Mahubiri ya Mlimani—Hasira Yenye Kuendelezwa Yaweza Kudhuru Sana
BAADA ya kusema kwamba hakuja kutangua, bali kutimiza sheria ya Mungu, Yesu alishirikisha hasira inayoendelezwa na uuaji. Yeye alianza kwa kusema hivi: “Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, usiue; na mtu akiua, itampasa [mahakma ya] hukumu.”—Mt. 5:21.
Usemi ‘mmesikia walivyoambiwa’ unaweza kuhusu yaliyosemwa katika Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa kwa roho pamoja na mafundisho ya mapokeo ya Kiyahudi. (Mt. 5:21, 27, 33, 38, 43; Yohana 12:34) Sheria iliyoonyesha uuaji kuwa kosa kubwa sana ilijulikana kweli kweli kwa “watu wa kale,” yaani, watu wa vizazi vilivyokuwako kabla ya siku za Yesu. Kwa kweli, sheria ya namna hiyo yaweza kufuatishwa kurudi nyumba mpaka wakati wa Nuhu. —Mwa. 9:5, 6; Kut. 20:13; 21:12; Law. 24:17.
‘Kupaswa mahakma ya hukumu’ kulimaanisha kuhukumiwa na mojawapo “mahakma za mahali” (Kigiriki, Synedria, “Sanhedrin Ndogo”) zilizokuwako kila mahali nchini Palestina. (Mt. 10:17; Kum. 16:18) Mapokeo ya Kiyahudi yataja hesabu ya mahakimu katika mahakma hizi kuwa 23 katika miji yenye idadi ya wanaume waliokomaa 120 au zaidi.a Waliopatikana na hatia walipata adhabu ya kifo. Hata hivyo, katika wakati wa Yesu, mahakma za Kiyahudi zilipaswa kuomba ruhusa kwa adhabu zilizo nzito kutoka kwa maafisa wa Kirumi.—Yohana 18:31.
Yesu alitaja kwamba Mungu anaweza kumwona mtu kuwa anastahili adhabu nzito, hata ikiwa mtu huyo hakuwa ameua hasa. Akisema kwa mamlaka kama yeye aliyetumwa moja kwa moja na Mungu, Yesu alisema hivi: “Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa [mahakma ya] hukumu.”—Mt. 5:22a.
Kama alivyosema Yesu, ‘kila anayeendelea kumwonea ndugu yake hasira,’ ni mwenye hatia kama anayehukumiwa kwa uuaji. Hii ni kwa sababu kuruhusu hasira iwake kifuani mwa mtu hakika ni kumchukia mwanadamu mwenzako, na “kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji.” (1 Yohana 3:15) Ingawa kwa haki mtu anaweza akakasirika au kuwa na uchungu pindi fulani, hasira inayoendelezwa juu ya ndugu ya mtu au mwanadamu mwenzake yaweza ikawaletea hasara wote wawili.—Marko 3:5; Efe. 4:26; Yak. 1:19, 20.
“Anayemdharau ndugu yake,” akaendelea Yesu, “atapelekwa [Mahakma Kuu].” (Mat. 5:22b, HNWW) ‘Kumdharau’ linatafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki raca, ambalo Umetokana na Kiebrania na linamaanisha “kichwa-maji,” “mjinga,” “mpumbavu.” Ni gani maoni ya Mungu juu ya mtu anayesitawisha moyoni mwake si chuki na hasira inayotokeza uuaji tu, bali pia anayeionyesha kwa kutumia usemi wa dharau?
Kulingana na maneno ya Yesu, mtu wa namna hiyo ana kiasi fulani cha hatia inayolingana na ile ya mtu aliyehukumiwa kifo na “Mahakma Kuu” ya Kiyahudi. Hiyo ndiyo iliyokuwa Sanhedrin Kuu katika Yerusalemu, ambayo washiriki wake walikuwa “wakuu wa makuhani [waliokuwa waangalizi wa kazi za kikuhani hekaluni] . . . pamoja na wazee na waandishi.” (Marko 15:1) Baraza hii ya kufanya sheria, ambayo inaripotiwa kwamba ilikuwa na hesabu ya mahakimu 71, ilishughulika tu na kesi zenye uzito au ugumu usio wa kawaida na kusikiliza rufani kutoka kwa mahakma ndogo.b
Yesu alienda hatua zaidi, akisema: “Na mutu akisema, mupumbafu, itampasa Gehena ya moto.” (Mt. 5:22c, ZSB) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mupumbafu” ni mōré. Usemi wa Kiebrania wenye sauti inayofanana na hilo ni (moreh) linalomaanisha “-asi,” “-a kuasi.” Hali raca lamaanisha ujinga wa akili, mōré lamwonyesha mtu kuwa hana adili kabisa, mkufuru na mwasi Mungu. Katika kitabu chake Hebrew and Talmudical Escercitations, John Lightfoot anasema hivi: “‘Raca’ bila shaka huonyesha ‘chuki na tabia na maisha ya vivi hivi tu.’ Walakini ‘mpumbavu’ lahukumu kwa uchungu hali ya kiroho na ya milele, na kumhukumia mtu uharibifu hakika.”
Watu wanaowahukumu wenzao namna hiyo ‘ingewapasa Gehena ya moto.’ Hapa Yesu ataja Bonde la Hinomu (Kiebrania, Gei Hinnom) karibu na Yerusalemu, ambalo lilikuja kuwa mahali pa kutupa takataka ambapo moto uliwaka daima ili kuchoma takataka na mizoga iliyotupwa humo. Kulingana na Lexicon ya Liddell na Scott ya Kigiriki, “maiti za wahalifu walio wabaya zaidi zilichomwa” humo. Ikiwa mioto ya Gehena haikuichoma mizoga (maiti) hiyo, kabisa, nyungunyungu na funza waliozaana humo, waliimaliza.—Isa. 66:24; Marko 9:47, 48.
Yesu alitumia Gehena kama mfano ufaao wa uharibifu wa milele. Kwa kuwa mtu anayemhukumu mtu mwenzake kuwa ni “mpumbavu” anayestahili Gehena anamtakia uharibifu wa milele, kwa maoni ya Mungu mtu anayetamka hukumu ya namna hiyo anajiletea yeye mwenyewe hiyo hukumu kali.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 19:17-19.
[Maelezo ya Chini]
a Yosefo anasema kwamba mahakma za humo zilikuwa na mahakimu saba tu, hata hivyo, kila hakimu akiwa na Walawi wawili kama wasaidizi.—Antiguities of the Jews, Kitabu cha 4, Sura ya 8, fungu la 14.
b Kitabu The Theological Dictionary of the New Testament chasema hivi juu ya Sanhedrin kuu katika Yerusalemu: “Mbele ya baraza hiyo, iliyokutanika katika boule [chumba cha baraza] . . . kuhani mkuu alisimama. Ndiye aliyekuwa kiongozi cha Wayahudi; yeye peke yake ndiye angeisimamia Sanhedrin. Kumzunguka walikuwako archiereis [wakuu wa makuhani], wakuu wa kikuhani, Masadukayo waliowaunga mkono. Kwa uwezo wa cheo makuhani wakuu hekaluni walikuwa na cheo na mamlaka katika Sanhedrin na walifanyiza chama chenye nguvu nyingi. Wazee walikuwa kikundi cha pili. Ni kweli kwamba hapo kwanza washiriki wote wa gerousia [baraza ya wanaume wazee] waliitwa wazee. Hata hivyo, polepole, neno hilo likawa na maana fulani ya pekee, ikawa kwamba viongozi wa jamaa zenye mamlaka katika Yerusalemu peke yao ndio walioitwa Presbyteroi [wazee]. Vilevile, wakuu hawa wote, walikuwa wa imani ya Masadukayo. Mafarisayo walifaulu kuingia katika Baraza Kuu katika siku za Malkia Aleksandra [76-67 K.W.K.]. Tangu wakati huo uweza na uongozi wa grammateis [waandishi] uliendelea kuwa imara katika Sanhedrin. Wakati wa kipindi cha Warumi archierieis [wakuu wa makuhani] walikuwa wangali na cheo cha kwanza, walakini kwa kweli maamuzi hayangefanywa au kufikilizwa pasipo kibali ya waandishi wa Kifarisayo.”