Songeni Mbele, Ninyi Wahudumu wa ule Ufalme!
“Fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza [kabisa] huduma yako.”—2 Timotheo 4:5.
1. Ni nini tofauti kati ya hali ya kiroho ya Babeli Mkuu na ile ya Mashahidi wa Yehova?
LEO, katika nchi nyingi, malisho ya kiroho ya dini ya uongo yamenyauka na maji ambayo juu yake Babeli Mkuu ameketi yanakauka. Jambo hilo linakumbusha unabii mmoja wa Isaya unaotimizwa katika wakati wetu, yaani, ule unaopatikana katika Isaya 65:13: “Tazama, watumishi wangu watakula, bali ninyi mtaona njaa; tazama, watumishi wangu watakunywa, bali ninyi mtaona kiu; tazama, watumishi wangu watafurahi, bali ninyi [mtaona aibu].” Hivyo ndivyo ilivyo kwa sababu watu wa Yehova kwa hakika wanatafuta Ufalme kwanza, wakifanya kila jitihada kuhakikisha kwamba habari njema za ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Mwanawe aliye Mfalme, Kristo Yesu, zinatangazwa duniani pote.—Ufunuo 14:6-8; 16:12; 17:5, 15.
2. Ni nani wenye wajibu wa kusonga mbele wakiwa wahudumu wa Ufalme?
2 Mwito wenye kuamuru katika siku zetu ni ‘Songeni mbele, ninyi wahudumu wa ule Ufalme!’ Ili kutii mwito huo tukiwa jamii ya wafuasi wa Bwana yetu Yesu Kristo Mashahidi wa Yehova wote, wale walio katika vyeo vya uangalizi, pamoja na wengine wote, wanaume, wanawake, wavulana na wasichana, wana daraka la kuunga mkono ufalme wa Mungu. (Zaburi 145:10-12; 148:12,13; 2 Timotheo 4:2, 5) Hivyo ndivyo ilivyo hata ingawa wengine, kwa sababu ya hali, hawawezi kufanya mengi kama wengine. Hata hivyo utendaji wao unakumbusha yule mjane aliyetoa vyake vyote ingawa jumla yake ilikuwa sarafu mbili tu za thamani ndogo.—Luka 21:1-4.
3. Wanadamu wanazihitaji habari njema za Ufalme wakati huu kwa kadiri gani, na ujumbe huo wa Ufalme unatia nini?
3 Je! wanadamu leo wanauhitaji ufalme wa Mungu? Oo, wanauhitaji huo Ufalme kama nini! Wanauhitaji ili maumivu, magonjwa huzuni na kifo vikomeshwe na pia ili ukomeshe ukosefu wote wa haki, uovu wote, uhalifu wote, jeuri na vita, ndiyo, kukomesha uonezi wote, ubaguzi wote. (Isaya 9:7) Sisi tunaposonga mbele tukiwa wahudumu wa Ufalme tunawapa watu kitu cha kutumainia, kitu cha kuwategemeza mpaka Har–Magedoni ikomeshe taratibu ya mambo ya Shetani. Kwa sababu ya kuongezeka kwa uvunjaji wa sheria lazima tusonge mbele, tukiwa na ujumbe wa upendo na tumaini, na pia tukiwa na ujumbe wa kuonya kuhusu ‘siku ya kisasi upande wa Mungu.’—Isaya 61:2, NW.
4. Ni nini linalopasa kuwa kusudi la kwanza la kumfanya mtu awe mhudumu mwenye kutenda wa ufalme wa Mungu?
4 Hata hivyo, katika ulimwengu uliojaa vichocheo visivyofaa na uliojawa na roho ya kujipendeza, tunawezaje kuendelea tukiwa na roho ya kujinyima kwa kuwa wahudumu wa Mungu kwa ulimwengu? Kwanza kabisa, kwa sababu ya fadhili za upendo za Yehova tunazoonyeshwa, tunapaswa kutaka kusonga mbele kwa sababu ya kumpenda yeye, kwa sababu ya kuthamini yote ambayo ametufanyia, yote ambayo anatufanyia sasa na yote ambayo atatufanyia wakati ujao. Ni kama mtume Yohana anavyotukumbusha kwamba kupenda Mungu ni kuzitii amri zake, na mojayapo ya amri zake ni kuhubiri habari njema za ufalme wake. (Mathayo 24:14; 1 Yohana 5:3) Vilevile, Yehova Mungu analaumiwa kwa ajili ya taabu za wanadamu na anachongewa kuwa Mungu mwenye kuleta mateso ya milele. Hakika kumpenda Yehova, Baba yetu wa kimbinguni mwenye upendo, kutatusukuma tusonge mbele tukiwa wahudumu wake, na kusaidia kuondolea jina lake uchongezi huo mwingi wenye uovu.
5. Tuna kusudi gani zaidi la kutufanya tusonge mbele tukiwa wahudumu wa Mungu?
5 Vilevile kupenda watu wenzetu kutafanya tusonge mbele tukiwa wahudumu wa ufalme wa Mungu. Kupenda jirani yetu kutatufanya tuweke faida zake za kiroho, mambo yake ya milele, mbele ya starehe zetu za kimwili. Upendo utatusukuma tueneze eneo letu mara kwa mara na kufanya hivyo kikamilifu. Upendo utatuchochea tufanye ziara za kurudia na kukubali daraka la kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani ya kila juma pamoja na watu wenye kupenda kweli. Hiyo inamaanisha tunataka kuwa wenye fadhili, wenye kustahimili, wapole na wenye busara, na kuwafikiria wengine na kuwahurumia.
6. Kupuza huduma yetu kunawezaje kutunyang’anya furaha yetu?
6 Je! tunaliamini Neno la Mungu kweli kweli? Linatuambia kwamba “kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Tukipuza utumishi wa shambani tunaonyesha kwa vitendo vyetu kwamba kweli kweli hatuyaamini maneno hayo ya Yesu. Vilevile tunahakikishiwa kwamba ‘tukipanda kwa wingi tutavuna kwa wingi na ‘nafsi yenye ukarimu itafanikiwa’ na ‘yeye anyweshaye atanyweshwa.’ Hayo si maneno tu ya kupendeza bali ni kweli zisizoepukika ambazo zinajaribu upendo wetu kwa Yehova Mungu na kwa jirani yetu, ushikamanifu wetu kwa ufalme wa Mungu.—2 Wakorintho 9:6, NW; Mithali 11:25, NW.
7. Mtu anaweza kuonyeshaje kwamba hana hatia ya damu ya mtu ye yote?
7 Si maisha ya wengine yanayohusika peke yake. Lazima tusonge mbele tukiwa wahudumu wa ufalme wa Mungu ili tuwe huru na hatia ya damu. Kumbuka maneno ya Ezekieli 33:2-4: “Mwanadamu, sema na wana wa watu wako, uwaambie, Hapo nitakapoleta upanga juu ya nchi, watu wa nchi hiyo wakimtwaa mtu mmoja miongoni mwao, na kumweka awe mlinzi wao; ikiwa, aonapo upanga unakuja juu ya nchi hiyo, apiga tarumbeta na kuwaonya watu; basi mtu awaye yote aisikiaye sauti ya tarumbeta, wala haonywi, upanga ukija na kumwondoa, damu yake itakuwa juu ya kichwa chake mwenyewe.” Tunataka kuweza kusema kama alivyosema mtume Paulo: “Sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote.”—Matendo 20:26, 27.
NAMNA HUDUMA HIYO INAVYOTIMIZWA
8. Kwa kufaa ni maulizo gani yanayoulizwa juu ya namna huduma hiyo inavyotimizwa?
8 Hata hivyo, tunawezaje kusonga mbele? Kwa nguvu zetu wenyewe? Tukiwa na maelekeo ya kiburi, ya kujitegemea? Kutumaini uwezo wa kimwili? Au, kwa upande ule mwingine, kuwa waoga-waoga, wenye moyo nusu-nusu na wenye kuonyesha kuwaogopa wanadamu? Je! tutasonga mbele kwa kujitegemea, na kupuza uongozi wa wale wanaoongoza kati yetu? Sivyo kabisa! Kuna mambo matatu makuu hasa ya kuweka akilini:
9. (a) Mtu anakwendaje katika huduma hiyo kwa nguvu za Yehova? (b) 1 Petro 3:15 inatoa mwongozo gani kuhusu mwenendo wetu katika huduma hiyo?
