Magonjwa Ni Ishara ya Siku za Mwisho?
WANASAYANSI wanafanya maendeleo ya haraka sana katika kufasiri maana ya vipokeza-urithi vya chembe ya mwili wa kibinadamu. Wengine wanaamini kwamba wanakaribia kuyakomesha yale maelekeo ya kupatwa kwa mtu na magonjwa kwa sababu alizaliwa akiwa na chembe za urithi zenye hali ya kuambukiwa upesi na magonjwa. Inadaiwa kwamba hivi karibuni itawezekana kuponya magonjwa fulani kwa kubadili kidogo chembe zako za urithi.
“Uwezo wa kuingiza chembe za urithi ili kuponya magonjwa ukiisha kupatikana, kutakuwa pia na uwezekano wa kuingiza chembe za urithi kwa makusudi ya kubadili maumbo ya mwili,” anadai Dakt. W. French Anderson wa Taasisi za Kitaifa za Afya. Anaongeza kusema: “Itawezekana kuanza kuchezea-chezea miili yetu ya kibinadamu kwa kuibadili-badili.” Hilo ni dai la kujitanguliza mno. Je! linaonyesha kwamba sayansi inaendelea kupata ushindi wa kupambana na magonjwa na maradhi?
Jambo la kupendeza ni kwamba, miaka zaidi ya 1,900 iliyopita, Yesu Kristo alionyesha kuwa kuwako kwa magonjwa na maradhi kungekuwa “ishara” yenye kuonyesha “siku za mwisho” zimefika. Alikiita kipindi hicho “umalizio wa mfumo wa mambo.” Yesu alisema: “Kutakuwako . . . mahali hapa na mahali hapa magonjwa ya kipuku.” Kulingana na Albert Barnes, mwanachuo wa Biblia, hayo ni “magonjwa yenye kuenea kwa nguvu nyingi, yenye kupata watu wengi sana kwa kipindi kimoja.—Mathayo 24:3-7, NW; 2 Timotheo 3:1, UV; Luka 21:10, 11, NW.
‘Lakini sikuzote kumekuwa na magonjwa ya kipuku, au maradhi,’ huenda wewe ukasema hivyo. Hiyo ni kweli. Lakini, kuna mambo mawili yanayostahili kuangaliwa juu ya utabiri wa Yesu.
Kwanza, Yesu hakusema kwamba magonjwa au maradhi ndiyo pekee yangekuwa ile “ishara.” Bali, yeye alitoa ishara yenye mambo mengi ndani. Jisomee mwenyewe unabii wake wenye maelezo marefu kama ulivyopangwa katika Mathayo 24 na 25, Marko 13 na Luka 21. Tukio moja silo pekee linalokuwa ile “ishara.” Bali, “ishara” yenyewe ingeonekana wakati tu mambo yote yaliyotabiriwa na Yesu yangekipata kizazi kimoja.—Mathayo 24:32-34.
Pili, lingeelekea kuwa jambo lisilo na upatani maneno ya Yesu juu ya magonjwa ya kipuku, au maradhi, kuwa yanatimia leo. Kwa sababu gani? Kwa sababu wakati huu ndipo maendeleo ya kisayansi yamefikia hali ya juu kuliko nyakati zote zilizotangulia. Sehemu na vifaa vya kufanyia matibabu zimepata maendeleo makubwa sana kuliko zamani. Sasa ndio wakati ambao maarifa ya tiba yameenea sehemu nyingi zaidi ya zamani zilizopita.
Kwa hiyo, je! mambo ya uhakika yanaonyesha nini? Je! maneno ya Yesu yanatimia kweli kweli? Ni jambo la maana tujue, kwa maana utimizo wa unabii wa Yesu ungeonyesha kwamba tunaishi katika kipindi kilicho cha hatari zaidi ya vipindi vingine vyote vya historia ya kibinadamu.