Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Kama mwanamume (au, mwanamke) angekimbia na mwenzi wa mtu mwingine, je! angeweza kusamehewa na kukubaliwa tena kwenye kundi la Kikristo?
Jambo hilo linatokea mara nyingi kati ya wale wasiojaribu kuishi kulingana na kanuni za Biblia. Kwa kulinganisha na hilo, si jambo linalotokea mara nyingi kati ya wale wanaoshirikiana na watu wa Yehova, kwa sababu hiyo linapotokea linatisha sana. Hata hivyo, hakuna haja ya kufikiri kwamba kisa kama hicho kinapaswa kushughulikiwa kulingana na amri ya kibinadamu. Kama zilivyo dhambi nyinginezo, kabla ya mtu wa namna hiyo kukubaliwa na Mungu na watu wake, mtenda dhambi huyo angepaswa kutubu na kuonyesha waziwazi matunda ya toba.
Kushughulika kwa Mungu na Waisraeli kunaonyesha msamaha wake, nyakati nyingine, akisamehe hata dhambi ya kutisha yenye kuendelea. (Kum. 4:30; Isa. 55:7; 57:16-18; Zek. 1:3, 4) Yesu alitaja juu ya “furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.” Kisha akaonyesha jambo hilo kwa njia ya mfano akitumia hadithi ya mwana mpotovu aliyeponda fedha zake kwa maisha ya uasherati akiishi pamoja na malaya. Fahamu zilipomrudia mwana huyo, alirudi na kutafuta msamaha kwa ajili ya kutenda dhambi juu ya mbingu na babaye, baba huyo alimsamehe kwa shauku.—Luka 15:1-7, 11-24.
Hata hivyo, Biblia inaonyesha vilevile kwamba Mkristo anayetenda dhambi asitubu anapaswa kufukuzwa kutoka kwa kundi ili kuliendeleza liwe safi kiroho. (1 Kor. 5:1-5, 11-13) Jambo hilo lilimpata mwanamume mmoja katika Korintho ambaye kwa waziwazi aliishi maisha ya uasherati. Maandiko yanaonyesha kwamba ili akubaliwe tena katika kundi mwanamume wa namna hiyo anapaswa kutubu, aukatae mwendo wake wa uasherati, ageuke na kuzaa matunda yanayostahili toba. Kwa wazi alifanya hivyo baadaye. Katika Wakorintho wa Pili, barua inayodhaniwa kuwa iliandikwa muda unaopungua mwaka mmoja baadaye, mtume Paulo alisihi kundi limsamehe mkosaji, bila shaka akizungumza juu ya mwanamume yule aliyetengwa ambaye kwa lazima alikuwa ametubu.—2 Kor. 2:5-10; Mt. 3:7, 8; Matendo 26:20.
Mpango huo wa kutenga na ushirika Kimaandiko unatumiwa na makundi ya shahidi wa Yehova leo, pia. Na kwa kulingana na mfano huo, hakuna kipindi cha wakati kilichowekwa kabla ya mtu kurudishwa; kunategemea toba ya kweli, ambayo huenda hata ikachukua miaka mingi.
Katika kisa hicho kisichokuwa cha kawaida ambacho kimetajwa katika swali, kutunga hila na udanganyaji huenda vikawa vilionyeshwa. Kwa mfano, mwanamume (pengine ameoa) anapumbazwa na mke wa mtu mengine. Hapo paweza kuwa kucheza-cheza kwa siri, kukutana kisiri na wonyesho usiofunuliwa bado wa tamaa. Uongo na udanganyifu huenda vikatumiwa ili kuwaficha wengine jambo hilo, sana sana mwenzi au wenzi wasiojua kitu. Baada ya muda watu hao wanaweza kutoroka, na baada ya talaka isiyo ya kimaandiko wakaoana. Huenda wakawa walikuwa wamefikiria juu ya matokeo yake, wakitambua kwamba kutengwa na ushiriki kutafuata. Walakini wanafikiri kwamba “pengine baada ya mwaka mmoja au hivi” wanaweza kudai kutubu na kurudishwa, hivyo mambo yawe kama walivyoyataka. Hata hivyo, ni kosa zito kutumia vibaya rehema ya kimungu. Wagalatia 6:7 linahakikisha hivi: “Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.” Kwamba Yehova hakubali uasherati inaonekana katika maandiko mengi nalo jambo hilo halipaswi kusahauliwa na wale wanaoendeleza tamaa mbaya.—Linganisha Ufunuo 21:8; 22:15.
Iwapo baada ya wakati fulani mtu huyo aliyetengwa na ushirika anawaendea wazee wa kiroho wanaowakilisha kundi naye aombe arudishwe, mambo yaliyotokea, pamoja na maoni ya mkosaji, yanapaswa kufikiriwa. Kuhusiana na umoja wa imani, hauongozwi na ‘hila ya watu, kwa ujanja, ukizifuata njia za udanganyifu.’ (Efe. 4:13, 14) Hiyo ni kweli katika kuepuka kosa la mafundisho na ndiyo ilivyo katika kuepuka kurudisha kundini watu ambao kwa kukusudia wametumia hila na ujanja kutimiza maovu.—Linganisha 2 Wakorintho 11:13; Zaburi 101:7; 119:118.
Halmashauri ya wazee inayoshughulikia ombi la kurudishwa inapaswa kufikiria tofauti kati ya mtu anayeangukia dhambi wakati wa udhaifu na mtu anayetunga hila afanye dhambi. Twaweza kukumbuka kwamba Mungu alimwonyesha Petro rehema baada ya kumkana Yesu mara tatu; hata hivyo Mungu aliua Anania na Safira, ambao walitunga hila mioyoni mwao juu ya namna wangetenda udanganyifu wao.—Matendo 5:1-11.
Kwa hiyo wazee wanahitaji kujihadhari sana katika visa ambavyo kujifanya kwa unafiki na kutunga hila vinahusika. Huenda mtu akadai kwamba anahuzunika na kutubu, lakini kama angekuwa mahali pale pale alipoanzia, “je! angerudia jambo ilo hilo tena”? Je! angemwacha mwenzi wake aende kwa mwingine? Bila shaka, sasa ameingia katika ndoa mpya na hivyo hawezi kuikomesha tu naye arudie mambo yaliyokuwa kabla; ndoa ile ya kwanza ilikoma wakati wa talaka, uzinzi na kuoa tena. (Mt. 19:9) Lakini, je! anaonyesha toba ya kweli, “amepondwa” na kukatwa moyoni? (Isa. 57:15, NW) Je! anachukizwa na dhambi aliyofanya, wala si huzuni tu kwa kuwa ametengwa na ushirika naye hawezi kufurahia ushirika wa Kikristo? Je! kwa muda wenye kutosha, ambao haukuamuliwa kimbele, amezaa matunda yanayostahili toba? Wazee wangepaswa kusadikishwa, bila shaka, kwamba kuna toba ya kweli. Iwapo kwa unyofu hawana uhakika wa jambo hilo, huenda wakaamua kungojea na kukutana tena kurudia jambo hilo baada ya ushuhuda zaidi kukusanywa.
Wazee wanapaswa kuona sana daraka lao la kulinda kundi, hata hivyo wakati wote wakikumbuka rehema ya Mungu na tamaa yake ya kutaka watu wapate uzima. (Rum. 2:4) Wanatambua kwamba hawana uwezo unaozidi wa kibinadamu wa kujua mioyo na nia za watu kwa ukamilifu, kama vile alivyo Yehova, ambaye mkosaji atamtolea hesabu. (Ebr. 4:13) Kwa hiyo watajitahidi kuongoza kufikiri kwao na kuamua kwao kulingana na Neno la Mungu na yale ambayo wanaweza kuamua juu ya maoni na hali ya moyo wa mtu aliyetengwa na ushirika. Iwapo baada ya muda fulani halmashauri ya wazee inakata kauli kwamba mkosaji huyo ametubu kweli kweli na kufanya bidii kusafisha moyo wake, kumrudisha kunafaa, kama ilivyokuwa kwa mwanamume yule aliyekuwa Korintho. (Yak. 4:8) Walakini hakuna wakati uliowekewa jambo hilo. Na hata ingawa huenda kundi likamrudisha mkosaji huyo, inapaswa kukumbukwa kwamba bado atalazimika kusimama “mbele za Mungu” atoe hesabu.—Rum. 14:10-12.