Ishara za Nyakati—Zina Maana Gani Kwako?
“Kutakuwako ishara katika jua na katika mwezi na katika nyota, na duniani huzuni kuu ya mataifa. . . . Lakini mambo hayo yanapoanza kutokea, jiinueni wima na kuviinua vichwa vyenu juu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”—Luka 21:25, 28, NW.
1. Yesu alijibuje ombi la Wayahudi la kutaka “ishara itokayo mbinguni”?
KUELEKEA mwisho wa huduma ya Yesu, viongozi wa kidini Wayahudi walimkabili aonyeshe “ishara itokayo mbinguni.” Akiwakemea, Yesu alisema hivi: “Kizazi kibaya na cha zinaa chataka ishara; wala hakitapewa ishara, isipokuwa ishara ya Yona.” Jambo hilo lilionyesha kwamba wao hawakuweza kufahamu maana ya ishara za nyakati, ama sivyo, walikuwa wakizipuza.—Mathayo 16:1, 4.
2. Kwa sababu gani ishara za nyakati zina maana kwetu leo?
2 Je! ishara za nyakati zina maana kwetu leo? Ndiyo, zina maana! Na tukitenda kulingana na maana ya ishara hizo, tutaokolewa na msiba mkubwa zaidi ya wo wote uliopata kutokezwa na hali mbaya zaidi ya hewa. Basi, na tuchunguze ishara hizo.
3. Matukio ya nyakati za Biblia yangali na maana kwetu sisi katika njia gani?
3 Matabiri ya kiunabii yaliyoonyeshwa katika Biblia Takatifu yanatupasha habari tele za ishara za nyakati na maana ya ishara hizo leo. Kwa mfano, tunaelezwa kwamba matukio yaliyotendeka katika maisha za watu wa Israeli wa kale hayakuwa na ubora wa kukumbukwa tu katika historia, bali tunaelezwa pia kwamba “mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani.” (1 Wakorintho 10:11) Kwa hiyo sisi leo tumetangulia kuonywa juu ya matukio yanayokuja. Tutaweza kuchukua hatua na kuuepuka msiba unaokielekea “kizazi kiovu na chenye kufanya uzinzi” kilichopo duniani tukiithamini maana ya matukio makubwa yanayotendeka siku hizi. Kwa njia hiyo hatutakuwa kama wale viongozi wa Kiyahudi wa karne ya kwanza ambao Yesu alisema hawakuweza kuijua maana ya ishara za nyakati.—Mathayo 16:4; Matendo 2:40, NW.
4. Yesu alitoa “ishara” gani yenye mambo mengi, nayo ilitia nini?
4 Yesu Kristo, yule Nabii Mkuu, alitoa “ishara” yenye mambo mengi ambayo yangetukia kuonyesha umalizio wa taratibu ya mambo ya leo ya ulimwenguni pote, licha ya kuuonyesha umalizio wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi katika karne ya kwanza. Licha ya kutabiri “vita na habari za vita,” yeye alitabiri kwamba kungetukia matukio yenye kuchacha duniani pote ambamo ‘taifa lingeinuka kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme. Pia, kungekuwako upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi mahali pamoja baada ya pengine.’—Mathayo 24:3-8, NW.
5. Manabii wa uongo wangekuwa na maoni gani kuhusu “ishara” hiyo?
5 Vilevile Yesu alitabiri kuja kwa manabii wengi wa uongo ambao wangetokea wakilitegemea jina lake, nao wangeuelekeza vibaya umati mkubwa wa watu kwa kuipuza maana ya “ishara” ambayo ingeonyesha kwamba yeye amekuwapo katika mamlaka ya Ufalme. Wao hawangeona maana yo yote katika ile “ishara” yenye mambo mengi iliyotolewa na Yesu, kama ilivyoandikwa katika Mathayo, sura za 24 na 25, wala hawangeona maana yo yote katika zile ishara nyingine ambazo zingeonyesha tumeufikia wakati wenye maana kubwa sana, kama vile kuharibika-haribika kwa jamii ya watu na kuharibiwa kwa dunia. Je! sisi tumeyashuhudia matukio hayo katika hii karne ya ishirini?
6. (a) Ijapokuwa wimbi la ghafula la taabu tangu mwaka 1914, viongozi wa kidini wameshindania nini? (b) Lakini hali za ulimwengu zinaharibikaje?
6 Lile wimbi kuu la taabu lililotokea kwa ghafula likawapata wanadamu kuanzia mwaka wa 1914 W.K., pamoja na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza hadi vita ya Ulimwengu ya Pili, halijapunguza nguvu mpaka sasa. Imekuwa hivyo ijapokuwa viongozi wa kidini wameviunga mkono vyama vilivyoundwa, kama ule Ushirika wa Mataifa uliotokomea, na Umoja wa Mataifa uliopo, ijapokuwa watu hao wanadai kwa mkazo wakisema tunachohitaji sasa ni kuwaweka katika vyeo vya kisiasa watu wanaofaa ili kuwe na uhakika wataturudisha upande wa Mungu tupate baraka. Hata hivyo, kila mahali kando yetu pana ushuhuda wa kuonyesha kwamba hali ya maisha duniani inazidi kuharibika, kwamba hali zinazidi kuwa mbaya zaidi, kwamba hofu na shuku, uhalifu na jeuri, yamekuwa ndiyo kawaida ya miaka hii ya kumalizia ya karne ya ishirini.
Wanayosema Viongozi wa Ulimwengu
7. Viongozi wa ulimwengu wanasema nini?
7 Je! hayo yanasikika kama kwamba ni kuona mambo kwa njia isiyo na tumaini? Kwa unyofu, watu wa siasa wanatambua hatari iliyopo. Kwa mfano, aliyekuwa balozi Mwamerika nchini Urusi, Thomas J. Watson, alitamka hivi alipokuwa akihojiwa: “Mimi nauona ulimwengu ukiwa wenye hatari zaidi ya vile umepata kuwa katika historia yake.” Halafu anasema yafuatayo Gunnar Myrdal, Mswedi anayeshughulikia mambo ya jamii ya watu na ya uchumi, ambaye kwa muda mrefu amekuwa mtu mwenye kutazamia matukio mazuri tu: “Kila kitu ni kibaya sana. Tuliamini tungesaidika tukifanya mabadiliko ya usimamizi, tukaamini elimu ingetusaidia. Sasa sisi tunaelekeana na ulimwengu ambapo ni vigumu kutazamia mambo mazuri tu wakati ujao.”
8. (a) Ni jambo gani lenye kutia wasiwasi lenye kuonekana sasa? (b) Ni mambo gani yaliyotabiriwa katika Ufunuo sura ya 6 yaliyo sehemu ya ishara za nyakati?
8 Je! unadhani hakuna sababu za kutosha zinazofanya kuwe na ukosefu huo wa kutazamia mambo mazuri kati ya viongozi mashuhuri wa ulimwengu wenye kufikiria mambo kwa uzito? Njia inayotumiwa sasa kulundika silaha nyingi mno kati ya mataifa ya dunia haijapata kuwa na kifani katika historia. Jambo hilo peke yalo latosha kuogopesha watu. Gharama ambazo zimetokana na jitihada hiyo ya kujipatia silaha nyingi zaidi zimefanya thamani ya fedha izidi kupungua na kuelekea kuharibu uchumi wa mataifa na kuyafanya yapandishe bei za bidhaa na za utumishi wa namna zote. Masimulizi ya Biblia katika Ufunuo yanatangulia kuonya kwamba bei za chakula zingepanda sana hata kibaba cha ngano kiuzwe kwa nusu rupia, au mshahara wa siku moja, wakati yanaposimulia uendeshaji wa wapanda-farasi wa Ufunuo wenye kufananisha vita, ukosefu mkubwa wa chakula na magonjwa. Lo! ndivyo ilivyo katika sehemu nyingi za ulimwengu wakati huu. Matukio hayo yenye kuogopesha ni sehemu ya zile ishara za nyakati, na kwa uhakika zina maana kubwa sana inayohusu maisha yetu.—Ufunuo 6:3-8.
ALiyotabiri Yesu Kristo
9. (a) Inaonekana ni hekima gani imepotelea mbali? (b) Ni unabii gani wa Yesu unaohusu sasa kabisa?
9 Inaonekana kwamba hekima ya wanasiasa na wanabiashara wenye hekima imepotelea mbali. (Isaya 29:14) Hakuna kiongozi wa siasa mwenye akili za uongozi aliye na utatuzi wenye kusadikisha watu kwamba atazimaliza taabu za ulimwengu au hata kumaliza matatizo ya taifa moja tu. Wao wanauogopa wakati ujao, sawa na alivyotabiri Yesu: “Kutakuwako . . . duniani huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea kwa sababu ya uvumi wa bahari na msukosuko wake, huku wanadamu wakizimia moyo kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu; kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.”—Luka 21:25, 26, NW.
10. (a) Ni kwa njia gani bahari imekuwa na “msukusuko”? (b) Ni kwa njia gani ‘nguvu za mbingu zimetikiswa’?
10 Kwa kuwa silaha za vita zinaongezeka upesi sana zisiweze kuacha kutengenezwa na mataifa, ile bahari halisi imejawa na vifaa vya vita vikiwa kwa namna ya manowari na sabmarini (meli ya kivita inayopita chini ya maji) zinazoweza kubeba makombora hatari ya nyukilia, yanayoweza kufagilia mbali mamilioni ya watu kwa mtupo wa kombora moja tu. Kweli bahari ina uvumi na “msukusuko.” Namna gani anga lililo juu yetu? Imekuwa kama Yesu alivyosema, kwamba “nguvu za mbingu zitatikiswa” kwa sababu ndege za vita, maroketi, makombora yanayoweza kurushwa mbali sana na kadhalika, vinaweza kuzipita bahari nyingi kuu na makontinenti zikapige vifaa vya maadui.
11. Njia za kupasha habari zinashuhudiaje kwamba mataifa ‘hawajui njia ya kutokea’?
11 Njia za kupasha habari zinashuhudia sana utimizo wa unabii huo kwamba mataifa ‘hawajui njia ya kutoka’ katika matatizo yao. Kwa mfano, yaangalie maelezo yafuatayo uliyopelekewa Umoja wa Mataifa katika ripoti yenye kurasa 300 ya tume yenye kuongozwa na aliyekuwa Waziri Mkuu wa Ujeremani ya Magharibi, Willy Brandt, yaliyoripotiwa katika gazeti Toronto Star la Mei 31,1980: “Jambo kuu la hiyo [ripoti] ni kwamba uchumi wa ulimwengu unaharibika, nayo mambo yakiendelea kuwa kama yalivyo sasa kutatokea machafuko makubwa sana. . . . Mambo mapya ambayo watu wanaweza kujivuna kwamba wamevumbua kila mahali ni kuweka kufuli mbili-mbili mlangoni, kuwa na walinzi wenye silaha na kuwa na woga wa kutoroshwa na wanyang’anyi na pia kuwa na woga wa kuuawa.” Halafu katika utangulizi wake binafsi kwenye ripoti hiyo, Brandt asema hivi: “Mara nyingi watu hufikiri vita ni pigano la kijeshi au hata uharibifu wa kijeshi. Lakini watu sasa wanazidi kujua kwamba hata machafuko makubwa ya raia yanaweza kuwa sawa na vita—machafuko yenye kuletwa na njaa waliyo nayo wengi, yenye kuletwa na uharibifu wa uchumi, misiba yenye kuharibu mazingira ya watu na uharamia pia.”
12. Ni kwa njia gani maneno ya Yeremia yanahusu wakati huu?
12 Basi, yamekwenda wapi tena yale mawazo ya kielimu na mipango ya kielimu inayopasa kutolewa na viongozi wa kisiasa na wa kibiashara katika hizi nyakati za hatari? Kama vile Yeremia nabii wa kale alivyoonyesha juu ya viongozi wa siku zake, ndivyo wakati wetu ulivyo: “Tazama, wamelikataa neno la [Yehova]; wana akili gani ndani yao?” (Yeremia 8:9) Wana akili ndogo sana!
13. Ni matukio gani duniani yanayoonyesha hali zenye kuwa mbaya zaidi za njaa, na jambo hilo linatimiza unabii gani?
13 Lazima wao wajue kwamba ongezeko kubwa la idadi ya watu na upungufu wa vyakula linaonyesha kwa mkazo kutokea kwa NJAA KUU, lakini sisi hatuoni hatua yo yote ya uthabiti wala mpango thabiti wa kuiondoa duniani pote hali hiyo ambayo tayari imekwisha kuharibika sana. Ripoti hiyo iliyotangulia kutajwa uliyopelekewa Umoja wa Mataifa inaeleza kwamba idadi ya watu ulimwenguni inaongezeka kama njugu—kila siku tano wanazaliwa watu wengine zaidi ya milioni moja, na inakadiriwa kwamba miaka ishirini inayokuja kutakuwa kumeongezeka watu wapatao bilioni mbili. Kadiri wanavyozidi kuongezeka ndivyo wanavyozidi kudai chakula, ingawa kuna mashaka mazito yenye kuonyesha kwamba labda nchi zenye kulima nafaka nyingi hazitaweza kuwatosheleza watu wengi sana wanaohitaji nafaka sasa. Ndivyo alivyotabiri Yesu, akasema “kutakuwa na njaa . . . mahali mahali” wakati wa hizi siku za kumalizia taratibu hii ya ulimwengu.— Mathayo 24:7.
14. Yesu alitabiri maovu mengine ya kisasa kwa maneno gani?
14 Halafu lifikirie ongezeko la uhalifu wenye jeuri unaotendwa katika mataifa yote yenye viwanda vikubwa vya kutengenezea vifaa. Vilevile Yesu alitabiri juu ya huko ‘kuongezeka kwa uvunjaji wa sheria.’ (Mathayo 24:12, NW) Je! kweli sisi tutaamini ati utatuzi wa mambo hayo ni kumpa kila raia bunduki yake mwenyewe na kumfundisha kuitumia? Lakini ni wazi kwamba hayo ndiyo mawazo ya viongozi wengi wa kilimwengu, kwa sababu wao wanasisitiza silaha za vita ziongezwe sana ili watu wapate amani kwa njia hiyo. Kwa sasa, wakati wanapoendelea kuwaza hivyo, inakadiriwa kwamba mamia ya mamilioni ya wanadamu wenzetu wanakufa njaa na hawapati chakula cha kuwatosha, na huku mamilioni wengine wanamalizwa na ugonjwa wa mbu (malaria) na kupata upofu unaotokana na mito—magonjwa hayo yakiwa ni magonjwa ambayo yangeweza kupunguzwa kama kisehemu kidogo tu cha pesa zinazotumiwa kuhusu silaha kingetumiwa. Hizo zote ni sehemu za ishara za nyakati ambazo Yesu alitabiri.—Luka 21:10, 11.
Wakati wa ‘Kuanza Kukimbia’
15. Kulingana na unabii wa Yesu, wale wanaotambua maana wanapaswa kuchukua hatua wakati gani, na jinsi gani?
15 Yesu Kristo, Nabii aliye mkubwa zaidi wa Mungu, alionyesha pia sehemu zenye maelezo marefu za ile ishara ya matukio mengi wanayopaswa kuyatii wale wanaotaka kuokoka uharibifu. Sehemu hizo zilikuwa gani? Yeye alisema: “Basi, mtamwona ‘Chukizo Haribifu’ aliyenenwa na nabii Danieli amesimama mahali patakatifu. (Hapo, msomaji na atambue maana yake). Wakati huo, walioko Yudea na wakimbilie milimani. Maana wakati huo kutakuwa na dhiki kubwa, ambayo haijapata kutokea tena.”—Mathayo 24:3, 15, 16, 21.
16. Mathayo 24:15, 16 ilikuwa na utimizo gani wa kwanza?
16 Unabii huo ulikuwa na utimizo wa kwanza wakati majeshi ya Waroma yalipovamia Yudea na Yerusalemu katika mwaka 66 W.K., na yakarudi tena katika mwaka 70 W.K. Hata hivyo, maneno ya Yesu yanatoa taarifa yenye kuogopesha zaidi kwetu wote tunaoishi katika miaka hii ya 1980. Tunajuaje?
17. Kwa sababu gani Mathayo 24:21 inapasa kuwa na utimizo wa kumalizia wa kisasa?
17 Uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., sio msiba mkubwa zaidi katika historia. Kumekuwako misiba mibaya zaidi kabla na baada ya huo, ikaleta taabu nyingi kuliko ya wakati huo na kuua watu wengi. Lakini unabii huu unasema habari za dhiki ambayo haijapata kuwa na mfano wake. Naam, dhiki iliyo ya mwisho, kwa maana “haitapata kutokea tena.” Basi ‘chukizo haribifu’ ni nini? Tunaambiwa tulione ‘limesimama mahali patakatifu.’ Je! tunaona utimizo wa kisasa?
18. (a) Wakati huu ‘chukizo’ ni nini? (b) Linasimamaje katika “mahali patakatifu”? (c) Matokeo ya mwisho juu ya dini za Jumuiya ya Wakristo yatakuwa nini? (d) Kulingana na Ufunuo, uharibifu wa dini utakuwa mkubwa kadiri gani, na utatangulia hatua gani ya mwisho kabisa?
18 Katika nyakati za kisasa ‘chukizo’ linalopinga ufalme wa Mungu na lenye uwezo zaidi ya Milki ya Roma limesimama “mahali patakatifu.” Ndio Umoja wa Mataifa, ambao sasa unatia mataifa 157 pamoja na mataifa makubwa yenye silaha za nyukilia zinazotosha kulipua wanadamu mara nyingi sana na kuwafagilia mbali kutoka duniani. Kilichorithi Ushirika wa Mataifa ‘kinachukiza’ kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo na wanafunzi wake kwa sababu kinafanya kimbelembele kusimama mahali pa ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Mfalme wake aliyewekwa Yesu Kristo, katika mbingu. (Mathayo 5:35; Marko 13:14) Lakini Jumuiya ya Wakristo vilevile inadai ina “mahali patakatifu.” Ni milki yake ya utendaji ambayo tayari imekwisha chukuliwa katika sehemu-sehemu zilizo kubwa za dunia na washiriki wa Umoja wa Mataifa wanaopendelea mabadiliko. Karibuni mifumo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo, na madai yo yote inayofanya kuwa ni “mahali patakatifu,” itafanywa ukiwa kikamilifu kama ule mfumo wa Kiyahudi wenye kupinga Ukristo katika mwaka 70 W.K.a Kama Ufunuo 17:5, 16, 17 unavyoonyesha, visehemu vyote vya dini ya uongo ulimwenguni pote—“Babeli Mkuu”—vitafanywa ukiwa wakati uo huo, kutangulia vita ya Har–Magedoni, ambayo ni hatua ya mwisho ya “dhiki kubwa.”—Ufunuo 16:14, 16; 19:11-21.
19. (a) Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamekosa kushiriki katika utendaji gani uliotabiriwa na Yesu, na kwa sababu gani? (b) Ni nani wamechukua daraka hilo, na matokeo yamekuwa nini?
19 Yesu alitabiri pia kwamba wakati wa kuwako kwa hali hizi za ulimwengu zinazozidi kuwa mbaya shughuli kubwa sana ya kuhubiri duniani pote ingeendeshwa na wafuasi wake waaminifu. Yakumbuke haya maneno yake: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Hakuna utendaji wa duniani pote kama huo unaoongozwa na viongozi wa dini za Jumuiya ya Wakristo, kwa maana wao ni rafiki za taratibu ya mambo ya ulimwengu huu. (Yakobo 4:4) Basi, ni nani wanaoitimiza amri hiyo? Je! wafuasi washikamanifu wa Yesu waliopo duniani, ambao si sehemu ya ulimwengu, hawakuwa wakijishughulisha sana kuzihubiri habari hizo za Ufalme waziwazi na nyumba kwa nyumba kwa miaka zaidi ya 60 sasa, wakijijulisha kwa watu tangu mwaka 1931 kuwa wanaitwa Mashahidi wa Yehova? (Isaya 43:10, 12) Na je! wao hawakuifunika dunia yote kwa mabilioni ya vitabu vyenye zile “habari njema” zinazosema kwamba karibuni sana ule ufalme au serikali inayotawalwa na Kristo akiwa mbinguni itachukua nafasi zote kabisa za tawala za kibinadamu zisizo na ukamilifu na zenye uchoyo? Licha ya utendaji wao kuleta habari njema kwa kuonyesha watu maana ya zile ishara za nyakati, utendaji huo umekuwa pia onyo la kimungu juu ya siku ya Mungu ya kisasi inayokuja.—Isaya 61:2.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mnara wa Mlinzi wa Aprili 1, 1972, kurasa 149-165, na Desemba 15, 1975 (Kiingereza), kurasa 741-744; pia “Your Will Be Done on Earth,” kurasa 275-283.
Je! unakumbuka jinsi kila moja ya sehemu zifuatazo za “siku za mwisho” inasimuliwa katika unabii wa Biblia?
◻ Vita vya ulimwengu vyenye kuhusu mataifa
◻ Njaa kuu ya duniani pote, matetemeko, maradhi ya kuambukia
◻ Ongezeko kubwa la kutokutii sheria, uhalifu, machafuko
◻ Kutokea kwa viongozi wa kidini wa uongo wengi
◻ Taabu isiyo na kifani kati ya mataifa
◻ Msukosuko wa bahari unaletwa na silaha za sabmarini (meli za kivita zinazopita chini ya maji)
◻ Mbingu zasukwa-sukwa na zana za vita
[Picha katika ukurasa wa 8]
Viongozi wa kidini Wayahudi walipomkabili Yesu aonyeshe ishara, yeye alifanya nini?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kama vile jeshi la Waroma lilivyokuwa likipatisha “mahali patakatifu” pa Wayahudi, ndivyo mataifa yenye kutaka mabadiliko yanavyotisha ile ambayo Jumuiya ya Wakristo inadai kuwa milki yake ya utendaji wakati huu. Huu ndio wakati hasa wa kukimbia!