Ufahamu Katika Habari
“Kutazamiwa kwa Mambo Yanayokuja
● Uhakika wa kwamba wanadamu wanachunguza wakati ujao na kuogopa wanayoona ulitabiriwa na Yesu Kristo kuwa utakuwa sehemu ya kizazi chetu. Katika Luka 21:25, 26 NW, yeye alisema kwamba kungekuwako “huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea . . . huku wanadamu wakizimia moyo kwa sababu ya hofu na kutazamiwa kwa mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.”
Hati ya pekee yenye kurasa 800 yenye kichwa “Ripoti ya [mwaka] 2000 ya Duniani pote kwa Rais” kutoka kwa Idara na Baraza ya Ubora wa Mazingira ya Serikali ya U.S. inaonyesha usahihi wa maneno ya Yesu. Inaonya kwamba kuna “uwezekano wa kutokea matatizo ya duniani pote ya kadiri kubwa sana kufikia mwaka 2000.” Gazeti New York “Times” linasema kwamba, kulingana na ripoti hiyo, “wakati unamalizika wa tendo la mataifa yote kuchukuliwa kuzuia ulimwengu wenye kufa njaa, wenye kujaa watu sana, uliochafuliwa, wenye umaskini wa mali za asili.” Naye aliyekuwa rais wa Benki ya Ulimwengu Robert McNamara alitangaza hivi: “Inaonyesha ulimwengu wenye kutisha sana miaka ishirini kutoka sasa—isipokuwa tutende.”
Hali inayokatisha tamaa ya mambo yanayoweza kutokea inatia ndani: nusu ya misitu ya ulimwengu haipo, chungu za changarawe zinatokea mahali yalipokuwa mashamba yenye rutuba wakati mmoja, mwisho wa karibu namna milioni mbili za viumbe hai, watu elfu milioni 1.3 wasiolishwa chakula chenye afya, na matatizo mengine mengi ya duniani pote. Serikali zinajitahidi kuyatatua? Ripoti hiyo inasema hivi: “Masuluhisho peke yake . . . ni magumu na ya muda mrefu [kwa sababu magumu hayo] yanahusiana kwa njia isiyonyosheka na matatizo yenye kutia wasiwasi na yenye kuendelea ulimwenguni—umaskini, udhalimu na ugomvi wa kijamii.”
Upungufu wa Chakula—“Mamilioni watakufa”
● “Kutakuwapo upungufu wa chakula . . . mahali hapa na mahali hapa,” akasema Yesu. Taabu hiyo inaendelea kuwa sehemu yenye kutokeza sana ya kizazi chetu. Tengenezo la Chakula na Ukulima la Umoja wa Mataifa (FAO) hivi karibuni lilipanga mataifa 29 kuwa yanapatwa na taabu ya “upungufu wa chakula usio wa kawaida,” au njaa ambayo imeenea. Kati ya mataifa hayo yenye njaa, 23 yalikuwa katika Afrika, nao watu mamia wanaripotiwa kuwa wanakufa kila siku katika kontinenti hii. Zijapokuwako jitihada za kutoa msaada za mataifa yote, mtaalamu wa chakula wa FAO anasema hivi: “Hata tufanye nini sasa, mamilioni watakufa.”
Hali hiyo ipo hata ingawa, kama gazeti “Time” lilivyosema: “Katika miaka ya mapema ya kuanzia [19] 70, Baraza ya Chakula Ulimwenguni ya Umoja wa Mataifa yenye washiriki 36 iliazimia kutokeza ulimwengu usio na njaa kwa muda wa miaka kumi.” Mataraja ya kuondoa “upungufu wa chakula” ulimwenguni ni nini? “Time” lajibu hivi: “Leo lengo hilo la kutimiza mambo makubwa linaonekana kuwa mbali sana kuliko wakati mwingineo.”
Hata hivyo hali hizo zinatoa tumaini. Zinaonyesha “mwisho wa taratibu hii ya mambo” ambayo ipo sasa, ifuatwe na taratibu mpya ya mambo iliyo bora.—Mt. 24:3, NW; Ufu. 21:1-4.