NENO NA TENDO

23, 24. Ni kwa njia gani tunaweza kutoa ushahidi mzuri kuhusu viwango vya uadilifu vya Yehova?

23 Wengi huona siku za sherehe fulani zinazopendwa kuwa pindi za watu wa familia na marafiki kukutana. Hivyo, mtu akiwa na maoni yasiyofaa ya kwamba tunapita kiasi au kukosa upendo kwa sababu ya msimamo wetu wa Kimaandiko, tunaweza kumweleza kwa fadhili kwamba Mashahidi wa Yehova wanathamini pindi za kukutana pamoja na familia na marafiki. (Methali 11:25; Mhubiri 3:12, 13; 2 Wakorintho 9:7) Sisi hufurahia kuwa pamoja na watu tunaowapenda wakati mwingine wowote, lakini kwa sababu tunampenda Mungu na viwango vyake vya uadilifu, hatungependa kutia doa pindi hizo zenye furaha kwa kushiriki katika desturi zinazomchukiza.—Ona sanduku “Ibada ya Kweli Hutokeza Shangwe Kubwa Zaidi.”

IBADA YA KWELI HUTOKEZA SHANGWE KUBWA ZAIDI

Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” naye anataka watumishi wake wawe na furaha. (1 Timotheo 1:11) Jambo hilo linakaziwa katika maandiko yanayofuata:

  • “Mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.”—Methali 15:15.

  • “Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora kwao kuliko mtu kufurahi na kufanya mema maishani mwake; na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.”—Mhubiri 3:12, 13.

  • “Naye mtu mkarimu, ametoa shauri kwa ajili ya mambo ya ukarimu; naye atasimama kwa ajili ya mambo ya ukarimu.”—Isaya 32:8.

  • “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami [Yesu] nitawaburudisha ninyi. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28, 30.

  • “Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”—Yohana 8:32.

  • “Kila mmoja na [atoe] kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”—2 Wakorintho 9:7.

  • “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, . . . fadhili, wema.”—Wagalatia 5:22.

  • “Matunda ya nuru yana kila namna ya wema na uadilifu na kweli.”—Waefeso 5:9.

24 Mashahidi fulani wamefanikiwa kujibu maswali ya watu wanyoofu kwa kutumia hoja zilizo katika sura ya 16 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?h Hata hivyo, kumbuka kwamba lengo letu ni kuchochea mioyo ya watu bali si kushinda mabishano. Kwa hiyo, uwe mwenye heshima, dumisha upole, na ‘maneno yako na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi.’—Wakolosai 4:6.

25, 26. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao kukua katika imani na kumpenda Yehova zaidi?

25 Tukiwa Mashahidi wa Yehova tumeelimishwa vizuri. Tunajua kwa nini tunaamini na kufanya mambo fulani na kwa nini tunajiepusha na mengine. (Waebrania 5:14) Kwa hiyo, wazazi wafundisheni watoto wenu kutumia kanuni za Biblia. Mnapofanya hivyo, mnaimarisha imani yao, mnawasaidia kutumia Maandiko kuwajibu wale wanaouliza maswali kuhusu imani yao, na mnawahakikishia kwamba Yehova anawapenda.—Isaya 48:17, 18; 1 Petro 3:15.

26 Wote wanaomwabudu Mungu “kwa roho na kweli” hawaepuki tu sherehe zisizopatana na Maandiko bali pia wanajitahidi kuwa wanyoofu katika maisha yao yote. Leo, watu wengi wanaona kwamba hakuna faida za kuwa wanyoofu. Lakini kama tutakavyoona katika sura inayofuata, sikuzote njia za Mungu ndizo bora.

a Ona sanduku “Je, Nijiunge na Wengine Katika Maadhimisho?” Sherehe na siku “kuu” kadhaa zimeorodheshwa katika Fahirisi, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

b Kwa kutegemea historia na tarehe za Biblia, inaonekana Yesu alizaliwa mwaka wa 2 K.W.K. katika mwezi wa Kiyahudi wa Ethanimu, ambao unalingana na mwezi wa Septemba/Oktoba katika kalenda tunayotumia leo.—Ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 56-57 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 21, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

c Ona sanduku “Siku ‘Kuu’ Katika Dini za Kishetani.

d Kulingana na agano la Sheria, mwanamke alipaswa kumtolea Mungu toleo la dhambi baada ya kuzaa. (Mambo ya Walawi 12:1-8) Takwa hilo la kisheria liliwakumbusha kwamba wanadamu wanawapitishia watoto wao dhambi, nalo liliwasaidia Waisraeli kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu kuzaliwa kwa mtoto, na huenda hata liliwazuia wasifuate desturi za kipagani za siku za kuzaliwa.—Zaburi 51:5.

e Pia, Ista alikuwa mungu wa kike wa uzazi. Kulingana na kamusi The Dictionary of Mythology, “Ista alikuwa na sungura mwezini ambaye alipenda mayai na nyakati nyingine alionyeshwa akiwa na kichwa cha sungura.”

f Ona makala tatu kuhusu arusi na tafrija katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 2006, ukurasa wa 18-31.

g Ona Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 2007, ukurasa wa 30-31.

h Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

KUFANYA MAAMUZI KWA HEKIMA

Nyakati nyingine, tunaweza kujikuta katika hali zinazopima upendo wetu kwa Yehova na jinsi tunavyoelewa kanuni za Biblia. Kwa mfano, huenda mume au mke asiye mwamini akamwalika mwenzi wake wa ndoa, ambaye ni Mkristo, ajiunge na watu wa ukoo katika mlo wa kuadhimisha sikukuu ya kilimwengu. Huenda dhamiri za Wakristo fulani zikawaruhusu kukubali mwaliko huo, na za wengine zikawazuia. Mkristo akikubali mwaliko huo, mwenendo wake unapaswa kuonyesha wazi kabisa haadhimishi sikukuu hiyo na kwamba ameenda tu ili kufurahia mlo pamoja na watu wa ukoo.

Ni jambo la hekima Mkristo azungumze kwa busara na mwenzi wake wa ndoa mapema, akimweleza aibu inayoweza kutokea ikiwa Shahidi huyo atakataa kushiriki utendaji fulani wa sikukuu hiyo pamoja na watu wa ukoo. Huenda mwenzi huyo asiyeamini akaamua watembee siku nyingine.—1 Petro 3:15.

Baada ya kusikiliza maoni ya mke wake, mwanamke Mkristo anaweza kufanya nini ikiwa mume wake bado anasisitiza kwamba lazima waandamane pamoja? Anaweza kukata kauli ya kwamba kwa kuwa mume ndiye kichwa cha familia, ana wajibu wa kuandalia familia yake chakula. (Wakolosai 3:18) Katika kisa hiki, chakula hicho kinapatikana nyumbani kwa watu wa ukoo. Huenda hata akapata nafasi ya kutoa ushahidi katika pindi hiyo. Kula chakula hicho wakati wa sikukuu ya kilimwengu hakufanyi kiwe na kasoro. (1 Wakorintho 8:8) Mkristo anaweza kukiona kuwa chakula cha kawaida naye asishiriki katika salamu, nyimbo, kugonganisha bilauri katika kutakiana heri, na kadhalika.

Jambo lingine la kufikiria ni jinsi wengine watakavyoona ukishiriki mlo katika mwadhimisho huo. Mke Mkristo anapaswa kufikiria uwezekano wa kwamba huenda wengine wakakwazika wakijua alishirikiana na watu wa ukoo katika siku hiyo.—1 Wakorintho 8:9; 10:23, 24.

Pia, je, inawezekana kwamba mkazo kutoka kwa familia utamfanya mke huyo Mkristo alegeze msimamo wake? Kutotaka kuwa katika hali yenye kuaibisha kunaweza kumfanya mtu alegeze msimamo wake! Kwa hiyo, mtu anapaswa kufikiria hali hiyo mapema vya kutosha, akifikiria kila moja ya mambo hayo, bila kusahau dhamiri yake mwenyewe ya Kikristo.—Matendo 24:16.

Je, Nikubali Marupurupu Yanayotolewa Wakati wa Krismasi?

Wakati wa msimu wa Krismasi, huenda mtu aliyemwajiri Mkristo akaamua kutoa zawadi au marupurupu. Je, Mkristo anapaswa kukataa? Inategemea. Huenda hata mwajiri wake asifikiri kwamba kwa kukubali marupurupu hayo, anayeyapokea anaadhimisha Krismasi. Huenda mwajiri huyo anawagawia tu wafanyakazi wake kiasi fulani cha faida ambayo kampuni ilipata. Au huenda marupurupu hayo yakawa njia ya kuonyesha shukrani zake kwa huduma zilizotolewa mwaka mzima na pia kuwachochea kuendelea kufanya kazi kwa bidii. Huenda mwajiri huyo akawapa zawadi wafanyakazi wote—Wayahudi, Waislamu, au watu wa dini nyinginezo—bila kujali ikiwa wao huadhimisha Krismasi au sivyo. Kwa hiyo, kwa kuwa tu zawadi hiyo inatolewa wakati huo au kwa kuwa inahusianishwa na sikukuu fulani, haimaanishi kwamba mmoja wa Mashahidi wa Yehova hawezi kuikubali.

Pia, hata ikiwa zawadi inatolewa katika sikukuu ya kidini, hilo halimaanishi kwamba anayeipokea ana imani ileile ya kidini. Huenda mfanyakazi au mtu wa ukoo akamwambia Shahidi, “Najua kwamba wewe huadhimishi sikukuu hii, hata hivyo, bado ningependa upokee zawadi hii kutoka kwangu.” Ikiwa dhamiri ya Mkristo haitamsumbua, anaweza kuamua kuipokea zawadi hiyo na kumshukuru pasipo kuihusianisha na sikukuu hiyo. (Matendo 23:1) Huenda Mkristo akaeleza kwa busara msimamo wake wakati ambapo haielekei kwamba kufanya hivyo kutamwudhi mtu.

Hata hivyo, namna gani ikiwa yule anayeitoa zawadi hiyo anakusudia kuonyesha waziwazi kwamba Mkristo huyo hashikamani na imani yake au atalegeza msimamo wake ili kupata faida za kimwili? Katika hali kama hizo ingefaa kuikataa zawadi hiyo. Bila shaka, tunataka kujitoa kumtumikia Yehova peke yake.—Mathayo 4:8-10.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki