Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
Hata Upumbavu Mdogo Tu Unaweza Kuleta Madhara
Tendo moja tu la upumbavu linaweza kuharibu sifa ya mtu. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Mainzi mafu huvundisha marhamu ya mwuza marashi; kadhalika upumbavu haba ni mzito kuliko hekima na heshima.” (Mhu. 10:1) Jina au sifa nzuri inalinganika na mafuta yenye harufu nzuri (marashi) yanayoweza kuharibiwa kwa wepesi na kitu kidogo tu kama mainzi wafu. Harufu mbaya ya wadudu hao itafanya mafuta yavunde na kuchacha. Vivyo hivyo, huenda mtu akapoteza sifa njema ya kuwa mwenye hekima na mheshimiwa kwa sababu ya tendo fulani la upumbavu, “upumbavu haba.”
Hiyo ni kwa sababu watu wanatazamia kuona mambo mazuri zaidi katika mtu anayejulikana sana kuwa mwenye hekima. Basi, lazima aangalie sana usemi na matendo yake. Sifa yake njema inaweza kuharibiwa na mambo kama vile kutoa hasira ya ghafula mara moja tu, au kutenda kosa moja baya kwa sababu ya kutumia vileo au tendo moja chafu pamoja na mwanamke au mwanamume.
Mahali Ambapo Moyo Unapasa Kuwa
Ili kuepuka mambo ya upumbavu, mtu anahitajiwa awe na moyo wenye makusudi mema. Mwenye hekima alisema hivi: “Moyo wake mwenye hekima upo upande wa kuume; bali moyo wake mpumbavu upo mkono wa kushoto. Naam, huyo mpumbavu tena, aendapo njiani, hupungukiwa na fahamu zake; hata humwambia kila mtu ya kuwa yeye ni mpumbavu.”—Mhu.10:2, 3.
Mara nyingi Biblia inatumia “upande wa kuume” kufananisha cheo chenye upendeleo. (Linganisha Mathayo 25:33.) Basi, moyo wa mwenye hekima ukiwa upande wake wa kuume, hiyo ingeonyesha kwamba unamwelekeza kwenye njia nzuri, yenye upendeleo. Lakini, mpumbavu anaelekezwa kwenye njia mbaya, maana moyo wake unakuwa “mkono wa kushoto.” Yeye yuko kama mtu mwenye kutumia mkono wa kuume tu, asiyeweza kufanya kazi yo yote kwa mkono wake wa kushoto ikiwa mkono wake wa kuume umekuwa hauwezi. Mpumbavu anajulikana upesi kwa sababu “moyo” wake hauko upande wa kuume, hana kusudi jema. Ni kama kwamba ‘anamwambia kila mtu ya kuwa yeye ni mpumbavu.’ Kwa sababu hataki kuonyeshwa makosa wala kushauriwa, mtu wa namna hiyo anafanya haraka pia kuwaita wale wanaojaribu kumsaidia ‘wapumbavu.’
Kosa Kubwa
Wakati mtawala anapofanya kosa kubwa kwa kuchagua watu wasiofaa wawe na cheo kikubwa, kunakuwa na madhara mengi. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema kwamba kosa la namna hiyo ni baa (msiba). Aliandika hivi: “Liko baa nililoliona chini ya jua, nalo ni kama kosa litokalo kwake yeye atawalaye; ya kuwa upumbavu huwekwa mahali pa juu sana, nao wakwasi [ “matajiri,” ZSB] hukaa mahali pa chini. Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu juu ya nchi kama watumwa.—Mhu. 10:5-7.
Sulemani anasema kwamba wale wanaostahili kuwa na cheo kikubwa ndio “matajiri.” Tusidhani kwamba yeye alipendelea utawala wa matajiri peke yao. Bila shaka Sulemani alikuwa akiwataja watu wanaotumia uamuzi mzuri na kusimamia mambo yao vizuri. Hakika watu wa namna hiyo wanaonyesha wana uwezo mwingi zaidi wa kusimamia mambo kuliko wale ambao wameponda mali zao au wakazitumia vibaya.
Kwa sababu ya mwenye mamlaka kufanya uamuzi mbaya, huenda watu bora au wenye fahari wakakosa kupewa heshima wanayoistahili, na huenda wakatendwa kama watumwa. Lakini, huenda watu wasiostahili sana, watumishi wa vivi hivi tu, wakawekwa wapande farasi kama wakuu. Hali hiyo inaletea raia magumu kwa kulazimishwa wanyenyekee wakuu ambao kwa kweli hawastahili kuwa katika vyeo walivyopewa. Hakika maneno ya Sulemani yanaonyesha ubora wa kuchagua watu wanaostahili wafanye kazi iliyo ya maana sana.
Watu Wasio na Ujuzi Wanaopata Cheo Wasionewe Kijicho
Hapo kwanza huenda ikakosa kuonekana kwamba mtu hawezi jambo. Watu fulani wanajua kujifanya waonekane na wengine kama kwamba wana busara nyingi. Huenda wakachaguliwa watimize madaraka fulani, na huku watu walio na hekima ya kweli wakisahauliwa. Wakati watu wasiostahili wanapokuwa katika cheo chenye madaraka, huenda wengine wakawa na maelekeo ya kuwaonea kijicho (wivu). Lakini, watu wasioweza kazi hawafai kuonewa kijicho. Nyakati zote wao wanakuwa katika hatari ya kuweza kuondolewa katika cheo walichopata. Kwa sababu ya kutokuwa na hekima inayohitajiwa, baadaye huenda wakaonekana jinsi walivyo hasa na kuondolewa katika vyeo vyao, na hapo waumie na kuona aibu.
Bila shaka wakati Sulemani alipotaja mambo mengine yenye hatari alikuwa akionyesha kwamba kutoweza kazi kunaweza kuwa hatari. Aliandika hivi: “Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake [kwa sababu shimo lililo wazi linakuwa hatari nyakati zote]; na yeye abomoaye boma, nyoka [anayekaa katika kuta za zamani] atamwuma. Mwenye kuchonga mawe ataumizwa kwayo; naye apasuaye miti huona hatari katika hiyo.” (Mhu. 10:8, 9) Kazi za kuchonga mawe na kupasua miti zinaweza kuwa hatari kwa uhai wa mtu na viungo vyake vya mwili, kwa hiyo yampasa azifanye kwa uangalifu.
Kwa uhakika, mtu anayeweza mambo yu afadhali kuliko mwingine aliye na uwezo bila hekima ya kuutumia vizuri. Akitoa mfano wa jambo hilo, Sulemani anasema hivi: “Iwapo chuma hakipati, wala mtu hakinoi; ndipo hana budi kutumia nguvu zaidi.” Ungekuwa upumbavu kukata vitu kwa shoka butu, huku ukijikakamua kwa nguvu na bado usiweze kufanya kazi nzuri. Basi, Mfalme Sulemani anaendelea kusema kwamba “yafaa kutumia hekima, na kufanikiwa.” (Mhu. 10:10) Naam, jambo la maana ni kutumia hekima. Huenda mtu akawa ana maarifa. Lakini maarifa hayo yangekuwa na faida gani ikiwa hajui kuyatumia? Sulemani anasema hivi: “Nyoka akiuma asijatumbuizwa, basi hakuna faida ya mtumbuizi.” (Mhu. 10:11) Uwezo wa kutumbuiza nyoka ni wa bure ikiwa mtumbuizi anaumwa kabla ya kumtumbuiza nyoka. Septuagint Version inasema: “Nyoka akiuma anapoendelea kutumbuizwa, hakuna faida kwa yeye anayetumbuiza.” Kwa hiyo lazima usemi wa mtu uwe na matokeo mazuri.
Basi, badala ya kuonea kijicho watu wasioweza mambo wanaopata vyeo vyenye mamlaka, inampasa mtu afahamu kwamba wengine wamo katika hatari ya kuweza kupoteza vyeo vyao, kisha yeye mwenyewe atumie kwa hekima maarifa na uwezo mbalimbali alio nao. Hata ikiwa hapo kwanza uamuzi wake mzuri hauonekani, mwishowe mwenye hekima anakuwa afadhali kuliko mtu asiyeweza mambo aliyetukuzwa.