Ushindi wa Kimungu—Maana Yake kwa Wanadamu Wanaotaabika
“Ushindi na uwezo na milki vimepatwa milele na Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake, sasa kwamba mtesi, aliyewashtaki ndugu zetu mchana na usiku mbele za Mungu wetu, ameshushwa chini.”—Ufu. 12:10, “The Jerusalem Bible.”
1. Ni nini maana ya usemi “ushindi wa kimungu”?
USHINDI WA KIMUNGU! Kwa usemi huo twamaanisha ushindi wa mtu wa kimungu. Hatumaanishi mungu wa kike Niʹke (Ushindi) mwenye mabawa wa hadithi za Kigiriki, ambaye jina lake liliambatanishwa na silaha ya kutupa juu angani ya majeshi ya Kiamerika, yaani, silaha ya Niʹke-Hercules. Sivyo, bali twamaanisha ushindi wa Mungu Muumba wa mbingu na dunia, Muumba wa wanadamu duniani. Ushindi wake waweza kumaanisha mema kwa wanadamu katika taabu yao kuu ya leo.
2. Neno “ushindi” limeshirikishwa sana na nini?
2 Wakati wa historia yote ya kibinadamu neno “ushindi” limeshirikishwa sana na vita, na, walau, na mashindano, mabishano, au na hali zisizopendeza zinazopaswa kushindwa. Bila shaka, taabu iliyopo na huzuni kuu ya mataifa yote ya dunia ni hali isiyofaa inayopaswa kuondolewa kwa ajili ya faida ya milele ya wanadamu.
3. Kwa sababu ya maana inayoshirikishwa na “ushindi wa kimungu,” ni maulizo gani tunayouliza juu ya Mungu, na yafaa tufanye nini?
3 Basi je!, tukate shauri kutokana na usemi “ushindi wa kimungu” kwamba Mungu wa uumbaji wote yu karibu kujitia vitani, katika mashindano, katika mabishano? Je! ikiwa vita hiyo inakusudiwa na Mungu itawahusu wanadamu? Je! itawahusu wanadamu wote—kutufaidi sisi katika taabu yetu? Iwapo jibu la maulizo haya ni Ndiyo!, basi sababu yaonyesha inatupasa tupendezwe na vita hiyo. Ndiyo, inatupasa tujue yafaa tujipange katika upande gani wa vita hii, kwa kuwa tunautamani sana ushindi wa kimungu.
4. Kwa sababu gani taabu ya mataifa yote na huzuni kuu ya leo vyatuhitaji tupate maana ifaayo juu ya “ushindi wa kimungu”?
4 Watu mbalimbali wana maoni yanayotofautiana juu ya yeye aitwaye “Mungu.” Wakomunisti wenye kupinga dini wanayo maoni yao juu ya Mungu. Ule uitwao ulimwengu wa Kikristo, Kristendomu, unayo maoni yake juu ya Mungu. Ulimwengu wa Kiislamu unayo maoni yake juu ya Mungu wake Allah. Ulimwengu wa Kiyahudi unayo maoni yake wenyewe. Sehemu nyingine zilizobaki zisizo za Kikristo za wanadamu zina maoni yazo zenyewe juu ya Mungu. Kwa hiyo, kila kikundi cha kidini, au kikundi kisicho cha kidini, huenda kikawa na maoni yacho chenyewe juu ya kinachoweza kumaanishwa na “ushindi wa kimungu” wakati ujao kwa wanadamu. Kwa akili, kusingekuwa na mapatano kati ya maoni haya yote juu ya kinachomaanishwa na “ushindi wa kimungu.” Kwa hiyo, isingeshangaza kwamba ushindi wa kimungu wa kweli unaokaribia utakuwa tofauti na vile ambavyo wote wangeutazamia umaanishe. Bila shaka, taabu na huzuni kuu ya mataifa yote leo vinatuhitaji tupate ufahamu ufaao juu ya shauri hili.
5. Tutaiendea mamlaka gani tupate habari juu ya vita hii, nayo mamlaka hiyo yamalizia maandishi yake kwa kichwa gani?
5 Ni wazi kwamba lazima tuendee Mamlaka itakayovikwa taji ya ushindi wa kimungu kwa habari ya vita hii. Mamlaka hii ni kitabu ambacho kimeenea duniani pote kwa maelfu ya mamilioni ya nakala katika mamia ya lugha kubwa za wanadamu. Kitabu hiki ndicho Biblia Takatifu. Ndicho kitabu cha pekee ulimwenguni kinachoisimulia hii vita ya ulimwengu wote ambamo Mungu, Muumba wa Pekee wa mbingu na dunia, atajishuhudia kwa ushindi wa kukata maneno. Kwa hiyo lazima tuyaendee maandiko matakatifu ya Biblia Takatifu tupate taarifa ya kweli juu ya habari hii ya maana sana. Tunaposema Biblia twamaanisha, si “vitabu ishirini na vinne vya Maandiko Matakatifu” tu wanavyovisoma Waebrania au Wayahudi, bali Biblia yote iliyo na Maandiko ya Kikristo pia yaliyoongozwa na roho ya Mungu wala si hayo Maandiko Matakatifu ya Kiebrania tu. Kitabu cha mwisho katika Biblia hiyo iliyokamilika kiliandikwa karne kumi na tisa zilizopita na mtume wa Kikristo Yohana nacho chaitwa Ufunuo. Kwa kufaa sana, kinaimalizia hii Biblia ya Mungu iliyoongozwa na roho yake kwa kichwa cha ushindi wa kimungu.
6. Kuna maoni gani yaliyochanganyika juu ya kama Kristendomu atafaidika kutokana na ushindi huo wa kimungu?
6 Ni kweli kwamba mashirika ya Biblia ya Kristendomu yamefanya mengi kuieneza Biblia Takatifu ulimwenguni pote, naye Kristendomu mwenyewe anajidai kushikamana na Biblia. Kwa sababu hii, je! Kristendomu ndiye atakayefaidika kutokana na ushindi wa kimungu ujao? Je! vita ijayo iliyotabiriwa katika Biblia itapiganwa kwa ajili ya Kristendomu ili yeye ahifadhiwe? Ndivyo ambavyo watu wa kidini wa Kristendomu wangependa kufikiri. Wakomunisti wasioamini kuwako kwa Mungu na ulimwengu usio wa Kikristo hawapendi kufikiri hivyo, nao wanayo sababu nzuri ya kutolipenda jambo hilo.
7. Nchi za Kristendomu na za Kikomunisti zinalinganaje kwa habari ya idadi ya watu, na kwa sababu gani Kristendomu anadhani kwamba aweza kushinda vitani?
7 Wakati mambo yanapoonwa kutokana na maoni ya kidini, kwa nje hali inaelekea kumpendelea Kristendomu. Wanakanisa wake na viongozi wa kidini wanadhani kwamba Kristendomu hana mabishano na Mungu wa Biblia Takatifu. Lakini kwa habari ya Wakomunisti wa asili, wao wamo katika vita ya wazi na Mungu, mungu wa kila namna ya dini licha ya Mungu wa Biblia. Nchi za Kikomunisti za Ulaya zilijidai wakati mmoja kuwa za Kikristo, lakini sasa zinamkana Kristendomu na kujiona si sehemu yake. Hata hivyo, zinapendezwa na kuyatumia matengenezo ya kidini zinayoyaruhusu yatende kazi katika nchi zao, kwa makusudi ya kisiasa na kwa msaada wa vita. Kwa kadiri ambavyo idadi zinavyohusika, majeshi ya Wakomunisti wenye kumpinga Mungu Ulaya, Asia na Afrika yanaelekea kuwa mengi zaidi ya majeshi ya Kristendomu mwenye kufuata dini. Kulingana na makadirio ya karibuni zaidi Kristendomu anajivunia kuwa na ushirika wamakanisa wa watu 985,363,400. Walakini, kwa kuwa anadhani Mungu yuko upande wake, Kristendomu anafikiri kwamba anaweza kushinda majeshi yote yenye kumpinga Mungu.
8. Mataifa ya Kristendomu yalimtupiaje Mungu mzigo nyakati za vita, na nini kilichoamua kuupata ushindi?
8 Si jambo geni kwa mataifa ya kidini kumshirikisha mungu wao au miungu yao na vita vya kitaifa. Ndivyo ambavyo imekuwa tangu nyakati za kale sana, hata kabla ya Kristendomu kuanzishwa katika karne ya nne ya Wakati wetu wa Kawaida. Wamisri wa kale, Waashuru, Wababeli, Wamedi na Waajemi, Wagiriki, na Warumi wote walikuwa na miungu yao waliyoiomba wapate ushindi katika vita vyao. Hata Wakomunisti wenye elimu wanajua hilo. Hata hivyo, ajabu ni kwamba kwa habari ya Kristendomu, mataifa yake yamepigana yenyewe kwa yenyewe, nayo mataifa hayo yalisali kwa Mungu yule yule mmoja yalipokuwa vitani. Wakatoliki walipigana na Wakatoliki. Wakatoliki walipigana na Waprotestanti. Waprotestanti walipigana na Waprotestanti. Hivyo walimtupia Mungu mzigo aamue angeupendelea upande gani wa Kristendomu kwa ushindi, na ni sala za mataifa yapi angezijibu kwa upendeleo. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, iliyoanza ndani ya Kristendomu, na ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, iliyoanza ndani ya Kristendomu vile vile. Chini ya hali hizo, katika vita hivyo vyote vya Kristendomu, je! uamuzi wa Mungu ndio ulioonyesha upande wenye kushinda, au vilikuwa ni vifaa vya kijeshi na ujuzi wa kupiga vita?
9. Ukitolewa na Mungu, kwa sababu gani ushindi wa Kristendomu usingeleta faraja ya milele kwa wanadamu wanaotaabika?
9 Walakini, je! Mungu atasukumwa atende na vita ya atomiki kati ya Kristendomu mwenye kufuata dini na Wakomunisti wa mataifa yote wasiomcha Mungu, hata Mungu aupendelee upande wa kidini kuliko upande wenye kupinga dini? Kama sote tujuavyo, matayarisho yamekuwa yakifanywa kwa makumi ya miaka juu ya “vita ya mwisho” kati ya jamii ya mataifa ya kidemokrasi yenye utajiri na jamii ya mataifa ya Kikomunisti yasiyoamini kuwako kwa Mungu. Je! Mungu wa kweli wa pekee aliye hai aweza kutumainiwa amsaidie Kristendomu? Ushindi kwa Kristendomu ungemaanisha ataendelea kuhifadhiwa. Lakini, kwa kuamua kulingana na historia ya Kristendomu mpaka sasa, je! yeye anastahili kuhifadhiwa? Inakubaliwa waziwazi na viongozi wa kidini wa Kristendomu kwamba unafiki wake na kushindwa kuishi kulingana na Ukristo wa kweli ndivyo vimefanya Wakomunisti wa mataifa yote wapate mamlaka ya ulimwengu. Kwa hiyo, kuna sababu gani ya kuamini kwamba kuhifadhiwa kwa Kristendomu baadaye kusingefanya Wakomunisti wasiomcha Mungu watokee tena na hivyo mwishowe kutokee vita nyingine ya pande zote mbili kwa mara nyingine tena? Kwa hiyo, ushindi wa Kristendomu hautoi uhakikisho wa faraja kwa wanadamu wanaotaabika.
KULIACHA NENO LA MUNGU LILILOANDIKWA LIMSEMEE YEYE
10. Twajuaje kama Mungu yuko upande wo wote, au hayuko, na kwa hiyo, jibu ni nini?
10 Kwa hiyo sasa ulizo linatujia, Je! Mungu atakuwa upande wo wote katika vita hiyo ya kijeshi kati ya Kristendomu mwenye kufuata dini na Wakomunisti wenye kupinga dini? Je! yeye amepata hata kuwako upande wo wote katika “vita ya umwagaji wa damu” ambayo imekuwa ikiendelea kwa miaka mingi kati ya jamii hizi mbili za mataifa? Njia ya pekee kwetu kulipata jibu la kweli na lenye kuridhisha kama watu wasiopendelea ni kumwacha Mungu ajisemee mwenyewe. Yeye anafanya hivi, kupitia kwa kurasa za Neno lake la unabii lililoongozwa na roho yake, Biblia Takatifu. Jibu lake li wazi na hakika. Yeye hapendelei jamii yo yote ya mataifa kati ya hizi. Zote mbili zinampinga Yeye.
11, 12. Ni kulingana na kanuni gani ya kimungu hakuna kosa juu ya kumtaja Kristendomu kama adui ya Mungu?
11 Inapatana kuwaza kwamba Mungu asingeweza kuwapigania adui zake. Ndiyo, lakini je! Kristendomu ni adui ya Mungu? Ebu yatazame mamia ya maelfu ya makanisa yake. Zitazame madhehebu elfu moja au zaidi za kidini zilizomo ndani yake. Yatazame mamia ya maelfu ya viongozi wa kidini wanaotumikia katika makanisa yake na kumtolea Mungu sala nzito katika jina la Yesu Kristo. Basi, bila shaka lazima kuwepo kosa fulani katika kumtia Kristendomu kati ya adui za Mungu. Lakini hamna kosa katika hili. Si kwamba tu Mungu hawapendi wale walio adui zake wa wazi bali pia hawapendi wale walio rafiki za adui Zake. Wakati mfalme wa kale wa Yerusalemu aliporudi kutoka kumpa mfalme mwovu msaada wa kijeshi, Mungu alimwambia hivi: “Je! imekupasa kuwasaidia waovu, na kuwapenda wamchukiao [Yehova]? Kwa ajili ya hayo ghadhabu i juu yako itokayo kwa [Yehova].” (2 Nya. (Sik.) 19:1, 2) Na muda mwingi baadaye, Mungu uyu huyu alisema hivi kupitia kwa mwanafunzi wa Kikristo Yakobo:
12 “Hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”—Yak. 4:4.
13. Kwa sababu gani kuwamo kwa Kristendomu katika “vita ya umwagaji wa damu” juu ya Wakomunisti hakukanushi kwamba yeye si rafiki wa ulimwengu?
13 Nani awezaye kukana kwamba Kristendomu si rafiki wa asili wa ulimwengu huu? “Vita ya umwagaji wa damu,” ukatili, kati ya mataifa ya Kristendomu na jamii ya Wakomunisti havikani kwamba Kristendomu si rafiki mkubwa wa ulimwengu mzima. Matatizo yaliyomo kati ya mataifa ya Kristendomu na jamii ya Wakomunisti hayakusababishwa na ulizo la dini. Siasa ndilo ulizo. Mawazo ya vikundi viwili vya kisiasa vinavyotofautiana sana yanahusika. Mataifa makubwa ya Kristendomu yalikuwa rafiki ya Urusi ya Wakomunisti wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Na sasa, katika tengenezo la Umoja wa Mataifa lenye mataifa washirika 132, mataifa yote kabisa ya Kristendomu ni washirika kando-kando ya Urusi ya Wakomunisti, Uchina ya Wakomunisti, na mataifa mengine ya Wakomunisti. Kwa kweli, walau nusu ya washirika wa Umoja wa Mataifa si mataifa yaitwayo ya Kikristo. Mataifa ya Kristendomu yanadumisha mapatano na serikali za ulimwengu huu. Yanafanya biashara kwa kawaida na mataifa hayo kulingana na mikataba. Yanapeana mazao ya ukulima. Mji wa Vatican, unaosimamiwa na mkuu wa tengenezo kubwa kupita yote ya kidini ulimwenguni, unabadilishana wasuluhishi na nchi nyingi za ulimwengu kama uwezavyo.
14. (a) Je! Yakobo angesema kwamba Kristendomu amejifanya rafiki wa ulimwengu kwa mwendo wake? (b) Maoni ya Mungu ni nini, na Yeye atatazamiwa kufanya nini wakati Kristendomu atakapopatwa na shambulio la mwisho?
14 Mataifa ya Kristendomu yanajaribu kudumisha uhusiano wa kirafiki na mataifa yaliyoko nje ya Kristendomu. Yanajitia katika siasa za ulimwengu huu. Na wakati wanapoyaiga mataifa ya kilimwengu kwa kuchukua silaha zenye kufisha wasuluhishe kutopatana kati yao, makanisa ya Kristendomu yanaziunga serikali zao za kisiasa mkono kabisa, viongozi wao wa kidini wakijaribu kumtia Mungu katika vita vya mataifa yote kwa kumwita Yeye katika sala. Je! mwanafunzi wa Kikristo Yakobo angeyaita haya yote wonyesho wa “kuwa rafiki wa dunia” kwa upande wa Kristendomu? Je! angesema kwamba Kristendomu “hujifanya kuwa adui wa Mungu,” akiwa rafiki wa ulimwengu? Ndiyo! Kusingekuwa na jibu jingine lo lote lililo la kweli. Bila ya kujali uanadini wake wote, Kristendomu ni adui wa Mungu anayestahili lawama zaidi sana. Yeye, pamoja na Wakomunisti wasiomcha Mungu na watu wengine wa ulimwengu, anampinga yeye. Kwa hiyo Mungu anampinga yeye. Mungu hamwungi mkono. Mungu hawezi kutazamiwa amtetee Kristendomu wakati majeshi ya kisiasa ya ulimwengu yatakapoungana katika shambulio la ulimwengu juu ya dini kabla wao wenyewe hawajaingia katika vita ya Har–Magedoni. (Ufu. 17:1-16) Faraja yo yote kwa wanadamu waliotaabika haiwezi kutazamiwa kutoka kwa Kristendomu.
15. Lazima isemweje juu ya kama ni vita ya kidini inayopangwa na washindani, na kwa hiyo ni nani wanaoendelea kutaabika?
15 Kristendomu hawezi kutazamiwa ashiriki katika ushindi wa kimungu penye vita ijayo ya vizazi. Kwa kweli kujitayarisha kwa mataifa yake kwa vita pamoja na jamii ya Wakomunisti wenye kuamini mambo yanayoonekana tu si kwa ajili ya kuuhifadhi Ukristo. Ni kwa ajili ya kuhifadhi utawala wa kisiasa, ili haki ya namna zake za kisiasa za serikali ibaki. Si vita ya kidini inayopangwa na washindani. Shauri kubwa linaloshindaniwa ni, Dunia ni ya nani? N’nani atakayeitawala dunia? Na kwa sababu ya ugomvi mkali juu ya ulizo hili la mataifa yaliyogawanyika kwa kisiasa, wanadamu wanaendelea kutaabika, kuona huzuni kuu.
16. Ni ulizo gani kubwa litakalojibiwa sasa kwa mara ya mwisho na ni sala gani ifaayo itakayojibiwa kwa njia hiyo?
16 Kuliko wakati mwingine wo wote wa historia ya kibinadamu uliotangulia, wakati umefika wa ulizo hili la kiserikali kujibiwa kwa mara ya mwisho, N’nani atakayeitawala dunia? Aliye wa pekee awezaye kulijibu ulizo hilo ifaavyo na kuleta amani ya milele ni Mungu, Muumba na Mwenye dunia. N’nani aliye na haki zaidi ya kusema atakayeyatawala makao haya ya kidunia ya wanadamu wote kuliko Yeye? Katika Neno lake lililoandikwa lisilobadilika, Biblia, yeye amelitangaza kusudi lake la kutoa usemi Wake katika wakati wake. Wakati huo unakaribia sana! Wakati wake wa kuijibu sala ambayo imetolewa kwake kwa vizazi vingi vilivyopita umefika. Ndiyo sala iliyofundishwa na Mwanawe mwenyewe aliyetoka mbinguni miaka mia kumi na tisa iliyopita. Ndiyo sala ambayo Yesu Kristo aliwafundisha wanafunzi wake wa kweli kusali. Kwa kutii wafuasi wake waaminifu wameisali sala hiyo hata sasa, “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mt. 6:9, 10.
KUIJIBU SALA YA UTAWALA WA KIMUNGU
17. (a) Sala hiyo inaombea nini, na je! Kristendomu imeonekana kuwa jibu kwa sala hiyo? (b) Kwa hiyo, ni nini lazima iende zake, na ni nini lazima uje, kwa kuijibu sala ya nani?
17 Hiyo ni sala ya utawala wa kimungu, ya serikali ya kimungu, ndiyo, ya ushindi wa kimungu! Kwa kutoielewa maana ya sala hiyo, maelfu ya mamilioni ya watu wa Kristendomu wameisali sala hiyo kwa karne nyingi nyumbani na makanisani mwao, lakini vita vya umwagaji wa damu vilivyopiganwa na mataifa ya Kristendomu vimeshindwa kuuleta ufalme huo. Njia yao siyo njia ya Mungu ya kuiletea serikali yake ya kimungu. Kristendomu haikuonekana kuwa ufalme wa Kristo, kama jina Kristendomu linavyodokeza. Kristendomu haikuutimiza unabii wa Biblia juu ya fahari, uzuri na baraka za ufalme wa Kristo kwa wanadamu wote. Kristendomu imeuwakilisha ufalme wa Kristo vibaya. Mungu hawezi kuikubali Kristendomu kama ufalme wa kweli wa Mwanawe Yesu Kristo. Lazima Kristendomu iende zake! Lazima ufalme wa kweli wa Mungu kwa njia ya Kristo uje! Sala tuliyofundishwa na Mwana wa Mungu mpendwa haitapita bila kujibiwa. Wanafunzi wake wa kweli wasio wanafiki hawakuitoa sala hiyo bure.
18. (a) Jibu kwa sala hiyo litamaanisha ushindi juu ya nani? (b) Viongozi wa kidini wamekuwaje waasi kuhusiana na wanasiasa kwa habari ya Majira ya Mataifa?
18 Tofauti na wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo, makundi ya Kristendomu ya ulimwengu mwingine wote hayautaki ufalme wa Mungu. Ndiyo sababu kusimamishwa kwa ufalme Wake ukiisimamia dunia yote kabisa kutakuwa na maana ya ushindi wa kimungu kweli kweli. Juu ya nani? Juu ya mamlaka zote za kidini na za kisiasa zinazoupuza uenyeji wa Mungu wa dunia na zinazopigania utawala wa kitaifa wa serikali za kisiasa zilizoundwa na wanadamu uendelee. Washindani hawa wa utawala wenye kuendelea wa serikali za kibinadamu za kisiasa juu ya dunia wanakataa kukubali kwamba Majira ya Mataifa yamekwisha. Mungu aliyaweka hayo Majira ya Mataifa ili mataifa ya kilimwengu yaitawale dunia yote bila ya kukatizwa na ufalme Wake, nayo majira hayo yalikoma katika vuli ya mwaka wa 1914 C.E. (Luka 21:24) Viongozi wa kidini wa Kristendomu hawajapata kuwaonyesha watawala wa kisiasa wa mataifa uhakika huu. Hawajapata kuonyesha kwamba mwishoni mwa Majira ya Mataifa kinyume cha yaliyotukia mwanzoni mwa majira hayo katika mwaka wa 607 B.C.E. kingetokea.
19. Mwanzoni mwa Majira ya Mataifa, Mungu aliondoa nini duniani, na kwa njia gani?
19 Mwanzoni mwa Majira ya Mataifa katika vuli ya mwaka huo Mungu aliuondoa duniani ufalme wa Mungu wa mfano na kuziacha mamlaka za Mataifa yasiyo ya Kiyahudi ziuchukue usimamizi wa nchi zote. Mungu alifanya hivi kwa kuyaruhusu majeshi ya Babeli ya kipagani yamvue taji Masihi wa mfano, mfalme wa Yerusalemu, na kuuharibu mji mtakatifu na hekalu lake, na kuuacha Yerusalemu na nchi ya Yuda iwe ukiwa kwa miaka 70.
20. (a) Kinyume chake, Mungu alifanya nini mwishoni mwa Majira ya Mataifa? (b) Kwa sababu gani tendo la Mungu halikuonekana na watawala wa kisiasa duniani?
20 Kinyume cha hili, mwishoni mwa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 C.E., Mungu aliurudisha ufalme wake, si kwa njia ya mfano ukiwa na mfalme wa mfano wa Kimasihi, bali kwa njia halisi, kwa njia iliyofananishwa. Ndiyo sababu mwaka huo hakuusimamisha tena ufalme wa jamaa ya kifalme ya Daudi Yerusalemu katika Mashariki ya Kati. Bali, aliusimamisha ufalme mikononi mwa Yesu Kristo aliyekuwa mzao wa asili wa Mfalme Daudi wa kale, alipokuwa mwanadamu duniani. Vile vile, kwa kuwa Yesu Kristo si mwanadamu tena duniani bali alifufuliwa kutoka kifo cha kushindania imani kwenye uzima wa kiroho wa kimbinguni, Mungu aliusimamisha ufalme wa huyu Mzao wa Mfalme Daudi mbinguni, katika unaoitwa “Yerusalemu wa mbinguni.” (Mt. 1:1; 1 Pet. 3:18; Ebr. 12:22) Ndiyo sababu kuzaliwa kwa ufalme huo wa Kimasihi hakukuonekana mwaka wa 1914 C.E. na watawala wa kisiasa wa Kristendomu na wa milki ya upagani. Na hali kuzaliwa huko kulipaswa kutokee katika wakati wake, nako kulijionyesha kwa mambo kulikoyatokeza mbinguni na duniani pia.
21-23. (a) Kwa sababu gani “vita” hiyo mbinguni si jambo la kudhihaki kwa kutokuamini? (b) Yohana anakisimuliaje chanzo cha hili katika Ufunuo, sura ya 12?
21 Je! twafahamu kwamba vita ilitokea mbinguni kwa sababu ya kuzaliwa kwa matokeo mazuri kwa huo ufalme wa Kimasihi uliotoka kwa tengenezo la Mungu la kimbinguni kama mtoto aliyezaliwa karibuni na mwanamke? Hili si jambo la kudhihaki kwa kutoamini, kwa maana vita yo yote ina matokeo yake nayo vita hii isiyoonekana ya kimbinguni ilikuwa na matokeo yake juu yetu hapa duniani. Matokeo ya vita hiyo si jambo la kuchekelewa nasi, kwa maana tunayaona kwa maumivu. Haya ndiyo yanayolihakikisha jambo hili. Chanzo chake kisichoonekana cha kimbinguni kilionyeshwa kwa njozi kwa mtume wa Kikristo Yohana kwa njia ya unabii. Yeye anatupa masimulizi yafuatayo, kulingana na The New English Bible ya 1970:
22 “Yeye [yaani, tengenezo la Mungu la kimbinguni] akazaa mtoto wa kiume, aliyewekwa kutawala mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Lakini mtoto wake akanyakuliwa juu kwenye Mungu na kiti chake cha enzi; . . . Kisha vita ikatokea mbinguni. Mikaeli na malaika zake wakapiga vita juu ya yule joka. Yule joka na malaika zake wakapigana, lakini hawakuwa na nguvu za kushinda, wala hawakuachiwa mahali pa kuwekea miguu mbinguni.
23 “Kwa hiyo yule joka mkuu akatupwa chini, yule nyoka wa zamani aliyeupotoa ulimwengu wote, aitwaye Shetani, au Ibilisi—akatupwa chini duniani, nao malaika zake pamoja naye. Ndipo mimi [Yohana] nikasikia sauti mbinguni ikitangaza kwa sauti kuu: ‘Hii ndiyo saa ya ushindi wa Mungu wetu, saa ya enzi yake kuu na uwezo, wakati ambapo Kristo wake aja kwenye utawala wake wa haki! Kwa maana mshtaki wa ndugu zetu amepinduliwa, aliyewashtaki mchana na usiku mbele za Mungu wetu. Kwa dhabihu ya Mwanakondoo wamemshinda, na kwa ushuhuda walioutoa; kwa maana wao hawakuuona uhai wao kama wenye thamani mno wasiweze kuutoa. Furahini basi, enyi mbingu nanyi mkaao humo! Lakini ole ni wenu, dunia na bahari, kwa maana Ibilisi amewashukieni akiwa mwenye ghadhabu nyingi, akijua kwamba wakati wake ni mfupi!’”—Ufu. 12:5-12, NE; pia The Jerusalem Bible.
24. (a) Hiyo “vita . . . mbinguni” iliendelea kwa muda gani? (b) Kwa sababu gani matokeo ya vita hiyo yalipaswa kuwa “ole” kwetu nchini na baharini?
24 Katika maandishi haisemwi ni kwa muda gani hiyo “vita . . . mbinguni” kati ya malaika watakatifu na mashetani wa kiibilisi iliendelea; lakini haielekei sana kwamba iliendelea kwa muda mrefu zaidi kuliko Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, iliyokwisha Novemba 11, 1918. Bila ya kujali ilivyokuwa, jambo la kipekee zaidi ni, Vita hiyo ilituhusuje sisi duniani tusiokuwa tumejua kutokea kwake mbinguni? Mbingu takatifu ziliagizwa zifurahie ushindi wa Mungu, ushindi wa kimungu, lakini namna gani sisi hapa duniani? Sauti kuu mbinguni ilisema: “Lakini ole ni wenu, dunia na bahari!” Kwa sababu gani “ole” kwetu, kama ni nchini au baharini? Kwa maana “Ibilisi amewashukieni akiwa mwenye ghadhabu nyingi, akijua kwamba wakati wake ni mfupi!”—Ufu. 12:12, NE.
25, 26. (a) Ni maulizo gani yanayotolewa kwa watu wanaokudhihaki kuwapo kwa Shetani na malaika zake wa kishetani juu ya mambo ya kibinadamu tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza? (b) Mwisho, kwa habari ya chanzo na matokeo, twauliza ulizo gani?
25 Huenda wadhihaki wa Biblia wakayaona maoni haya ya Shetani Ibilisi na malaika zake wa kishetani kutupwa chini kwenye ujirani wa dunia yetu kama utani. Lakini je! wanaweza kutania au wanaitania “ole” inayoipata dunia na bahari pia leo? Sivyo, wadhihaki hao hawawezi kumwona Shetani Ibilisi kwa macho yao ya asili, lakini wana sababu ya kujua kwamba yeye na majeshi yake ya malaika za kishetani wako karibu, katika ujirani wetu. Ikiwa hawaamini, basi na wajibu ni kwa nini Ushirika wa Mataifa uliotengenezwa muda mfupi baada ya kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza haukuwa tengenezo la mataifa yote la amani na usalama wa ulimwengu. Kwa sababu gani haukuwazuia wanasiasa wenye kutumia nguvu na wenye kutaka vita wasitokee Ulaya? Kwa sababu gani haukuizuia Vita ya Ulimwengu ya Pili katika mwaka wa 1939 isitokee, vita iliyofikia upeo kwa kupasuka kwa makombora mawili ya atomiki yakileta ole kwa wakaaji wa Hiroshima na Nagasaki?
26 Pia, Kwa sababu gani tengenezo la Umoja wa Mataifa halijavizuia vita vyote na mapinduzi, ugomvi juu ya mipaka ya nchi, na ghasia nyingine za kisiasa mpaka sasa, tangu liundwe mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili mwaka wa 1945? Kwa sababu gani mamlaka kuu za ulimwengu zinafanya matayarisho ya kuogofya ya vita ya atomiki? Kwa sababu gani kuna shida ya fedha? Kwa sababu gani migogoro inaendelea kati ya wafanya kazi na matajiri wao, hata kati ya wafanya kazi wa serikali na serikali yenyewe? Kwa sababu gani kuna utukuzo mwingi mno wa kitaifa? Kwa sababu gani kuna ugomvi mwingi wa kikabila na chuki isiyo na sababu nzuri? Kwa sababu gani uvunjaji wa sheria unaongezeka? Kwa sababu gani adili zinaharibika? Kwa sababu gani magonjwa ya kaswende na kisonono yanaongezeka sana? Kwa sababu gani makao ya kidunia ya mwanadamu yanaharibiwa na uchafu? Kwa sababu gani chakula cha idadi ya watu inayoongezeka ya dunia kinazidi kupungua? Kwa sababu gani mambo yako kama vile Yesu Kristo alivyotabiri kwa wakati wetu, “katika nchi dhiki ya mataifa wakishangaa kwa uvumi wa bahari na msukosuko wake; watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu. Kwa kuwa nguvu za mbinguni zitatikisika”? (Luka 21:25, 26) Kwa kila tokeo pana chanzo. Ni nini chanzo cha matokeo haya yote yenye kutaabisha?
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 462]
Je! Kristendomu ataushiriki ushindi wa kimungu? Anajitia katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu. Biblia yasema: “Kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu”
[Picha]
Papa Paulo wa Sita akihutubu mbele ya Kusanyiko Kuu la Umoja wa Mataifa, Oktoba 4, 1965
[Picha]
Maandishi penye Kibanda cha Vatican, Maonyesho ya Ulimwengu ya New York, 1964-1965
(Ulimwengu na ujue hivi: Kanisa linaufikiria ulimwengu kwa akili nyingi, kwa kuusifu kwa moyo mweupe na kwa kusudi la unyofu si la kuushinda bali la kuutumikia, si la kuudharau bali la kuuthamini, si la kuulaani bali la kuutia nguvu na kuuokoa.
Papa Paulo wa Sita)