Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 2/1 kur. 11-16
  • Yehova—Tumaini Letu la Kuingia Taratibu Mpya

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova—Tumaini Letu la Kuingia Taratibu Mpya
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JUMUIYA YA WAKRISTO YENYE UNAFIKI HAITATETEWA
  • WATAZAMIA AMANI KUMBE HAIFAI KITU!
  • “Watapigana Nawe”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Katiwa Nguvu Kunena Maneno ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • “Mchungaji” wa Kifalme wa Unabii wa Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Wakisema “Amani” Wakati Haipo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 2/1 kur. 11-16

Yehova​—Tumaini Letu la Kuingia Taratibu Mpya

1. Sababu gani wengi wamepoteza kwa hakika tumaini la uwezekano wa taratibu mpya?

NI NANI asiyetaka taratibu mpya ya mambo hapa duniani? Watu wengi wangependa kuwa na taratibu ya mambo yenye haki na yenye afya zaidi walakini sasa wanalo tumaini dogo la jambo hilo kuwezekana. Hali ya adili ya wanadamu inayoharibika zaidi haiwapi msingi wo wote wa kutumaini mambo kuwa afadhali. Kwa hakika wamepoteza tumaini kwa sababu hakuna tumaini lenye kutegemeka na la kweli walilojulishwa. Bado hawajatambua kwamba taratibu hii mpya yenye kutamanika imeahidiwa na mtu mwenye uwezo kamili na kwamba sasa i karibu kuonekana. Mtu huyo aliyetangulia kutajwa mwenye uwezo ndiye tumaini letu. Yeye ndiye Tumaini la wote ambao kwa unyofu wa moyo wanatamani kuingia kwenye taratibu mpya yenye haki.

2. Kulingana na Yeremia 14:8, 9, Yehova alikuwa nini kwa taifa la Israeli, walakini hali ilionekana kuwa namna gani?

2 Sasa, katikati ya giza linaloongezeka ulimwenguni pote, ndio wakati unaofaa kumwendea huyu aliye Tumaini la pekee, kama vile nabii Yeremia alivyofanya wakati mambo hayakuonyekana kuwa maangavu katika taifa lake mwenyewe. Katika kilio chake kwa ajili ya msaada, Yeremia alisema hivi: “Wewe uliye tumaini la Israeli, wewe uliye Mwokozi wake wakati wa taabu, kwa nini wewe umekuwa kama mtu akaaye katika nchi, hali ya mgeni, na kama mtu mwenye kusafiri, ageukaye upande ili kukaa usiku mmoja tu? Kwa nini wewe umekuwa kama mtu aliyesituka, kama shujaa asiyeweza kuokoa? lakini wewe, [Yehova], u katikati yetu, nasi tunaitwa kwa jina lako; usituache.”​—Yer. 14:8, 9.

3. Kulingana na Yeremia 14:22, kwa nini kuna sababu nzuri kwetu tumwendee Yehova kama Tumaini letu la pekee?

3 Kuna sababu nzuri ya kumfanya Mungu uyu huyu Tumaini letu leo. Sababu gani yeye, wala si kitu kingine? Sababu yeye ndiye Muumba na ndiye anayeongoza nguvu zote za asili na utendaji juu ya dunia yetu na ujirani wake. Ni kama vile Yeremia anavyotaja anapozungumza na Mungu na kusema hivi: “Je! katika vitu vya ubatili vya mataifa, kiko kitu kiwezacho kuleta mvua? je! mbingu [ambazo wanajimu wanategemea] zaweza kutoa manyunyu? Je! si wewe, Ee [Yehova], Mungu wetu? kwa sababu hiyo tutakungoja; kwa kuwa wewe umevifanya vitu hivi vyote.”​—Yer. 14:22.

4. Kwa kuwa jina la Mungu lilikuwa likiitwa juu ya taifa la Israeli, mambo yaliyotokeza maulizo ya Yeremia yalionekana kuwa namna gani?

4 Watu wa Israeli ya kale walipata kuwa na jina la Mungu likiitwa juu yao, na kwa hiyo twapaswa kuwazia kwamba kuwapo kwake kwa kimungu kulikuwa nao. Sababu gani, basi, alikuwa amekuwa kama asiyekuwa “tumaini la Israeli,” kama mgeni ambaye alikuwa akikaa kati yao kwa muda tu, au kama msafiri ambaye alikuwa akipitia nchini mwao tu, ambaye siku ya leo alikuwako na kisha kesho hakuwako? Sababu gani alikuwa amekuwa kama mtu mwenye wasiwasi kwa ajili ya tatizo lenye kumwelekea, yeye akiwa hawezi kukabiliana nalo? Au kama shujaa ambaye hata hivyo hawezi kusaidia watu wenye kuhitaji kuokolewa kutokana na matokeo ya mwendo wao wenyewe wa kutenda? Basi, Yehova alimtajia Yeremia sababu gani?

5. Yehova alitoa sababu gani za kuacha kwake Israeli, na kwa sababu gani katika kufananisha huku alitaja Mkushi na chui?

5 Sababu ya shida ya Waisraeli haikuwa ya ki-juu-juu. Kupuza kwao agano na Mfanya-mvua Yehova kulikuwa kumeiingia ndani sana, vilevile kuchukizwa kwao na jina lake na kuchanganya ibada yake safi na dini ya mataifa ya kipagani yenye kuwazunguka. Basi, si jambo la ajabu kwamba waliambiwa hivi: “Je! Mkushi [Mwethiopia au Mnubi] aweza kuibadili ngozi yake, au chui madoa-doa yake? Kama aweza ndipo na ninyi mwaweza kutenda mema, ninyi mliozoea kutenda mabaya. Kwa sababu hiyo nitawatawanya, kama makapi yapitayo, kwa upepo wa jangwani. Hiyo ndiyo kura yako, fungu lako ulilopimiwa na mimi, asema [Yehova]; kwa kuwa umenisahau, na kuutumainia uongo. . . . uzinifu wako, na ubembe wako, na uasherati wa ukahaba wako, juu ya milima katika mashamba. Ole wako, Ee Yerusalemu! hutaki kutakaswa; mambo hayo yataendelea hata lini?”​—Yer. 13:23-27.

6. Usemi huo wa mambo ya hakika unaonyesha nini kwa habari ya mambo kati ya Yehova na Israeli na vilevile Jumuiya ya Wakristo?

6 Je! usemi huo wa jambo hakika unaonyesha kwamba Yehova alikuwa na kesi na Israeli? Je! unaonyesha vilevile kwamba ana kesi na Jumuiya ya Wakristo, ambayo hudai kuwa watu wa Mungu wa Biblia Takatifu? Bila shaka Ndiyo! Kwa hiyo, anasema kwamba kwa wakati wake ataisuluhisha kesi hii, kwa kuwa ndiye Hakimu Mkuu.

7. Kwa kupatana na Yeremia 17:1-4, kumbukumbu la Jumuiya ya Wakristo la uasi na uulimwengu limeandikwa kwa kadiri kubwa namna gani, nayo ni matokeo gani yatakayofuata?

7 Kwa sababu ya dai lake kuwa ya Kikristo, Jumuiya ya Wakristo yapaswa kuwa mfano mzuri kwa ulimwengu wote. Hata hivyo, imejifanyia kumbukumbu la uasi wa kidini na uulimwengu usiofutika. Kumbukumbu lake ni kama lile la Yerusalemu wa kale na nchi ya Yuda:

“Dhambi ya Yuda imeandikwa kwa kalamu ya chuma, na kwa ncha ya almasi; imechorwa katika kibao cha moyo wao, na katika pembe za madhabahu [ya ibada ya uongo] zenu; na wakati huo watoto wao wazikumbuka madhahu zao, na maashera [ya ibada ya sanamu] yao, karibu na miti yenye majani mabichi juu ya milima mirefu. Ee mlima wangu wa uwandani, nitatoa mali zako na hazina zako zote ziwe nyara [kwa wafikilizaji wangu wa hukumu], na mahali pako palipoinuka, kwa sababu ya dhambi, katika mipaka yako yote. Nawe, naam, wewe nafsi yako, utaachana na urithi wako niliyokupa [katika Nchi ya Ahadi]; nami nitakulazimisha kuwatumikia adui zako katika nchi usiyoijua [yaani, Babeli]; maana umewasha moto katika hasira yangu, utakaowaka milele.”​—Yer. 17:l-4.

JUMUIYA YA WAKRISTO YENYE UNAFIKI HAITATETEWA

8, 9. Ijapokuwa Jumuiya ya Wakristo inalichukua jina la Kristo, sababu gani asingeweza kuitetea kama vile kwa habari ya Israeli ya kale?

8 Jumuiya ya Wakristo hujivunia jina la Kristo. Walakini je! ataitetea taratibu hiyo ya kidini ambayo imedumu katika kuchanganya mafundisho ya Biblia na dini ya kipagani kwa zaidi ya karne 16? Sivyo, hata kidogo, kwa kuwa yeye anapatana kabisa na Baba yake wa Kimbinguni Yehova Mungu. Yeye alisema: “Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 5:30) Karne sita kabla ya Kristo, katika siku za Yeremia, Yehova alisema hivi kwa kutaja mfano wa kwanza wa Jumuiya ya Wakristo.

9 “Hata wangesimama mbele zangu, Musa na Samweli, moyo wangu usingewaelekea watu hawa [Israeli]; [ningewatupa], watoke mbele za macho yangu, wakaende zao.”​—Yer. 51:1.

10. Sababu gani inaelekea kwamba kutetewa na Musa na Samweli kungekuwa na matokeo kwa Mungu, walakini sasa ni nini yaliyokuwa maoni ya Mungu kuelekea Israeli isiyotubu?

10 Musa ambaye alikuwa ametumiwa kuzitoa Amri Kumi kwa Israeli, alikuwa amewaombea kwa matokeo. Kwa habari ya Samweli wa karne nne baadaye, alianzisha mfuatano wa pekee wa manabii ambao ulitia ndani Yeremia na ambao uliendelea mpaka kwa nabii Malaki. (Matendo 3:22-24) Vilevile Samweli aliliombea taifa la Israeli, sana sana baada ya wao kuomba mfalme wa kibinadamu mwenye kuonekana. Walakini sasa, zaidi ya karne nne baada ya Samweli, hata yeye wala Musa wasingalisikilizwa na Yehova ikiwa wangewatetea. Kwa hiyo ipotelee mbali Israeli isiyotubu!

11. Waisraeli wasiotubu wangetoka mbele za uso wa Yehova wakakabiliane na vitu gani vyenye kuleta kifo?

11 Ipotelee mbali wapi? Mtu anayeihurumia Jumuiya ya Wakristo huenda akauliza. Tunao wonyesho wa kiunabii wa mahali penyewe katika yale ambayo Yehova alimwambia Yeremia: “Kisha itakuwa, hapo watakapokuambia, Tutoke, tuende wapi? utawaambia, [Yehova] asema hivi, Walioandikiwa kufa [kwa tauni], watakwenda kufa [kwa tauni]; au kufa kwa upanga, watakufa kwa upanga; au kufa kwa njaa, watakufa kwa njaa, au kutekwa nyara, watakuwa mateka. Nami nitaamrisha juu yao namna nne [au, jamaa nne], asema [Yehova]; [1] upanga uue, na [2] mbwa wararue, na [3] ndege wa angani, na [4] wanyama wakali wa nchi, wale na kuangamiza. Nami nitawafanya kuwa kitu cha kutisha katika falme zote za duniani, kwa sababu ya Manase, mwana wa Hezekia, mfalme wa Yuda, kwa sababu ya mambo aliyoyatenda katika Yerusalemu. Maana ni nani atakayekuhurumia, Ee Yerusalemu? au ni nani atakayekulilia? au ni nani atakayegeuka upande ili kuuliza habari za hali yako? Umenikataa mimi asema [Yehova], umerudi nyuma [kutoka kwangu].”​—Yer. 15:2-6; pia 16:4.

12. Mitajo kama iyo hiyo ya vitu vyenye kuleta kifo ilitajwa na nani na kwa nani kwa habari ya Yerusalemu wa karne ya kwanza na taratibu ya mambo iliyopo?

12 Tauni yenye kuua (au, maradhi ya kuambukiza), upanga (au, vita), njaa (au, upungufu wa chakula) na kutekwa! Maneno haya yaliyosemwa kwa Yeremia kuhusiana na Yerusalemu wakati wake wa mwisho (647-607 K.W.K.) katika siku zake ni maneno vilevile yaliyotumiwa na Yesu Kristo katika unabii wake kuhusu “wakati wa mwisho” wa Yerusalemu katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. (Mt. 24:3-7, 21, 22; Luka 21:10, 11, 20-24) Vilevile, katika unabii wake katika kitabu cha mwisho cha Biblia fikira zetu zinakazwa kwa mambo ayo hayo kwa kutumia mifano, kutia na wanyama mwitu wa kondeni. (Ufu. 6:1-8) Unabii huo wa mwisho unauchukua utimizo wa matabiri hayo yenye msiba mpaka muda mrefu sana baada ya kuandikwa kwa Ufunuo katika mwaka 96 W.K. na kuendelea. (Dan. 12:4) Kwa hiyo, unabii huo katika utimizo wake wa kumalizia, unaihusu taratibu mbovu ya mambo iliyopo iliyohukumiwa maangamizi, kutia na Jumuiya ya Wakristo iliyoasi.

13. Ni tangu wakati gani tumekuwa na mambo kama ayo hayo kwa kadiri yenye kutisha?

13 Je! ye yote wetu apaswa kupofusha macho yake asione uhakika wa kwamba tangu mwisho wa Majira ya Mataifa katika mwaka 1914 tumekuwa na vita (upanga), njaa, maradhi ya kuambukiza, vilevile matetemeko ya dunia kwa kadiri kubwa kutisha? Imekuwa kama vile tu ilivyotabiriwa, kama ilivyoonyeshwa kwa mfano kwa habari ya Yerusalemu wa siku za Yeremia na Yerusalemu wa siku za mitume wa Yesu.

14. Kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo haikuepuka kupatwa na mambo hayo yenye kuleta msiba?

14 Jumuiya ya Wakristo, mfano wa kisasa wa Yerusalemu na Yuda zilizoasi, haijapata kuwa tofauti juu ya kupata mambo hayo yenye kuleta msiba. Sala za viongozi wake wa kidini hazijaifaa kitu. Sababu ya hili ni kama ile ile kwa habari ya Waisraeli katika siku za Yeremia: “Nimewaondolea watu hawa amani yangu, asema [Yehova], hata fadhili zangu na rehema zangu. Maana [Yehova] wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Mimi, mbele ya macho yenu, na katika siku zenu, nitaikomesha sauti ya furaha na sauti ya kicheko, mahali hapa; sauti ya bwana arusi, na sauti ya bibi arusi.”​—Yer. 16:5, 9.

WATAZAMIA AMANI KUMBE HAIFAI KITU!

15. Kwa habari ya Israeli katika siku za Yeremia kulikuwa kutumaini nini, na ni mahakikisho gani ambayo manabii wale wengine walikuwa wakiwapa Waisraeli?

15 Kwa Jumuiya ya Wakristo katika huu “wakati wa mwisho,” hali imekuwa kama vile tu ilivyokuwa kwa Waisraeli wakati wa siku zile Yeremia alipowatangazia ujumbe wa hukumu ya Yehova: “Tulitazamia amani, lakini hayakuja mema yo yote; tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika tu!” (Yer. 14:19) Hata hivyo, viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanadumu katika kupinga yale ambayo jamii ya Yeremia, jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” imekuwa ikitangaza kama onyo kwa watu wote. Hawa mashahidi watiwa mafuta wa Yehova wanakabiliana na hali ile ile kama Yeremia na ambayo aliisimulia, akisema: “Aa, [Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova]! tazama, manabii huwaambia, Hamtauona upanga [mkononi mwa mwuaji wa Yehova], wala hamtakuwa na njaa; bali nitawapa amani iliyo thabiti mahali hapa.”​—Yer. 14:13; Mt. 24:45-47.

16. Ni maneno na matendo gani ya viongozi wa kidini yanayowafanya washiriki wa kanisa wa Jumuiya ya Wakristo wasisikilize onyo linalotolewa na Mashahidi wa Yehova?

16 Kutabiri huko kwamba hakuna maelekeo ya kupata msiba kutoka kwa Mungu kunakusudiwa kutulize woga wa watu. Kunatokeza matumaini ya uongo mioyoni mwa washiriki wa kanisa wa Jumuiya ya Wakristo. Kunawafanya wasijihadhari kuhusiana na kutokea kwa ghafula kwa ‘dhiki kuu.’ Kama matokeo, kama vile mwivi usiku itakuja juu yao, nao watapata hasara ya milele. Kwa sababu viongozi wa kidini wanaiharibia sifa jamii ya Yeremia na kuudharau ujumbe wao unaotolewa kwa wakati wake, hii inawafanya washiriki wake wa kanisa wenye kuridhika na nafsi zao kuwa wenye kupuza hata zaidi lile onyo ambalo Yehova anatoa kupitia kwa mashahidi wake.

17, 18. (a) Kwa ajili ya viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo, ni nini kimekuwa kama hali ya kudumu, tena isiyoponyeka kwa jamii ya Yeremia? (b) Ni mwendo gani ambao jamii ya Yeremia imepaswa kuendeleza kwa habari ya urafiki na viongozi wa kidini?

17 Ili kuusisitiza zaidi wonyesho uliofanywa na mahakikisho yao ya amani, viongozi wa kidini wanawatesa walio wa jamii ya Yeremia na wenye kuwaunga mkono. Wanayachochea mamlaka ya kisiasa juu yao. Mateso na kusutwa ambako jamii ya Yeremia inaendelea kuvumilia yamekuwa kama jambo la kudumu pamoja nao, kama maradhi kwao yasiyoponyeka kwa ruhusa ya Yehova, kana kwamba anawakana. Hawawezi kuridhiana na jamii ya viongozi wa kidini na kuingia kwenye urafiki nao. Yehova ndiye Mtu wa kutolea kesi yao, na wanafurahia msaada wake, kama vile Yeremia alivyosema:

18 “Ee [Yehova], unajua wewe; unikumbuke, unijilie, ukanilipie kisasi juu yao wanaoniudhi; usiniondoe kwa uvumilivu wako; ujue ya kuwa ni kwa ajili yako nilivyopatikana na mashutumu. Maneno yako yalionekana, nami nikayala; na maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina lako, Ee [Yehova] Mungu wa majeshi. Sikuketi katika mkutano wao wanaojifurahisha, wala sikufurahi [na wafanya mizaha wale wanaofikiri amani imehakikishwa]; naliketi peke yangu kwa sababu ya mkono wako; kwa maana umenijaza ghadhabu [uchungu, LXX; huzuni, JP].”​—Yer. 15:15-17, UV; Septuagint Version [LXX], chapa ya Bagster, pia Charles Thomson; The Jewish Publication Society of America, chapa ya 1973.

19. Yajapokuwa mateso juu ya jamii ya Yeremia, sababu gani wanaoteswa waweza kushangilia na kujivuna?

19 Mateso yanayoendelea kuipata jamii ya Yeremia kama maradhi ya kudumu yenyewe hayapendezi. (Yer. 15:18) Walakini wenye kuteswa wanaweza kushangilia katika Neno la Yehova, Maandiko Matakatifu, yaliyohifadhiwa kwa ajili ya kutufariji. (Rum. 15:4) Twaweza kufurahi kwa sababu ya kupata katika Maandiko hayo maneno ya unabii yanayoeleza nyakati zetu ngumu na yanayotupa tumaini jangavu la taratibu mpya baada ya Har–Magedoni. Kwa sababu hii twaweza kujivuna katika Yehova.​—Yer. 9:23, 24.

20, 21. (a) Sababu gani leo moyo wa kibinadamu umejionyesha kuwa “mdanganyifu,” ndiyo, ‘hatari sana’? (b) Kulingana na Yeremia 17:5-8, ni mwendo gani wa kutenda unaoongoza kwenye laana ya Mungu na ni mwendo gani unaoongoza kwenye baraka yake?

20 Katika wakati huu wa ‘mwisho wa taratibu ya mambo,’ wakati uvunjaji wa sheria unapoongezeka naye Yehova akingojea wakati wake wa kuadhibu uovu wenye kuenea, moyo wa kibinadamu umejionyesha kuwa “mdanganyifu,” ndiyo, ‘hatari sana,’ kadiri jamii ya kibinadamu inavyojipata imekazwa sana. Iwapo tutajaribu kutosheleza moyo katika njia zinazotofautiana na shauri na kanuni za haki za Mungu, utatuletea hukumu yake kali. (Yer. 17:9-11) Chini ya mikazo ya leo yenye kuelekeza kuchukua mwendo mbaya wa kutenda, mioyo yetu na isitudanganye na kutusukuma tufanye mambo yasiyo ya Kimaandiko, mambo ya kipumbavu. Kumbuka: mwendo wa kutenda tunaochukua utaamua kama twastahili kupata laana au baraka. Yehova ameweka mbele mwendo utakaoongoza kwenye laana yake na mwendo utakaongoza kwenye baraka yake, akisema hivi:

21 “Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake, Na moyoni mwake amemwacha [Yehova]. Maana anakuwa kama fukara nyikani, Hataona yatakapotokea mema; Bali atakaa jangwani palipo ukame, Katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu. Amebarikikwa mtu yule anayemtegemea [Yehova], Ambaye [Yehova] ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, Uenezao mizizi yake karibu na mto; Hautaona hofu wakati wa hari ujapo, Bali jani lake litakuwa bichi; Wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, Wala hautaacha kuzaa matunda.”​—Yer. 17:5-8.

22. Waisraeli wa siku za Yeremia walionyeshaje kwamba walimfanya ‘mwanadamu kuwa kinga yao’?

22 Watu walio mashujaa wana maelekeo ya kutumaini mwanadamu wa kidunia na kumtegemea awaokoe. Si ajabu basi kwamba wanakuwa kama mti ulio peke yake katika jangwa kavu, tena lenye kujaa chumvi. Wamefanya kama Waisraeli wa siku za Yeremia: Wakati majeshi ya adui, yakinguruma kama simba, yalipowaogopesha Waisraeli hawa, hawakumwomba Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Waliwaendea wanadamu wenye ushujaa, wenye ujuzi wa vita vyenye kutumia jeuri, kwa msaada wa kijeshi. Kwa hiyo hawakumkaribia Yehova kusudi wanywe maji ya wokovu kutoka kwake akiwa Chanzo cha ukombozi. Mahali pake, walikimbilia Misri kunywa maji ya wokovu kutoka kwa Mto Nailo. Au walikimbilia Ashuru kunywa maji ya wokovu kutoka kwa Mto Frati, wakati Ashuru ilipokuwa ikitawala.

23. Waisraeli ‘walijichimbiaje mabirika yaliyovuja maji,’ nayo matokeo yakawa nini?

23 Kwa njia hiyo, kusema kwa njia ya mfano, Waisraeli wasio na imani ‘walijichimbia mabirika, mabirika yavujayo, yasiyoweza kuweka maji.’ Walimwacha Yehova, “chemchemi ya maji ya uzima.” Na kama matokeo, hakuna wokovu uliotoka kwake. Kwa kukatiza tamaa, mamlaka za ulimwengu za Misri na Ashuru zenye nguvu nyingi za kijeshi hazikujaza “mabirika yavujayo” ya Waisraeli kwa maji yenye kuwaokoa kutokana na adui zao wa kisiasa. Kwa hiyo hawakupata maji yenye kutoa uhai kutoka Shihori, Mto Nailo au kutoka Mto Frati uliokuwa chini ya utawala wa Ashuru. Kwa ajili ya kumwacha Yehova akiwa Chanzo cha wokovu, Waisraeli wenye kuasi walikuja chini ya laana yenye kukausha nafsi.​—Yer. 2:13-18.

24. Hata hivyo, ni wapi, ambapo jamii ya Yeremia na ‘‘mkutano mkubwa” wanaelekeza heshima na tumaini lao, na wanamwabudu wapi chanzo cha kweli cha maji ya uhai?

24 Tofauti na Waisraeli hao, wale walio wa jamii ya Yeremia leo wamemfanya Yehova kuwa Tumaini lao. Wanakiheshimu kiti chake cha enzi kuu ya ulimwengu wote. Wanamwabudu yeye kama Mungu wao katika hekalu lake la kiroho au mahali patakatifu. Wanamtumainia yeye, wala si mwanadamu wala mamlaka ya ulimwengu ya kibinadamu yenye silaha za nuklia (za atomiki). Wauongoza “mkutano mkubwa” leo katika kuweka tumaini lao na uhakika wao katika Yehova. Wakijiepusha na njia ya Jumuiya ya Wakristo iliyoasi, kwa hekima wanasema hivi: “[Kuna] kiti cha enzi, cha utukufu, kilichowekwa juu tangu mwanzo, ndicho mahali patakatifu petu. Ee [Yehova], tumaini la Israeli, wote wakuachao watatahayarika [kukatishwa tamaa]. Wao watakaojitenga nami wataandikwa katika mchanga, kwa sababu wamemwacha [Yehova], kisima cha maji yaliyo hai.”​—Yer. 17:12, 13.

25. Basi, tutaingia kwenye Taratibu Mpya chini ya Yesu aliye Masihi, kwa kufuata mwendo gani?

25 Na tuyaache, basi, “mabirika yavujayo” yaliyofanywa na wanadamu yasiyo na maji ya kuokoa kutokana na msiba wa ulimwengu. Na tumgeukie Yehova. Yeye aweza kutulinda wakati wa “dhiki kubwa” na kutuingiza salama kwenye taratibu yake mpya chini ya Yesu aliye Masihi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki