Mlinzi Akasema: “Umeanguka!”
1. Sababu gani twapaswa kupiga mioyo yetu konde tuchunguze “maono” ya kutuambia aliyo nayo Isaya?
MAONO ya yale yanayokuja katika wakati ujao unaokaribia kwa haraka sana ni magumu. Hivyo ndivyo jambo hilo lilivyosemwa kwa ajili yetu na nabii Isaya wakati wa siku za Milki ya Ashuru ambayo wakati huo ilikuwa ikiutawala ulimwengu. Je! “maono” hayo ni “magumu” sana kwetu tusiweze kuyachunguza leo? Hata hivyo tupige moyo konde tusikie yale anayosema Isaya: “Nimeonyeshwa maono magumu; atendaye hila anatenda hila, mharibu anaharibu.”—Isa. 21:2.
2. (a) Nani anayejulikana kuwa “mharibu,” na yeye “atendaye hila,” na sababu gani? (b) Huyo “atendaye” sana sana alikuwa mwenye “hila” kuelekea nani, na sababu gani?
2 Yule ambaye alikuwa anatokeza sana kama “atendaye hila,” ingawa hajatajwa, anajulikana. Ilikuwa Babeli ya kale, ambayo ilipata kuwa Mamlaka ya Tatu ya Ulimwengu. Ikawa yenye sifa mbaya sana kwa kuharibu mji wa Yerusalemu, hata kuharibu Patakatifu Zaidi pa hekalu la Yehova katika mahali hapo. Kweli, Yehova alitumia mfalme wa Babeli, Nebukadreza, kama “mtumishi” wake ili kuadibisha ufalme wa Yuda, hata hivyo Babeli iliwatendea hila watu wa agano la Yehova. Haikuwaweka huru wahamishwa Wayahudi wapate kurudi kwenye nchi yao waliyopewa na Mungu, hata ingawa miaka 70 ilikuwa imekaribia kufika. (Isa. 14:3-17) Mshindi wa Mamlaka ya Babeli ndiye aliyefungua njia ya kurudi nyumbani kwa “wafungwa” katika mwaka 537 K.W.K. Basi, kwa haki, “maono” aliyopewa mlinzi Isaya yalikuwa “magumu” juu ya Babeli, mharibu wa mataifa, sana sana mharibu wa watu wa Mungu wa Isaya.
3. Namna gani juu ya mfano wa kisasa wa Babeli kwa habari ya kuwa mwenye ‘kutenda hila’ na “mharibu”?
3 Namna gani mfano wa kisasa wa Babeli ya kale? Katika kutendea Wakristo wale walio katika uhusiano wa agano pamoja na Yehova Mungu, amewatendea kwa hila vivyo hivyo kwa habari ya mafundisho ya Ukristo. Pasipo huruma ameharibu Wakristo hao kwa sababu wanatii amri za Yehova Mungu na kutimiza kazi ya kutoa ushuhuda juu ya Mfalme wake aliyetawazwa, Yesu Kristo. (Ufu. 12:17) Jumuiya ya Wakristo imekuwa yenye kuongoza katika programu hiyo ya kutenda kwa hila na kuharibu, sana sana tangu siku za Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Ndiyo hasa itakayopatwa na uzito wa hayo “maono magumu” yatakapotimizwa juu ya milki ya ulimwengu ya kisasa ya dini ya uongo, Babeli Mkuu. Lakini Yehova atatumia nani katika kutimiza hayo “maono magumu” hivi karibuni?
4. Katika Isaya 21:2, nani wanaoitwa washambulie Babeli, na sababu gani Waajemi hawatajwi hapo?
4 Isaya anaweka msingi wa jibu la ulizo hilo anapoendelea kusema hivi: “Panda juu, Ee Elamu; husuru, Ee Umedi; mimi ninakomesha maombolezo yake yote.” (Isa. 21:2) Elamu ilikuwa mashariki mwa Mto Tigri nayo ikawa sehemu ya kulikoitwa Uajemi, hali leo eneo hilo ni la Irani.a Umedi ilikuwa sehemu ile kubwa zaidi katika mashariki mwa bonde la Mesopotamia. Karibu miaka 200 baada ya unabii wa Isaya, Koreshi (wa Pili) aliwashinda Wamedi hivyo kuupa ufalme wa Uajemi utawala juu ya Umedi. Hata hivyo, mama yake alikuwa Mmedi, na wengi wa askari katika jeshi lake walikuwa Wamedi. Koreshi huyu ndiye Koreshi, aliyetabiriwa na Isaya akiongozwa na roho. (Isa. 44:28 mpaka 45:7) Wakati wa Isaya Milki ya Umedi-Uajemi haikuwa imetokea, na hivyo Waajemi hawakuwa wanaongoza. Kwa hiyo Yehova alitaja kwa jina Elamu na Umedi tu zishambulie Babeli.
5. Yehova alifanyaje ‘kuomboleza kwake kote’ kukome, na je! “mfungwa” huyo aliwekwa huru apate kurudi nyumbani?
5 Je! washambulizi hao wangefaulu na kubadili mambo katika kusini-magharibi mwa Asia na Mashariki ya Kati? Ndiyo! Jambo hilo lilionyeshwa na maneno ya Isaya yaliyofuata: “Mimi ninakomesha maombolezo yake yote.” Hakika hayo ni maneno ya ‘Yehova wa majeshi,’ Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. Kwa kutumia Elamu na Umedi kama vyombo vyake alisababisha ‘kuomboleza kote’ kwa ajili ya uonezi wa Babeli kukome. Katika kumsihi Yehova Mungu akomboe kutoka kwa watekaji wasiojali kitu hata Waisraeli wakioza katika hali yao ya ufungwa, mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alisema hivi: “Kuugua kwake aliyefungwa na kuingie mbele zako. Kwa kadiri ya uweza wa mkono wako uwahifadhi wana wa mauti.” (Zab. 79:11-13; Isa. 14:17) Sala hiyo ilijibiwa katika mwaka wa 70 wa uhamisho wa Wayahudi katika Babeli kwa amri ya kifalme ya Koreshi Mkuu.—Isa. 35:8-10.
KUTENDA KWA KIBINAFSI KUHUSIANA NA KUANGUKA KWA BABELI
6, 7. Isaya anasimuliaje matokeo ya kuanguka kwa Babeli kwa wale wenye kupatwa na mabaya?
6 Kuanguka kwa Mamlaka ya Tatu ya Ulimwengu yenye nguvu katika mwaka 539 K.W.K. kukifaidi nchi ndogo ya Israeli lilikuwa jambo gumu sana kuwazia. Jambo hilo lilitia ndani badiliko kubwa sana katika mwendo wa historia ya ulimwengu. Watu mmoja mmoja waliopatwa na matokeo mabaya ya kuanguka kwa Milki hiyo iliyokuwa mahali palipo makao makuu katika ‘jangwa la bahari’ hawakuwa na budi kupatwa na maumivu. Matokeo juu ya watu hao yanafananishwa katika maneno ya Isaya yanayosema juu ya “maono magumu,” kama ifuatavyo:
7 “Kwa sababu hiyo viuno vyangu vimejaa maumivu, utungu umenishika, kama utungu wa mwanamke azaaye; ninaumwa sana, nisiweze kusikia; nimefadhaishwa kwa hofu, nisiweze kuona. Moyo wangu unapiga-piga, utisho umenitaabisha, gizagiza la jioni nilipendalo limegeuka likanitetemesha.”—Isa. 21:3, 4.
8. Maneno yenye kusimulia ya Isaya yanaonyesha nini kwa habari ya viongozi wa kidini katika Jumuiya ya Wakristo na upagani wakati wa kuanguka kwa milki ya ulimwengu ya dini ya uongo?
