Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 2/1 kur. 3-8
  • Aliwapenda Mpaka Mwisho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Aliwapenda Mpaka Mwisho
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Fanyeni hivi”—Kwa sababu gani?
  • Kujichunguza
  • Ukumbusho (Mlo wa Jioni wa Bwana)
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Nisani 14—Siku ya Kukumbukwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Mlo wa Jioni wa Bwana Huadhimishwaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • “Nitamfufua Katika Siku ya Mwisho”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 2/1 kur. 3-8

Aliwapenda Mpaka Mwisho

MTUME Yohana alifurahia uhusiano mzuri sana pamoja na Yesu. Ndiye “ambaye Yesu alikuwa anampenda sana,” kama inavyotajwa katika Injili yake. Wakati wa “chakula cha jioni” cha mwisho, Yohana alikaa karibu na Yesu, naye ndiye ambaye Yesu, alipokuwa juu ya mti wa mateso, alimpa pendeleo la pekee la kumchukua nyumbani kwake Mariamu, mama ya Yesu, awe akimtunza kana kwamba alikuwa mama yake mwenyewe.—Yohana 13:23; 19:25-27; 20:2; 21:20.

Upendo huu uliokuwa kati ya Yesu na Yohana haukutokea kwa sababu ya kuvutwa na sura ya nje. Wala Yohana hakuwa mtu mwenye kuongozwa na maono ya moyoni kama ambavyo wengine wamekata kauli, ijapokuwa ni kweli kwamba yeye alisema mengi juu ya upendo. Kwa kweli, upendo kama wa Mungu ulio wa kweli na wa unyofu ni sifa yenye nguvu na safi, inayofungamana karibu karibu na ushikamanifu. Katika maandishi yake yote, Yohana alionyesha namna alivyowapenda na kuwa mshikamanifu kwa Yesu Kristo na Yehova. Yesu, ‘aliyejua yaliyomo ndani ya mwanadamu,’ alithamini jambo hilo sana sana, na kwa hiyo wakawa na upendo mkubwa sana kati yao.—Yohana 2:25.

Tunapoifikiria jioni hiyo ya mwisho aliyokuwa nayo Yesu pamoja na wafuasi wake, ni vigumu kwetu kujiweka katika hali yao. Hakuna hata mmoja wao, kutia na Yohana mwenyewe, aliyekuwa na wazo lo lote la ambayo yangempata Yesu usiku huo. Ulipofika wakati wa Yesu kusema, “Ninyi nyote mtachukizwa kwa ajili yangu usiku huu,” naye Petro akakataa kwa nguvu kwamba hakuna jambo kama hilo ambalo lingetukia kwa upande wake, na zaidi sana kuhusiana na yeye kukana Bwana yake, ndipo “wanafunzi wote wakasema vivyo hivyo.” (Mt. 16:21-23; 26:31-35) Lazima uwe ulikuwa mshangao mkubwa kama nini wakati mambo yalipotukia sawasawa kama yalivyotabiriwa! Kwao, chakula hicho cha jioni kilikuwa kimeanza kama chakula kingine zaidi cha kukumbuka kile chakula cha jioni cha kwanza cha Sikukuu ya Kupitwa. Walakini, kwa Yesu, kilikuwa na maana kubwa zaidi, kama inavyoonyeshwa na yote ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake na aliyosema kwa Baba yake katika sala, na hasa wakati, “baada ya kula chakula cha jioni,” alipoanzisha ukumbusho wa kifo chake mwenyewe. Twaweza kujifunza mengi juu ya jambo hilo kwa kusoma Injili ya Yohana sura 13 mpaka 17.

Masimulizi hayo yenye mambo mengi sana yaliandikwa yapata miaka 65 baada ya kutukia kwa matukio hayo, na bila shaka jambo hilo lathibitisha maneno ya Yesu kuhusiana na ‘msaidizi, roho takatifu’: ‘[Huyo] Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.’ (Yohana 14:26) Ndiyo, Yohana aliyependwa sana alikuwa amefundishwa vizuri sana, nasi twaweza kuwazia kina cha maono yake na kuthamini alipoandika hivi kuhusu Yesu:

“[Basi,] Yesu alijua kwamba saa yake ya kuondoka ulimwenguni na kwenda kwa Baba ilikuwa imefika. Alikuwa amewapenda daima watu wake walioko duniani; naam, aliwapenda mpaka mwisho!”—Yohana 13:1, HNWW.

Lazima Yohana awe alijikumbusha mara nyingi maajabu ya upendo huo mshikamanifu usioshindwa ulioonyeshwa na Yesu, ukionyesha wingi wa fadhili zisizostahilika. Wanafunzi hao walikuwa na hakika sana juu yao wenyewe; hata hivyo walikuwa dhaifu nao walishindwa wakati walipopatwa na jaribu. Si kwamba walikuwa na moyo mbaya. Ulikuwa tu udhaifu wa kibinadamu, ambao Shetani alitumia kwa faida yake, walakini kwa wakati huo tu.—Luka 22:32.

“Fanyeni hivi”—Kwa sababu gani?

Sasa tunakaribia tarehe ya kila mwaka ya kifo cha Yesu Nisani 14, 33 W.K., pamoja na mwadhimisho wa chakula cha “Bwana cha jioni.” Mwadhimisho huo utakuwa Jumapili, Aprili 19, 1981, baada ya jua kutua, katika makundi yote ya Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, ni mawazo gani tunayopaswa kuwa nayo akilini mwetu? Ni kwa sababu gani Yesu, baada ya kuwapa wanafunzi wake kwanza mkate kisha kikombe, akarudia maneno haya: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu”?—1 Kor. 11:20, 23-26.

Kwamba Yesu mwenyewe alijua yote yaliyomaanishwa na maneno hayo inaonyeshwa na yale aliyosema siku chache zilizotangulia, wakati alipotoa mfano huu rahisi, lakini wenye nguvu, akijifananisha na mbegu ya ngano: “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi.” (Yohana 12:24) Maneno yake yanayofuata yanaonyesha kwamba alikuwa akitazamia sana si yale mateso yenye kutaabisha tu pamoja na aibu iliyokamatana na kifo chake penye mti wa mateso bali vilevile na matokeo mazuri sana na ya muda mrefu ya mfano huo bora wa upendo wake wa kujinyima. Katika maneno hayo Yesu alionyesha tamaa yake ya moyoni ya kulitukuza jina la Baba yake, na katika pindi iyo hiyo Yehova akaitikia kusihi kwa Mwanawe, kwa kuwa ikaja sauti kutoka mbinguni, Nimelitukuza, nami nitalitukuza tena.”—Yohana 12:25-33.

Yesu aliweka mfano wa upendo wa namna ile ile aliokuwa nao Baba yake, kama alivyotangulia kutaja katika huduma yake: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Ndiyo, yeye ndiye aliyekuwa “mwanadamu, Kristo Yesu, ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote.” ‘Aliionja mauti kwa ajili ya kila mtu.’ (Yohana 3:16; 1 Tim. 2:4-6, NW; Ebr. 2:9) Kwa kweli yeye alichukua mahali pa mwenye dhambi, kama inavyoelezwa vizuri sana katika Isaya 53:4-7, 10, naye mtume Paulo katika Wafilipi 2:5-11, anathibitisha namna hicho ‘kifo penye [mti wa mateso]’ kilivyowafaidi wanadamu katika njia yenye utukufu sana. Lingekuwa jambo zuri kwetu sisi sote kuyasoma maandiko hayo kwa ukamilifu, na kuyatafakari, kipindi cha Ukumbusho kikaribiapo.

Pamoja na matokeo ya muda mrefu ambayo tumezungumza hivi sasa, kulikuwako na matokeo ya maana ya wakati uo huo ambayo sana sana ndiyo aliyokuwa akifikiria Yesu alipokuwa akianzisha ukumbusho wa kifo chake. Ni kweli kwamba katika pindi moja alisema juu yake mwenyewe kuwa “chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni,” na kisha akasema: “Na [kwa kweli] chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” (Yohana 6:51) Walakini, baada ya kukatizwa na Wayahudi fulani waliokuwa wakisikiliza, Yesu aliendelea kuzungumza habari iyo hiyo, akiwa na maana kubwa kwa wale waliohusika. Alikuwa amekwisha kutaja juu ya kula “chakula” hicho cha mfano, walakini sasa aliendelea akasema hivi:

“Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. . . . Aulaye mwili wangu na kunywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake.” (Yohana 6:53-56)

Maneno ya kustaajabisha haya! Yaliwakwaza hata “wengi miongoni mwa wanafunzi wake . . . wasiandamane naye tena.” Ni nini yaliyo maelezo yake?—Yohana 6:60-66.

Yesu alijua kwamba ulimwengu wa wanadamu, unaotajwa katika maandiko yanayotangulia ungekuwa na nafasi ya kujifaidi na dhabihu ya ukombozi wakati wa ufalme wake, wakati ambapo kungekuwako na “mbingu mpya na nchi mpya,” na wakati ambapo “mauti haitakuwapo tena.” (Ufu. 21:1-4; Luka 23:42, 43, NW) Lakini alijua vilevile kwamba ilikuwa furaha ya Baba yake kwamba baadhi ya washiriki wa jamaa ya wanadamu wenye dhambi washiriki pamoja naye katika kiti cha enzi chake cha kimbinguni wakiwa kama wafalme na makuhani pamoja naye. (Luka 22:28-30; Ufu. 3:21; 20:6) Yeye alijua kwamba ijapokuwa yeye [“aliye] Kristo” ndiye kwa msingi aliyekuwa uzao wa Ibrahimu, hata hivyo, hao wengine wa kundi la Kikristo “katika [umoja na] Kristo Yesu,” walio washiriki wa “Israeli wa Mungu” wa kiroho, wangekuwa pia “uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.” (Gal. 3:16, 28, 29; 6:16) Kwa hakika huo ulikuwa wonyesho wa “fadhili zisizostahilika juu ya fadhili zisizostahilika.”—Yohana 1:16, NW.

Mitume 11 waaminifu waliokuwa pamoja na Yesu usiku huo, Nisani 14, ndio waliokuwa wa kwanza kualikwa waushiriki mkate huo usiotiwa chachu na kunywea kikombe hicho cha divai, ambavyo, kama alivyosema Yesu, vilifananisha mwili wake usio na dhambi na damu ya uhai wake. (1 Kor. 11:23-26) Wengine wangefuata ambao, kama vile alivyosema Yesu, “watakaoniamini kwa sababu ya neno lao.” (Yohana 17:20) Kwa habari ya waamini hao, angalia namna maneno “katika umoja na” yanavyorudiwa-rudiwa mara nyingi na ambayo yanatumiwa tu kuhusiana na Yehova na Kristo Yesu na wale wa kundi la Kikristo lililotiwa mafuta, kama inavyoonyeshwa katika Yohana 6:56; 10:38; 14:10, 11, 20; 15:4-7; 17:21-23, 26, tafsiri ya New World. Tafsiri ya Union Version ya Kiswahili hutumia maneno ‘ndani ya-.’

Washiriki wa kundi hilo wanatendewa kipekee, ingawaje si kwa sababu ya wema wo wote kwa upande wao. (Efe. 2:5; 1 Yohana 2:2) Wamezaliwa kwa roho ya Mungu kwa tumaini la kimbinguni, tumaini la kushiriki pamoja na Kristo katika ufufuo wake wa kimbinguni, mradi tu kwanza wanajihakikisha kuwa waaminifu, kama alivyosema Paulo, katika “kushiriki mateso yake, na kufanana naye katika kifo chake.” (Flp. 3:10, HNWW) Mwendo huo wa kujinyima unaanza wakati mtu anapochaguliwa na Mungu kuwa mshiriki wa kundi hilo la Kikristo, linalofanywa kuwa “mwili wa Kristo,” kama inavyoelezwa katika Mathayo 16:24 na 1 Wakorintho 12:12-27. Washiriki hao wanaingizwa katika lile “agano jipya,” lililohalalishwa kwa damu ya Kristo iliyomwagwa, nao wanashiriki huduma ya agano hilo.—1 Kor. 11:25; 2 Kor. 3:6; 4:1-7.

Kungaliko duniani baadhi ya wale walio “katika umoja na Kristo Yesu” na walio na ushuhuda wa roho ya Mungu wa kuwa ‘wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho na “warithi washirika pamoja na Kristo.” (Rum. 8:1, 14-17, NW) Watakumbuka sana akilini mwao kweli hizi zenye thamani sana watakapokuja pamoja kwa ajili ya “chakula cha Bwana cha jioni.” Hata hivyo, idadi kubwa ya Mashahidi wa Yehova watakaokutana jioni hiyo hawana tumaini hilo la kimbinguni. Wao wanajua kwamba si wa lile “kundi dogo,” bali wanajitambulisha wenyewe na ule “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” ambao Yesu alisema juu yake. (Luka 12:32; Yohana 10:16; Ufu. 7:9) Wao pia, wanaiamini damu ya Yesu iliyomwagwa. (Ufu. 7:14) Wao wana tumaini la ‘kuurithi Ufalme,’ kwa vile watajifurahisha baraka za uzima wa milele duniani, kama alivyoahidi Yesu katika Mathayo 25:31-40. Vilevile wanafurahia ushirika wa karibu pamoja na “ndugu” za Kristo wanaotajwa katika mfano huo. Wakilinganishwa na Waisraeli wa kiroho, ni “wageni,” nao wanathamini sana pendeleo la kushiriki daraka pamoja nao la kuzaa matunda ya Ufalme. (Isa. 56:6, 7; 61:5; Mt. 21:43) Baadhi yao hata wamekufa kwa sababu ya msimamo wao wa uaminifu kuhusiana na kweli na kwa kuutangaza ujumbe wa Ufalme kwa ujasiri. Walakini, ijapokuwa huenda wakafa kifo cha mfia-imani, wao hawafi kifo cha dhabihu kama kile cha Yesu pamoja na wale “warithi washirika pamoja na Kristo” katika ufalme wa kimbinguni. Wakitambua tofauti hii, wao hawashiriki kula mifano ya mkate usiotiwa chachu na kunywea kikombe cha divai ambavyo huonyesha si kule kupokea faida za kifo cha Kristo tu, bali pia kushiriki pamoja naye katika mwendo ule ule wa kujinyima.

Kujichunguza

Ijapokuwa idadi kubwa ya wale ambao leo ni washiriki wa lile “kundi moja [chini ya] mchungaji mmoja” wanathamini tofauti hii, huenda wengine wakauliza namna mtu anavyojua kama yeye amealikwa kwenye mwito wa kimbinguni. Hilo si jambo linaloweza kuamuliwa sasa kwa ushuhuda wa nje-nje kama vile ilivyokuwa wakati vipawa vya roho vilipokuwa vikitolewa katika siku za mwanzo-mwanzo wa kundi la Kikristo. Jambo lililokuwa la maana hata zaidi kuliko vipawa hivyo lilikuwa lile tumaini lenye utukufu la kupata urithi wa kimbinguni lililokuwa limetolewa kwa wale walioitwa “wana wa Mungu” na waliokuwa “wenye kuushiriki mwito wa mbinguni.” (Ebr. 3:1; 1 Yohana 3:1-3) Wakati huo kulikuwako tumaini hilo moja tu, lakini leo, wakati sehemu hiyo ya “usimamizi” wa Mungu inapokaribia kukamilishwa, malango ya Ufalme yamefunguliwa wazi ukiwako na mwaliko kwa “mkutano mkubwa” upate baraka za kidunia, kama ilivyotangulia kutajwa. Hasa imekuwa hivyo tangu mwaka 1935 na kuendelea, wakati huo “mkutano Mkubwa” ulipotambulishwa waziwazi kuwa jamii ya kidunia yenye tumaini la kuwa na uzima usio na mwisho katika dunia ya paradiso.—Efe. 1:10, NW; Ufu. 7:9-17.

Je! Mtu ndiye anayejichagulia ni tumaini gani atakalokuwa nalo, la kimbinguni ama la kidunia? Hapana. Kabla mtu hajakuwa na tumaini lo lote la kibinafsi, hatua ya kujiweka wakf bila masharti yo yote na kubatizwa lazima ichukuliwe na mtu huyo akikubali kufanya mapenzi ya Mungu tangu wakati huo, wala si mapenzi yake mwenyewe. Mungu hufanya mapenzi yake yafanywe kwa kuitendesha roho yake takatifu. Namna roho hiyo inavyotenda juu ya wale waliochaguliwa na Mungu kuwa washiriki wenye taraja wa lile “kundi dogo,” ikiamsha ndani yao tumaini la kimbinguni, imeelezwa katika Warumi 8:14-17. Wakristo hao walikuwa na ushuhuda usio na mashaka ndani yao wenyewe kwamba walikuwa wameitwa kwenye ufalme wa kimbinguni.

Je! watumishi hao waliojiweka wakf wanaokubaliwa na Mungu kama washiriki wa huo “mkutano mkubwa,” wanapokea roho ya Mungu vilevile? Bila shaka ndiyo, kama ilivyokuwa kwa wale watumishi waaminifu wa Mungu wa nyakati zilizotangulia Ukristo, wasiokuwa na tumaini la kimbinguni, kama vile Musa na Yohana Mbatizaji. (Mt. 11:11) Mungu anashughulika leo na kila mmoja wa watumishi wake waliojiweka wakf, akisitawisha ndani yao tumaini la uzima katika ufalme wake. Paulo aliwaambia Wakristo hao wa kwanza kwamba walikuwa ‘wakiokolewa kwa tumaini hilo,’ lile la kimbinguni. Vilevile alizungumza juu ya tumaini la “viumbe,” wengine wote wa jamii ya kibinadamu, waliokuwa ‘wakikungojea kufunuliwa kwa wana wa Mungu’ wenyewe wakiwa na taraja la kufurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu” wakiwa watoto wake wa kidunia waliorudishwa kwenye ukamilifu.—Rum. 8:18-25, NW.

Kwa hiyo kila mmoja apaswa kuokolewa katika tumaini fulani. Lapaswa kuwa tumaini lenye kujaa sana akilini na pia lapaswa kuwa hakika kabisa kwako. Ikiwa, baada ya kujichunguza kwa unyofu, unaona kwamba kuna kadiri fulani ya kutokuwa na hakika, au ikiwa unatambua kwamba maono yenye nguvu ya moyoni ndiyo yaliyokufanya uamue kwamba ulikuwa umepokea mwito wa kimbinguni, au pengine kwamba mwito kama huo ulikufanya uwe tofauti na wengine kwa njia fulani na pengine mkubwa kuliko wao, na kukupa sababu ya kutendewa kipekee na kwa heshima, basi una sababu nzuri za kuichunguza upya hali yako. Kwa unyofu na kwa unyenyekevu, usisite kumwomba Mungu akupe hekima na uongozi pamoja na msaada wa kufanya mapenzi yake. Yeye hatakukemea. “Mungu awatendea kama wana,” awapendao.—1 Kor. 11:28; Ebr. 12:4-11; Yak. 1:5-8.

Wote walio wa mfano wa kondoo kweli kweli wanaohudhuria “chakula cha Bwana cha jioni,” ama wakiwa watazamaji ama wenye kushiriki mifano, wanafurahia kuwapo “kwa ukumbusho” wa yote aliyofanya Yesu katika kuthibitisha upendo wake mshikamanifu kwa Babaye, na vilevile kwa kila amwaminiye. Kama vile Yesu ‘alivyowapenda mpaka mwisho,’ acheni nasi tuonyeshe roho iyo hiyo ya uvumilivu na ya ushikamanifu mpaka mwisho. Yohana alisema juu ya wafuasi wa Yesu kama wakiwa “ulimwenguni.” Ili tutiwe moyo, Yesu alikubali hilo, akaongeza hivi:’ “Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 13:1, HNWW; 16:33) Kwa hiyo, kama alivyosihi mtume Paulo, sisi sote na “tuifanye karamu [kila siku] . . . kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli.”—1 Kor. 5:8.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki