Kukimbilia Kimbilio la Kweli la Ufalme
1. (a) Ubaya wa tengenezo lililofananishwa na “mti” wa punje ya haradali ya mfano wa Yesu umeonyeshwaje? (b) Ni kwa njia gani watu walio wengi katika Jumuiya ya Wakristo wamekuwa kama inavyosimuliwa katika Isaya 6:8-10?
TENGENEZO linalofananishwa na “mti” uliokua kutokana na punje ya haradali katika mfano wa Yesu limefunuliwa wazi kuwa baya na mashahidi wa Yehova wa Kikristo kwa kuhubiri ulimwenguni pote. (Mt. 13:31, 32) Ni Wakristo wachache wa kujidai ambao wamelikimbia tengenezo hilo la kidini, yaani, Jumuiya ya Wakristo, wakapata kimbilio chini ya ufalme wa Mungu wa Kimasihi unaotangazwa na mashahidi wa Yehova wa Kikristo. Kama nabii Isaya wa karne ya nane K. W. K., mashahidi hawa wamekwenda na wangali wakienda-enda kwa watu wa Jumuiya ya Wakristo, lakini wengi sana wa waliomo katika Jumuiya ya Wakristo wanajionyesha kuwamo katika hali gani ya kiroho? Ni kama nabii Isaya alivyosema mapema kwa unabii, yaani, wamefumba kabisa macho yao, masikio yao hayasikilizi na mioyo yao ya kuthamini haiuitikii ujumbe wa Ufalme.—Isa. 6:8-10.
2. Ni hata lini watu hao wagonjwa kiroho watakaa ndani ya Jumuiya ya Wakristo?
2 Hata lini watu hao watakaa katika hali hiyo ya ugonjwa wa kiroho, wakiwa ndani ya Jumuiya ya Wakristo? Kwa unabii Yehova alilijibu ulizo hilo kwa maneno yaliyoandikwa katika Isaya 6:11-13. Watakaa humo mpaka Jumuiya ya Wakristo, “mti” wa mfano wa punje ya haradali, ufutiliwe mbali katika “dhiki kubwa” inayokuja. (Mt. 24:21, 22) Tazama makala “Wewe Umesema: ‘Mimi Hapa, Nitume Mimi’?” katika toleo la Watchtower la Desemba 15, 1966.
3. Kwa sababu gani watu wenye kumcha Mungu wamekimbilia chini ya ufalme uliosimamishwa wa Mungu wa Kimasihi, Naye amewaingiza wapi?
3 Watu hao wenye kumcha Mungu ambao wameikimbia Jumuiya ya Wakristo iliyohukumiwa maangamizi wameyachunguza mambo na matukio ya ulimwengu tangu mwaka wa 1914 kulingana na unabii mbalimbali wa Biblia. Kwa kulinganisha hivyo wamefahamu kwamba ufalme wa Mungu wa Kimasihi uliomo mikononi mwa Yesu Kristo ulizaliwa mbinguni mwaka huo wenye kujawa na vita. Wao hawakukimbilia Ushirika wa Mataifa kama “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani,” wala Umoja wa Mataifa wa kisasa kama “tumaini la mwisho” la mwanadamu. Kwa kukataa maoni hayo yanayotajwa mapadre wa Jumuiya ya Wakristo, watu hao wenye kufungua macho, wenye masikio yenye kusikiliza, wenye moyo yenye kuitikia wamekimbilia Mungu uliosimamishwa, twaweza kusema, wamekimbilia “milimani” kusiko na hatari kabla ya “dhiki kubwa” kutokea. (Mt. 24:16-22) Hivyo wameingia katika “paradiso” ya kiroho, ambayo Yehova Mungu ameanzishia watu wake waliorudushiwa katika hali inayofaa tangu 1919, kutimiza unabii wa Biblia wa kurudishwa kwao.—Isa. 35:1-10; 65:17-25.
4, 5. (a) Amani na usalama wa wale wanaoingizwa katika paradiso kiroho inasimuliwaje katika Isaya 32:1, 2, 17, 18? (b) Kwa utimizo wa unabii huu, “wakuu” wanaotajwa ni akina nani, nao wanasaidiaje kuongeza hali za utulivu za paradiso hiyo?
4 Amani na usalama walio nao sasa chini ya Ufalme wa Kimasihi inasimuliwa kwa njia ya kupendeza katika Isaya 32:1, 2, 17, 18, kwa maneno haya: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu. Na [wakuu watakuwa] kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu. Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na tumaini daima. Na watu wangu watakao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.”
5 Wale walioko duniani wanaolingana na “wakuu” wanaosimuliwa hapa sio “wakuu wa Kanisa” katika Jumuiya ya Wakristo hata kidogo. Wao ni “wazee,” “waangalizi” waliowekwa wa zaidi ya makundi 38,000 ya watu wa Yehova waliorudishwa katika hali inayofaa. Kwa kuwa wao wanapaswa kuonyesha wanavyofanya kazi yao kwa Mfalme wa kimbinguni, Yesu Masihi, kwa hekima wanaendelea kuangalia kundi kama wachungaji “kwa haki.” Kwa njia hiyo wanasaidia kuleta amani, utulivu, kutumainika na usalama wa paradiso ya kiroho ambamo Yehova amewaingiza waabudu wake waliorudishwa kwenye hali inayofaa tangu mwaka wa 1919 W. K.
CHINI YA UTAWALA UNAOKUJA WA MILEANI WA MASIHI
6. Ni kwa njia gani taratibu mpya ya Mungu duniani itakavyoanza ikiwa na paradiso ya kiroho, lakini ni kazi gani ya kidunia itakayokuwa mbele ya wale watakaokuwamo katika paradiso hiyo?
6 Kama vile safina isiyopenywa na maji ilivyochukua Nuhu na jamaa yake na wawili wawili wa wanyama na ndege wa namna zote wakapita gharika ya dunia ya 2370-2369 K. W. K., paradiso ya kiroho inayolindwa na Yehova itaokoka gharika inayokuja ya “dhiki kubwa.” Waabudu waaminifu wa Yehova wanaokaa ndani ya paradiso hiyo ya kiroho wataokoka pamoja nayo wapite hiyo “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Mt. 24:21, 22; Ufu. 7:9-14) Kwa sababu hiyo taratibu mpya ya Mungu yenye haki duniani itakayofuata dhiki hiyo itaanza ikiwa na paradiso ya kiroho ‘ikijawa na kumjua Yehova’ na kukaliwa na waabudu wake waaminifu. (Isa. 11:9) Kutakuwako kazi ya kurembesha dunia halisi iwe kama paradiso, kama Bustani ya Edeni ya dunia nzima, kwa “mkutano mkubwa” wa waokokaji wanaolingana na wana watatu na binti-wakwe za Nuhu. Kwa hiyo dunia itakayokaliwa na watu wakati ujao itakuwa paradiso halisi chini ya utawala wa miaka elfu wa Yesu Kristo na wafalme wenzake 144,000. Yesu Kristo mwenyewe aliitaja paradiso hiyo kwa jina.—Luka 23:43, Swahili Congo Bible.
7, 8. (a) Ni nani waliookoka pamoja na Nuhu na jamaa yake katika safina? (b) Kwa sababu gani jamaa ya Nuhu haikutoka safinani ikiogopa viumbe vya chini vya kidunia?
7 Huko nyuma mwaka wa 2369 K. W. K., baada ya safina ya Nuhu kutua juu ya mlima wa Ararati naye akaruhusiwa kuufungua mlango aliokuwa amefunga Yehova Mungu, Nuhu na jamaa yake walitoka nje. Lakini si wao peke yao, kwa maana Mwanzo 8:19 unatuambia, “kila mnyama, na kila kitambaacho, na kila ndege, kila kinachokwenda juu ya nchi kwa kabila zao, wakatoka katika safina.” Vilipaswa viongezeke duniani sawa na waokokaji wa kibinadamu wa gharika.—Mwa. 1:20-25.
8 Uhusiano wa viumbe hivyo vya chini vya kidunia ungekuwa nini pamoja na mwanadamu? Mungu aliuonyesha uhusiano huo alipokuwa akimbariki Nuhu na jamaa yake, kwa kusema: “Kila mnyama wa katika nchi atawaogopa ninyi na kuwahofu, na kila ndege wa angani; pamoja na vitu vyote vilivyojaa katika ardhi, na samaki wote wa baharini; vimetiwa mikononi mwenu.” (Mwa. 9:1, 2) Kwa hiyo wanadamu hawakutoka katika safina ya wokovu wakihofu cho chote, hata wanyama. Mwanadamu hakuwa na hofu juu ya wanyama ndani ya safina, ambamo hata simba alikula majani, kama ng’ombe.
9. Hiyo inaonyesha Mungu atafanya nini baada ya “dhiki kubwa” ili kutimiza yale ambayo Yeye aliamuru Adamu na Hawa kuhusu viumbe vya chini vya kidunia?
9 Bila shaka huo ulikuwa wonyesho wa vile dunia inayokaliwa na watu itakavyokuwa wakati ujao kwetu wenyewe. Viumbe vya kidunia vya chini vitahifadhiwa pamoja na waabudu wa kibinadamu wa Yehova waliomo katika paradiso yao ya kiroho kwa matumizi ya mwanadamu na kumfurahisha yeye. Bila shaka, baada ya “dhiki kubwa,” Mungu atawaondolea mashaka waabudu wake wenye kuokoka duniani juu ya samaki, viumbe vyenye kuruka na wanyama wa nchi kavu. Muumba Mwenye Nguvu Zote atatia hofu iliyomo ndani ya mwanadamu katika viumbe vyote hivyo vya chini vya kidunia, hata havitamsumbua mwanadamu. Kulingana na vile Mungu alivyoamuru mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, wanadamu watatiisha viumbe hivyo vya chini. Vitakuwa raia watiifu na wasiodhuru mwanadamu.—Mwa. 1:27, 28.
10. Je! viumbe vyote vya chini vya kidunia sasa vimetiishwa kwa mwanadamu, naye Daudi alionyeshaje kwa unabii mtu ambaye vingetiishwa kwake?
10 Zaidi ya miaka mia kumi na tisa iliyofuata Gharika, wakati Mfalme Daudi wa Yerusalemu alipoiandika zaburi ya nane, si viumbe vyote vya kidunia vya chini vilivyokuwa vitiifu kwa mwanadamu kwa habari ya kufugwa naye na kutomdhuru. Lakini katika zaburi hiyo Daudi alionyesha kwa unabii mwanadamu ambaye angetiisha vyote. Katika zaburi hiyo Daudi alisema hivi: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie? Umemfanya mdogo punde kuliko [wenye mfano wa Mungu]; umemvika taji ya utukufu na heshima; umemtawaza juu ya kazi za mikono yako; umevitia vitu vyote chini ya miguu yake. Kondoo, na ng’ombe wote pia; naam, na wanyama wa kondeni; ndege wa angani, na samaki wa baharini; na kila kipitiacho njia za baharini.”—Zab. 8:3-8.
11. Ni wapi na kwa njia gani jina limepewa na mtu ambaye Mungu amekusudia vitu vyote vya kidunia vitiishwe kwake?
11 Sasa, ni nani “mtu” ambaye Yehova Mungu amekusudia vitu vyote vya kidunia vitiishwe kwake? Kitabu kilichoongozwa na Mungu cha Waebrania, sura ya pili, mistari ya tano mpaka tisa, kinatueleza kwa kusema hivi: “Hakuuweka chini ya malaika ulimwengu ule ujao tunaounena, ila mtu mmoja ameshuhudia hivi mahali fulani, akisema, Mwanadamu ni nini hata umkumbuke, ama mwana wa binadamu. hata umwangalie? umemfanya mdogo punde kuliko malaika, umemvika taji ya utukufu na heshima, umemtawaza juu ya kazi za mikono yako; umeweka vitu vyote chini ya nyayo zake. Kwa maana katika kuweka vitu vyote chini yake hakusaza kitu kisichowekwa chini yake. Lakini sasa bado hatujaona vitu vyote kutiwa chini yake. ila twamwona yeye aliyefanwa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu aionje mauti kwa ajili ya mtu.”
12. Katika “ulimwengu ule ujao,” ni viumbe gani vya kidunia vilivyo hai ambavyo pia vitatiishwa chini ya nyayo za Yesu?
12 Hiyo yamaanisha kwamba, baada ya “dhiki kubwa” na kutiwa mnyororo kwa Shetani Ibilisi na mashetani wake na kufungwa kwao katika shimo refu lisilopimika, “ulimwengu ule ujao” utakuwa umetiishwa chini ya nyayo za Yesu Masihi. Vitatiishwa pia vitu vyote vilivyomo katika dunia inayokaliwa na watu, kutia na “kondoo, na ng’ombe wote pia; naam, na wanyama wa kondeni; ndege wa angani, na samaki wa baharini; na kila kipitiacho njia za baharini.” (Zab. 8:7, 8) “Wanyama wa kondeni” wanatia na wanyama-mwitu wote wakali na walio hatari kwa mwanadamu, kama vile simba, dubu, chui, fira na nyoka mwingine ye yote mwenye sumu. “Kila kipitiacho njia za baharini” kitatia na samaki wenye kula watu na wanyama, papa na nyangumi wauaji.
13. Yesu Kristo ambaye sasa ametukuzwa mbinguni ataonyeshaje kwamba viumbe vyote hivi vya chini vya kidunia vimetiishwa kwake katika “ulimwengu ule Ujao”?
13 Yesu Masihi, ambaye sasa amevikwa utukufu na heshima mbinguni, hajaishiwa na uwezo wake juu ya wanyama-mwitu wasiofugika. (Marko 1:13; 11:2-7) Ataonyesha kwamba viumbe hivyo vilivyo hatari sasa vimetiishwa chini yake. Namna gani? Kwa kuvitiisha kwa “mkutano mkubwa” wa warithi wa paradiso ya wakati ujao ya kidunia watakaoiokoka “dhiki kubwa” waingie katika taratibu mpya ya Mungu ya dunia yetu. Hivyo, wanyama-mwitu wakali na walio hatari leo watafanywa kuwa wasiodhuru waabudu wa kidunia wa Yehova Mungu. Uhusiano usio wa madhara kati ya mnyama-mwitu na mwanadamu utakaokuwako wakati huo utalingana na masimulizi ya Isaya 11:6-9, ambayo imekwisha timia katika paradiso ya kiroho inayofurahiwa sasa na mashahidi wa Yehova wa Kikristo.
14. Kwa sababu gani wafu wa kibinadamu waliokombolewa hawatakuwa na cha kuogopa watakapotokea katika “ulimwengu ule ujao”?
14 Hivyo kusudi la kwanza la Mungu Muumba kutiisha wanyama wote duniani kwa mwanamume na mwanamke wakamilifu katika Bustani ya Edeni ya dunia nzima litatimia. Paradiso ya duniani pote itakuwa mahali pa amani na usalama. Wafu wote waliokombolewa wa kibinadamu watakaotolewa katika makaburi yao na kukaa katika “ulimwengu ule ujao” hawatakuwa na cha kuogopa. (Matendo 24:15; Yohana 5:28, 29; Ufu. 20:11-14) “Simba angurumaye,” Shetani Ibilisi, na mashetani wake hawatakuwa katika ujirani. “Mwana wa Adamu” aliyetukuzwa mbinguni atafikiliza amani duniani pote kati ya mwanadamu na mwanadamu na kati ya mwanadamu na mnyama na kati ya mnyama na mnyama. ‘Watu wakaao duniani watajifunza haki,’ nayo haki hiyo itasaidia kuleta amani, utulivu, matumaini ya kweli na usalama duniani mwote. (Isa. 26:9; 32:17, 18) Lo! dunia itakuwa mahali pazuri namna gani pa kukaliwa na mwanadamu milele pakiwa makao yake ya paradiso! Yote hayo yatakuwa kwa sababu “ulimwengu ule ujao” utakuwa chini ya “ufalme wa mbinguni” wa kweli.—Mt. 4:17; 5:3, 10.
15. Sasa tuna pendeleo na nafasi ya kufanya nini juu ya watu waliomo hatarini kwa sababu ya “dhiki kubwa” inayokaribia sana?
15 Huo ndio “ufalme wa mbinguni” ambao sasa ndilo pendeleo na nafasi yetu kuutangaza ulimwenguni pote. Sisi ambao tayari tumekimbilia chini yake tunahangaikia usalama wa wengine katika wakati huu wa taabu ya ulimwengu isiyolinganika. Dhiki ya dhiki zote inakaribia sana. Kwa hiyo, acheni tuendelee kuelekeza watu wote wenye kufundishika kwenye “ufalme wa mbinguni” wa kweli wa Kimasihi na kuwasaidia wapate kimbilio salama chini yake. Wokovu wao kutoka taabu iliyo kubwa zaidi ya ulimwengu unategemea kufanya hivyo!
—Kutoka The Watchtower, Oct. 1, 1975.