Ujihadhari na Mawazo ya Uadui
JE! WEWE umekwisha kusikia maneno kama haya: “Usiyaamini maneno hayo hata chembe!” au, “Yeye anajiona ni nani?” au, “Hiyo si ajabu sana. Kama ni mimi ningefanya vizuri zaidi”? Bila shaka sote tumekwisha kuyasikia, lakini ingekuwa bora kama nini kama mambo hayo yasingesemwa! Au, zaidi ya hayo, kama mtu asingekuwa hata na mawazo hayo ya uadui!
Nini kinachowafanya wengine kuwa na mawazo ya uadui juu ya wengine? Basi, huenda mtu mwingine anaangaliwa kwa kadiri isiyofaa, au huenda anasifiwa sana. Au pengine mwingine ataonyesha wazi shauku ya kuangaliwa na kusifiwa. Kwa hiyo yaweza kuwa kwamba katika itikio la mtu kwa hali hiyo dalili ndogo ya wivu imo ndani.
Biblia ina maonyo mengi mazuri ya kutulinda na tabia hizo mbaya. Inatuonya tuzizuie ndimi zetu, lakini inaonyesha vile vile haja ya kuyalinda mawazo yetu. Hata yasiposemwa kwa maneno, mawazo ya uadui hata hivyo yanaweza kudhuru. Yanaelekea kuharibu ukamatano na wengine. Huenda yakamdhuru anayeyawaza vile vile. Hii ni kwa sababu kile kinachokuwa na matokeo mabaya juu ya akili kinakuwa na matokeo mabaya juu ya mwili vile vile.
Kati ya mawazo ya uadui ambayo inatupasa tujihadhari nayo ni yale yanayoonyesha shuku. Kwa sababu gani? Basi, angalia mfano. Biblia yasimulia juu ya shuku isiyo ya haki ya wakuu wa watu walioitwa Waamoni. Watu hawa, wajapokuwa walikuwa wakiwashambulia Waisraeli mara nyingi, hawakuwa wameshambuliwa nao wakati wo wote, kwa maana Israeli walikuwa wamepokea maagizo ya wazi kutoka kwa Yehova wasifanye hivyo. (Kum. 2:19) Na hali Mfalme Daudi wa Yerusalemu alipotuma wajumbe wakawapelekee masikitiko yake, kwa sababu ya kifo cha mfalme wao, wakuu hao waliwashtakia wajumbe kuwa wapelelezi nao wakawavunjia heshima sana. Shuku zao hata ziliwafanya kutoa rushwa kwa taifa lililo jirani liungane nao katika vita juu ya Israeli. Mwishowe walipatwa na mabaya kwa sababu ya shuku zao zisizo haki kwa kushindwa na kutiishwa na Israeli. Twaweza kujifunza kutokana na maono yao.—1 Nya. (Sik.) 19:1 mpaka 20:3.
Tunaposhughulika na marafiki, watu wa ujamaa, wasiri na, zaidi, na Wakristo wenzetu, ni afadhali kuwaamini wengine. Hata kama magumu yakitokea, wahesabu kuwa haki. Ni afadhali kukata tamaa mara kwa mara kuliko kuwa wenye shuku, kana kwamba kila mtu alikuwa tayari kukulaghai. Waume wengi na wake wanafanya maisha zao zenye huzuni kwa sababu ya kuwa na shuku ya kadiri isiyofaa juu ya mmoja na mwenzake. Ndoa yao ingekuwa yenye furaha zaidi namna gani kama wangeweza kufikiriana mmoja na mwenzake kwa njia ya fadhili!
Zaidi kwa habari ya maoni yetu juu ya makusudi ya watu wengine yamepaswa yalindwe juu ya kuwa na mawazo ya uadui. Usisahau kwamba Ibilisi mwenyewe ndiye aliyewageuza wengine kwanza kwa makusudi ya kichoyo, akifanya hivyo bila sababu ya haki. Yeye aliuanza mwendo wake mwovu kwa kufikiri mawazo ya uadui juu ya Mungu, nako kukatokeza kumchongea Muumba. (Mwa. 3:1-5) Nyumaye alitilia shaka makusudi ya watumishi wote wa Mungu. Hii imeelekeza kwenye nini? Yeye anafanya yote awezayo kuzihakikisha shuku zake kuwa kweli. Ikumbukwe, hiyo ni sababu nyingine kwa kutokuwa wenye shuku kwa kadiri isiyofaa; sikuzote ipo hatari ya kujaribu kuzihakikisha shuku za mtu kuwa kweli, na kwa njia hiyo kujifanya adui ya wengine.—Ufu. 12:10.
Vile vile mawazo ya uadui yanatokana na kuwa wenye kulaumu mno, kutazamia mengi mno kutoka wa wengine. Ni vema kujua kwamba linaloweza kuelekea kuwa dogo na hafifu kwetu laweza kumaanisha ushindi mkubwa au kazi bora kwa upande wa mwingine. Katika nyumba ambamo mna kutengana kwa wazazi na watoto, je! sana sana si kwa sababu ya wazazi kuwa wenye kulaumu mno watoto wao, na watoto kuwalaumu wazazi wao mno? Wangeweza kujifunza kutokana na mithali ya Kituruki: “Yeye atafutaye rafiki bila kosa atakaa bila mmoja.”
Zaidi kuna haja ya wasafiri kujihadhari na mawazo ya uadui, yenye kulaumu kwa kadiri isiyofaa wanapotembelea nchi za kigeni. Kuona mambo ya ajabu na desturi huenda nako kukamfanya mtu azilinganishe na hali azionazo katika nchi yake mwenyewe. Kuliko kuwa hivyo, je! isingekuwa afadhali kutumia huruma, kuwaza mtu mwenyewe angalifanya nini kama mwenyewe angalikuwamo katika hali hizo? Akifanya hivyo, mtu ataweza kuhesabia mema, akifahamu ni kwa kadiri gani ambavyo waliomo wamepatwa na hali hizo. Akiwa na maoni mema, mtu aweza kufurahia kwa unyofu yale wanayoweza kutimiliza chini ya hali zilizoko.
Jifunze kuyafurahia yanayofanywa na wengine kwa kuyaangalia mambo yao mema mahali pa kuwa mwepesi mno kuyaona makosa yao. Usiwe kama mtu mpumbavu ambaye, alipoona kurudia-rudia kwa msemaji maneno fulani, alizidi kuhesabu ni mara ngapi msemaji aliyatumia. Angalifaidika zaidi namna gani kutokana na hotuba kama angekaa sana juu ya sababu zilizotolewa na kuufurahia unyofu wa msemaji!
Kwa hiyo, kwa faida yako mwenyewe na kwa ajili ya ujamaa mwema na watu wengine, ujihadhari na mawazo ya uadui. Mahali pake, litii shauri lililoongozwa na roho ya Mungu: “Hatimaye, ndugu zangu, mambo yo yote . . . yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema; ukiwapo wema wo wote, ikiwapo sifa nzuri yo yote, yatafakarini hayo.”—Flp. 4:8.