8 Maneno hayo yenye kusimulia ambayo yanahusu kuanguka kwa Mamlaka ya Tatu ya Ulimwengu yenye hila yanafananisha wimbi la kugutusha ambalo litapata mwundo wa jamii ya ulimwengu ya kidini wakati mfano wa kisasa wa Babeli utakapoanguka. Jambo hilo litahuzunisha Wababeli wa mfano wa kisasa kwa kadiri kubwa zaidi ya ujumbe wenye kupiga kwa nguvu unaotolewa sasa na Mashahidi wa Yehova wakati wa huu “wakati wa mwisho” tangu mwaka 1914. (Dan. 12:4) Makasisi na wakuu wengine wa baraza za kidini za Jumuiya ya Wakristo na upagani watatiwa bumbuazi, wataduwazwa kama kwamba hawawezi kuona wala kusikia juu ya yale yanayotokea. Mioyo yao haitakuwa na uimara wo wote, raha yo yote, uwezo wo wote wa kutegemea bila kuyumba-yumba miungu iliyoabudiwa wakati mmoja. Hali yenye kuchukiza sana kuweza kufanya mtu atetemeke inawaogopesha, sana sana kwa sababu unafiki wao wa kidini unafunuliwa. “Gizagiza” kama lile linalokuja likiahidi kuleta raha na kustarehe mwishoni mwa kazi ya siku litakuwa wakati wenye kutia giza wa matetemeko kwao. Siku zao za kuongoza vibaya watu na kuonea watu katika matengenezo yao ya kidini zitakoma kwa njia yenye kuogopesha sana. Watatetemeka kama wanawake wanaokamata viuno vyao kwa uchungu wakati wa kuzaa.
9. Tamasha aliyofunuliwa Isaya inabadilika ghafula kwa sababu ya amri gani ya Yehova?
9 Ghafula tamasha ya mambo aliyofunuliwa nabii Isaya inabadilika kama vile wakati wa kubadilika kwa sehemu za kuigiza katika nyumba ya michezo ya kuigiza. Anaisikia amri hii kutoka kwa Yehova: “Wanaandika meza, wanaweka ulinzi, wanakula, wanakunywa. Simameni, enyi wakuu, itieni ngao mafuta. Maana [Yehova] ameniambia hivi.”—Isa. 21:5, 6.
10. Amri hiyo ya kimungu ilionyesha nini, nalo jambo hilo lililoonyeshwa lilifikia kumdharau Yehova Mungu wakati gani?
10 Kwa ufupi hayo yanaionyesha tamasha katika nyumba ya mfalme huko Babeli wakati wa usiku wa mwisho wa kuutawala ulimwengu. Maandishi hayo yanaeleza karamu ya Belshaza, mwana wa mfalme Nabonido ambaye hakuwako. Kisha, hakika, kukawa kupanga viti kwa ajili ya wakuu wa Babeli elfu moja. Kukawapo kula na kunywa kwa furaha. Walakini jambo hilo likafikia kumdharau Yehova Mungu, wakati walipoanza kula na kunywa kwa kutumia vyombo vyake ambavyo vilikuwa vya hekaluni mwake hata Wababeli walipoutwaa Yerusalemu na kuharibu hekalu lake.
11. Sasa Yehova alifanya nini kimwujiza katika karamu hiyo yenye kumdharau ya Belshaza, naye Danieli alitumikaje kama mfasiri katika pindi hiyo?
11 Sasa karamu ya Belshaza inakuwa ya kumdharau Mungu, kwa kuwa inamwingiza Yehova katika hali hiyo. Kwa mwujiza yeye akatuma mkono uandike juu ya ukuta wa jumba la karamu, mahali ambapo mfalme angeweza kuuona, maneno haya: “Mene, mene, tekel na parsin.” Ili kufumbua fumbo la maneno hayo nabii mhamishwa Danieli alilazimika kuletwa. Neno la mwisho la mwandiko huo, parsin, ni hesabu ya wingi ya neno la Kikaldayo peres nalo lamaanisha “migawanyiko.” Kwa hiyo, katika ufasiri wake ulioongozwa na Mungu, Danieli alisema hivi: “PERES, ufalme wako umegawanywa na kupewa Wamedi na Waajemi.”—Dan. 5:28, NW.
12. “Ngao” ambayo ingetiwa mafuta na wakuu wa kifalme ilikuwa nini, nayo amri ya kutia mafuta “ngao” hiyo ilionyesha nini?
