Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 5/15 kur. 4-8
  • Yale Ambayo Dini ya Kweli Yaweza Kufanyia Vijana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yale Ambayo Dini ya Kweli Yaweza Kufanyia Vijana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUHESHIMU MAMLAKA YA WAZAZI
  • KUTUMIA HEKIMA ITOKAYO JUU
  • BABU ALIYE MZEE ZAIDI, “MZEE WA SIKU”
  • Kumpendeza Yehova Kama Jamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vijana—Mnawezaje NINYI Kuwa Wenye Furaha?
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Je! Watoto Wako ni Wanafunzi wa Kristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 5/15 kur. 4-8

Yale Ambayo Dini ya Kweli Yaweza Kufanyia Vijana

IKIWA washiriki wote wa jamaa zote wangechunguza Biblia kwa uangalifu mwingi na kujaribu kutumia mashauri mazuri ya Biblia, hata kama si kwa ukamilifu, jamaa zote zingefurahia umoja na furaha nyumbani. Na zaidi, mashindano na vita vingekoma kati ya jamaa, makabila na mataifa. Lakini kwa wakati huu wa sasa sivyo ilivyo ulimwenguni pote. Nyakati nyingine ni mshiriki mmoja tu wa jamaa anayechukua mwendo huu mzuri. Namna gani ikiwa ndivyo ilivyo​—⁠ tuseme, ni mwana au binti peke yake anayejaribu kwa bidii kutumia kanuni za Biblia? Je! hili linaleta hali yenye furaha ya jamaa? Sivyo ilivyo mara nyingi. Lakini matokeo yanakuwa na maongozi yenye kuleta umoja zaidi. Na bila shaka Mungu anasaidia mwana au binti huyo ashindane na gumu hilo vizuri zaidi, kuwa na amani nyingi zaidi ya akili na kutoa maongozi yafaayo katika jamaa.

Tunapofikiria mtajo huu juu ya matokeo yenye kuleta umoja ya Mkristo, huenda wengine wakakumbuka kwamba Yesu alisema, katika Luka 12, mistari ya 52 na 53, kwamba alikuja kuleta mgawanyiko​—“katika nyumba moja watakuwamo watu watano wamefarakana, watatu kwa wawili, wawili kwa watatu. Watafarakana baba na mwanawe, na mwana na babaye; mama na binti yake, na binti na mamaye; mkwe mtu na mkwewe, na mkwe na mkwe mtu.” katika kusema hilo, Yesu hakuwa akitia moyo mgawanyiko katika uhusiano wa jamaa. Yesu hakupingana na ndugu zake wa kimwili. Kwa upande mwingine, ndugu zake hawakumtia moyo, bali walikuwa na maelekeo ya kusingizia madai yake. Hata hivyo, mwendo wa Yesu ulifanya nduguze waamini “habari njema” alizofundisha wakawa Wakristo baadaye.​—Yohana 7:3-5; Matendo 1:13, 14.

Kwa yale yaliyompata maishani mwake, na kwa maneno yake pia, Yesu alionyesha kwamba wanafunzi wake, wangekataliwa, wadhihakiwe na hata kuteswa na jamaa Zao wenyewe. Hata hivyo, chanzo cha uadui hakikupaswa kitokane na mwamini kwa kuwa mjeuri au kwa sababu ya mwenendo wake usio wa heshima. Kwa kweli hiyo ingekuwa kinyume cha Ukristo, na ingeweza kuwa mtego ambao katika huo Mkristo, sana sana kijana, angaliweza kuangukia kwa urahisi. Kijana wa kiume au wa kike huenda akawa alikuwa hana heshima kabla ya kupata maarifa ya Biblia. Walakini kweli ya Biblia inaweza kufanya mabadiliko ya ajabu katika Mkristo, kwa kuwa anaweza kuonyesha mfano wake wenye thamani isiyobadilika, hivyo ajipatie sifa kwa kila dhamiri na mbele za Mungu.​—2 Kor. 4:2.

Kwa habari ya wale ambao huenda wakaonyesha wazi upinzani mkali, kwa sababu ya kutofahamu au kutothamini mwendo uliobadilika wa Mkristo, Yesu aliamuru: “Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni (Mt. 5:44, 45) Wakati wote tumaini la Mkristo ni kwamba huenda watu kama hao wakawa waamini mwishowe.

Kweli inapopingwa, Mkristo, kama vile Bwana wake Yesu Kristo, atasimama imara kwa ajili ya kweli. Walakini uimara si lazima uwe ukali. Wakati wote atakuwa mwenye fadhili. Hatajifikiria kuwa bora kuliko wengine, wala kuwa mjeuri na kurudisha maneno kwa ukali anaposemewa (mazoea yanayoonyeshwa sana sana na vijana wengi leo). Vilevile, wakati wa kudhihakiwa au kutukanwa, Mkristo atafanya vema kukumbuka maneno ya Petro “Mwe tayari sikuzote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu.”(l Pet. 3:15) Sana sana huu upole na “hofu” ionyeshwe washiriki wa jamaa. Kujibu kwa namna hiyo kunahitaji unyofu wa moyo, bidii, kujifunza kwa uangalifu mwingi na jitihada. Wote, hata Wakristo walio vijana, wanapaswa wawe wanaweza kutoa sababu zilizo kamili na wazi za imani yao. Ikiwa sivyo, iko wapi imani?

KUHESHIMU MAMLAKA YA WAZAZI

Kijana anayepata kuwa Mkristo anajifunza aliyosema Yesu, kwamba “kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Kijana wa kiume (au wa kike) anapata kujifunza kwamba kuna uhuru kweli kweli kutokana na mengi yanayoongoza, ndiyo, hata kufanya vijana wengi wawe watumwa leo​—kuogopa wenzao, mikazo ya kijamii ili kufuata wingi wa watu, kuabuda watu wenye sifa, wivu, mashindano, tamaa mbaya, kushuka moyo na misiba inayotokana na maongozi ya rafiki wabaya. Lakini vijana wanapaswa kufahamu kwamba hawako huru kabisa. Wanapaswa kukubali mamlaka zilizowekwa, mojawapo ya kwanza kabisa ikiwa ni mamlaka ya wazazi. Mungu mwenyewe ndiye aliyewapa wazazi daraka la kuzoeza watoto katika njia ifaayo na kuamua lililo zuri zaidi kwa kila mtoto.​—Kum. 31:12, 13.

Mamlaka ya wazazi inatia ndani “fimbo” ya adhabu. Mithali 23:13, 14 inasema hivi: “Usimnyime mtoto wako mapigo; maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa. Utampiga kwa fimbo, na kumwokoa nafsi yake na [kaburi].” Nyakati nyingine, watoto wanaweza kujisikia kwamba adhabu hiyo haitolewi inavyofaa, lakini wanapaswa kukumbuka kwamba wazazi watamtolea Mungu hesabu juu ya namna wanavyotumia mamlaka yao, na ikiwa adhabu inatolewa isivyofaa, hata hivyo, Mungu anaweza kuifanya imfaidi mtoto anayetii.​—Rum. 8:28.

Kutii mamlaka ya wazazi kunakuwa rahisi zaidi ikiwa kijana anafikiria maneno ya mtume Paulo: “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” (Ebr. 12:11) Kijana anayethamini hilo anaweza kushukuru kwa adhabu anayopata kutoka kwa wazazi na walio wazee kundini, vilevile shuleni. Atafanya maendeleo upesi na atafurahia dhamiri njema na uhuru wa kusema, kwa sababu anapotii mamlaka, ingawa wakati mwingine haionekani kuwa kitu cha furaha, kijana huyo huwa anamtumikia Bwana Yehova na Mwanawe Yesu Kristo. Mtume huyo aliwafikiria kipekee walio vijana, apate kuwafariji, alipoandika hivi: “Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Kol. 3:20) Kijana atatii katika mambo yote ila tu anapoombwa afanye jambo lisilompendeza Bwana.

KUTUMIA HEKIMA ITOKAYO JUU

Unapomwabudu Muumba, huenda usipokee msaada kutoka kwa washiriki wa jamaa au rafiki. Ili uendelee kuwa na kiasi chini ya hali hizo, unaweza kuomba na utapata hekima kutoka kwa Mungu. Mwanafunzi Yakobo, ndugu mzazi mmoja na Yesu, aliwaandikia wanaopata magumu hivi: “Mwione kuwa furaha yote, ndugu zangu, mnapopatwa na majaribu ya namna nyingi.” “Kwa hiyo, ikiwa ye yote kati yenu anapungukiwa na hekima, acheni yeye aendelee kumwomba Mungu, kwa kuwa yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kuwalaumu; naye atapewa hiyo.”​—Yak. 1:2, 5, NW.

Vilevile Yakobo anaieleza “hekima itokayo juu” kuwa “kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki.” (Yak. 3:17) Ifikirie kila moja ya sifa hizi kwa uangalifu, na kwa unyofu uone kama wewe unazionyesha, na maendeleo yanayoweza kufanywa. Sifa hizi zitakusaidia ufahamu hali ya wengine na wanavyosikia hata na wewe pia.

Inapaswa kukumbukwa kwamba washiriki wa jamaa yako kwa kawaida wanapendezwa nawe, ingawa huenda wakawa na maarifa ya kadiri fulani tu juu ya namna Ukristo wa kweli ulivyo. Pengine umeanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Watu wa jamaa yako na rafiki zako huenda wasifahamu Mashahidi wa Yehova ni watu wa namna gani hasa. Basi huenda wakaona kwamba ‘dini hii inachukua wakati wako mwingi.’ Kwa sababu ya unafiki unaoonekana leo katika dini nyingi, ni jambo lenye kufahamika sababu gani wazee huenda wakaogopa na kuwa waangalifu. Wanapoona juhudi yenu ya ujana kuelekea dini, wanaogopa kwamba mwendo wenu huenda ukawa si wa akili nzuri, bali ni maono tu ya moyoni. Ikiwa wanaonyesha upinzani waziwazi, unaweza kuwathibitishia kwa majibu ya heshima katika roho ya amani na akili nzuri, kwamba umefanya uamuzi wa akili na wenye msingi mzuri.

Kwa hiyo jiulize hivi: Kweli mimi ni mwenye amani na akili? Je! ninaionyesha jamaa yangu maoni hayo, ingawa wao, kwa kiasi fulani, wanapinga ninayoamini? Naweza kufanyaje nipate kuleta maendeleo katika umoja wa jamaa na hivyo kufanya utumishi wangu kwa Muumba kwa nafsi yote? Katika hili, je! upangaji wangu wa mambo unaonyesha kiasi na akili, nipate kuangalia madaraka ya jamaa na kushiriki katika utangazaji wa “habari njema” katika njia yenye matokeo?

Kwa kutumia hekima ya Biblia inayotoka juu, Mkristo anapaswa afanye maendeleo wakati wote katika mwenendo na mazungumzo pamoja na washiriki wa jamaa. Huenda jamaa na rafiki zako wasikupinge, lakini ikiwa wanafanya hivyo, maneno ya mtume Petro yanaonyesha unalopaswa kufanya. Aliwafariji Wakristo na maneno yafuatayo: “Nanyi mwe na dhamiri njema, ili katika neno lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale wautukanao mwenendo wenu mwema katika Kristo. Maana ni afadhali kuteswa kwa Kutenda mema, ikiwa ndiyo mapenzi ya Mungu, kuliko kwa kutenda mabaya.”​—1 Pet. 3:16, 17.

Mara nyingine, mwenendo wa Mkristo unavuta wengine kwa nguvu nyingi kuliko maneno.

Katika Hong Kong, wakati msichana fulani wa miaka 20 hivi alipoanza kuhudhuria kwa kawaida mikutano ya kujifunza Biblia, jamaa iliudhika, sana sana ndugu zake wakubwa. Hata hivyo, mmoja aliona kwamba, hapo kwanza dada yake alikuwa akijitia katika mabishano yenye kelele nyingi pamoja na mama yake, alipozidi kujifunza Biblia alianza kufanya mabadiliko na aliendelea kuonyesha roho ya upole zaidi. Lakini bado nduguye alikuwa na mashaka na hakuwa na uhakika kwamba maendeleo haya yalikuwa yakiletwa na maongozi ya dini yake mpya. Kwa kweli aliona kwamba dadaye alikuwa akidanganywa na kwamba mwenendo wake uliobadilika ulikuwa wa kijuujuu tu.

Ili kuhakikisha jambo hili, ndugu huyu alienda safari moja pamoja na dada yake kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la mahali hapo. Alishangazwa, kutoona chama cha kijamii au kipindi cha kupitisha kisahani cha michango, bali, kikundi cha watu wenye shauku na urafiki wanaopendezwa kujifunza Biblia na kuitumia maishani. Muda si muda, naye pia, akawa akijifunza Biblia. Sasa, wakiwa Mashahidi waliobatizwa, ndugu huyu na dada wanahudhuria mikutano pamoja na wameanza kuwaleta washiriki wengine wa jamaa. Kupendezwa na Mungu na Neno lake kuliamshwa na upinzani ukageuka kuwa umoja na furaha ya jamaa​—kwa sababu tu binti alitumia mashauri ya Biblia katika kusitawisha upole na roho ya kutamani kusaidia wengine.

Nyakati nyingine huenda ikaonekana kwamba mwenendo mzuri hauonwi na wapinzani, lakini hili halipaswi kumvunja Mkristo moyo.

Msichana kijana ambaye hapo kwanza alielekea kujitia katika matata na kutaka kujitegemea alifanya bidii kubadilisha utu wake uwe wa Kikristo. Hapo kwanza, jambo hili halikutokeza maneno yo yote na kwa wazi halikuwa na matokeo yo yote juu ya wazazi wake. Ndipo, siku moja, alipomsikia mama yake akimwambia jirani hivi: “Nalikuwa nikimpinga binti yangu alipojiunga na dini hii [Mashahidi wa Yehova] walakini nimeona maendeleo katika mwenendo wake hata sitampinga tena, kwa sababu ni lazima hii iwe dini nzuri bila shaka.”

BABU ALIYE MZEE ZAIDI, “MZEE WA SIKU”

Ni kitu gani kinachofanya vijana kati ya Mashahidi wa Yehova wafuate Biblia kwa ushikamanifu hata jamaa inapokataa? Je! ni kwa sababu wanafunzwa kutoheshimu watu wa jamaa? Sivyo kabisa! Tofauti yake, wanafuata mazoea yaliyo ya zamani kama vile jamii ya kibinadamu, yaani, kumheshimu na kumtii Babu aliye mzee zaidi. Katika mashirika ya kijamii ulimwenguni pote, kufikia hivi karibuni, mshiriki wa jamaa wa kiume aliye wa umri mkubwa zaidi ndiye aliyetumainiwa kutoa mashauri, hekima na uongozi. Neno lake lilikuwa ni sheria na lilitangulizwa juu ya yale ya wengine​—mwana, kitukuu, kining’ina. Watu wengi katika nchi za Mashariki (Asia) hata wanaabudu mababu wao waliokufa na kutumainia uongozi kutoka kwao. Walakini Wakristo wa kweli wanamsikiliza babu aliye mzee zaidi, aishiye, “Mungu aliye hai,” yaani, Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu.​—Yer. 10:10-12.

Kitabu cha Biblia cha Danieli (7:9) kinamtaja Mungu kuwa “Mzee wa Siku.” Yeye amekuwako tangu milele na ndiye chanzo cha uzima wa wanadamu wote. (Zab. 36:7, 9; Matendo 17:24, 25, 28) Kwa hiyo, wote wanapaswa kumtii yeye, kama vile vijana waliozoezwa vizuri wanavyopaswa kuwa wepesi katika kuwasikiliza wazazi na babu na nyanya zao. Kwa kufuata hekima na mashauri ya “Mzee wa Siku” twaweza kuitwa watoto wake. (1 Pet. 1:14; 1 Yohana 3:1; 2 Kor. 6:18) Basi ni jambo la kufahamika kwamba watumishi vijana wa Muumba wanaona kwamba kwa ajili ya dhamiri zao inawapasa kumsikiliza mzazi huyu mkuu zaidi na kuona kuwa ndiye mamlaka ya mwisho wakati kunapokuwa kupingana kwa amri, ingawa wataendelea kuheshimu na kuwapenda wazazi wao.

Kwa kuwa Yehova ndiye mwanzishi wa jamaa na maisha ya jamaa, basi vijana wanaomtumikia watapata kuwa washiriki wema zaidi wa jamaa. Wana na mabinti hawataaibisha wazazi wao wa kidunia kwa kufuata mitindo, uasherati na mwenendo mbaya wa ulimwengu huu. Watakuwa tayari kusaidia nyumbani na hivyo wawaletee wazazi sifa kwa mwenendo wao safi na mnyofu nyakati zote. (Tito 2:6-8) Kwa kuangalia mambo haya, ambayo yanapendeza zaidi ya kushindana na mamlaka, vijana walio Wakristo wa kweli wanamletea Muumba sifa. Vilevile Baba yao wa mbinguni anapata utukufu kutokana na hilo na anawabariki kwa ajili ya upendo na imani yao.

Katika pembe zote za dunia, katika hali ziwazo zote, maelfu ya vijana wanafuata mwendo unaompendeza Mungu. Pengine vingine vya vitu vya ulimwengu vinavyovutia vijana zaidi, na mikazo mikubwa zaidi inapatikana katika mataifa yanayosemekana kuwa ya kisiku-hizi, ambako roho inayoenea pote ni ile ya kupenda mali za kimwili. Je! Ukristo wa kweli unaweza kuwapa vijana mambo wanayohitaji ili wapate uradhi na furaha na wajitenge wasivutwe na roho ya ulimwengu ya kupenda mali za kimwili? Kielelezo bora kinapatikana katika Mwungano wa Jamhuri ya Ujeremani ya wakati uliofuata baada ya vita.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki