AZAZELI
(Azazeli) [Mbuzi Anayetoweka].
Neno “Azazeli” linapatikana mara nne katika Biblia, katika maagizo kuhusu Siku ya Kufunika Dhambi.—Law 16:8, 10, 26.
Watu wana maoni tofauti-tofauti kuhusu asili ya neno hilo. Tukifuata jinsi neno hilo linavyoandikwa katika maandishi ya Kiebrania ya Wamasora, inaonekana ʽazaʼ·zelʹ ni muunganiko wa mizizi ya maneno mawili yanayomaanisha “mbuzi” na “kutoweka.” Basi maana inakuwa “Mbuzi Anayetoweka.” Kulingana na chanzo kingine kinachotegemea wazo la kwamba konsonanti mbili zimebadilishana, neno hilo linamaanisha “Nguvu za Mungu.” Vulgate ya Kilatini hulitafsiri neno hilo la Kiebrania kuwa caper emissarius, yaani, “mbuzi-mjumbe,” au “yeye anayesingiziwa makosa ya wengine.” Katika Kigiriki usemi unaotumiwa kwenye Septuajinti unamaanisha “yule anayechukua (kuepusha) uovu.”
Kila mwaka, kuhani mkuu alichukua kutoka kwa Waisraeli mbuzi wawili (wanambuzi wa kiume) ili watumiwe katika Siku ya Kufunika Dhambi. Kwa kupiga kura, mbuzi mmoja alichaguliwa kuwa wa “Yehova” na yule mwingine kuwa wa “Azazeli.” Baada ya ng’ombe dume kutolewa kuwa dhabihu kwa ajili ya kuhani mkuu na nyumba yake (bila shaka ilitia ndani Walawi wote), mbuzi aliyechaguliwa awe wa Yehova alitolewa akiwa dhabihu ya dhambi. Hata hivyo, mbuzi aliyechaguliwa awe wa Azazeli alihifadhiwa hai kwa muda fulani “mbele za Yehova ili dhabihu ya kufunika dhambi itolewe juu yake, kusudi aachiliwe aende zake nyikani akiwa wa Azazeli.” (Law 16:5, 7-10) Kufunika dhambi kwa ajili ya mbuzi huyo aliye hai kulitokana na damu ya mbuzi wa Yehova, aliyetoka tu kuchinjwa akiwa dhabihu ya dhambi, kwa kuwa uhai wa nyama umo katika damu. (Law 17:11) Kwa njia hiyo, thamani ya damu, au thamani ya uhai ya mbuzi aliyechinjwa ilihamishwa kwa mbuzi aliye hai, au mbuzi wa Azazeli. Ingawa si kuhani aliyemchinja, mbuzi huyo aliye hai alikuwa na thamani ya uhai au uwezo wa kufunika dhambi. Kwa kuwa mbuzi huyo alitolewa mbele za Yehova, ni wazi kwamba Yehova alitambua kuhamishwa kwa uwezo huo au nguvu za kufunika dhambi. Jambo linalofanana na hilo ni njia iliyopendekezwa ya kumtakasa Mwisraeli aliyeponywa ukoma, au kutakasa nyumba kutokana na tauni hiyo. Katika kisa hicho ndege aliye hai alitumbukizwa katika damu ya ndege aliyekuwa amechinjwa. Kisha ndege huyo aliye hai aliachiliwa aende zake, akichukua dhambi.—Law 14:1-8, 49-53.
Mbuzi wote wawili hakupaswa kuwa na kasoro, na walipaswa kufanana kadiri iwezekanavyo. Kabla ya kupigiwa kura, kila mbuzi alikuwa na fursa ya kuteuliwa awe kwa ajili ya Yehova. Baada ya kumtoa dhabihu mbuzi wa Yehova, kuhani mkuu aliweka mikono yake juu ya kichwa cha mbuzi aliye hai na kuungama dhambi za watu juu yake. Kisha mbuzi huyo alipelekwa nyikani na “mtu aliyechaguliwa.” (Law 16:20-22) Kwa njia ya mfano mbuzi wa Azazeli alibeba dhambi za watu za mwaka uliopita na alitoweka nazo nyikani.
Mbuzi wote wawili walikuwa kwa ajili ya dhabihu moja ya dhambi. (Law 16:5) Mbuzi wawili walitumiwa ili kukazia jambo lililotimizwa na uandalizi huo wa kufunika dhambi za watu. Mbuzi wa kwanza alitolewa dhabihu. Yule wa pili, alibeba dhambi za watu juu yake na akapelekwa nyikani, na hilo linaongeza uzito kwenye msamaha ambao Yehova huwapa wanaotubu. Zaburi 103:12 inatupatia uhakikisho huu: “Kama mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali sana na sisi.”
Kama mtume Paulo alivyoeleza, Yesu alipotoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi za wanadamu, alitimiza mengi zaidi ya yaliyotimizwa na “damu ya ng’ombe dume na ya mbuzi.” (Ebr 10:4, 11, 12) Kwa njia hiyo akawa “yeye anayesingiziwa makosa ya wengine,” na ‘mbebaji wa magonjwa yetu,’ yule ambaye “alichomwa kwa sababu ya makosa yetu.” (Isa 53:4, 5; Mt 8:17; 1Pe 2:24) ‘Alichukua’ dhambi za wote wanaoonyesha imani katika thamani ya dhabihu yake. Alionyesha uandalizi wa Mungu wa kuondoa dhambi kabisa. Kwa njia hizo, mbuzi “wa Azazeli” anafananisha dhabihu ya Yesu Kristo.