12 Kama zawadi Danieli alipendelewa kwa kupewa mavazi ya kifalme naye akafanywa “mtawala wa tatu” katika milki hiyo. Walakini huo haukuwa utimizo wa amri ya Yehova uliokusudiwa kwa ajili ya wakuu wa kifalme wa Babeli: “Simameni, enyi wakuu, itieni ngao mafuta.” (Isa. 21:5) Wala haikuwa amri kwa wakuu wa kifalme kupaka mafuta ngao zao za kivita kwa kupiga vita na watekaji wa Babeli. Mahali pake, usemi “ngao” ulihusu kichwa cha kifalme cha taifa hilo. (Linganisha Zaburi 89:18.) Basi, amri ya ‘kutia ngao mafuta’ inamaanisha nini? Jambo hili: kwamba Mfalme Belshaza alikuwa anakaribia kuuawa, jambo hilo likitaka mwingine achukue mahali pa ‘mtawala wa pili’ katika Milki ya Babeli. Walakini kuleta huko kwa “ngao” mpya ya mfano kwa njia ya kutia mafuta hakukutokea kamwe. Kuuawa kwa jeuri kwa Belshaza hakukutokeza nafasi kwa mrithi kutoka kwa jamii ya kifalme.
13. Kwa hiyo je! amri iliyokuwa imetolewa katika Isaya 21:2 ilikuwa imetolewa bure, nacho cheo kipya alichokuwa amepewa Danieli kiliendelezwa katika utawala huo mpya?
13 Danieli 5:30, 31 lasema hivi: “Usiku uo huo Belshaza, mfalme wa Wakaldayo, akauawa. Na Dario, Mmedi, akaupokea ufalme, naye umri wake alikuwa na miaka sitini na miwili.” Lilikuwa badiliko la haraka namna gani katika siasa za ulimwengu! Yehova hakuwa ametoa amri yake hii bure: “Panda juu, Ee Elamu; husuru, Ee Umedi.” (Isa. 21:2) Babeli ilipoanguka kwa Wamedi na Waajemi, Dario Mmedi ndiye aliyetwaa mahali pa ‘mtawala wa pili’ katika Babeli. Cheo kipya alichopewa Danieli cha kuwa “mtawala wa tatu” katika Babeli hakikuendelezwa katika utawala wa Umedi-Uajemi. Hata hivyo Danieli hakuuawa pamoja na Belshaza.
14. Kuanguka kwa Babeli ya kale kunatangulia kuonyesha nini, nao wenye kupaswa na jambo hilo watapatwa na matokeo gani?
14 Kuanguka kwa kustaajabisha kwa Babeli ya kale kunatangulia kuonyesha kuanguka kwa ghafula kwa mfano wake wa kisasa, Babeli Mkuu. Jambo hilo litawafumania wanadini wa ulimwengu. Kwa hiyo ikiwa waamini wa kutoweza kushindika kwa milki ya ulimwengu ya dini ya uongo hawaitazamii ianguke hivi karibuni, kinaya (kutosheka) chao kitagutushwa vibaya sana!
MAMBO YA KURIPOTI ALIYO NAYO MLINZI
15. Amri iliyotolewa baada ya maelezo ya kiunabii ya karamu ya Belshaza inaonyesha nini kuhusu Babeli ya kale na mfano wake?
15 Hata hivyo, sababu gani Isaya anatangulia kutuonyesha karamu ya Belshaza wakati wa usiku ule wenye kuhuzunisha wa mwaka 539 K.W.K.? Ilikuwa ni kwa sababu ya yale ambayo yangefuata, yaani, kuripoti kwa tukio hilo lenye kutokeza la karne hiyo kwa watu wa agano wa Yehova, ambao wangefurahia kuanguka kwa yeye “atendaye hila.” Isaya 21:5, 6 laonyesha yale ambayo yangefuata karibu karibu kuanguka kwa Babeli, likisema hivi: “Simameni, enyi wakuu, itieni ngao mafuta. Maana [Yehova] ameniambia hivi, Enenda, weka mlinzi; aonayo na ayatangaze.” Aha, ulimwengu wote ungearifiwa juu ya tukio hilo! Vivyo hivyo, pia, kuanguka kwa Babeli Mkuu lazima kufanyize habari kuu!
16. Ni jambo gani linaloweza kusemwa juu ya “mlinzi” aliyewekwa kwa habari ya Babeli ya kale na yule ambaye amewekwa kwa habari ya Babeli Mkuu?
16 Isaya ndiye aliyeambiwa aweke “mlinzi” aripoti yale ambayo angeyaona karibuni. Isaya hakuendelea kuishi apate kuona kwa macho yale aliyotabiri na ambayo alituandikia. Kwa hiyo mtu mwingine kutoka kwa watu wa Isaya mwenyewe angepaswa kutumikia kama mlinzi aliyewekwa. Katika siku hizo zinazotangulia kuanguka kunakokaribia kwa Babeli Mkuu mlinzi amewekwa. Hiyo ni jamii ambayo imewekwa mafuta na roho ya Yehova, jamii ambayo kwa kufaa inashirikiana na gazeti ambalo lingali na jina Mnara wa Mlinzi. Ushuhuda umekaribia upate kuonyesha kwamba kupitia kwa Yesu Kristo, Yehova Mungu ameweka jamii hiyo ya “mlinzi.” Imeendelea kutumikia katika cheo hicho hata wakati huu wenye kuogopesha wa “usiku” ambao unatia giza ulimwengu wote. (Mt. 24:45-47) Vipi, sasa, tutazamie “mlinzi” huyo atuambie nini katika wakati uliofika?
17. “Mlinzi” aliyewekwa aliona nini, nalo hilo liliwakilisha nini?
17 Unabii wa Isaya unaohusu “mlinzi” unaendelea kusema hivi: “Naye [akaona] kundi la wapanda farasi, wakienda wawili wawili, na kundi la punda, na kundi la ngamia; [akasikiza] sana, akijitahidi kusikiliza.” (Isa. 21:7) Magari hayo ya vita kwa wazi yanakaribia kwa mwendo wa kasi wa farasi wa walinzi Waajemi nao wanatoka “[jangwa la] bahari [lililoshindwa].” Inaelekea ni vikosi vya magari ya vita. Kikosi cha magari ya vita yanayovutwa na punda kinafananisha majeshi ya Umedi chini ya Dario Mmedi. Kikosi cha magari ya vita yanayovutwa na wale wanyama wakubwa zaidi, ngamia wanaoweza kukimbia haraka kuliko farasi, kinafananisha majeshi ya Uajemi chini ya Koreshi Mkuu.b Kwa kweli Mwajemi huyo alikuwa mwenye amri juu ya mwungano wa majeshi ya Wamedi na Waajemi. Si Dario Mmedi, bali Koreshi Mwajemi ndiye mshindi ambaye Yehova kupitia kwa Isaya alisema kwamba Angemwita kwa jina lake binafsi. Kabla ya hayo Koreshi huyo, Yehova Mungu angemfungulia malango ya chuma na milango ya Babeli apate kupanda kutoka bonde la Mto Frati na kuingia kwenye mji wenye kuta kubwa wa Babeli.—Isa. 44:27 mpaka 45:4; linganisha Danieli 8:1-4, 20.
18. Kulingana na Isaya 21:8, 9, “mlinzi” aliyewekwa angekuwa wa namna gani, na je! ndivyo imekuwa?
18 Mlinzi huyo aliyewekwa angekuwa mwaminifu na mwenye kutegemeka kwa kadiri gani? Isaya 21:8, 9 laonyesha jambo hilo kwa kusema hivi: “Ndipo akalia kama simba, Ee [Yehova], mimi nasimama daima juu ya mnara wakati wa mchana, na kila usiku ninakaa katika zamu ya ulinzi wangu. Na, tazama, linakuja kundi la watu, wapanda farasi, wakienda wawili wawili.” Alikaa macho, kabisa, akashikamana na zamu yake hata macho yake yenye kuona sana yalipoona mambo yenye maana ambayo alikuwa akiangalia ayaone bila kuchoka. Vivyo hivyo jamii ya “mlinzi” ya leo imenguruma kwa sauti kubwa na bila woga katika kutimiza mgawo iliogawiwa na Mungu kwa kutumia magazeti ya Mnara wa Mlinzi na vitabu vinginevyo vya kitheokrasi na hotuba za watu wote. Kwa uwezo wa Yehova unaoendelea itazidi kufanya hivyo hata itakapoweza kutoa tangazo ambalo limetamanika kwa muda mrefu.
19. Ni jambo gani linaloonyesha kama kwamba mlinzi huyo alipata maana sahihi ya magari ya vita yaliyokuwa yanakaribia?
19 Mlinzi huyo alipata maana ya magari ya vita aliyoyaona yakija kwenye upeo wa macho ya mnara wa mlinzi ambao alikuwa amesimama juu yake. Kulingana na wakati uliowekwa na Yehova—miaka 70 ya kukaa ukiwa kwa nchi ya Yuda—na kulingana na unabii uliotolewa na mhamishwa Danieli kabla ya karamu ya Belshaza yenye kumdharau Mungu katika mwaka 539 K.W.K., mlinzi huyo angeweza kufasiri kwa usahihi maana ya kusonga mbele bila kuzuiwa kwa magari ya vita yasiyokuwa ya Kibabeli. Isaya 21:9b lasema, “Akajibu na kusema, Babeli umeanguka, umeanguka; na sanamu zote za miungu yake zimevunjwa chini.”
20. Sababu gani si wahamishwa Wayahudi katika Babeli waliovunja sanamu zilizochongwa za miungu yake, naye aliyevunja sanamu hizo alikuwa nani?
20 Mvunja sanamu anayesemwa hapa ni Yehova, Mungu wa pekee anayeishi na wa kweli, Mungu mwenye wivu au “Mungu anayetaka ibada ya pekee.” (Kut. 20:5, NW) Kwa kuruhusu Wamedi na Waajemi ambao hawakuabudu miungu ya Babeli waishinde, Yehova alionyesha uongo wa miungu-sanamu ya Mamlaka ya Tatu ya Ulimwengu, haikuwa hai. Si wahamishwa Wayahudi katika Babeli waliojiinua katika kuasi na kupindua Mamlaka ya Tatu ya Ulimwengu; Yehova Mungu wao hakuwapa ruhusa wala amri ya kufanya jambo hilo. Mahali pake, alimtumia Dario Mmedi na Koreshi Mwajemi kuleta anguko la Babeli yenye kuabudu sanamu ikiwa mamlaka ya ulimwengu. (Dan. 2:32, 36-38) Kwa hiyo si “mlinzi” aliyesababisha kuanguka kwa yeye “atendaye hila,” Babeli. Yeye alitoa ushuhuda tu wa kuanguka huko, kwa kuondolewa lawama kwa Yehova akiwa Mungu wa unabii na akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu.
21. Ni tangazo gani linalofanana na hilo ambalo “mlinzi” wa unabii wa Isaya alitangaza linalongojea kutangazwa?
21 Tangazo la maana la ulimwenguni pote kama lile la “mlinzi” wa unabii wa Isaya lilitabiriwa kuwa lilikuwa karibu kutangazwa katika wakati wetu. Mtume Mkristo Yohana, aliyeishi hata mwishoni mwa karne ya kwanza, aliona njozi ya yeye mwenye kutoa tangazo hilo na kuandika hivi: “Baada ya hayo, nilimwona malaika mwingine akishuka kutoka mbinguni. Alikuwa na uwezo mkuu, na dunia ikamulikwa kwa mng’ao wake. Basi akapaaza sauti kwa nguvu akisema, “Umeanguka; Babuloni mkuu umeanguka! Sasa umekuwa makao ya mashetani na pepo wachafu; umekuwa makao ya ndege wachafu na wa kuchukiza mno.”—Ufu. 18:1, 2, HNWW.
22. Ni nani atakayefanya Babeli Mkuu awe ukiwa, naye atatumia chombo gani kutimiza jambo hilo?
22 Koreshi Mkuu Zaidi, Yesu Kristo aliyetukuzwa, Ndiye atakayesababisha kuanguka halisi kunakokuja kwa Babeli Mkuu, hivyo awe mahali pa ukiwa panapoepukwa. Leo Wakristo mashahidi wa Yehova wanaweza kuhubiri kwa kadiri wanavyotaka katika ulimwengu wote kuhusu ufalme wa Yehova na siku ya kisasi chake, walakini hilo kamwe haliwezi kuleta anguko la milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Kwa shauku wanangojea wakati watakapotoa tangazo kwamba Babeli Mkuu ameanguka. (Ufu. 18:2, HNWW) Kwa kuwa Koreshi Mkuu Zaidi hatumii wanafunzi wake duniani wenye amani wapindue Babeli Mkuu, sura ya 17 ya Ufunuo inaonyesha kwamba yeye atatumia chombo kinachofanana na mnyama; kinafananishwa kama mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu, mwenye pembe 10. Vichwa vyake saba vinafananisha zile mamlaka saba za ulimwengu za historia ya Biblia. Kahaba wa mataifa yote, Babeli Mkuu, amepanda juu ya mnyama huyu wa mfano wa karne ya 20, wakati Ushirika wa Mataifa ulipoundwa baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.
23. Waliokuwa wakitegemeza mnyama wa mfano sasa wote watageukia nani, naye Koreshi Mkuu Zaidi atafanya nini?
23 Mpaka sasa Babeli Mkuu amepanda juu ya Umoja wa Mataifa, ambao ulifuata Ushirika ule. Walakini, karibuni sasa, wategemezaji wa kisiasa wa Umoja wa Mataifa watachoshwa na kutawalwa na milki ya ulimwengu ya dini ya uongo nao watamtupa chini na kumharibu. Kisha, baada ya “mlinzi” kusema kwa sauti kuu, “Babuloni mkuu umeanguka,” wote watageukia mashahidi Wakristo wa Yehova wanaobaki. Hapo ndipo Koreshi Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, “Mfalme wa wafalme,” atakapojiingiza na kuharibu waliokuwa wategemezaji wa Umoja wa Mataifa katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. Jamii ya “mlinzi” aliyetiwa mafuta na Yehova pamoja na “mkutano mkubwa” ambao umeitikia habari inayosemwa kwa sauti kuu na jamii ya “mlinzi” wataokoka vita hiyo ya mwisho chini ya ulinzi wa kimungu, ili kuondolea lawama Yehova Mungu akiwa Mwenye Enzi Kuu ya mbingu na dunia yote.
24. Israeli wa kale alikuwaje “mwana” wa sakafu ya kupuria nafaka ya Yehova, na leo ni kupurwa kwa nani kwa namna iyo hiyo kutakakokomeshwa, na namna gani?
24 Wayahudi waliohamishwa kwa miaka 70 katika Babeli ya kale walipewa adabu kwa njia hiyo kama kwamba kwa ‘kufikichwa.’ Kwa kusema kwa njia ya mfano, ndio waliokuwa “mwana” wa sakafu ya kupuria ya Yehova. Baada ya kuanguka kwa Babeli kutiwa adabu kama ‘kufikichwa’ kungekoma. Likitaja hilo, Isaya 21:10 kwa huruma na kwa kufariji lasema hivi: “Ewe niliyekufikicha, na nafaka ya sakafu yangu; Hayo niliyoyasikia kwa [Yehova] wa majeshi, Mungu wa Israeli, nimewapasha habari zake.” Vivyo hivyo, Babeli Mkuu ameruhusiwa afikiche (apure) mashahidi waaminifu wa Yehova. Walakini baada ya kuanguka kwake katika uharibifu, ‘kufikicha’ kote kwake kutakoma. Hawara (wenzi) zake za kisiasa watajaribu kuendeleza kufikicha (kupura) huko. Kama adhabu wao wenyewe watapurwa kwenye uharibifu katika sakafu ya kupuria ya mfano ya Yehova.—Ufu. 14:14, 15; Yoeli 3:13-16; Mik. 4:12, 13.
25. Kwa sababu ya anguko linalokaribia la Babeli Mkuu, sababu gani kuliko wakati mwingine wo wote huu ndio wakati wa “watu” wa Yehova kusikizisha amri yake, kukiwa na jambo gani mwishowe?
25 Kwa sababu ya anguko linalokaribia la Babeli Mkuu, sasa kuliko wakati mwingine wo wote ndio wakati wa jamii ya “mlinzi” na “mkutano mkubwa” kusikizisha amri ya kimungu: “Watu wangu, ondokeni kwake! ili msishirikiane naye katika dhambi yake, msije mkaipata adhabu yake.” (Ufu. 18:4, HNWW) Ndiyo, “ondokeni kwake,” si ili mpate kujiunga na hawara zake za kisiasa au vikosi vya ulimwengu huu visivyo na imani, vinavyompinga Mungu, bali kuwa sehemu ya “watu wangu,” watu wa Yehova waliojiweka wakf. (Yer. 51:45) Chukua hatua sasa ya kutenda kulingana na ‘tangazo juu ya jangwa la bahari’ lililotolewa na Isaya.—Isa. 21:1-10.
26. Tunapaswa kumshukuru ‘Yehova wa majeshi,’ kwa ajili ya nini, nao wenye kuitii wana tumaini gani lililobarikiwa?
26 Basi, shukrani zote zimwendee ‘Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli,’ kwa kutokeza na kuweka jamii ya “mlinzi” kwa kuipa ripoti nzuri hiyo ya kusikizisha mbali na karibu! Wote wanaotii ripoti hiyo iliyotolewa na Mungu wana tumaini lililobarikiwa la kuokoka “usiku” wenye kuleta msiba juu ya ulimwengu huu na la kukaribisha “asubuhi” yenye utukufu ya taratibu mpya ya mambo yenye haki chini ya utawala wa Koreshi Mkuu Zaidi, Yesu Kristo Mkombozi. Hiyo itampendeza na kumsifu ‘Yehova wa majeshi,’ Bwana yetu Mwenye Enzi Kuu. —Kutoka The Watchtower July 1, 1980.
[Maelezo ya Chini]
a Blblia The Jerusalem Bible (Kifaransa) yasema hivi, juu ya Isaya 21:2: “Elamu ndilo jina la wakaaji wa kale wa sehemu tambarare iliyo juu ambayo katika hiyo Waajemi walitoka. Wamedi walikuwa wamekuwa vibaraka wa Koreshi kabla ya kutekwa kwa Babeli.”
b Kwa habari ya matumizi ya Koreshi Mkuu ya ngamia katika vita, tazama kitabu The History of Herodotus, Kitabu cha Kwanza chenye kichwa “Clio,” ukurasa 29.
Tafsiri ya Kifaransa ya Biblia Takatifu ya M. L’Abbe chapa ya 1884, inatoa maelezo juu ya Isaya 21:7 kama ifuatavyo: “Wapanda farasi hawa wawili wenye kubebwa juu ya gari la vita, ni wafalme wawili waliopaswa kutwaa Babeli, Dario Mmedi na Koreshi. Kama ambavyo Menokio [mfafanuzi wa Biblia wa karne ya 17 aliyekuwa Mwitalia mwanadini Myesu] aelezavyo jambo hilo vizuri sana, kupanda kwao kunafananisha Wamedi na Waajemi.”
Tazama maelezo kama hayo juu ya Isaya 21:7 yaliyotolewa katika kitabu cha Dakt. Adam Clarke, Commentary on The Old Testament, Kitabu cha 4, ukurasa 2724.
Juu ya maarifa ya Koreshi ya vita ya kutumia ngamia, tazama Sura ya 20 yenye kichwa “Wagiriki na Waajemi,” ya kitabu “The Outline of History” cha H. G. Wells, ukurasa 257, mafungu 2, 3, chapa ya 1971.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Karamu ya Belshaza yenye kumdharau Mungu ilitokeza hukumu ya Yehova ya uharibifu juu ya Babeli
[Picha katika ukurasa wa 17]
Katika kuwaadhibu kwa ‘kufikicha’ Mashahidi wa Yehova, kwanza milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, kisha hawara zake za kisiasa, wao wenyewe ‘watafikichwa’ hata kuharibiwa