Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 3/1 kur. 14-19
  • Mwe Kama Wanaume Wanaoelekeana na Har–Magedoni Bila Kuogopa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwe Kama Wanaume Wanaoelekeana na Har–Magedoni Bila Kuogopa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kinachohitajiwa Sasa na Wanaume Walio wa Mungu
  • Kuokoka Katika Upande Wenye Kushinda Katika Har–Magedoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Faida za Wanadamu Kutokana na Ushindi Katika Har–Magedoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Chanzo cha Taabu ya Wanadamu Chakaribia Kuondolewa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Njia ya Uzima au Njia ya Mauti—Njia Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 3/1 kur. 14-19

Mwe Kama Wanaume Wanaoelekeana na Har–Magedoni Bila Kuogopa

1. Katika kutaja Har–Magedoni, ni kwa njia gani Theodore Roosevelt alikosea kuhusiana na mtajo wake wa wakati?

INASEMEKANA kwamba wakati Theodore Roosevelt alipokuwa akigombea urais wa United States (Amerika), yeye alipaza sauti hivi: “Tunasimama penye Har–Magedoni, nasi tunampigania Bwana!” Roosevelt alijua kutokana na Biblia kwamba kungekuwa na pigano la kukata maneno kwenye “mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har–Magedoni.” (Ufunuo 16:16) Yeye alitangaza jambo hilo mapema sana, kwa maana alikufa Januari 6, 1919, au muda unaopungua miezi miwili baada ya kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Pigano hilo halikusonga mbele likawe “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni.

2. Wakati wa ile vita ya vita vyote, ni jambo gani litakaloamua kama tutaiokoka au hatutaiokoka?

2 Walakini, katika mwaka huu wenye misukosuko wa 1983, vionyesho vyote vinatuonyesha kwamba tunaelekeana na vita ya vita vyote. Kuokoka kwetu au kutokuokoka vita au pigano hilo kutaamuliwa hasa na hali tutakayokutwa tukiwa nayo katika uhusiano wetu na Mungu Mwenye Nguvu Zote.

3, 4. Kwa sababu ya msimamo ambao Wakristo hawa watachukua kwenye vita hiyo, watahitaji kuonyesha nini ili ‘waendelee kama watu wa kiume’?

3 Kwa kweli “roho [au semi zenye kuogozwa na] mashetani” ndizo zinazoelekeza watawala wa ulimwengu wajikusanye pamoja kumpinga Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote ili wapambane naye vitani kwenye Har–Magedoni.​—Ufunuo 16:14-16.

4 Jina la Kiebrania Har–Magedoni linamaanisha “mlima wa kusanyiko la askari wa vita.” Lina maana ya kivita! “Askari wa vita” ni hao “wafalme wa ulimwengu wote,” kutia ndani watawala wa kisiasa wa Jumuiya ya Wakristo. Mashahidi waliojiweka wakf na kubatizwa wa Yehova hawamo kati ya askari hao. Wao hawatahitaji kupigana kwa kutumia silaha za kimwili, bali watakalofanya tu ni kuwa watazamaji wa pigano hilo. Kwa kuwa mashahidi washikamanifu wa Yehova watakuwa ndio lengo kuu lenye kuonekana la shambulio kwa sababu wanatetea kwa uthabiti ufalme wa Yehova kupitia Kristo, watahitajiwa kuwa na ushujaa kama wa Kristo ili waweze ‘kuendelea kama wanaume.’​—1 Wakorintho 16:13, NW; linganisha 2 Mambo ya Nyakati 20:17.

5, 6. Mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, wakati mabaki wenye kuokoka wa watu wa Yehova walipoelekeana na kazi iliyokuwa mbele yao, walijisikia kama nabii gani aliyeelekeana na uharibifu wa Yerusalemu muda wa maisha yake?

5 Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipokuwa imekwisha mwaka wa 1918, hali za mabaki ya Waisraeli wa kiroho na kazi iliyokuwa mbele yao zilifanana na hali za kijana mwanamume aliye huko katika Mashariki ya Kati yenye misukosuko mingi. Kijana huyo alikuwa kuhani Myahudi jina lake Yeremia mwana wa Hilkia. Mji wa Yerusalemu, ambao ndani ya hekalu lake alitumikia akiwa kuhani, ulikuwa umetabiriwa kupatwa na maangamizi muda wa maisha yake mwenyewe. Hata Jumuiya ya Wakristo, inayodai kuwa ndiyo mfananishwa wa kiroho na mchukua- nafasi ya Israeli wa kale katika upendeleo wa Mungu, inaelekeana na uharibifu, muda mfupi tu kabla ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni. Kwa sababu ya kuwa mwokokaji wa uharibifu wa Yerusalemu wa karne ya saba kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, Yeremia aliweza kuandika kitabu cha Maombolezo ya magofu yake kwa kuongozwa na Mungu.

6 Wakati kazi hiyo ya kiunabii ilipowekwa mbele ya kijana Yeremia ili aifanye, yeye alisema: “Aa, Bwana [Yehova]! tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” Lakini Yeremia aliambiwa hivi: “Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao; maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe, asema [Yehova].”​—Yeremia 1:4-8.

7. (a) Yeremia alipaswa kutumikia akiwa nabii kwa watu wangapi, na ni kwa ajili ya watu wangapi “nabii” anahitajiwa kutumikia leo? (b) Je! Kutumikia kwake kwa kadiri hii kunamaanisha kwamba atapata mafanikio kuhusiana na mataifa, au ni kwa ajili ya nani huruma ingali ikionyeshwa?

7 Yeremia alipaswa kutimiza sehemu ya mwanamume mtu mzima, kwa maana mambo aliyoongozwa na Mungu wake ayaandike yangekuwa ya maana kwa wanadamu wote, hata leo. Yehova alimfanya awe “nabii wa mataifa.” (Yeremia 1:5) Sasa leo, kinachohitajiwa zaidi sana ni “nabii wa mataifa,” huku mataifa yenye kutetea sana nchi zao na kung’ang’ania kauli yao wenyewe yanapoendelea kukusanywa bila kubembelezwa yakafikie kivumbi chenye kukata maneno kabisa kwenye Har–Magedoni. Hiyo si kusema kwamba ule ujumbe wa Mungu uliopewa kwa “nabii wa mataifa” wa kisasa utaweza kuyageuza yauache mwendo unaoyaongoza kwenye uharibifu wao hakika. Lakini kuna wanadamu mmoja mmoja wanaohusika. Watu hao wasio na hesabu wasingetaka wapotelee mbali na mataifa walio raia zayo, baada ya kuonywa. Ikiwa watu hao wanaweza kuchukua hatua wasiangamie, wao hawataki kukutwa wakipigana kwa kumpinga Mungu Mwenye Nguvu Zote ati kwa sababu tu wananufaisha (wanasaidia) serikali ya kibinafsi ya wanadamu. Yehova ameonyesha huruma akatokeza “nabii wa mataifa” kwa ajili ya watu hao wenye mioyo inayofaa. Yehova amefanya hivyo katika huu “wakati wa mwisho,” tangu ilipomalizika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza Novemba 11, 1918.​—Danieli 12:4.

8. “Nabii” ambaye Yehova ametokeza na ambaye ni lazima kazi yake imalizwe kabla ya Har–Magedoni anatambulishwa kuwa nani au nini?

8 Yehova ametokeza “nabii” kwa ajili ya watu hao ambao kwa mioyo yao wanatafuta utawala wa Mungu badala ya utawala wa mwanadamu. “Nabii” huyo si mwanamume mmoja kama alivyokuwa Yeremia, bali ni jamii ya watu wengi. Washiriki wa jamii hiyo wako kama kuhani-nabii Yeremia. Wamejiweka wakf kabisa kwa Yehova Mungu kupitia Kristo na, kwa kuzaliwa kwa roho takatifu ya Yehova, wamefanywa wawe sehemu ya “mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki [ya pekee].” (1 Petro 2:9) Wakati huu ambao siku zimekwenda sana, ni mabaki wachache tu wa hii jamii ya “nabii” ambao wangali duniani. Ile “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni haiwezi kuanza kabla “nabii” huyo mwenye washiriki wengi hajamaliza kazi yake.

9. (a) Yeremia alishuhudia kwa macho yake mamlaka gani ya ulimwengu ikiushinda mji mkuu wa watu wa kali wa Yehova? (b) Ni mji gani wa kali unaofananisha Jumuiya ya Wakristo? (c) Jumuiya ya Wakristo imekuwa sehemu ya nini? (d) Wakati Babeli Mkuu atakapoharibiwa, ni jambo gani litakalopata Jumuiya ya Wakristo, na kwa sababu gani?

9 Sasa kuna jambo moja la hakika: ikiwa jamii ya “nabii,” yaani jamii ya Yeremia, inaelekeana na Har–Magedoni, inaelekeana pia na anguko la Babeli Mkuu. Ni kweli kwamba Yeremia wa zamani hakushuhudia kwa macho yake anguko la Babeli wa kale, lakini alitoa sana unabii juu ya kupinduliwa kwa hiyo mamlaka ya ulimwengu ya tatu ya historia ya Biblia. Milki hiyo ya ulimwengu ilipata chanzo chake katika Babeli ule wa kwanza, au Babiloni, ulioanzishwa na Nimrodi “mwindaji hodari wa nguvu katika kumpinga Yehova.” Milki hiyo iliambukiza ulimwengu wa kale wa wanadamu dini yake ya uongo. (Mwanzo 10:8-12, NW) Yeremia alishuhudia kwa macho yake ushindi ambao Babeli ya kale ilijipatia juu ya Yerusalemu mwaka wa 607 KWK. Kwa njia hiyo yeye alishuhudia mahali pakuu pa kale pa dini ya uongo pakiushinda mji mkuu uliokuwa na hekalu la Yehova lakini ukawa umeichafua dini safi ambayo Yeye alikuwa ameukabidhi. Kwa sababu hiyo Yerusalemu wa kale unafananisha Jumuiya ya Wakristo ya kisasa. Jumuiya ya Wakristo imeonyesha inadai kiuongo kuwa ndiyo makao ya Ukristo wa kweli. Imeshikwa mateka na dini ya Kibabeli kisha ikawa sehemu kubwa ya Babeli Mkuu wa kisasa, yaani ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Wakati Babeli Mkuu atakapoharibiwa na wanasiasa wenye kuchukizwa, kama ilivyotabiriwa katika Ufunuo, sura ya 17 na 18, Jumuiya ya Wakristo itadidimia pia ndani ya uharibifu huo.

10. Kuokoka kwa Yeremia anguko la Yerusalemu kulitangulia kufananisha nini, na muda mfupi baada ya kifananishwa hicho, ni jitihada gani ya mataifa itakayoshindwa kutimiza lengo lake?

10 Yeremia aliokoka anguko la Yerusalemu na makao ya mji huo mwaka wa 607 KWK, na hiyo ilimhakikishia kwamba alikuwa ndiye mnenaji wa kweli wa Yehova. Kwa utimizo wa mfano huo wa kiunabii, jamii ya leo ya Yeremia itaokoka anguko linalokaribia lenye mshindo mkubwa la Jumuiya ya Wakristo. Muda mfupi baada ya hapo watu wasio wa kidini wa huu mfumo wa mambo watajitahidi kwa ukali mwingi kuifutilia mbali jamii ya Yeremia itokomee, lakini jitihada zao zitakomeshwa ndi​—kwenye Har–Magedoni.​—Ufunuo 16:16; 19:19-21.

11. Yule mtu asiye Myahudi aliyefanya urafiki na Yeremia akiwa katika shida kubwa huko Yerusalemu alitangulia kufananisha nani, na hawa wanalingana na nani katika mfano wa Yesu ulio kwenye Mathayo 25:31-46?

11 Ebed-meleki Mwethiopia ni mtu asiyekuwa Myahudi aliyeuokoka uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 KWK. Masimulizi yanayomhusu yametolewa katika Yeremia sura ya 38 na 39. Yeye alimsaidia Yeremia akiwa katika uhitaji mkubwa sana, na kwa sababu hiyo ikawa anaweza kuwaogopa Wayahudi wale mashuhuri waliokuwa wakitaka kumnyamazisha Yeremia kwa kumwua. Lakini, kwa unabii wa pekee uliotolewa kupitia nabii huyo aliyekuwa amemwokolea uhai wake kwa ujasiri, Ebed-meleki alihakikishiwa na Yehova kwamba angeipata nafsi yake kama nyara na kwa hiyo angeokoka uharibifu uliokuwa ukiijia nchi ya Yuda na Yerusalemu mji mkuu wake. Katika mambo hayo Ebed-meleki Mwethiopia alitangulia kufananisha kondoo wa mfano wa Yesu uliohusu kondoo na mbuzi. Unapatikana katika Mathayo 25:31-46. Kwa sababu ya kuwa rafiki za mabaki ya “ndugu” za kiroho wa Yesu Kristo na kuwafanyia mema ya moja kwa moja katika huu “wakati wa mwisho,” hao kondoo wa mfano hawatakatiliwa mbali pamoja na jamii ya “mbuzi” kwenye Har–Magedoni. Wakiwa chini ya ulinzi wa Yehova kupitia Mfalme anayetawala, Yesu Kristo, watauingia mfumo mpya wa mambo bila ya hesabu yao yote kumalizika duniani kwa kufa. Mbele yao watakuwa na nafasi ya kupata uzima wa milele katika paradiso ya kidunia.

Kinachohitajiwa Sasa na Wanaume Walio wa Mungu

12. Hali za kuogopesha za nyakati zetu zinalingana na unabii gani wa Yesu Kristo kuhusu “wakati w mwisho”?

12 Nyakati tunazoishi sasa zinakuwa za kutia hofu nyingi zaidi na zaidi. Huu ni utimizo barabara wa mambo ambayo Yesu Kristo mwenyewe alitabiri yangekuwa ushuhuda wa kwamba tunaishi katika “wakati wa mwisho,” wakati ambao kifananishwa cha kisasa cha uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 70 WK kitatukia. (Luka 21:5-7) Ili kutufaidi sisi leo zaidi ya mitume na wanafunzi wa karne ya kwanza, Yesu aliendelea kusema hivi: “Pia, kutakuwako ishara katika jua na katika mwezi na katika nyota, na duniani huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea kwa sababu ya uvumi wa bahari na msukosuko wake, huku wanadamu [Kigiriki anʹthro·poi] wakizimia moyo kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa. Na halafu wao watamwona Mwana wa mtu akija katika wingu kwa uwezo na utukufu mkuu.”​—Luka 21:25-27, NW.

13. Yesu alionyeshaje kwamba kunapasa kuwe tofauti kati ya nia ya mioyo na akili za watu wa ulimwengu na ile ya wanafunzi wake wenye kuelimishwa?

13 Hapo Yesu alitofautisha kati ya “wanadamu” (anʹthro·poi), au watu, walio wa ulimwengu huu au mfumo wa mambo na wanafunzi wake wenye nuru ya elimu ambao hasa ndio aliowatolea unabii wake wenye maelezo ya wazi ili wafaidike. Wafuasi wake wenye habari na ufahamu wasingekabwa na “huzuni kuu ya mataifa,” wala mioyo yao ‘isingezimia kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.’ Hawakupaswa kuacha vichwa vyao viiname kwa majonzi, kwa kukosa tumaini. Basi, walipaswa kuwa na nia gani, maoni gani ya akilini na moyoni? Walipaswa kuwa kama vile Yesu alivyoendelea kusema: “Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.”​—Luka 21:28.

14. Je! “ukombozi” unaokaribia unamaanisha kutukuzwa kwa mabaki mbinguni, na ni akina nani duniani watakaoelekeana na lile taraja zuri ajabu litakalofuata baada ya huo “ukombozi”?

14 Hivyo shida zinazozidi kuongezeka sana zitakazofikia upeo katika vita kwenye Har–Magedoni ni uthibitisho wa uharibifu unaokaribia kwa wanadamu walio wa ulimwengu huu. (Wafilipi 1:28) Jambo hilo linafanya Mkristo wa kweli leo apaswe kuwa mtu mwenye imani yenye nguvu katika Mungu Mwenye Nguvu Zote na ahadi zake alizowatolea waaminifu. “Ukombozi” ambao sasa umekaribia kwa watu hao wenye imani sio kwanza kutukuzwa mbinguni kwa mabaki ya wanafunzi wa Kristo waliozaliwa kwa roho kisha kuondolewa kwao katika mazingira ya kidunia yenye dhiki, ingawa wamewekewa jambo hilo akibani walipate mwishowe. Bali, “ukombozi” unaotajwa ni kukomeshwa kwa vita, njaa kali, magonjwa ya kipuku, matetemeko ya ardhi na mateso ya kiwazimu yanayofanywa juu ya wafuasi wa kweli wa Mfalme anayetawala, Yesu Kristo. Mambo hayo yatakomeshwa kwa kuwaharibu adui wote wa ufalme wa Yehova kupitia Kristo katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye ile inayoitwa Har–Magedoni. Ndipo kutakapokuwa na taraja zuri ajabu mbele ya mabaki ya warithi wa ufalme wa kimbingu na wenzi wao washikamanifu waliotangulia kufananishwa na Ebed-meleki, yule msaidiaji shujaa wa nabii Yeremia!

15. Ili ‘waendelee kama wanaume,’ wanahitaji kufanya nini kulingana na Maandiko ili wawe na vifaa vya kazi?

15 Ili hawa sasa waweze ‘kuendelea kama wanaume’ au kujitokeza kama wanaume, ni lazima wafikie kukomaa kwa Kikristo na kuwa na vifaa vya kazi ya kutoa ushuhuda wa mwisho ulimwenguni pote juu ya ule ufalme wa Kimasihi. (1 Wakorintho 16:13, New World Translation, Authorized Version, Revised Standard Version; Mathayo 24:14) Hiyo ndiyo sababu tulipewa Biblia ikiwa na Maandiko matakatifu. Ni sawa na vile mtume Paulo alivyomwandikia kijana Timotheo: “Andiko lote liliongozwa na Mungu na ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kutengeneza mambo, kwa kuadibisha katika haki, ili mtu wa Mungu apate kuwa na uwezo wa kutosha, aliye tayari kabisa kwa kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17, NW) Kulingana na The New English Bible, mstari wa 17 unasema: “Ili kwamba mtu aliye mali ya Mungu apate kuwa mwenye uwezo na mwenye vifaa kwa ajili ya kazi nzuri ya kila aina.” The Jerusalem Bible inasema: “Hivi ndivyo mtu aliyewekwa wakf kwa Mungu anakuwa kikamili na vifaa na kuwa tayari kwa kazi nzuri yo yote.” Hiyo inaonyesha kwamba “mtu wa Mungu” anahitaji kujifunza kwa ukawaida Maandiko yaliyoongozwa na Mungu na kuishi kulingana nayo, akitimiza kazi ambayo kujifunza kwake kumemtayarisha aifanye kwa njia ya kuiweza.

16. Kwa sababu gani sasa inafaa sana wale wanaoendelea kukua wakawe watu wazima wakimbie tamaa za ujanani, zaidi sana kuliko siku za Noa zilizotangulia gharika?

16 Tunaishi katika wakati ulio hatari zaidi ya nyakati zote katika historia yote ya kibinadamu! Tunaelekeana na kupitilia mbali kwa ulimwengu, ulimwengu wenye mapana na marefu makubwa kuliko wa siku za Noa. Kwa hiyo tumo katika kazi iliyo kubwa na ya maana zaidi ya kazi zote ambazo wanadamu wamepata kuzifanya mpaka sasa. Hakika huu sio wakati wa shahidi ye yote wa Yehova Mungu aliyejiweka wakf na kubatizwa kufurahisha tamaa zake za ujana na nyege zenye kuondosha fikira zake upande unaofaa. Ni kama vile Paulo alivyomwandikia Timotheo mwenye hali ya ujana: “Zikimbie tamaa za ujanani.” “Walakini, wewe, Ee mtu [Kigiriki, anʹthro·pos] wa Mungu, toroka kutoka mambo haya.” (2 Timotheo 2:22; 1 Timotheo 6:11, NW) Leo, zaidi sana kuliko wakati mtume Yohana mwenye kuongozwa na Mungu alipoandika maneno haya, imekuwa kwamba “ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”​—1 Yohana 2:17, NW.

17. Ni akina nani tusiopaswa kuwadharau ambao walikuwa wanaume wa Mungu wa zamani, lakini tunapaswa kutegemea nani ambaye ndiye mfano mkamilifu wa wanaume hao?

17 Katika hizi siku zinazohitaji watu waonyeshe uanaume wa Kikristo, tunahitaji kuutazama mfano mkamilifu wa Yule ambaye Gavana Pontio Pilato alimtaja akiwa mbele ya kundi la Wayahudi wengi wenye zahama, wakati aliposema: “Tazama, mtu huyu!” “Tazama, mfalme wenu!” (Yohana 19:5, 14, NW) Muda mrefu kabla ya Kristo kuja walikuwako wanaume wa Mungu, kama “Musa, huyo mtu wa Mungu [wa kweli],” na Eliya na Elisha mwenzi wake, na wengine. (Kumbukumbu la Torati 33:1; 1 Wafalme 17:18, 24; 20:28; 2 Wafalme 1:9-12; 4:7, 9, 16) Lakini, ingawa hatutawapuza wala kuwadharau hao wanaume wa Mungu wa nyakati za kabla ya Ukristo, inatupasa tumtegemee Yule anayebaki kuwa ‘mwanamume wa Mungu’ anayepita wote waliopata kuwa duniani. Huyu ndiye Yesu Kristo, ambaye sasa anatawala akiwa Mfalme katika mbingu tangu kumalizika kwa majira ya Mataifa mwaka wa 1914. (Waebrania 11:1 mpaka 12:3; Luka 21:24) Tukijitokeza wenyewe kama wanaume wa mfano wake, tunaweza kuelekeana bila kuogopa na uharibifu wa huu mfumo wa mambo uliohukumiwa maangamizi kwenye Har–Magedoni.

18. Ni kwa njia gani tunaweza kutimiza daraka letu lililo kubwa ajabu la kushiriki katika kuondolea lawama enzi kuu ya ulimwengu mzima ya Yehova Mungu?

18 Wakati ulimwengu wa zamani unapoendelea kushuka, sisi tunajifanyia kumbukumbu lisilofutika na lisilotoweka wakati huu wa hukumu. Je! kumbukumbu hilo litatuletea ustahili na sifa, au litatuletea laana ya milele pamoja na ulimwengu, jamani? Kwa kuendelea kama wanaume katika kuiga mfano wetu usio na kosa, Yesu Kristo, tutathibitisha kwamba ‘mungu wa ulimwengu huu,’ Shetani yule Ibilisi, siye mtawala wetu wa kiroho. (2 Wakorintho 4:4) Bali, tutakuwa kwa njia hiyo tukitetea enzi kuu ya ulimwengu mzima ya Yehova Mungu. Hivyo tutashiriki kuiondolea lawama iliyoletwa juu yake mbele ya viumbe vyote vilivyo hai. Lo! tuna daraka kubwa kama nini katika jambo hili! Lo! ni nafasi yenye utukufu kama nini!

19. Zaidi ya kukesha na kuwa imara katika imani, ni kwa njia gani sisi kama “wanaume” tunahitaji kukua, na ni nani chanzo cha jambo hilo?

19 Lililobaki kwetu ni kuendelea kukesha tuone pendeleo na nafasi yetu ya ‘kusimama imara katika imani.’ Yehova asiache tudhoofike maana sisi ni watu wa kiume walio wa Mungu, waliojiweka wakf kwa Mungu! Kwa kusudi hilo linalostahili tunahitaji kutii onyo la upole linalotolewa na mtume Paulo kwa wakati unaofaa kabisa, “Iweni wenye nguvu.” (1 Wakorintho 16:13, NW) Tutaweza kufanya hivyo na hakika tutafanya hivyo tukiendelea kumtegemea na kumpelekea Yeye sala kupitia Mfalme wetu, Yesu Kristo. Katika Isaya 40:29 tunaambiwa kwamba: “[Yeye] huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo.” Tutakapokwisha kushuhudia kwa macho yetu ushindi wa kimungu kwenye Har–Magedoni, na liwe pendeleo letu wakati huo kuyarudia kwa sauti maneno yaliyotamkwa na Musa baada ya kupinduliwa kwa majeshi ya Farao katika Bahari Nyekundu: “Yehova ni mtu mwanamume [Kiebrania, ish] wa vita. . . . Nguvu zangu na uweza wangu ni Yah, kwa kuwa yeye anatumikia kwa wokovu wangu.”​—Kutoka 15:3, 2, NW.​—Kutoka The Watchtower, October 1, 1982

Je! unaweza kujibu maulizo haya?

□ Ni jambo gani litakaloamua kama tutaiokoka au hatutaiokoka ile vita kwenye Har​—Magedoni?

□ Ni hali gani za leo za watumishi wa Yehova waliotiwa mafuta zinazofanana na zile za mtumishi wake wa kale Yeremia?

□ Ni katika mambo gani utumishi uliofanywa na Ebed-meleki ulitangulia kufananisha utendaji wa “kondoo” wa mfano wa Kristo ulio katika Mathayo 25:31-46?

□ Kulingana na unabii wa Kristo katika Luka sura ya 21, nia ya wafuasi wa Kristo inatofautianaje na ile ya watu wa mataifa?

□ Ni “ukombozi” gani unaotajwa katika Luka 21:28?

□ Sisi sote tukiiga mfano wa Yule aliyetambulishwa kuwa “mtu huyu!” matokeo mazuri yatakuwa nini?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Ni utendaji wa nani uliotangulia kufananishwa na tendo la Ebed-meleki la kumsaidia Yeremia nabii wa Mungu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki