Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
Tumia Nafasi Iliyopo
Nyakati nyingine kunakuwa na nafasi nzuri sana za kufanya mema au za kujipatia kitu fulani chenye kufaa. Lakini, kwa sababu ya kutotegemeka kwa hali katika hii taratibu iliyopo, kadiri fulani ya imani inahitajiwa katika kutumia hali fulani kwa faida inayofaa. Walakini, tukiwa na mashaka katika hali kama hiyo, huenda tukapoteza kitu chenye kufaa sana. Huenda tukakosa kuwa kitia-moyo kwa wengine.
Mfalme mwenye hekima Sulemani alitoa shauri lenye kufaa sana kuhusu jambo hili. Aliandika hivi: “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi. Uwagawie sehemu watu saba, hata wanane; maana hujui [ni msiba] gani [utakaokuwa] juu ya nchi.” (Mhu. 11:1, 2) Kwa kawaida maneno haya yameonwa kuwa yakitia watu moyo wawe wakarimu.
Mtu hajui hata kidogo jambo ambalo huenda likatokezwa na matendo yake ya ukarimu. Huenda ikaonekana kwake kama kwamba anatupa kitu usoni pa “maji,” pasipo kuonekana matokeo yo yote mara hiyo. Hata hivyo, matendo yake ya ukarimu huenda yakamfanya apendwe na wengine, yakiwafanya wamwonyeshe ukarimu akiwa na uhitaji wa kweli. Sio kwamba mtu aliye mkarimu kweli kweli anapaswa kuwa akitazamia kulipwa. Mahali pake, yeye anafurahia kuwapa wengine akiwa na hakika kwamba sikuzote yeye atapata kile anachohitaji. Kwa hiyo, yeye hawapi wachache tu anaowachagua, wawili au watatu tu, bali yeye huwa mkarimu kwa moyo wote, akiwapa watu “saba, hata wanane.” Watu wengine waangalifu huenda wakafikiri kwamba hili ni jambo lisilo la hekima kabisa, wakiogopa kwamba mtu anaweza kupatwa na hali ya uhitaji ikiwa kungetokea msiba. Walakini, inaelekea sana sana kwamba mtu mkarimu ndiye anayeweza kusaidiwa ikiwa angepatwa na msiba. Yesu Kristo alionyesha wazo linalolingana na hilo aliposema: “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu.”—Luka 6:38.
Matendo ya mtu ya ukarimu hata yanaweza kulinganishwa na mchele unaopandwa katika udongo unaofunikwa na maji. Baada ya “siku nyingi” kile kilichopandwa namna hiyo kinaiva na kutoa mazao mengi.
Baada ya hapo, Sulemani anazungumza juu ya sheria fulani zilizowekwa akionyesha kwamba kutokuwa na uthabiti katika mambo ya maisha sio mwendo unaofaa. Anasema hivi: “Mawingu yakiwa yamejaa mvua, yataimimina juu ya nchi; na mti ukianguka kuelekea kusini, au kaskazini, paangukapo ule mti, papo hapo utalala.” (Mhu. 11:3) Mambo haya yanatendeka tu; hayawezi kuzuiwa na mwanadamu. Kwa hiyo, sababu gani usite-site kuwa mkarimu au juu ya kutimiza jambo linalohitaji kutimizwa. Ikiwa kutanyesha mvua, kutanyesha. Ikiwa mti utaanguka kuelekea upande fulani, papo hapo ndipo utakapoanguka. Na ndivyo ilivyo kwa habari ya mambo mengine mengi ya maisha. Kutotenda peke yake hakutahakikisha kwamba hayatatukia.
Ikiwa mtu angejaribu kusawazisha maisha yake kwa kujaribu kujua mapema yale ambayo huenda yakatokea au yasitokee, hangetimiza jambo lo lote. Kama alivyosema Sulemani: “Mwenye kuangalia upepo hatapanda [akiogopa kwamba mbegu zitapeperushwa na upepo]; naye ayatazamaye mawingu hatavuna. [akiogopa kwamba akikata nafaka italoweshwa na mvua kabla hajaiweka ghalani.]”—Mhu. 11:4.
Kwa hiyo, inatupasa sisi tuendelee kufanya linalohitaji kufanywa, tukijua kwamba mambo yasiyotazamiwa hayana budi kutukia. Hatuwezi kufahamu kabisa kazi ya Mungu, yaani, kufumbua kanuni fulani ambayo katika hiyo tunaweza kujua barabara yale ambayo huenda akafanya au akaruhusu ili kutimiza kusudi lake halafu tufanye mambo yetu kulingana na kanuni hiyo. Sulemani alionyesha kwamba kazi ya Mungu huwa isiyofahamika na wanadamu sawa na kukua kwa mtoto tumboni. Aliandika hivi: “Kama vile wewe [usivyojua] njia ya [roho] ni ipi, wala jinsi mifupa ikuavyo tumboni mwake mjamzito; kadhalika huijui kazi ya Mungu, afanyaye mambo yote.”—Mhu. 11:5.
Kwa sababu ya mambo yasiyotazamiwa yanayotukia maishani pamoja na kutoweza kwa wanadamu kugeuza sheria fulani zilizowekwa, Sulemani anatoa shauri hili: “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa, kama ni hii, au kama zote zitafaa sawasawa.” (Mhu. 11:6) Kwa hiyo, mwendo unaofaa ni kuendelea kufanya kazi zetu kwa bidii, bila kujiachilia tuhangaishwe na mambo ambayo huenda yakatukia bila kutazamiwa kiasi cha kutufanya tushindwe kutimiza kazi zetu, ziwe ni zile za kiroho, za kimwili au matendo yetu ya ukarimu.
Hii inaweza kusaidia mtu awe na maoni yenye furaha juu ya maisha. Sulemani aliandika hivi: “Kweli nuru ni tamu, tena ni jambo la kupendeza macho kutazama jua. Naam, mtu akiishi miaka mingi, na aifurahie yote.” (Mhu. 11:7, 8) Kwa kuwa walio hai peke yao ndio wanaoweza kuthamini nuru na jua, hapa Sulemani anaonyesha kwamba ni jambo jema kuwa hai na kwamba mtu anapaswa kufurahia maisha. Walakini, yeye anatoa wazo hili lenye busara: “Na azikumbuke siku zijazo za giza, kwa maana zitakuwa nyingi. Mambo yote yajayo ni ubatili.” (Mhu. 11:8) Mtu hapaswi kusahau kwamba huenda akapoteza nguvu zake wakati wa “siku zijazo za giza,” au anapokuwa mzee. Akiwa mdhaifu kwa sababu ya uzee, huenda akaona kwamba, namna maisha yanavyoendelea, mwaka baada ya mwaka kila siku ni ubatili, ikionekana kuwa tupu na isiyo na maana. Kwa hiyo, anapaswa kujitahidi kufurahia maisha katika njia inayofaa, wakati anapoweza kufanya hivyo, akitumia uamuzi mzuri na kutafuta uongozi wa Mungu katika yote anayofanya.