Tito Anashughulika na Mgawo Mgumu
“KWA Tito, mtoto wa kweli kulingana na imani wanayoshiriki watu kwa ujumla.” Bila shaka maneno hayo yalichangamsha moyo wa Tito alipoanza kusoma barua yenye kumpa mgawo, aliyopelekewa na mtume Paulo. Yeye alikuwa ameachwa Krete atumikie akiwa mwangalizi mwenye kusafiri, akizuru makundi tofauti-tofauti. Tito alikuwa amejithibitisha ‘kuwa wa kweli’ na kwa hiyo aliyastahili madaraka aliyokuwa amekabidhiwa.—Tito 1:4, NW.
Miaka 12 au zaidi kabla ya hapo, Paulo alikuwa ameenda na Tito huko Yerusalemu. Bila shaka Mkristo huyo “wa kweli” Mgiriki asiyetahiriwa alikuwako wakati mitume na wanaume wazee walipofikia uamuzi sahihi juu ya lile suala la tohara. Baada ya wao kuchunguza ushuhuda mwingi, waliamua kwamba haikuwa lazima Wakristo Mataifa, kama Tito, watahiriwe na kushika matakwa yote yaliyokuwa katika Torati ya Musa. Hakika lilikuwa tukio lenye kutia imani nguvu nyingi kwa kuwa kwenye mkutano huo wa maana sana!—Matendo 15:1-29: Wagalatia 2:1-3.
Hata hivyo katika Krete walikuwako wanaume walioshirikiana na makundi ambao waliendelea ‘kuishikilia tohara.’ Wao walikataa kukubaliana na baraza lenye kuongoza la huko Yerusalemu. Badala ya kujiwekea wenyewe maoni yao kwa kunyamaza, hao “wanaume watukutu” walikuwa wakifundisha kwamba ilikuwa lazima mtu apate tohara ndipo aweze kupata wokovu. Halafu ubaya uliozidi huo ni kwamba, hao “waongeaji wa mambo yasiyo na faida” waliunga mkono “hadithi za Kiyahudi” na amri zisizopatikana katika Torati ya Musa. “Wadanganyaji” hao walikuwa wakivunja-vunja imani ya “jamaa nzima-nzima.” Makundi katika Krete yalielekewa na tisho la kuwa na mgawanyiko.—Tito 1:10, 11,14, NW.
Tisho jingine lilikuwa mazingira yenye tabia mbaya sana ambamo Wakristo Wakrete walikuwa wametoka. Nabii mmoja Mkrete alikiri hivi: “Wakrete ni waongo sikuzote, hayawani wabaya, walafi wavivu.” Kama uneni huo ulivyoonyesha, Wakrete walikuwa kama wanyama-mwitu wanaovunja maungo ya mwili na kuua; walifurahia kuvunja-vunja sifa njema za wengine kwa kupiga porojo za uongo. Vitabia vibaya hivyo vilikuwa vimejipenyeza ndani ya makundi ya Kikristo ya Krete.—Tito 1:12; 3:2.
Katika barua yake, Paulo anapanga waziwazi namna matatizo hayo yalivyopasa kushughulikiwa. Tito alipaswa kutimiza mahitaji mawili ya maana: “Kwa sababu hii nilikuacha wewe katika Krete, [1] upate kusahihisha mambo yaliyokuwa na upungufu na [2] upate kuweka wanaume wazee mji baada ya mji, kama nilivyokupa maagizo”—Tito 1:5, NW.
Kusahihisha Mambo Yenye Upungufu
Huo ulikuwa mgawo mgumu. Kwa kukabiliwa na watokeza matata, Tito alipaswa kusimama imara kuitetea kweli, “kushikamana kwa imara na neno la uaminifu.” Wengine wangemdharau, watokeze mwito wa ushindani juu ya mamlaka yake. Lakini Tito alikuwa na tegemezo la kitheokrasi. Yeye angeweza kuelekeza kwenye barua ya kumpa mgawo wake, iliyosema: “Endelea kusema mambo hayo na kutia moyo na kukaripia ukiwa na mamlaka kamili ya kuamuru. Mtu ye yote asikudharau wewe kamwe.”—Tito 1:9; 2:15, NW.
Namna gani kama mtu alikataa karipio, akajaribu kuomba wengine katika kundi wamwunge mkono? Kwa rehema, watu wa namna hiyo wangepokea “onyo la upole la kwanza na la pili.” Kama jambo hilo halikufanikiwa, Tito aliagizwa hivi: “Mkatae huyo.” Maana yake ni kwamba mtu huyo angeondolewa katika ushirika, au atengwe na ushirika.—Tito 3:10,11, NW.
Wakristo fulani Wakrete waliyachukua mashauri kivivi-hivi tu kwa sababu ya kuwako kwa hali ya kutokujali sana mambo. Tito alipaswa ‘kuendelea kuwakaripia hao kwa ukali.’ Hata ndugu wenye umri wa uzee walihitaji kupewa kikumbusho cha ‘kuwa na kiasi katika tabia, kuwa wazito katika mambo.’—Tito 1:13; 2:2, NW.
Kuwekwa kwa Waangalizi
Makundi katika Krete yalikuwa na uhitaji wa kupata uangalizi mzuri. Je! Tito alipaswa kuchagua mshiriki aliye na ushawishi mkubwa zaidi na kumwagiza rasmi huyo awe kama “padri” juu ya kundi? Hapana, maagizo aliyopewa ni kwamba aweke “wanaume wazee mji baada ya mji.” Maana yake ni kwamba alipaswa kuhakikisha baraza la wazee liliwekwa kuangalia utendaji mbalimbali wa kundi.—Tito 1:5, NW.
Paulo anapanga matakwa kadha ya kutoa mwongozo katika uchaguzi wa waangalizi hao. Matakwa hayo yanategemea mwenendo hasa. Sifa ya kwanza ilikuwa kwamba lazima mwanamume ‘awe bila shtaka.’ Ingawa elimu ya juu haikutakwa, wanaume hao walipaswa kulijua “neno” la Mungu na kushikamana nalo kwa imara wakati wa kufundisha na ‘kukaripia wale wanaopinganisha.’ Matakwa hayo yana umaana ule ule wakati wa kufikiria wanaume watakaochukua vyeo vya uangalizi leo. Kwa mfano, Paulo aliandika hivi: “Yampasa mwangalizi awe . . . mshikamanifu.” Ushikamanifu huo unaonyeshwa kwa “kushikamana kwa imara na neno la uaminifu” kama linavyoelezwa katika vichapo vya tengenezo la Yehova la kisasa la Kikristo.—Tito 1:6-9, NW.
Yalikuwako mambo mengine ya maana ambayo kuhusu hayo Tito alihitaji “kufanya madai imara daima.” (Tito 3:8, NW) Mambo hayo yanaweza kugawanywa katika sehemu nne—tamaa, usemi, matendo na nia.
Kukaza Fikira juu ya Tamaa Zinazofaa
Katika barua aliyomwandikia Tito, Paulo anataja mara mbili ‘tumaini la uzima wa milele.’ Sisi tunaweza kuwa salama kwa kuweka mioyo yetu juu ya tumaini hilo kwa sababu ‘Mungu asiyeweza kusema uongo ndiye ameliahidi.’ (Tito 1:2; 3:7, NW) Kwa upande mwingine, ni jambo lisilo na upatani tena la hatari kuruhusu “tamaa za kilimwengu” zisongamane na kuzifunika hilo “tumaini la furaha,” linalotia ndani “kufunuliwa kwenye utukufu kwa Mungu mkuu na kwa Mwokozi wetu, Kristo Yesu.—Tito 2:11-14, NW.
Huko “kufunuliwa kwenye utukufu” wa Mungu kupitia Mwokozi wetu, Kristo Yesu, kunakaribia sana. Utakaohusiana na kufunuliwa huko ni uharibifu wa mfumo mbovu wote na wa watu wote ambao wametegemeza maisha yao juu ya vitu vya kimwili vyenye kuvuta tamaa za mwili. Basi, ni jambo la maana sana sisi tung’oe katika mioyo yetu, ndiyo, ‘tuzikatae kabisa tamaa za kilimwengu kisha tuishi pamoja na utawa katikati ya huu mfumo wa mambo ya sasa’!—Tito 2:11-14, NW.
Tuangalie Usemi Wetu
Watu “wenye maneno yasiyo na maana,” “waongo,” ‘wenye kujibu kwa ukaidi,’ ‘wenye kusema kwa njia yenye madhara’ na kuwa na “uulizaji wa kipumbavu”—maneno hayo yanafunua kwamba matumizi ya ulimi yalikuwa yakifanywa kwa njia mbaya katika kisiwa cha Krete. Hata ilikuwa lazima Tito aonye dada wenye umri wa uzee wasiwe “wachongezi.” Mashauri ayo hayo yanahitajiwa leo.—Tito 1:10, 12, UV; 2:3, 9; 3:2, 9, NW.
Kwa mfano, ingawa dada mmoja mzee-mzee alikuwa mwenye juhudi katika utumishi wa shambani katika kundi moja, yeye alikuwa na maelekeo ya kuwanenea-nenea vibaya watoto wake walio wakf waliokuwa wamefikia umri wa watu wazima, hata akawa akinenea mume wake asiyeamini. Ikawa lazima mmoja wa wazee atolee kundi hotuba juu ya jambo hilo, bila kutaja jina. Kwa kweli, je! sisi tuna haki ya kunenea kwa matusi mwanadamu ye yote aliye hai? Barua ya Paulo iliyoongozwa na Mungu ambayo aliandikia Tito inajibu: “Usiseme kwa njia yenye kuletea madhara mtu ye yote.” Badala ya hivyo, ni lazima Wakristo wakaze fikira zao juu ya kutumia “usemi unaofaa ambao hauwezi kulaumiwa.”—Tito 3:2; 2:8, NW.
Matendo Yanayopendeza Mungu
“Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana.” (Tito 1:16) Watokeza matata katika makundi ya Krete walilingana na maelezo hayo. Paulo anatofautisha matendo yao kwa kukazia uhitaji wa kuwa na “matendo mema.” (Tito 2:7,14; 3:8,14) Kwa kuweka mfano katika tendo lililo jema zaidi, Paulo alitaja “kuhubiri kule ambako mimi nilikabidhiwa.” (Tito 1:3, NW) Yesu aliwakabidhi wafuasi wake wote kazi hiyo ya maana; kwa hiyo kazi hiyo inapasa kupangiwa nafasi ya kwanza katika orodha yetu ya “matendo mema” tunayoyafanya kwa ukawaida.—Mathayo 28:19, 20.
Vilevile zinazotiwa kati ya “matendo mema” zingekuwa ni jitihada za akina baba za kulea “watoto waaminio.” Kwa wake hizo zingetia ndani “kufanya kazi nyumbani mwao, . . . kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe.” Wale wanaojitia katika kazi ya kimwili wangefuata kanuni inayopatikana katika Tito 2:9, 10 kwa kuwatii matajiri wao wa kazi kwa heshima, ingawa hawako chini ya utumwa Pia, Wakristo wanatakwa “kunyenyekea . . . serikali na mamlaka kama watawala na “kuwa tayari kwa kila kazi nzuri.”—Tito 1:6; 2:5, UV; 3:1, NW.
Kudumisha Nia Sahihi
Wakristo Wakrete walihitaji kudumisha nia sahihi kuelekea watenda dhambi wa kilimwengu, wasiwe wakiwanenea kwa njia ya matukano bali ‘waonyeshe upole wote kuelekea watu wote.’ Sisi leo tunahitaji kufanya ivyo hivyo. Au sivyo, jitihada zetu za kuwasaidia waukubali ujumbe wa Ufalme hazitapata matokeo. Pia, sawasawa na ilivyokuwa katika Krete ya kale, sisi tunahitaji kujihadhari na mashirika yetu Tusipofanya hivyo, ni kwa njia gani nyingine tunaweza kuitii amri ya ‘kukataa kabisa hali ya kutokumwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu kisha tuishi pamoja na utawa katikati ya huu mfumo wa mambo ya sasa’?—Tito 3:2; 2:12, NW.
“Hata sisi wakati mmoja tulikuwa hatuna akili, tulikuwa wasiotii, tukawa tukipotezwa njia,” ndivyo alivyosema mtume Paulo. Je! Yehova alikuwa na wajibu wa kutuokoa sisi katika hali hiyo yenye dhambi? Hapana, ‘haikuwa kwa sababu ya kazi zo zote za uadilifu tulizokuwa tumefanya bali ni kulingana na rehema yake yeye alituokoa.’ Kwa kujizoeza imani katika damu ya Kristo iliyomwagwa, Wakristo wanapata msamaha wa dhambi zilizopita na kulipokea “tumaini la uzima wa milele” lililo zuri ajabu. Hizo ni “fadhili Zisizostahilika” za namna bora kabisa, tena ni sababu yenye nguvu ya kutufanya tuepuke tamaa mbaya na kudumisha usemi unaofaa, matendo mema na nia yenye rehema kuelekea jirani zetu—Tito 3:3-7, NW.
Kwa uhakika Tito alishukuru sana kwa msaada huo wenye upendo aliopewa katika mgawo wake mgumu! Bila shaka alirudia mara nyingi kuisoma barua ya Paulo, akataja-taja maneno ya barua hiyo alipokuwa akifundisha na kutoa mashauri. Mamilioni leo wanaitumia ivyo hivyo barua hiyo iliyoongozwa na Mungu ili kujifaidi wenyewe na wengine. Yaliyomo katika barua hiyo ni mambo mema na yenye kufaidi kweli kweli.