Baraka za Kutolipa Kisasi
● Biblia inatuambia hivi juu ya Yesu: “Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya.” (1 Pet. 2:23) Wale ambao wanamwiga Yesu kwa kutolipa kisasi wamepata baraka nyingi.
Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya kijana mmoja mwanamke katika Nigeria aliyehubiri mara ya kwanza hadharani akiwa pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ingawa alielezwa kwamba mwenye nyumba mmoja alikuwa mpinzani mkali, bado alitaka kuongea naye. Ikawaje?
Mwenye nyumba alishika kibaba cha mafuta ya mitende akammwagia kijana huyo mwanamke. Yalimmwagikia usoni, mavazini na katika mkoba wake. Yeye alianza kujipangusa usoni bila kusema lo lote. Dakika chache zilipita. Mtu huyo alipoona hali ya kutaka amani ya kijana huyo, aliaibika kidogo. Akamwambia amweleze sababu ya kumtembelea nyumbani kwake. Wakati huu alisikiliza.
Muda mfupi baadaye alianza kufunzwa Biblia. Leo yeye pia anashiriki katika kazi ya kuhubiri hadharani akiwa shahidi wa Yehova aliyebatizwa.
Katika nchi iyo hiyo, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alikuwa akitolea watu vitabu vya habari za Biblia, halafu akafikiwa na mtu aliyedai kuwa “nabii Mkristo.” Mtu huyo alimnyang’anya vitabu, akavirarua-rarua. Shahidi alinyamaza tu akainama na kuviokota vipande vilivyoraruliwa na kuviingiza katika mkoba wake. Ndipo mtu mmoja aliyeona mambo hayo alipomwendea Shahidi, akasema: “Nilikuwa barabarani nikitazama ulilotendwa na nabii wetu, lakini wewe hukumtukana hata kidogo.” Baada ya kumsifu Shahidi, mtu huyo aliendelea kusema: “Kuanzia leo mimi niko tayari kuwa mmoja wenu.” Alitimiza ahadi yake, na leo yeye anaeleza jirani zake kweli ya Biblia.
Kwa kweli, kuiga mfano wa Yesu wa kutolipa kisasi kunasaidia watu wanyofu.