Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 11/1 kur. 4-8
  • Unaweza Kupata Furaha!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unaweza Kupata Furaha!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MSAADA KWA MATATIZO YA PESA
  • KUKABILIANA NA UPWEKE
  • Matatizo ya Kifedha—Kuna Msaada Gani?
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Kupata Furaha ya Kweli kunategemea Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Ni Nini Ufunguo wa Kupata Furaha?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Unaweza Kushindana na Matatizo ya Maisha
    Furaha​—Namna ya Kuipata
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 11/1 kur. 4-8

Unaweza Kupata Furaha!

JE! NYAKATI zote matatizo yanaelekea kuharibu furaha yako? Yanaharibia wengi.

Kwa sababu hiyo, watu wengine wanakataa kufuata kanuni zo zote na kujaribu kufanya lo lote tu wapate msisimko wa raha au furaha ya namna fulani. Wengine wanajiachilia wafuate maisha yenye matatizo, wakitumainia wakati ujao wenye furaha katika Nirivana (hali ya kupumzika kabisa bila masumbufu ya maisha ya zamani kulingana na imani ya Kibanyani), mbinguni au mahali penginepo.

Ingawa Mungu anaweka mbele yetu wakati ujao wenye furaha katika taratibu mpya yenye haki, yeye anatutaka tupate furaha sasa, pia. Na kweli tunaweza kuipata!—2 Pet. 3:13; Tito 1:2; Ebr. 11:6.

Kufanya mambo kwa njia ya Mungu ndio ufunguo wa furaha ya sasa na ya wakati ujao. Ndivyo ilivyo sasa, kwa maana kwa kufuata njia ya Mungu tunaweza kuepuka matatizo ambayo yangetuharibia kufurahia maisha. Na kufanya mambo kwa njia yake kunaleta namna ya maisha yanayofanya maisha ya kila siku yapendeze zaidi sasa. Ili kuacha kusema juu ya mambo yasiyoonekana sasa, acheni tufikirie matatizo mawili ya kawaida—pesa na upweke—tuone jinsi shauri la Mungu na njia ya maisha ya Kikristo inavyoweza kutusaidia tuwe wenye furaha.

MSAADA KWA MATATIZO YA PESA

Wewe unajua jinsi pesa zinavyohitajiwa sana. Mwandikaji mmoja wa Biblia alieleza jambo hilo kwa njia hii: “Kufanya karamu hukufanya wewe ufurahi na divai hukuchangamsha wewe, lakini wewe huwezi kuwa na cho chote cha hivyo pasipo pesa.” (Mhu. 10:19, Today’s English Version) Kwa sababu ya kuwapo kwa infuleshoni, kila siku inagharimu pesa zaidi ili kuweza kuishi. Biblia inaweza kusaidiaje?

Kwanza, matumizi ya mafundisho ya Biblia yanaweza kukusaidia upate kazi na kuchuma pesa unazohitaji. Kwa mfano, Maandiko yanakazia thamani ya kuwa mwenye bidii na mnyofu.

“Nafsi ya mtu mvivu hutamani asipate kitu; bali nafsi ya mwenye bidii itanenepeshwa. Je! wamwona mtu mwenye bidii katika kazi zake? Huyo atasimama mbele ya wafalme.”​—Mit. 13:4; 22:29.

“Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe.”​—Efe. 4:28.

“Lifanyeni liwe lengo lenu kuishi maisha matulivu, kujali shughuli yenu wenyewe, na kuchuma riziki yenu wenyewe, . . . Katika njia hii . . . hamtakuwa na lazima ya kutegemea mtu ye yote kwa mnachohitaji.”​—1 The. 4:11, 12, “TEV.”

Fikiria jinsi mashauri hayo yanavyofaa. Eh, ni kweli kwamba watu wengine wanasonga mbele kwa kupunja, kuiba na kuhonga au kwa kutumia watu mashuhuri. Lakini kwa ujumla na hatimaye, wewe ukitumia mashauri hayo ya ki-Biblia utafanikiwa zaidi ya wale wanaoyapuza. Kwa sababu gani?

Labda umeona kwamba matajiri wa kazi na wasimamizi wanalalamika mara nyingi juu ya wafanya kazi kuja wakiwa wamechelewa, kukaa-kaa kilofa au kutokutumainika. Kwa hiyo mtu ambaye, kwa sababu ya kutumia mashauri ya Mungu, anafika kazini kwa wakati unaofaa, anayefanya kazi kwa bidii na mwenye unyofu anaweza kwa kawaida kupata kazi, tena anathaminiwa. Huenda yeye akalipwa pesa nyingi zaidi na inaelekea atabakizwa kazini wakati wengine wanapoachishwa kazi kwa muda kwa sababu ya kazi kupungua. Vifikirie visa viwili hivi:

Duka moja lenye vifaa vya umeme katika Afrika ya Kusini liliumia kwa sababu ya kuibiwa na wafanya kazi, halafu msimamizi akawakusanya wafanya kazi wote Waafrika akasema wamefukuzwa kazini. Lakini kesho yake, akiwa ndani ya gari-moshi alilolitumia kwa ukawaida wakati wa kwenda kazini, mfanya kazi mmoja alikuta mfanya kazi mwingine na kumwuliza, ‘Imekuwaje kwamba wewe unakwenda kazini?’ Jibu likawa: Msimamizi yule alikuwa amemwambia kwa faragha kwamba kwa sababu ya unyofu wake yeye hangefukuzwa kazini. Ilikuwa vivyo hivyo kwa yule mfanya kazi wa kwanza. Walipofika kazini wakakuta mfanya kazi wa tatu aliyekuwa ameambiwa lilo hilo. Wote walikuwa Wakristo wa kweli.

Mkurugenzi wa shirika la Kiingereza lenye kujenga barabara alimwambia Robert aeleze wapigaji simu wo wote kwamba yeye hayupo. Lakini wakati Robert alipopokea simu ya mkurugenzi akaeleza kwamba mtu huyo alikuwa na shughuli nyingi. Alipolaumiwa kwa kufanya hivyo, Robert alieleza kwamba akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova yeye asingeweza kusema uongo. (Efe. 4:25) Baadaye, wakati alipokuwa akifikiriwa kupandishwa cheo, mfanya kazi mwingine alitokeza mashaka juu ya unyofu wa Robert. Lakini mkurugenzi alimtetea kwa kutumia mambo ya hakika. Robert akapandishwa cheo.

Katika pande nyingine, pia, kufuata mashauri ya Biblia kunaweza kukusaidia uepuke au uweze kukabili matatizo ya pesa na, kwa hiyo, kunaweza kukuongezea furaha.

Kwa imara Neno la Mungu linaonya mtu awe na busara juu ya kukopa pesa. Linasema: “Akopaye ni mtumwa wake akopeshaye.” (Mit. 22:7) Ingawa Biblia haikatazi kukopa, namna hii ya mashauri yenye hekima inatoa msaada zaidi ili mtu avizuie vishawishi vya kununua vitu kwa mkopo, kisha kuja kuvilipia kwa kuongeza faida kubwa na kuingia katika deni.

Biblia inahimiza waabudu wa kweli waheshimu na kutunza mali ya wengine. Inaonyesha pia kwamba usafi ni wa maana. (Kum. 22:1-4; 23:12-14; Kut. 30:18-21) Wakristo wanaotunza nyumba wanayokodi kwa njia hiyo wanathaminiwa mara nyingi kama wapangaji na kwa hiyo wanaweza kukodi nyumba kwa pesa chache zaidi. Kutoka mji mkuu mmoja wa Afrika inakuja habari hii yenye maana:

Jamaa moja ya Kikristo iliweka nyumba yao ya kukodi katika hali ya usafi na kulipa kodi bila kukawia. (Rum. 13:8) Walipokuwa karibu kuondoka hapo, walimjulisha mwenyeji kwa jamaa nyingine ya kundi hilo. Yeye akasema kwamba kwa ukawaida yeye huongeza kodi, lakini kwa sababu aliwajua watu hao kuwa wenye kutegemeka na safi akaiacha kodi iwe ile ile, karibu nusu ya kodi ambayo hutozwa kwa kawaida katika eneo hilo.

Njia nyingine ya kuongeza furaha kwa kukubali mashauri ya Mungu ni kuepuka tabia na mazoea fulani yanayoumiza watu ki-uchumi. Moja ni kunywa sana, hata ulevi, mambo ambayo Biblia inakataza. Inagharimu pesa nyingi kununua vileo, na ulevi unafanya sana watu wakose kwenda kazini na kutokeza visa vingi. Kwa ukweli Biblia inaonya hivi: “Usiwe miongoni mwao wanywao mvinyo . . . kwa maana mlevi na mlafi huingia umaskini, na utepetevu humvika mtu nguo mbovu.” (Mit. 23:20, 21) Hivyo, kwa kufanya mambo kwa njia ya Mungu mtu anaweza kupunguza au kuepuka matatizo ya pesa, tena anaweza kuwa mwenye furaha zaidi katika pande mbalimbali.

Mwishowe, tunachukua hatua kubwa kuelekea kupata furaha tunapokubali maoni ya Mungu juu ya utajiri au mali. Je! hiyo inamaanisha kukataa pesa kabisa? Sivyo, kwa maana pesa zinaweza kuwa ulinzi. (Mhu. 7:12) Hata hivyo Neno la Mungu linakazia kuridhika. Katika jambo hili Yesu anatushauri tusijitahidi sana kupata utajiri, bali tutosheke na tulivyo navyo au vile ambavyo tunaweza kuvipata bila kusumbuka sana. Tafuta wakati uyasome maneno yake yenye maana juu ya jambo hili kwenye Luka 12:22-31. Tena, Biblia inahimiza hivi: “Tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Tim. 6:8) Hayo ni maneno yenye faida sana. Kwa kweli, hata wataalamu wenye maarifa ya jinsi akili zinavyoongoza mwenendo wa watu wameanza kuona kwamba ukiwa na maoni hayo juu ya pesa, utakuwa mwenye furaha zaidi.

KUKABILIANA NA UPWEKE

Lakini namna gani kama huzuni yako haihusiani na matatizo ya pesa bali inahusiana na upweke wenye kukuvunja moyo? Ikiwa hilo silo tatizo lako binafsi, labda ni tatizo kwa watu wengi unaowajua. Katika uchunguzi wa watu 52,000, zaidi ya asilimia (%) 40 walisema kwamba ‘mara nyingi wanajiona wapweke.’ Maono hayo ndiyo yaliyozidi kuharibu furaha ya wazee na vijana, wanaume na wanawake.

Kwa kuwa huenda hili likawa ni tatizo linalohusu kukosa kwa mtu jamaa ya karibu au rafiki, kufanya mambo kwa njia ya Mungu kunaweza kusaidiaje? Biblia inasema habari gani juu ya jambo hili inayoweza kuongeza furaha?

Kwanza, mara nyingi upweke huleta hali ya kushuka moyo na mtu anaacha kujiheshimu. Lakini ikiwa unapendezwa na kufanya mambo kwa njia ya Mungu unasitawisha uhusiano mzuri pamoja naye. Jambo hilo linaweza kusaidia kuondoa upweke, kwa sababu unajisikia kuwa mtu mwenye thamani kubwa, ukijua kwamba Muumba wetu anapendezwa binafsi na wewe, naye ana nia ya kukusaidia.​—Mt. 18:10.

Tena, Biblia ina mashauri mengine zaidi ya yale ya kawaida wanayopewa watu wapweke—“kuendelea kuwa na shughuli nyingi”​—kwa kuwahimiza Wakristo wawe wenye bidii katika kazi njema. Tafadhali soma katika Matendo 9:36-42 jinsi mwanamke mmoja Mkristo, ambaye labda angaliweza kuwa mpweke, alivyofanya jambo hilo. Angalia jinsi yeye alivyotumia wakati akitengenezea wengine vitu. Katika kufanya hivyo alipata rafiki wengi wapendwa wa Kikristo kisha akapata furaha inayotokana na kutoa.​—Matendo 20:35.

Kazi moja njema na ambayo ni namna ya kutoa inayotokeza sana katika Ukristo wa kweli ni kufundisha wengine ile kweli ya Neno la Mungu. Kufanya hivyo kunaendelea kuwafanya Wakristo wenye juhudi wawe na shughuli nyingi zenye faida. Kunafanya mtu akutane na watu wa namna mbalimbali. Tena kunaridhisha sana sana, kwa maana kwa njia hiyo unasaidia wengine wamkaribie zaidi Mungu na kupata furaha. Kwa hiyo, ingawa tangazo hili la waziwazi la “habari njema” ni wajibu—sehemu ya kufanya mapenzi ya Mungu sasa—ni chanzo cha kujipatia furaha binafsi pia.

Pia, Mungu anahimiza Wakristo wakutane pamoja kwa ukawaida wajifunze Biblia na kushirikiana. (Ebr. 10:24, 25) Ingawa kuwa kati ya watu wengine siko peke yako kunakolitatua kabisa tatizo la upweke, ushirika wa ukawaida na wenye uchangamfu pamoja na Wakristo wenye upendo unasaidia kwa uhakika. Tunakutia wewe moyo uhudhurie mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Huko unaweza kuona jinsi kufuata mashauri ya Biblia kunavyosaidia wengi waweze kukabiliana na upweke, na vilevile kushughulika na matatizo yanayohusu pesa, ndoa, mikazo na mambo mengine-mengine ambayo huharibu furaha kwa kawaida.

Maadamu taratibu ya mambo ya sasa ipo, unaweza kutazamia kwamba matatizo yatakuwapo. Lakini badala ya kujiachilia yakushinde au kujaribu njia fulani-fulani zisizo imara za kukabili matatizo hayo, kwa nini usifanye jambo ambalo kwa uhakika linaweza kukuletea ufanisi na furaha kubwa zaidi? Yaani, kujifunza maoni ya Mungu kisha uyatumie. Kama mamilioni ya watu kote kote duniani wanavyojua kutokana na mambo waliyojionea wenyewe, kufanya hivyo kutakusaidia uepuke matatizo mengi ya kawaida na kuweza kuyakabili vizuri zaidi yale yatakayobaki. Hivyo utaona kwamba njia ya kupata furaha haitazibwa. Utakuwa umekwisha kuupata ufunguo wa njia hiyo na kuutumia.

Basi utakuwa na maisha yenye maana zaidi, utapata kibali ya Mungu na furaha iliyoongezeka.

[Picha katika ukurasa wa 6]

“KUIPATA ILE HALI YA FURAHA INAYOELEKEA KUTOKUPATIKANA”

Dakt. Joyce Brothers, mtaalamu wa mambo ambayo akili zinaongoza watu kuyafanya, alieleza kwamba ‘tunaposema juu ya mambo tunayotaka maishani, tunakuwa hasa tukisema juu ya furaha.’ Je! pesa ndio ufunguo wake? Daktari huyo wa kike akasema:

“Mtu mwenye mapato ya dola 100,000 huenda akawa mwenye starehe zaidi, mwenye mavazi mazuri zaidi, na huenda akaishi maisha mazuri zaidi ya mtu mwenye mapato ya dola 20,000, lakini hatakuwa mwenye furaha zaidi sana. . . .

“Mambo ya hakika ni kwamba mapato ya kiasi cha kutosha yanaleta furaha na kwamba ni mara chache mapesa mengi yanapoleta furaha. Pesa zinadanganya macho. Zinaweza pia kuwa mtego, kitanzi cha kukuzuia usiifikie miradi unayoipenda sana kabisa.”‏

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

“Katika maisha yao wenyewe ya kikundi Mashahidi wanakuwa jamii ya kweli yenye kutumainiana na kukubali watu. . . . Mashahidi wa Yehova wanatolea [mtu] njia ya maisha yenye maarifa zaidi inayowapa wenye kuifuata jinsi ya kutambuliwa na watu wengine na kujiheshimu wenyewe, kukubaliwa na wengine, na kuwa na tumaini la wakati ujao.”​—Kitabu “Religious Movements in Contemporary America.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki