Ibada ya Kweli Inahitaji Maamuzi Imara
WAKATI Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani alionyesha wazi kwamba kuwa mmojawapo wa wanafunzi wake kulihitaji maamuzi imara yanayohusu mabadiliko katika maisha ya mtu. Alisema hivi: “Kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.” (Luka 14:33) Hii maana yake—si kwamba kila mtu anayejaribu kuwa mwanafunzi wa Yesu amepaswa aharibu mali zake—bali kwamba kila mtu lazima avione vitu vyake vya kimwili kama vyenye maana ndogo, kutokuacha cho chote kimzuie asimtumikie Mungu kama mwanafunzi mwaminifu wa Mwanawe.—Linganisha 1 Timotheo 6:17-19; Waebrania 13:5.
Kila mwaka maelfu na maelfu ya watu wanaonyesha kwamba hivi ndivyo ilivyo kwa upande wao. Wana nia ya kufanya mabadiliko makubwa sana katika njia yao ya maisha, mabadiliko ambayo wengine wanafikiri ni yenye kuwakosesha faida fulani, ya kipumbavu.
Msichana mmoja wa Brazil anaeleza mabadiliko aliyokuwa na nia ya kuyafanya apate kuishi kulingana na maongozi yaliyomo katika Biblia. Akieleza sababu yeye alikubali kwa hiari ajifunze Biblia na mashahidi wa Yehova, anasema hivi:
“Sikuzote nilikuwa nimeifikiria Biblia kama fumbo. Walakini, wakati huo nilikuwa mwenye shughuli nyingi sana nikijitahidi nipate kazi ya michezo ya kuigizwa katika chuo kikuu. Nilipozidi kufanya maendeleo katika funzo langu la Biblia, ndivyo nafasi za kuwa mchezaji zilivyozidi kuwa nyingi. Katika VII National Amateur Theater Festival nilipata zawadi kwa kuwa mchezaji wa pili kwa ubora.
“Kwa sababu ya kuwa na shughuli nyingi niliacha kujifunza Biblia kwa kitambo. Lakini Shahidi aliyekuwa amejifunza nami aliendelea kunitembelea. Alikuwa akinitia moyo niendelee kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano na kusoma Biblia na vitabu vya kusaidia kujifunza Biblia.
“Kidogo kidogo, dhamiri yangu ilianza kunisumbua. Nilianza kujiuliza hivi: ‘Ningeweza kuomba baraka ya Mungu huku nikienda jukwaani kufanya jambo lililopingana na kanuni za Biblia? Je! mwenendo mchafu haukatazwi na Mungu?’
“Nilitatizwa sana akilini, kwa maana nilipenda michezo ya kuigizwa kweli kweli. Niliombwa mara nyingi nifanye kazi ndani na nje pia ya chuo kikuu. Ujapokuwa haukuwa uamuzi mwepesi, mwishowe niliamua kuacha kuigiza michezo nifanye utumishi wa Yehova.
“Sasa ni mwenye furaha sana; dhamiri yangu imetulia. Najisikia salama kati ya ndugu zangu na dada zangu wa kiroho, wote ambao wanatumia nguvu zao na akili kuzidisha faida za ufalme wa Mungu.”
Kwa habari ya msichana huyu ibada ya kweli ilihusu kuacha kazi katika jumba la michezo, lakini ni mwenye furaha zaidi katika kufuatia mradi wa kuwa mwanafunzi mwaminifu wa Yesu Kristo.
Msichana mwingine katika Brazil aliona kwamba kuwa mwanafunzi wa Mwana wa Mungu, ilimpasa abadili mwenendo wake, akichagua ama faida za fedha au utii kwa Mungu.
Wakati alipokuwa akijifunza Biblia na mmoja wa mashahidi wa Yehova, mazungumzo yaliingia ya ubaya wa ngono kati ya watu wasiooana. Alisema kwamba hakuweza hata kidogo kuona ubaya wake. Hata alipoonyeshwa maandiko zaidi juu ya maoni ya Mungu ya adili, hakuyakubali mafundisho ya Biblia.
Shahidi aliyekuwa akijifunza naye alijua kwamba isingefaa kitu kuendelea kulizungumza jambo hili. Kwa hiyo akaeleza kwamba, baadaye, msichana huyo bila shaka angeyathamini maoni ya Maandiko na kumtia moyo asome maandiko mengine mbalimbali ya Biblia juu ya habari hiyo.
Yule msichana aliyasoma maandiko na, juma iliyofuata, akakubali kwamba Mungu hakubali uasherati wala uzinzi. Ndipo alipoungama kuwa anaishi na mwanamume aliyeoa na kuwa ana mimba yake. Mwanamume huyu alikuwa akimpa mahitaji yake yote ya fedha, hata kumpa chumba kizuri kando ya bahari. Alitaka ajue imempasa afanye nini katika habari hii. Shahidi akaeleza Biblia inavyosema na kuonyesha wazi kwamba uamuzi ungekuwa wake.
Shauri la Biblia liliufikia moyo wa msichana huyo. Juma iyo hiyo alikomesha uhusiano wake na mwanamume huyo. Karibuni rafiki zake wakaanza kumlaumu, wakisema kwamba alikuwa mwenye kichaa kumwacha mwanamume aliyekuwa amemruzuku vema kimwili. Jamaa zake pia walimtia moyo aendelee kushirikiana naye, kwa maana mwanamume huyo alikuwa amewasaidia wao pia kwa fedha.
Lakini yeye alishikamana na uamuzi wake. Miezi kadha baadaye akazaa kitoto kivulana ni baada ya hapo akabatizwa akikata kauli kumtumikia Mungu kama mwanafunzi wa Mwanawe. Ijapokuwa sasa inamlazimu kujiruzuku mwenyewe na mtoto, anafurahia kuwa na dhamiri safi mbele za Yehova.
Kwa kweli, ingawa huenda ikawa lazima mabadiliko makubwa sana yafanywe na mtu kuelekea kuhasirika machoni pa ulimwengu, mtu anayeufanya uamuzi wake awe mwanafunzi mwaminifu wa Yesu Kristo anapata yaliyo ya thamani zaidi. Anapata dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu na kuona uradhi wa kweli katika kufanya mapenzi ya Mungu.