Mahubiri ya Mlimani—Msihangaike
BAADA ya kutoa mashauri juu ya kuepuka kupenda mali, Yesu aliwaonya kwa upole wasikilizaji wake waepuke kuwa na wasiwasi usiofaa juu ya kupata vitu vya lazima maishani: ”Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi?”—Mt. 6:25.a
“Kwa sababu hiyo,” yaani, kwa sababu mtu ‘hawezi kutumikia Mungu na mali,’ wanafunzi wa Yesu wangepaswa kuepuka kuwa na wasiwasi mwingi hata kwa habari ya kupata mahitaji ya kila siku. (Mt. 6:24) Mwana wa Mungu hakuwa akitaka kuwavunja moyo watu wasihangaike ifaavyo na kufanya kazi kwa jitihada kwa ajili ya kupata chakula na mavazi. (Mhu. 2:24; Efe. 4:28; 2 The. 3:10-12) Walakini hakuna uhitaji wa ‘kuhangaika’ kupata vitu hivyo. ‘Maisha na mwili’ (hapa mtu kwa ujumla) ni mambo ya maana zaidi kuliko chakula na mavazi. Kwa kuwa Mungu aliwapa wanadamu uzima wa kimwili, hakika anaweza kuona kwamba waabudu wake wanapafa vitu vya lazima vya kujiruzuku navyo.
Yesu alikazia jambo hilo kwa mfano huu: “Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao.”—Mt. 6:26a.
“Ndege wa angani” ambao huruka kama watakavyo angani hawalimi. Hata hivyo Mungu anahakikisha kwamba wanapata chakula cha kutosha. (Linganisha Ayubu 38:41; Zaburi 147:9.) Hilo lilikuwa jambo la ‘kuangalia’ sana, kutafakari kwa uzito. Wayahudi waliokuwa wasikilizaji wa Yesu wangeweza kuzungumza juu ya Mungu akiwa ‘Baba yao wa mbinguni,’ sana sana kwa sababu Waisraeli walikuwa ‘wamechaguliwa’ kama watu wa Mungu wa agano. (Kum. 7:6) Akiwatofautisha na ndege wa angani, Yesu aliuliza hivi: “Ninyi je! si bora kupita hao?” (Mt. 6:26b) ikiwa Mungu anaruzuku viumbe warukao, basi si atafanyia waabudu wake zaidi?
Akionyesha ubatili wa kuwa na wasiwasi usiofaa juu ya kupata vitu vya lazima maishani, Yesu aliendelea kusema hivi: “Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja?” (Mt. 6:27) Mara nyingi Maandiko hufananisha maisha yote ya wanadamu na safari, yakitumia mitajo kama vile “njia ya wakosaji” na “njia iliyonyoka.” (Zab. 1:1; 27:11) Kuhangaikia mahitaji ya kila siku hakuwezi kuongeza maisha ya mtu hata kwa kisehemu kidogo, “mkono mmoja.” Mahali pa kufaidi watu, wasiwasi usiofaa unaharibu afya na hata kufupisha maisha.
Kisha Yesu akatokeza mfano wa pili, akasema hivi: “Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti; nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama moja-wapo la hayo.”—Mt. 6:28, 29.
Inaelekea “maua ya mashamba” yanatia ndani maua kadha yenye rangi yenye kung’aa yanayotokea katika mashamba ya Galilaya. Kitabu cha Hasting, A Dictionary of the Bible kinasema hivi:
“Yote hayo yanakua kati ya nafaka, mara nyingi yakiinuka juu yake, na kuangaza mashamba makubwa kwa rangi mbalimbali za wekundu hivi na zambarau hata urujuani-zambarau na samawati, kweli kweli rangi za fahari. Ye yote ambaye amepata kusimama kati ya mashamba ya ngano ya Galilaya, na kuona kishada cha maua haya, yakiangalia pande zote juu ya nafaka zilizosimama ataona mara moja kufaa kwa mtajo wa Mwokozi wetu. . . . Hata hivyo, iwapo, twafahamu ‘yungiyungi ya kondeni’ maana yake ni yungiyungi ya mwituni, hayo pia yanatiwa ndani katika mtajo huo. Mlinganisho wa Mwokozi wetu ungelingana na ‘picha iliyounganishwa,’ mtajo wa rangi zote nzuri sana na maumbo mazuri ya mimea mingi ya mwituni inayotiwa ndani ya “jina yungi-yungi.”
Mtu anapofikiri “jinsi” maua hayo “yameavyo,” anaona kwamba yanafanya hivyo bila ‘kufanya kazi’ au ‘kusokota’ ambako wanadamu wanalazimika kufanya ili kutokeza nguo. Hata hivyo maua ya shambani ‘yamevikwa’ kwa uzuri ambao hakuna mavazi yo yote ya kibinadamu, yaweza kulingana nayo hata ya yule Mfalme Sulemani aliyejulikana sana kwa ajili ya mavazi yake mazuri.—2 Nya. 9:5-21.
Kwa habari ya ‘somo’ (NW) la mfano huo, Yesu alisema hivi: “Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa kalibuni, je! hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba?”—Mt. 6:30.
“Majani ya kondeni” yanatia ndani maua ambayo Yesu alitaja. Nyakati za kiangazi chenye joto cha Palestina, majani hayo hunyauka kwa muda wa siku mbili tu. Miti ya maua iliyokauka na nyasi ilikusanywa na kutumiwa kuwashia moto wa meko. Kwa kuwa Mungu ‘huvika’ vizuri majani yanayonyauka upesi hivyo, ulizo la Yesu ni zuri: “Je! hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba?” Watumishi wa Mungu ni bora zaidi kuliko maua. Wasiwasi mwingi juu ya kupata mavazi yenye kuhitajiwa ungekuwa wonyesho wa “imani haba.”b
“Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini?” akaendelea Yesu, “Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote.”—Mt. 6:31, 32.
Hiyo ndiyo iliyokuwa mara ya tatu katika mahubiri yake Yesu kuwafananisha wasikilizaji wake na “Mataifa,” au watu wasiokuwa Wayahudi. (Tazama Mathayo 5:47; 6:7.) Hawakuwa na uhusiano na Mungu, nalo jambo kubwa maishani mwao lilikuwa mali na anasa za mwili. Hivyo, iwapo watumishi wa Mungu wangetilia shaka uwezo na nia yake ya kuwapa vitu vya lazima, wangekuwa kama watu wa mataifa ambao walikuwa ‘hawana Mungu duniani.’—Efe. 2:11, 12.
Kwa kuwa Aliye Juu Zaidi ‘anajua mahitaji’ ya watu wake, wasikilizaji wa Yesu wangefanya vema kutii shauri alilotoa: “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mt. 6:33.
Wanafunzi wa Yesu walikuwa wamemkubali yeye kuwa Masihi, jambo ambalo liliwaweka katika njia ya kuwa sehemu ya serikali ya Mungu ya Kimasihi ya kimbinguni, au “ufaIme.” (Luka 22:28-30; Yohana 14:1-4; Dan. 7:13, 14, 18, 22, 27) Lakini wangepaswa kuendelea ‘kuutafuta’ “kwanza,” kuendelea kuufanya kuwa jambo la kuhangaikia zaidi maishani mwao. Vilevile wangepaswa kutafuta “haki yake [yaani, ya Mungu]” kwa kumwamini Masihi wa Mungu na kuzoea mwenendo unaopatana na amri nyinginezo za Mungu. Bila shaka, jambo hilo halipaswi kufanywa kwa maoni ya kuwa na haki kwamba kwa kufanya mambo yenye kuonekana ya kidini na vitendo vyenye sifa kunamlazimu Mungu ambariki mtu. Haki iliyo ya maana kwa Mungu inapaswa kutoka moyoni ikijaa upendo na kuthamini yale ambayo amefanyia wanadamu. (Tazama Warumi 10:3; 1 Yohana 4:19.) Watu wanaoweka ibada ya Mungu kwanza katika maisha yao wanaweza kuwa na uhakika kwamba ‘wataongezewa’ mahitaji yao “yote” ya kila siku na Mungu mfadhili wanayeabudu.
“Basi, msisumbukie ya kesho” akaendelea Yesu, “kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.” (Mt. 6:34) Kila siku ina magumu yake yanayoleta kadiri fulani ya kushuka moyo. Mara nyingi matatizo ya kila siku hutokea ghafula na yanaletwa na sababu zisizoweza kuzuiwa na wanadamu. (Angalia Mhubiri 9:11, NW.) Watumishi wa Mungu wanapaswa kuona shida hizo ‘zatosha kwa kila siku’ na kuelekeana nazo siku kwa siku. Mahali pa kufanya mambo yawe afadhali, kuhangaikia siku inayokuja kunaonyesha kukosa imani katika Mungu na kulifanya kuwa jambo gumu kukabiliana na “maovu” ya iliyopo.
[Maelezo ya Chini]
a Shauri la Yesu linalozungumzwa katika makala hii (Mt. 6:25-34) linaonekana pia katika Luka 12:22-31 likiwa tofauti kidogo. Vifungu vyenye kuzunguka habari hiyo katika Luka, kikao chake kilikuwa kama mwaka mmoja hivi baada ya Mahubiri ya Mlimani katika Galilaya, wakati wa huduma ya baadye ya Yesu Katika Yudea. Kwa wazi Yesu aliona inafaa kurudia onyo hilo la upole.
b Yesu alitumia mtajo “wa imani haba” kwa habari ya wanafunzi wake peke yao. Unaonekana pia katika Mathayo 8:26; 14:31; 16:8 na Luka 12:28. Kifungu hicho cha maneno kinapatikana katika maandishi ya kirabi, jambo hilo likionyeshwa kwamba ulikuwa ukifahamika vizuri. Kwa mfano, kitabu Babylonian Talmud kinasimulia hivi: “R[abi] Eliezeri mkuu atangaza hivi: Ye yote aliye na kipande cha mkate katika kikapu chake naye asema, ‘Nitakula nini kesho?’ Ni mmoja wa wale wa imani haba”