Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 11/1 kur. 503-504
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Habari Zinazolingana
  • Wafundishe Watoto Wako Kumpenda Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Je! Wewe Unafundisha Watoto Wako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 11/1 kur. 503-504

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

● Kijana akikatazwa na baba yake (au mama yake) asijifunze Biblia au asishirikiane na mashahidi wa Yehova wa Kikristo, je! ana wajibu wa kutii katika mambo haya?​—U.S.A.

Biblia inaamuru watoto: “Watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki.” (Efe. 6:1) “Watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Kol. 3:20) Kama mawakili imara wa Biblia, mashahidi wa Yehova wanawasihi vijana sikuzote walifuate shauri hilo la kimungu. Lakini, uhakika wa kwamba Bwana Yesu Kristo anatiwa katika shauri hili waonyesha kwamba utii kwa wazazi si ule upitao kadiri. Uwezo wa Yesu Kristo ni mkubwa zaidi sana kuliko ule wa baba ye yote wa kidunia. Yesu alikuwa amekwisha pewa “mamlaka yote mbinguni na duniani,” naye ndiye “kichwa cha kila mwanamume.”​—Mt. 28:18; 1 Kor. 11:3.

Kwa hiyo, wakati wo wote baba atakapo kwamba watoto wake wakose kuitii sheria ya Mungu, yeye anapita mpaka wa uwezo wake. Kwa hiyo, nyakati hizo itawapasa watoto kuamua watakalofanya. Kwa mfano, namna gani kama baba akimwamuru mwana wake akaibe, aseme uongo, adanganye au ajitie katika matendo mengine ya kuasi sheria? Huenda mwana anajua Mungu anakataza mambo haya. Kwa hiyo, mwana aweza kuchagua aitii sheria kuu ya Mungu na ya Kristo asimfuate baba yake.

Hata sheria ya nchi yaweka wajibu fulani juu ya watoto kwa habari hii. Huenda ikapasisha mtoto juu ya kutenda uhalifu akiamriwa na baba yake. Chasema hivi American Jurisprudence: “Mtoto anayetenda kwa kuamriwa na baba yake huenda akasamehewa uhalifu alioufanya, katika kisa cha pekee, ijapokuwa amri ya baba haikisamehei kitoto kichanga sikuzote kinapotenda uhalifu. Mtoto atendapo jambo la kuvunja sheria mbele ya baba yake, kwa kuamriwa naye, na kwa sababu ya nia ya uhalifu ya baba, lazima itaelekea kuwa mtoto alikuwa hana umri wa kutosha au akili haikuwa imekomaa naye akawa yu chini kabisa ya utawala, amri, na uongozi wa baba, mbele ya uhalifu kuwa ule wa baba, na si wa mtoto.”

Vivyo hivyo, sheria ya Mungu haisamehei watoto kwa matendo ya uasi ati kwa sababu wao ni watoto. Kwa mfano, wakati vijana wadogo wa kiume walipomdharau sana nabii Elisha, Yehova Mungu hakuwaachilia wasipate adhabu, ijapokuwa huenda ikawa nia ya wazazi wao juu ya Elisha ndiyo iliyowavuta kufanya hivyo. (2 Fal. 2:23, 24) Hii yaonyesha kwamba Yehova Mungu anapasisha watoto juu ya kuvunja amri zake kwa makusudi.

Bila shaka, watoto wachanga sana hawayajui wala hawayafahamu matakwa yote ya Mungu. Kwa hiyo, hata ikiwa ni mzazi mmoja tu aliye mtumishi wa kweli wa Mungu, kwa rehema watoto wachanga wanaonwa kama watakatifu au safi kulingana na maoni ya Mungu. (1 Kor. 7:14) Bila shaka, mzazi aaminiye analo daraka la kuwafundisha watoto mapenzi ya kimungu bila ya kujali nia ya mwenzi asiyeamini. (Mit. 6:20) Ndipo, watoto wanapozidi kukua, wanakuja chini ya wajibu mbele za Mungu kutenda kupatana na wayajuayo kuwa haki. Hii inatia na mambo ya ibada ya kweli. Ni mapenzi ya Mungu kwamba watumishi wake waliokubaliwa wajifunze Neno lake, wakusanyike pamoja na waamini wenzao na kutangaza kweli ya Biblia kwa wengine zaidi.​—Mt. 24:14; Yohana 17:3; Ebr. 10:24, 25.

Lakini, kama baba akiukataza utendaji huo wa Kikristo, watoto wanaweza kwa busara na kwa heshima kumweleza hali yao. Maelezo hayo yatakuwa yenye nguvu yakitegemezwa na mwenendo unaostahili kufuatwa. Kwa kweli baba hapaswi kupata lalamiko la haki juu ya watoto wanaojaribu kuyafanya mapenzi ya kimungu. Ikiwa watoto wanaweza kumsaidia afahamu kwamba wao wamepata kuwa wana bora na binti bora tangu walipoanza kujifunza Neno la Mungu, hii yaweza kusaidia sana kuvunja maoni yo yote mabaya yasiyo na msingi mzuri. Yaweza kumsaidia aone kwamba watoto wake wanamletea sifa kweli kweli nao ni tofauti kabisa na hesabu inayoongezeka ya vijana wasio na heshima na waasi katika ulimwengu leo. Akiisha kuwaza mambo hayo huenda asikatae hata kidogo watoto wake wasiendelee kufuata mwendo unaofanya mambo yawe mepesi kwake kama kichwa cha jamaa.

Kuna nyakati ambapo katika jamaa watoto peke yao ndio wanaotaka kujifunza Neno la Mungu. Huenda wakaja kwenye nyumba ya mmojawapo wa mashahidi wa Yehova na kuuliza maulizo ya Biblia au hata kuhudhuria mikutano penye Jumba la Ufalme. Ikiwa wazazi wanaagiza kwamba watoto wao wakomeshe ushirika wo wote na mashahidi wa Yehova, itawalazimu watoto kuamua watakalofanya juu ya msingi wa wanayoyajua kuwa haki. Wazazi wakianza kusimamia kila jambo la utendaji wa watoto wao moja kwa moja na kuwatenga na ushirika wote na mashahidi wa Yehova wa Kikristo, hii haizuii watoto kutokuonyesha tamaa yao kufanya mapenzi ya Mungu kwa kuendelea kuwa wenye mwenendo mwema, wakijifunza Biblia wenyewe na kusali kwamba huenda wakati ukaja watakapokuwa huru zaidi kufuata ibada ya kweli na kuendelea kutafuta ruhusa ya wazazi wao washiriki zaidi katika utendaji wa Kikristo.

Kwa upande mwingine, wajapokuwa wanakataa ombi la mtoto la kuhudhuria mikutano ya Kikristo au kuruhusu mhudumu aje na kujifunza Biblia naye, pengine wazazi hawamsimamii zaidi kupita kadiri. Je! n’nini wajibu wa mashahidi wa Yehova wa Kikristo juu ya mtoto huyo? Kwa kufaa mashahidi wa Yehova wanayaheshimu matakwa ya wazazi juu ya litakalofanywa nyumbani mwao. Lakini hii haimaanishi kwamba mashahidi wa Yehova hawawezi kujibu maulizo ya Biblia waliyoulizwa na watoto wanaowatembelea au wakutanao nao barabarani au penginepo. Mashahidi wa Yehova hawana wajibu wa kuzuia watoto wasiingie katika Majumba yao ya Ufalme ati kwa sababu wazazi huenda wasitake wahudhurie mikutano huko. Biblia yasema hivi: “Na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” (Ufu. 22:17) Ikiwa vijana wamo kati ya wale wanaotamani maji ya uzima, n’nani apaswaye kuwazuia? Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao.”​—Mt. 19:14.

● Ni nini maana ya mfano wa Yesu, katika Mathayo 11:16, 17, juu ya kupiga filimbi na kulia kwa watoto wadogo wanaocheza?​—U.S.A.

Mathayo 11:16, 17 yasema hivi: “Lakini nitakifananisha na nini kizazi hiki? Kimefanana na watoto wanaokaa sokoni, wanaowaita wenzao, wakisema, Tuliwapigia filimbi, wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia.”

Yesu Kristo alikuwa akikilinganisha kizazi hicho na watoto pamoja na michezo yao mbalimbali. Akiitumia maana ya mfano wake, Yesu aliendelea kusema hivi: “Maana Yohana alikuja, hali wala hanywi, wakasema, Yuna pepo. Mwana wa Adamu alikuja, akila na kunywa, wakasema, Mlafi huyu, na mlevi, rafiki yao watoza ushuru na wenye dhambi!”​—Mt. 11:18, 19.

Kwa kweli wananchi wenzi wa Yesu walikuwa wakitenda kama watoto. Maisha ya vivi hivi ya Yohana Mbatizaji kama Mnadhiri hayakuwafaa, kwa maana hawakuombolezea dhambi zao wala kutubu. Nao hawakuwa na hali yenye furaha kama ya Yesu, maana hawakuzifurahia habari njema za ufalme alizozihubiri. Msingi wa hakumu yao haukuwa kanuni za Maandiko, bali maoni ya kipekee waliyokuwa wameyawaza hapo kwanza. Wao wasingeweza hata kidogo kupendezwa na ye yote wa wajumbe wa Mungu, ama Yohana ama Yesu. Wao hawakutaka hawa wawawekee hali ya kufuata kwa kuwaeleza moja kwa moja mapenzi ya Mungu kwao na haja yao ya kujipatanisha nayo. Wao hawakutaka kujipatanisha na mapenzi ya Mungu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki