Mahubiri ya Mlimani—“Usiape Kabisa”
BAADA ya kuzungumza juu ya uzinzi na talaka, Yesu alielekeza Mahubiri yake ya Mlimani juu ya viapo. Alisema hivi: “Tena mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, [usiape na ukose kufanya], ila mtimizie [Yehova] nyapo zako.”—Mt. 5:33.
Wayahudi waliomsikia Yesu walifahamu kwamba babu zao walikuwa wamesikia mengi juu ya viapo. Pindi fulani, kuapa kulikuwa kwa lazima. (Kut. 22:10, 11; Hes. 5:21, 22) Neno la Mungu linarudia kukazia umuhimu wa kutimiza nadhiri.—Hes. 30:2, 3; Kum. 23:21-23; Mhu. 5:4, 5.
“Lakini mimi nawaambia,” akaendelea Yesu, “Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi.”—Mt. 5:34-36.
Je! Yesu alikuwa na kusudi la kufutilia mbali viapo na nadhiri zote? Sivyo, kwa maana Sheria ya Mungu iliyoamuru kuapa pindi fulani ilikuwa ingali ikifuatwa. (Gal. 4:4) Alipokuwa akijibu mashtaka mbele ya kuhani mkuu, Yesu mwenyewe hakukataa kuapishwa. (Mt. 26:63, 64) Yesu aliposema kwamba watu ‘wasiape kabisa,’ alikuwa akizungumza juu ya kuharibika na kupotoka kwa viapo. Namna gani hivyo?
Viapo vinavyotajwa kwa kufaa katika Biblia kwa kawaida vilihusu mambo ya maana sana, kama vile maamuzi yanayohusu ibada ya kweli, kufanya maagano na kutoa ushuhuda mahakmani. (Mwa. 24:2-4, 9; 31:44, 50, 53; Kut. 22:10, 11) Hata hivyo, wakati ulipoendelea kupita, Wayahudi walizoea kutoa viapo kuhusiana na mambo mengi ya kila siku. Kwa mfano, maandishi ya kale ya waalimu wa kidini Wayahudi yanataja watu wakitoa viapo vya kutolala, kutozungumza, kutotembea, na kutofanya ngono na wake zao. Viapo vingi vilitotewa kwa kutumia neno “Korbani,” linalomaanisha “zawadi iliyowekwa wakf kwa Mungu.” Iliaminiwa kwamba kwa kutaja neno hilo, mtu angeweza kutangaza vitu fulani kuwa haviruhusiwi kutumiwa naye mwenyewe au na wengine kama vile zilivyokuwa dhabihu hekaluni. Kuhusu hili, Yesu aliwaambia Mafarisayo hivi:
“Vema! Mwaikataa amri ya Mungu mpate kuyashika mapokeo yenu. Maana Musa alisema, Waheshimu baba yako na mama yako, na Amtukanaye babaye au mamaye kufa na afe. Bali ninyi husema, Mtu akimwambia babaye au mamaye, Ni Korbani, yaani, [zawadi iliyowekwa] wakfu [kwa Mungu], kitu changu cho chote kikupasacho kufaidiwa nacho, huwa basi; wala hammuruhusu baada ya hapo kumtendea neno babaye au mamaye; huku mkilitangua neno la Mungu kwa mapokeo yenu [mliyopokezana].”—Marko 7:9-13.a
Vilevile mpango wa kutoa nadhiri ulikuwa umeharibika. Mahali pa kufuata mifano ya Maandiko ya kutoa viapo katika jina la Mungu, yalikuwa yamekuwa mazoea kuapa “kwa mbingu,” “kwa nchi,” “kwa Yerusalemu,” na hata “kwa kichwa” (au uhai) cha mtu mwingine. (Kum. 6:13; Dan. 12:7) Kulikuwako mabishano kati ya Wayahudi wenye maarifa juu ya ubora wa nadhiri nyingi zilizofanywa katika jina la vitu hivyo vilivyoumbwa. Kwa wazi watu fulani waliona kwamba wangeweza kutangua viapo vyao bila woga wa kuadhibiwa.—Linganisha Mathayo 23:16-22.
Walakini, Yesu alionyesha kwamba, kwa kuwa mbingu zilikuwa “kiti cha enzi cha Mungu,” nayo nchi “pa kuwekea miguu yake,” na Yerusalemu “mji wa Mfalme mkuu,” kuapa kwavyo kulikuwa sawasawa na kuapa katika jina la Mungu. (Isa. 66:1; Zab. 48:2) Vivyo hivyo, kutoa nadhiri kwa “kichwa,” au uhai wa mtu kulikuwa sawasawa na kutoa nadhiri hiyo katika jina la Mungu, kwa maana ndiye Mwanzishi na Mwendelezaji wa uhai; na hakuna mwanadamu aliye na uwezo juu ya uhai wake hata kuweza ‘kugeuza unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi.’—Zab. 36:9.
Baada ya kuvunja moyo juu ya kuapa vyo vyote, Yesu aliendelea kusema hivi: “Bali maneno yenu, yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu.”—Mt. 5:37.
Mazoea ya kuapa ili kukazia uzito wa mambo aliyokuwa akisema mtu yalitokea kwa sababu ya udanganyifu na uongo uliokuwako. Hata hivyo, Yesu alionyesha kwamba katika maisha ya kila siku. Ndiyo au Siyo nyepesi inapaswa kuaminika na haihitaji kutegemezwa na viapo. Watu wanaoona lazima ya ‘kuzidi’ hayo kwa ‘kuapa’ juu ya yale wanayosema, wanajionyesha wenyewe kwamba kwa msingi hawaaminiki. Wanaonyesha wazi roho ya “yule mwovu,” Shetani Ibilisi, ambaye Biblia inamwita ‘baba ya uongo.’—Yohana 8:44; Yak. 5:12.
[Maelezo ya Chini]
a Maana yake, mtu huyo angekuwa akiwaambia wazazi wake hivi: ‘Kwa habari yenu, mali yangu ni “Korbani,” zawadi iliyowekwa wakf kwa Mungu, na hamwezi kuitumia au kujifaidi nayo kwa vyo vyote.’ Kwa kutumia neno “Korbani,” haina maana kwamba mtu alikuwa akiweka mali yake wakf kwa Mungu. Kwa kawaida neno hilo lilimaanisha kwamba alikuwa tu akiifanya kuwa kama zawadi iliyowekwa wakf kwa Mungu, ili kwamba mtu au watu aliosema nao wasiweze kuitumia. Katika kitabu The Life and Times of Jesus the Messiah (Maisha na Nyakati za Yesu, Masihi), Alfred Edersheim anaandika hivi: “Haiwezi kupingwa kwamba nadhiri za namna hiyo, kuhusiana na wazazi, zingefuatwa, na kwamba kwa kweli zilitolewa.”