Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
Jihadhari Usipotolewe
KILA mtu, hata mtu mwenye hekima, anaweza kupotoka. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Kweli jeuri humpumbaza mwenye hekima, na rushwa huuharibu ufahamu.”—Mhu. 7:7.
Hata mtu mwenye hekima anaweza kufanya mambo haraka haraka, bila kufikiri, akitendwa jeuri muda mrefu. Huenda akakosa kujiweza na kujiacha avurugike akili kwa kutolea watu maneno ya ukali, au huenda akajaribu kujiondolea tatizo lake kwa kutumia njia haramu.
Kwa upande mwingine, labda andiko hilo linaeleza jeuri ambayo mwenye hekima mwenyewe anafanya. Mtu akijiacha atawalwe na roho ya jeuri, hata awe mwenye hekima namna gani, anafanya mambo bila kufuata adabu na huruma ya kibinadamu. Hajali maoni ya watu, tena anafunga macho na kujifanya haoni shida zao. Anajifikiria yeye mwenyewe na cheo chake tu. Anajidhani kuwa mfadhili mkuu na kwa hiyo anadhani ana haki ya kumnyamazisha mtu ye yote ajaribuye kumlaumu kwa sababu ya matendo yake.—Linganisha 2 Mambo ya Nyakati 16:10.
Rushwa (hongo) inaweza kupotoa mtu sawa na jeuri, ‘kumharibia ufahamu’ wa kufanya mambo mema. Huenda watu maskini wanaoumia kwa sababu ya ubaguzi na upendeleo wakatendwa mambo ya ukatili na wenye kukubali rushwa.
Jinsi ya Kuvumilia Udhalimu na Jeuri (Uonezi)
Mtu anaweza kufanya nini akitendwa udhalimu? Maneno yanayofuata ya Sulemani yanatusaidia: “Heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake, na mvumilivu rohoni kuliko mwenye roho ya kiburi. Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.”—Mhu. 7:8, 9.
Ni hekima kusubiri, kuwa na hakika kwamba mwishowe mambo yatabadilika yawafae sana watumishi wa Mungu. Naam, huenda mwisho wa jambo ukawa mzuri sana ukilinganishwa na mwanzo wake uliokuwa na masikitisho. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya Waisraeli waliotumikishwa Misri. Wakati Musa alipomwomba Farao mara ya kwanza awafungue Waisraeli, Farao aliendelea sana kuwaonea. (Kut. 5:1-9) Lakini, mwishowe, Yehova Mungu alijifanyia jina kuu kwa kuwafungua watu wake wenye kutumikishwa.—Kut. 12:31, 32.
Mwenye subira haelekei kutumia nguvu atengeneze mambo huku akijiumiza mwenyewe au wengine. Lakini mwenye kiburi anaona ni vigumu kuendelea kujiweza, kwa hiyo anakuwa na maelekeo ya kufanya haraka haraka, kisha anajiumiza mwenyewe. Mtu asiye na subira, ambaye haoni mambo aliyotazamia yakitimia upesi, anakasirika haraka. Anakuwa mwepesi wa kuudhika au kuweka kinyongo kingi moyoni. Anakiweka kinyongo hicho kama kwamba anakitunza vizuri kifuani pake mwenyewe. Sulemani anasema mtu huyo ni ‘mpumbavu’ anapofanya hivyo, kwa maana mwendo wake unamfanya aseme na kufanya mambo haraka haraka, bila kufikiri.
Kuwa na maoni ya kiasi juu ya nyakati zilizopita kunatusaidia sana pia kuvumilia hali za leo zisizopendeza. Sulemani alitushauri hivi: “Usiseme, Kwani siku za kale kupita siku hizi? Maana si kwa hekima uulizavyo neno hilo.”—Mhu. 7:10.
Mtu anayetamani mambo yawe mazuri kama zamani anasahau kwamba hata siku hizo zilikuwa zimejawa na matatizo na taabu za namna nyingine. Maisha hayawezi kamwe kuwa makamilifu katika taratibu hii. Huenda mambo fulani yakawa yalikuwa mazuri zaidi zamani, lakini mengine hayakuwa. Huenda tukakosa sana kiasi tukitamani mambo ya zamani. Ingawaje, hakuna mtu anayeweza kuyarudisha. Kwa hiyo ni upumbavu sana kuacha kutosheka tukidhani kwamba kuna wakati fulani katika ulimwengu huu uliokuwa bora katika mambo yote. Kuwaza hivyo hakutusaidii kuvumilia hali ya kibinadamu isiyobadilika, yenye kututatiza.