9 Jambo la kwanza ni: Tunasonga mbele tukiwa wahudumu wa ufalme wa Mungu kwa nguvu za Yehova Mungu, kutumaini roho yake ituchochee, itupe maarifa na kututia nguvu. Tukisonga mbele kwa nguvu za Yehova tunaweza kuonyesha uhuru ule wa kusema, kule kusema waziwazi, ule ujasiri ambao Petro na Yohana walionyesha katika kushughulika na maafisa (wakuu) wa kidini wa siku zao. (Matendo 4:13) Wakati ule ule tunataka kuwa waangalifu kutoa ujumbe wetu kwa upole na heshima nyingi.—1 Petro 3:15.
10. (a) Ni nini maana ya mtu kuwa ‘mchukuaji safi’ wa ujumbe wa Yehova? (b) Ni nini shauri la Wafilipi 1:10, 11 kuhusiana na jambo hilo?
10 Jambo la pili ni: Tunataka kusonga mbele tukiwa wachukuaji safi wa ujumbe wa Yehova, kwa kupatana na yale tunayosoma katika Isaya 52:11: “Iweni safi ninyi mnaochukua vyombo vya [Yehova].” Vyombo vya Yehova leo, kweli zenye thamani za Neno lake, ni zenye kutakata, safi bora na zenye haki. Kwa hiyo wale wote wanaozipeleka kwa watu wanapaswa kuendelea kuwa safi kiadili na wenye kufaa kiroho. Je! sisi hatuwaaliki watu wajisafishe kiadili, waondolee mbali kazi za mwili, kama alivyofanya Yesu, ‘akiwaita wenye dhambi watubu’? (Luka 5:32) Kisha je! hatupaswi kuwawekea mfano mzuri katika mambo hayo? Kumbuka, Paulo aliwashauri hivi Wakristo katika Filipi: “Mpate kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi, ili mpate kuwa bila hitilafu na kutokuwa mkikwaza wengine mpaka siku ya Kristo, na mpate kujawa na matunda yenye haki, ambayo yanakuja kupitia Yesu Kristo, na kumletea Mungu utukufu na sifa.”—Wafilipi 1:10, 11, NW.
11. (a) Kujipamba ni kwa maana kadiri gani kwa mhudumu wa Mungu? (b) Tunapaswa kuweza kufuata mfano mzuri wa nani kuhusiana na jambo hilo?
11 Jambo la tatu ni: Katika kusonga mbele sikuzote tunapaswa kutaka kuwa tumevaa vizuri. Ni vigumu kufahamu kwa sababu gani mtumishi ye yote wa Yehova anataka kuiga mitindo inayoonyesha visehemu vya ufisadi, vyenye kuasi vya ulimwengu wa Ibilisi. Kwa sababu gani ujaribu kuwa kama ulimwengu ambapo unawaambia watu unakaribia mwisho wake kupitia vitendo vya haki vya Mungu? Kwa sababu gani ujaribu kuwa kama ulimwengu na hivyo uonekane tofauti na watu wa Yehova? Mahali pake, je! hatupaswi kuonekana kama watu wa Yehova, na hivyo tuonekane tofauti tunapokuwa kati ya walimwengu? Sisi tunajaribu kumpendeza nani? Tunajaribu kupata kibali ya nani? Kwa sababu gani usiangalie mavazi na mapambo yanayofaa kutoka kwa ndugu na dada waliokomaa ambao wamo katikati yetu kundini? Je! hatuwezi kupata kionyo na kuiga mfano wao mzuri?—1 Timotheo 2:19; 1 Petro 3:3, 4, 16, 17.
12. Ingawa huenda huduma ya nyumba kwa nyumba ikawa ngumu, inatoa faida gani kwa wale wanaoishiriki?
12 Kama ilivyo, si rahisi kwa wengine kwenda nyumba kwa nyumba wakiwa na habari njema za ufalme wa Mungu. Walakini thamani na matokeo ya kufanya hivyo yameonyeshwa mara kwa mara. (Mathayo 10:7,11-13; Matendo 20:20, 21) Matumizi yetu mazuri ya njia ya kwenda nyumba kwa nyumba kuhubiri yamekuwa ‘chapa ya kutambulisha’ ya watumishi wa kweli wa Yehova. Na kuna matokeo katika utoaji wetu wa ushuhuda kwa wengine, na pia utendaji wa nyumba kwa nyumba unafaidi sana sisi sote tunaoushiriki. Uhakika wa kwamba huenda mwili wetu ukauepuka unafanya uwe ni ushindi kila wakati mhudumu Mkristo anapoushiriki.—1 Wakorintho 9:16, 27.
KUTUNZA NA KUSIMAMIA JAMAA
13. Pamoja na wajibu wa huduma ya mtu, ni daraka gani walilo nalo wengi, na hiyo inataka usawa gani?
13 Wajibu wetu wa kuwa wahudumu wa Ufalme unaongezewa daraka jingine walilo nalo wale walio na jamaa. Wahudumu wenye kusonga mbele wa Ufalme walio na jamaa lazima wawafundishe watoto wao wenyewe, kwa sababu ya mgawo wao waliopewa na Mungu wa kuwa wazazi. Kila mwaka hesabu kubwa ya wale wanaobatizwa ni vijana ambao wazazi wao waliwalea “katika adabu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4, NW) Inasikitisha kusema kwamba wajibu huo na nafasi hiyo imepuzwa na wengine, na ikawa huzuni nyingi kwao. Hakika ili kuwa wahudumu wanaosonga mbele inahitaji usawa. Hatutaki kupuza utendaji wa nyumba kwa nyumba kwa kutoa kisababu kwamba tunatoa ushuhuda vivi hivi; wala hatutaki kupuza nafasi za kutoa ushuhuda wa vivi hivi kwa sababu tunakwenda nyumba kwa nyumba. Vivyo hivyo, wazazi hawapaswi kuruhusu utumishi wa nyumba kwa nyumba au madaraka ya kundi na kazi nyingine zimalize wakati mwingi sana hata wapuze jamaa zao. Wajibu wao wa kwanza ni kuangalia mahitaji ya kiroho na ya kimwili ya jamaa.—1 Timotheo 5:8.
14. (a) Walio wazazi wanawezaje kupoteza wakati waliotumia, utunzaji waliotoa na fedha walizotumia katika kulea watoto? (b) Ni uhitaji gani unaoendelea kuwapo katika kulea watoto toka utoto mpaka watu wazima walio vijana?
14 Ndiyo, watoto wanahitaji wakati, uangalizi na fedha. Imekadiriwa kwamba inachukua maelfu mengi ya fedha kulea mtoto awe mtu mzima. Njia hakika ya kupoteza fedha hizo, pamoja na wakati ni kukosa kutoa usimamizi mzuri wa kiroho kwa wale tunaowaleta ulimwenguni. Zao kubwa la uasi wa vijana leo linashuhudia uhakika wa kwamba watoto wengi wanaachwa na wazazi wao wafanye wanavyotaka. (Mithali 29:15) Vitoto na watoto wadogo mara nyingi wanabembelezwa na wazazi, watu wa ukoo na wengine. ‘Ai, wao ni malidadi kama nini! Ai, ni wazuri kama nini! Kisichana kipendwa cha mama, na Kivulana kipendwa cha baba!’ Huenda hayo yote yakawa kweli. Walakini wanapaswa kukumbuka kwamba wakati watoto hao wanapokua na kuingia utineja (miaka 13 mpaka 19 hivi), halafu kuwa wanaume na wanawake, wangali wanahitaji kutunzwa na kuangaliwa, kupendwa na kutiwa adabu, na kupewa mazoezi na elimu ya kiroho. (Kumbukumbu la Torati 11:18-21) Hilo ndilo daraka la Kikristo la wazazi. Wahudumu wa Mungu hawatasahau wajibu huo walio nao.
UMOJA WA DUNIANI POTE WA WAHUDUMU WA MUNGU
15, 16. (a) Tunawezaje kuwa na hakika kwamba ujumbe wa Ufalme tunaohubiri uko wazi na ni wenye sauti kubwa yenye kusikika wazi na wale wanaosikia? (b) Tuna msaada gani wa kutuwezesha kusema kwa upatano duniani pote?
15 Hata hivyo, fikiria mfano mwingine wa wahudumu Wakristo. “Baragumu ikitoa sauti isiyojulikana, ni nani atakayejifanya tayari kwa vita?” (1 Wakorintho 14:8) Kwa kutumia maneno hayo mtume Paulo alitoa mwito kwa wafuasi wa Kristo watumie ndimi zao katika njia ambayo wengine wangeweza kufahamu yaliyokuwa yakisemwa. Katika siku zetu ujumbe wa Ufalme tunaohubiri unapasa kuwa wazi, mwito wenye sauti kubwa wenye kusikika wazi na wanadamu, kisha kwa lazima tunapaswa kusema kwa upatano. Katika Isaya 52:8 NW, inasema: “Sikiliza! Walinzi wako wamepaza sauti yao. Kwa umoja wanaendelea kulia kwa furaha.” Ili kushiriki katika mwito huo wenye kuleta umoja, unyenyekevu na upendo wa kidugu ni mambo yanayohitajiwa. Tunajua kwamba ili utoaji wetu wa ushuhuda uwe na matokeo lazima sisi sote tuhubiri ujumbe huo huo, kutangaza jina la Yehova, hekima na upendo wake na Ufalme wake kuwa ndio tumaini pekee la wanadamu. Katika 1 Wakorintho 1:10 Paulo alishauri kwamba sisi sote tunataka kusema kwa upatano.
16 Hatupaswi kuruhusu ujumbe wetu upunguzwe uzito kwa sababu ya kutokuwa wazi. Tumepewa amri tukiwa wahudumu wa Mungu. Isaya 61:1, 2 inaonyesha wazi ujumbe wetu ni nini. Mtumwa mwaminifu na mwenye akili wa Yehova anafanya kila jitihada atusaidie tuseme kwa sauti yenye umoja, na kuchapisha Biblia na vifaa vya Biblia katika lugha nyingi ili watu wafikiwe kwa ujumbe unaoweza kufahamika. Tunaweza kufanya sehemu yetu kwa kutaka kueneza “habari njema” tukiwa jamii yenye umoja ya waabudu wa Yehova.—Zaburi 66:1, 2; 68:11.
JE! TUTAUTUMIA WAKATI HUO?
17. Ni kujichunguza gani kwa unyofu tunakopaswa kufanya kuhusu sehemu yetu katika huduma hiyo?
17 Kwa habari ya sisi mmoja mmoja kusonga mbele, je! inawezekana kwamba tufanye maendeleo zaidi katika kadiri ya wakati tunaotumia katika huduma yetu? Kila mmoja wetu aliye mhubiri wa kundi mwenye afya nzuri na asiye na wajibu wa kulea watoto au wa kutunza wapendwa wazee-wazee angefanya vema kuuliza hivi: Ni jambo gani linalonizuia nisifanye utumishi wakati wote? Je! yaweza kuwa ni kushindwa kuthamini kikamilifu umaana wa huduma ya Ufalme? Je! yaweza kuwa ni kushindwa kuwa na roho ya kujinyima? Ikiwa unaona njia yako ina vizuizi usiweze kutumikia ukiwa painia wa kawaida je! unaweza kutafutia nafasi utumishi wa painia msaidizi maishani mwako? Ikiwa unaweza kufanya hivyo, hakika utakuwa ukisonga mbele ukiwa mhudumu Mkristo. Kujichunguza kwa unyofu huenda kukakufunulia yale ambayo wewe binafsi unaweza kufanya kuhusiana na kuongeza wakati unaotumia kila mwezi ukitumikia faida za serikali ya Ufalme wa Baba yetu wa kimbinguni na Mwanaye.—Zaburi 26:1, 2,11, 12; Marko 12:28-34.
18. Ni jambo gani litakalotusaidia tuendeleze uhusiano mzuri pamoja na Yehova na Kristo Yesu?
18 Yehova Mungu na Yesu Kristo wametuwekea mfano kwa kuwa wenye kutazama mbele na wenye kusonga mbele. Ili sisi binafsi tufanye hivyo, kwanza kabisa, tunahitaji kuwa na uhusiano mzuri na Yehova Mungu. Je! tunajitahidi sana kuendelea kuwa na dhamiri njema, bila kuwa na maoni ya kutokujali wakati wo wote yanayoweza kuichafua dhamiri yetu? Je! tunatumia vizuri pendeleo lenye thamani la sala, na kudumu katika sala? (Warumi 12:12) Je! tunatoa wakati kwa funzo la kibinafsi na kutafakari? Pengine kuna mabadiliko fulani katika namna yetu ya maisha yanayopasa kufanywa ili tuyape mambo hayo yaliyo ya maana zaidi uangalizi unaohitajiwa, ili huduma yetu ichukue mahali pa kwanza maishani mwetu kwa neno na kwa tendo.—Waefeso 4:22-24.
19, 20. (a) “Neno la Mungu” linalozungumzwa katika Waebrania sura ya 4 ni nini? (b) “Neno” hilo limejithibitishaje kuwa li hai na ni lenye makali zaidi ya upanga wo wote wenye makali mawili, na kwa sababu gani tutarudia mambo makuu ya baadhi ya kazi iliyofanywa wakati wa mwaka wa utumishi wa 1981?
19 Ni furaha kuripoti kwamba ulimwenguni pote, wahudumu wa Yehova wamekuwa wenye shughuli sana na wenye kutenda katika kutangaza hizi habari njema za Ufalme katika mwaka uliopita. Ujumbe huo umekuwa na matokeo makubwa na yenye kudumu maishani mwa mamia ya maelfu ya watu. Mabadiliko mazuri ajabu yamefanywa katika maisha ya hao kwa sababu ya uwezo wenye kugeuza wa Neno la Mungu. Hakuna shaka kwamba ujumbe wa “habari njema” uko hai na kwamba unatoa nguvu na ni mkali zaidi ya upanga wenye makali mawili. (Waebrania 4:2, 12, 13) Vilevile, wakati neno la Mungu linapofanya kazi yake nzuri likitumiwa na wahudumu wanaostahili, jina la Yehova linatukuzwa na ufalme wake unashangiliwa kuwa tumaini pekee la wanadamu.—Waefeso 6:17.
20 Ili kuwapa ufahamu juu ya yale ambayo Mashahidi wa Yehova wameweza kutimiza katika kipindi cha miezi 12 cha mwaka wa utumishi wa 1981, habari ifuatayo itaonyesha yale ambayo yametokea katika wakati huo kutokana na jitihada zenye umoja za jeshi hili dogo la Wakristo wanaotenda katika nchi na visiwa vya bahari 206. (Mithali 25:25) Tuna hakika utafurahia marudio haya ya haraka ya mambo makuu ya kazi ya wahudumu wa Mungu katika hii karne ya 20.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Tunamtumaini Yehova atutie nguvu katika utumishi wake
[Picha katika ukurasa wa 5]
Mavazi nadhifu na kujipamba vizuri ni mambo yanayowafaa wahudumu Wakristo
[Picha katika ukurasa wa 5]
Wahudumu wenye kusonga mbele wanalea watoto wao ‘katika adabu ya Yehova’
[Picha katika ukurasa wa 8]
Wahudumu wazee-wazee wa Ufalme wanaendelea kusonga mbele