Ile Minyororo ya Ushirikina
JE! WEWE ni mshirikina? Ikiwa ndivyo, hauko peke yako. Mchunguzi mmoja aliona vitu mbalimbali vya ushirikina zaidi ya 400,000 katika sehemu zote za ulimwengu. Kinachoonyesha kwamba ushirikina umo katika nchi za Wazungu, ni hoteli nyingi zisizo na orofa ya kumi na tatu, au kwa vile watu wanajaribu kuepuka kutembea chini ya ngazi au kuruhusu mapaka weusi kupita mbele yao. Uvutano uo huo usiofaa wa ushirikiana unaonwa katika Afrika, kama jambo hili lililoonwa linavyoonyesha.
Karibu miaka 20 iliyopita mume wa Wawa alikufa baada ya kuugua muda mrefu. Kwa muda wa siku tatu baada ya kufa kwake, Wawa alilala chini karibu na kitanda cha kufia cha mume wake akiwa analia na kuomboleza, huku watu wengi wenye kulia, wenye kuomboleza, wenye kucheza ngoma na kunywa pombe wakifanya makesha ya mfu huyo kumzunguka. Waombolezaji wengi hao walijishughulisha sana hivi kwamba wakakosa kulala usingizi na kufanya kazi. Kwa sababu gani? Walitaka kuthibitishia roho ya mwanamume huyo mfu na jamaa yake kwamba walikuwa rafiki zake.
Walio Hai Wanaogopa Wafu
Siku ya tatu maiti hiyo ilipelekwa kwenye makaburi, na kila mtu aliifuata. Sanduku la maiti lilitelemshwa katika kaburi na mawe madogo na vipande vya takataka vikatupwa juu yake. Kwa sababu gani? “Ili kuiambia roho ya mume wangu kwa heri,” asema Wawa. Kisha, kabla ya kufukia kaburi hilo, Wawa aliapa mbele ya kila mtu kwamba nyakati zote yeye alikuwa mwaminifu kwa mume wake. “Kama sikuwa hivyo,” akatangaza, “roho yake na inipige mpaka nife.” Tangu sasa na kuendelea maisha ya Wawa yalipasa yaongozwe na hali ya kuogopa roho hiyo ya mume wake mfu.
Jamaa ya mume wake ilizidi kumwambia Wawa hivi: “Ukifanya lo lote kirikiri [“la kipumbavu,” katika lugha ya Sango], roho yake itarudi ikuue.” Ili kuonyesha kwamba yeye alikuwa amempenda mume wake kweli kweli, hakuoga kabisa muda wa miezi mitatu, akavaa vazi la vivi hivi kuzunguka mwili wake na kulalia mkeka katika sakafu chafu-chafu. Wawa aliamini kwamba mumewe mfu alikuwa akitazama kila hatua yake. Sasa mwanamume ambaye alikuwa amependa akaonekana kuwa adui yake aliye mbaya zaidi.
Makabila mengine yanamtaka mjane anayeomboleza achukue kisu cha kuzuia kushambuliwa na roho ya mume aliyekufa. Ni lazima aepuke kuchungulia moto anapouwasha ili asije akamwona. Anaamka mapema usiku saa tisa au saa kumi kila asubuhi na kulia na kuomboleza ili aonyeshe kwamba angali anampenda. Naye anamtolea utumishi wa kwanza wa kila chakula kwa kutupa chini sehemu ya chakula hicho.
Wakati wa kumalizika kwa miezi mitatu Wawa alichukuliwa na jamaa ya mume akapelekwa kwenye kingo za mto uliokuwa karibu na kutumbukizwa majini. Hiyo ilikuwa ishara ya kwamba, mpaka hapa yeye alikuwa ameomboleza vya kutosha, hakuwa na roho zenye uovu. Wengine wanasema kwamba hiyo vilevile inaonyesha kwamba yeye hakuwa ameshiriki kumwua mume wake.
Lakini Sababu Gani Alikufa?
Katika akili za watu wengi katika sehemu hii ya ulimwengu, mtu hafi vivi hivi tu. Ni lazima mfu awe aliuawa kwa sababu ya ama kijicho cha kibinadamu au cha uwezo usio wa asili. Kwa sababu hiyo, wakwe wa Wawa hawakumsaidia katika taabu yake. Mara baada ya kufa kwa mume wake, ndugu mdogo ya mume wake alimpigia Wawa kelele, akisema: “Wewe ulimpa dawa ili akupende, lakini uliifanya ikawa na nguvu mno ikamwua!” Wengine walimshtaki wakisema: “Ulimloga hata akafa.”
Baada ya ‘kujiosha akawa safi’ katika mwezi wa tatu, walizidi sana kumsumbua. Nyakati zote alikuwa akilazimishwa awape fedha, chakula au pombe. Maskini Wawa alijilalamikia, akisema: “Mimi ndimi mwenye uhitaji. Sababu gani ni lazima nizidi kupelekea jamaa ya mume wangu vitu hivi?” Walakini, hakuthubutu kukataa, kwa kuogopa roho ya mume wake.
Mwishowe, baada ya miaka miwili yenye kujaa woga, kipindi cha kuomboleza cha Wawa kikamalizika. Alipewa nafasi ya kuolewa na kaka ya mume wake, kisha ndugu wadogo wa mume wake. Alipokataa matoleo yote hayo, alikuwa huru kurudi kwa jamaa yake mwenyewe. Lakini, hata hivyo, Wawa aliamini kwamba mume wake alikuwa akitafuta nafasi za kumwumiza.
Jambo la kusikisha ni la kwamba woga wote wa Wawa haukuwa na msingi wa kweli. Kulikuwa hakuna “roho za wafu” za kurudi kuja kuumiza wapendwa wao.Biblia inatuambia kwamba wafu hao ‘wanashuka kwenye kimya.’ Kwa kweli, wafu hao “hawajui neno lo lote . . . Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja.”—Zaburi 115:17; Mhubiri 9:5, 6.
Kwa tokeo zuri, tangu wakati huo Wawa amejifunza hayo. Sasa anajua kwamba woga wao mkuu ulikuwa wa kipumbavu ushirikina na bila msingi wo wote. Lakini mamilioni wengi wangali wana woga wa namna hiyo. Kwa sababu gani? Ni nini kinachotia watu katika minyororo ya ushirikina? Je! Minyororo hiyo inaweza kuvunjwa?
[Picha katika ukurasa wa 4]
Mume wa Wawa alipokwisha kufa, ndugu mdogo wa mume wake alimpigia Wawa kelele, akisema: “Wewe ulimpa dawa ili akupende, lakini uliifanya ikawa na nguvu mno ikamwua!”