Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Maelezo ya maneno “Jumuiya ya Wakristo” ni nini kama yanavyotumiwa katika vichapisho vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi?
Mara nyingi sana maneno “Jumuiya ya Wakristo’’ yanatumiwa katika vichapisho (vitabu) vya Sosaiti katika ile njia ya kifupi zaidi yenye kumaanisha “Ukristo”; yaani, Ukristo wa jina tu, ulio tofauti na Ukristo wa kweli wa Biblia. Matumizi hayo yanaelekeza fikira juu ya mambo ya kidini hasa. Walakini, nyakati nyingine maneno hayo yanatumiwa katika vichapisho vyetu katika maana ile ya pili ya kirefu, maana yake, “ile sehemu ya ulimwengu ambamo mna Ukristo.”
Maelezo yenye kuzunguka habari inayozungumzwa ndiyo yatakayoonyesha mtu kama maneno yenyewe yametumiwa kwa njia ile ya kifupi ya kidini au katika ile maana ya kirefu zaidi inayotia ndani sehemu kubwa ya eneo la ulimwengu. Kwa mfano, ikiwa Jumuiya ya Wakristo inatajwa kuwa sehemu ya milki ya ulimwengu ya dini ya uongo (‘Babeli Mkuu’), na kusemwa kwamba milki hiyo ya dini ya uongo ndiyo itakayoharibiwa kwanza kwenye “dhiki kubwa,” itakuwa wazi kwa msomaji kwamba maneno hayo yametumiwa kwa njia ile ya kifupi zaidi. Ndivyo ilivyo kwa kuwa sehemu za kisiasa na kibiashara za makao ya Jumuiya ya Wakristo hazitaangamizwa wakati mmoja na ile sehemu ya kidini.—Ufunuo, sura ya 17; Mathayo 24:21.