Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 11/1 kur. 22-24
  • Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Habari Zinazolingana
  • Maoni Yako Juu ya Ngono—Yanafanyiza Tofauti Gani?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Heshimuni Ndoa ya Kimungu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Maswali kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 11/1 kur. 22-24

Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

● Je! Biblia inatoa maelezo yo yote yaliyo waziwazi juu ya ngono za kati ya mume na mke ambazo ni safi na zisizo safi? Je! wazee wa kundi wana daraka la kujaribu kuongoza namna washiriki wa kundi wanavyopaswa kufanya ngono?

Ni lazima ikubaliwe kwamba Biblia haitoi kanuni zo zote zilizo wazi au kadiri mume na mke wanavyopaswa kufanya ngono. Kuna maelezo mafupi ya kuonyeshana mapenzi yanayofaa, kama vile katika Mithali 5:15-20 na mistari mbalimbali katika Wimbo Ulio Bora (1:13; 2:6; 7:6-8). Maandiko hayo na mengine kama Ayubu 31:9, 10, yanaonyesha iliyokuwa desturi au kawaida ya kufanya mapenzi na kufanya ngono na inapatana na inayoonwa kuwa desturi na kawaida ya leo.

Shauri lenye mkazo sana katika Maandiko ni kwamba imetupasa tumpende Mungu kabisa na kumpenda jirani yetu kama tunavyojipenda wenyewe; yampasa mume ampende mke wake kama anavyoupenda mwili wake mwenyewe, amtunze na kumheshimu. (Mt. 22:37-40; Efe. 5:25-31; 1 Pet. 3:7) Kama mtume anavyoeleza, upendo “haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu.” (1 Kor. 13:4, 5) Bila shaka huo ungezuia kutumia kwa nguvu mazoea yasiyo ya kawaida juu ya mwenzi wa ndoa, mazoea ambayo anaona kuwa yasiyofaa au hata yenye kuchukiza na yenye upotovu.

Maandiko hayatoi maongozi kuzidi hayo na, kwa sababu hiyo, sisi hatuwezi kutoa shauri kupita cheo cha yale ambayo Biblia inasema. Zamani maelezo fulani yametokea katika gazeti hili juu ya mazoea fulani ya kufanya ngono ambayo si ya kawaida katika ndoa kama vile kutia uume katika mdomo, na mazoea hayo yalipangwa katika hali iliyo sawa na uasherati. Kwa sababu hiyo uamuzi ulitolewa kwamba wale wanaofanya mazoea hayo bila kutubu wangetengwa na ushirika. Ilionwa kwamba wazee wa kundi walikuwa na mamlaka ya kuchunguza kisha kuwahukumu watu wenye mazoea hayo katika kufanya ngono.

Walakini, uchunguzi zaidi na wa uangalifu wa jambo hili unatusadikisha kwamba, kwa sababu Maandiko hayatoi agizo la wazi, hayo ni mambo ambayo ni daraka la mume na mke mbele za Mungu. Mambo hayo yanayopasa ngono hayako chini ya mamlaka ya wazee wa kundi kujaribu kuzuia wala si mambo peke yake yanayotoa msingi wa kuchukua hatua ya kutenga na ushirika.a Bila shaka mtu ye yote akitaka kumfikia mzee apate shauri, anaweza kufanya hivyo naye mzee huyo anaweza kuzungumza kanuni za Maandiko pamoja na mtu huyo, akifanya hivyo kama mchungaji lakini bila kujaribu kuchunguza-chunguza maisha ya ndoa ya mtu anayeomba shauri.

Lakini hilo lisionwe kama ni kuachilia mazoea ya ngono ya namna zote ambayo watu wanafuata, haimaanishwi hivyo hata kidogo. Jambo hilo linaonyesha tu kuona daraka na kuacha Maandiko yaongoze na kuacha kushikilia jambo fulani bila sababu ya kutosha. Linaonyesha vilevile kutumaini kwamba watu wote wa Yehova wanatamani kutenda mambo yote kana kwamba wanamtendea yeye na kuonyesha sifa zake bora katika mambo yao yote. Linaonyesha nia ya kumwachia Yehova Mungu na Mwanawe waamue juu ya mambo hayo, maana wana hekima na maarifa ya hali zote. Inafaa sote tukumbuke kwamba “sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu” na kwamba “kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu.” (Rum. 14:7-10, 12) “Imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyotenda kwamba ni mema au mabaya.”​—2 Kor. 5:10.

Inafaa tena kufahamu kwamba mtume alipoandika shauri lake katika Wakolosai 3:5, 6, hakuandikia watu wasiooa au wasioolewa tu, bali aliandikia watu waliooa na kuolewa vilevile. Alisema hivi: “Kwa hiyo, vitulizeni viungo vyenu vya mwili vilivyopo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, nyege, tamaa yenye kudhuru, na kutamani, ambayo ni ibada ya sanamu.” (Biblia ya Kiingereza tafsiri ya New World) Paulo anashauri tena katika 1 Wathesalonike 4:3-7, NW, akisema kwamba. “imempasa kila mmoja wenu ajue jinsi ya kumiliki chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika nyege za kutamani ambazo mataifa hayo yasiyomjua Mungu yanazo vilevile . . . Kwa maana Mungu alituita sisi, si kwa ruhusa yakufanya uchafu, bali kuhusiana na utakaso.”

Kwa kutaja hivyo “nyege,” mtume halaumu nyege za kawaida zinazoonyeshwa vya kufaa katika mpango wa ndoa. Tuna hamu ya kawaida ya kutaka kula na kunywa nasi twaweza kuitosheleza kwa kufaa. Lakini mtu anaweza kuwa mlafi au mlevi kwa kujitia katika ulaji na unywaji usio na kizuizi. Vivyo hivyo, mtu angeweza kuwa anafikiria mno kufanya ngono kwa kadiri ya kwamba kutosheleza nyege kunakuwa ndilo jambo kubwa kuliko kuwa jambo dogo la kuongeza kuonyesha mapenzi ambayo Biblia inatia moyo waliooana waonyeshane. Inapokuwa hivyo, hapo mtu huyo anafikia kiasi cha pupa ‘ambayo ni ibada ya sanamu,’ nazo nyege ndizo zinazoabudiwa.​—Efe. 5:3, 5; Flp. 3:19; Kol. 3:5.

Namna gani ikitukia kwamba mtu aliyeoa au kuolewa, labda mke anamfikia mzee wa kundi, akilalamika kwamba mwenzi wake wa ndoa anamfanyia mambo yasiyofaa kwa kutumia kwa nguvu mazoea ya ngono ambayo mke anakataa na kuyaona kuwa yenye kuchukiza sana na yenye upotovu? Ikiwa mwenzi wake wa ndoa anataka kuzungumza jambo hilo, labda mzee akiwa pamoja na mzee mwingine anaweza kujaribu kusaidia hao wawili waliooana waondoe ugumu wao, wakipewa shauri la Maandiko.

Namna gani ikiwa mtu aliyeoa au kuolewa anadai kwamba ngono fulani za mwenzi wake wa ndoa ni mbaya sana hata zinafanana na neno hili la Kigiriki porneia kama linavyotumiwa katika Mathayo 19:9 (“uasherati,” “fornication,” katika Biblia New World Translation)? Kama vile imekwisha kuonyeshwa, Maandiko hayatoi habari iliyo wazi inayosaidia kutambulisha ngono fulani zinazofanywa katika mpango wa ndoa kuwa ni porneia au si porneia. Na ifahamike ya kwamba neno hilo la Kigiriki limechukuliwa kutokana na neno ambalo maana yake asili ni “kuuza” au ‘kutoa au kujitoa kwa,’ na hivyo porneia maana yake ni “kuuza au kujitoa kwenye tamaa au uasherati.” Neno linaloonyesha kitendo (porneuo) linatia ndani “kufanya uasherati” kama mojawapo la maana zake. (Greek-English Lexicon, kamusi ya Liddell na Scott ya Kigiriki na Kiingereza) Ikiwa mtu aliyeoa au kuolewa anasadiki kwamba ngono za mwenzi wake, ijapokuwa hazifanywi pamoja na mtu asiye mwenzi wa ndoa, ni mbaya sana hata zinaonyesha kwamba anajitoa kwenye uasherati, huo utakuwa uamuzi na daraka lake mwenyewe.

Huenda mtu huyo akadai kwamba hali hizo zinatoa msingi wa Maandiko wa kuomba talaka. Ikiwa hivyo, mume au mke anapaswa kukubali daraka lote mbele za Mungu kwa hatua yote ya talaka inayoweza kuchukuliwa. Wazee hawawezi (kulingana na Maandiko) kutazamiwa kukubali talaka wasipokuwa na hakika ya sababu zake. Wakati uo huo hawana ruhusa ya kuzuia dhamiri ya mwingine ikiwa jambo hilo ni lenye kutiliwa mashaka. (Yak. 4:11, 12) Wakiisha kutoa shauri lo lote la Maandiko wanaloona kuwa lafaa, ndipo wanapoweza kumweleza wazi mtu huyo uzito wa jambo hilo na kwamba akiomba talaka hilo ni daraka lake kabisa. Ikiwa mtu anatafuta tu kisababu cha kuvunja ndoa, mtu huyo anaweza kutazamia kukosa kibali ya Mungu, kwa maana Mungu anasema kwa habari ya kufanya ukorofi huo juu ya mwenzi wa ndoa kwamba ‘amechukia kuachana.’ (Mal. 2:16) “Waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu” hata ye yote anayeomba talaka kwa kisababu kidogo tu kisha akaoa au akaolewa na mwingine, hataepuka hukumu hiyo. (Ebr. 13:4) Wazee wanaweza kutumaini kwamba katika wakati wake, Bwana “atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo.” (1 Kor. 4:4, 5) Ye yote anayepanda kwa udanganyifu na ukorofi hataepuka kuvuna taabu, maana “Mungu hadhihakiwi.”​—Gal. 6:7, 8.

Kama vile wazee wa kundi wanavyowapa ndugu na dada zao haki ya kutumia dhamiri yao wenyewe katika mambo yasiyotajwa waziwazi na Maandiko, vivyo hivyo wazee wana haki ya kufuata dhamiri zao wenyewe juu ya wanavyoona wale wanaofanya matendo yenye kutiliwa mashaka. Wakiona kwa hakika kwamba matendo ya mshiriki wa kundi katika mambo hayo yanaonyesha kwamba hawangeweza kuruhusiwa na dhamiri yao kupendekeza mume au mke afanye utumishi wo wote unaotaka mfano mwema katika kundi, wana haki ya kufuata dhamiri yao.​—1 Tim. 1:19; 3:2-12; 5:22.

[Maelezo ya Chini]

a Maneno ya mtume katika Warumi 1:24-27 yametajwa juu ya “matumizi ya asili” ya miili ya kiume na ya kike. Kama inavyoonekana wazi na kama vile imekubaliwa kwa kupatana, maneno hayo yanahusu hali ya kulalana wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake. Hayahusu moja kwa moja ngono zinazofanywa kati ya mume na mke hata kidogo. Inapaswa kukubaliwa vilevile kwamba hata mahaba (mapenzi) ambalo ni jambo la kawaida kabisa linalofanywa kati ya mume na mke, yangekuwa “yasiyo ya asili” yakifanywa kati ya wanaume kwa wanaume au wanawake kwa wanawake. Tena lingekuwa tendo la ufisadi ikiwa lingefanywa na watu wasiofunga ndoa. Kwa hiyo, uongozi wo wote unaotolewa na maneno hayo ya mtume, hauhusu moja kwa moja ngono zinazofanywa katika mpango wa ndoa. Lakini unapaswa uonwe kuwa wa namna ya kushawishi tu, si wa namna ya kukata maneno, yaani, sio msingi wa kuwekea kanuni za uamuzi ambazo hazina sababu nzuri. Lakini inaweza kuwa kwamba labda mwanzoni ngono nyingine zinazofanywa wakati huu na mume na mke zilifanywa kati ya wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake tu. Ikiwa ingekuwa hivyo, basi mwanzo wa mazoea hayo ungekuwa si mzuri kabisa. Kwa hiyo, kwa sababu maneno hayo yaliyo katika maandiko yaliyotangulia kutajwa hayahusu moja kwa moja watu waliofunga ndoa. Mkristo aliye na dhamiri asipuze jambo hilo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki