Umeenda Wapi Utii kwa Amri Inayosema ‘Waheshimu Wazazi Wako’?
BABA mmoja alisema hivi juu ya wana wake wawili: “Wakati ninapoeleza maoni yangu, wao wanatenda kama kwamba wamechoshwa sana na maneno yangu wasitake kuyavumilia. Umeenda wapi utii kwa amri inayosema ‘Waheshimu Wazazi Wako’? ” Vivyo hivyo, mkurugenzi wa shirika la kutumikia jamaa alisema hivi: “Siku hizi, si kwamba tu watoto wanarudishia wazazi wao maneno wakati wanaposemeshwa, bali pia wanaonyesha ukaidi kwa ukawaida juu ya mamlaka ya wazazi.”
Kama wewe ni kijana au ni mtu mzima, inaelekea umeona kwamba leo vijana wengi wanakosa kutii wazazi wao kisha wanawadharau. Hilo ni jambo wewe unapaswa kuhangaishwa nalo, kama wewe ni kijana au mzazi. Kwa sababu gani?
Kwa sababu hali za kutopatana unazoona ni sehemu ya kiolezo, mfululizo wa matukio, ambacho kinazionyesha nyakati hizi kuwa siku za mwisho. Kulingana na Biblia, kipindi kinachoitwa “siku za mwisho” kinakuja kabla ya uharibifu kamili wa mfumo wa mambo wa ulimwenguni pote. (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, kutakuwa na waokokaji ambao watafurahia maisha wakiwa chini ya serikali halisi ya kimbingu.—Danieli 2:44; Ufunuo 21:1-4.
Lakini kutokutii wazazi kunapatanaje na yale ambayo Biblia inasema juu ya wakati wa sasa na wakati ujao? Katika matoleo yaliyotangulia ya Mnara wa Mlinzi tumerudia kujikumbusha unabii wa Yesu Kristo kwenye Mathayo 24, Luka 21 na Marko 13 (NW ). Yesu alikaza fikira juu ya matukio ya ulimwengu ambayo yangeonyesha “umalizio wa mfumo wa mambo”: vita, matetemeko ya ardhi na kutokutii sheria, hayo yakiwa ni machache tu kati ya aliyoyataja. Lakini, sasa sisi tunakaza fikira juu ya maelezo ya kiunabii juu ya kipindi hiki cha wakati. Yanapatikana kwenye 2 Timotheo 3:1-5. Badala ya kutaja nguvu za nje zinazoleta mabadiliko fulani juu ya wanadamu, hapa Biblia inakazia maoni ya watu wenye kupatwa na matukio hayo yenye kutazamisha sana. Inasema hivi:
“Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi... hao nao ujiepushe nao.”
Angalia kwamba maneno hayo ya mtume Paulo yanaeleza namna siku za mwisho zingeleta matokeo yazo juu ya watu. Ona, pia, kwamba ‘kutokutii wazazi’ kungekuwa jambo lenye kutendeka sana wakati wa kipindi chenye hatari kinachoitwa siku za mwisho.
Jambo Hili Linatimizwa Siku Zetu?
Huenda wengine wakauliza, ‘Tunajuaje kwamba Paulo hakuwa akisema habari ya hali ya siku zake tu? ’ Kwa kuwa mtume alifuatisha unabii wake na mashauri kwa Mkristo mwenye kuitwa Timotheo, wengine kwa kufaa wanataka kujua kama kweli Paulo aliandika kuhusu siku zetu. (2 Timotheo 3:5, 14, 15) Lakini, angalia kwamba Paulo anasema kwamba “siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.” Bila shaka alikuwa akitaja tukio la wakati ujao. Timotheo aliambiwa ‘ajiepushe’ na watu wenye kudhihirisha vitabia visivyo vya kutamanika, kwa kuwa wengine walikuwa tayari wakifanya hivyo katika kundi. Lakini maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba katika siku za mwisho za wakati ujao hali ingekuwa ya hatari zaidi.—Linganisha 2 Wathesalonike 2:6-12; 3:6-14.
Hata hivyo, huenda ikawa wewe umekwisha kusikia wachunguzi fulani wakidai kwamba leo vijana walio wengi wanapatana na wazazi wao kwa kiasi cha kutosha. Kulingana na 2 Timotheo 3:1-5, wewe utayaonaje madai ya namna hiyo? Kabla hujakata maneno, acha turudie kujikumbusha unabii wa Paulo kwa kuulinganisha na hali za huko nyuma katika historia ya Biblia.
“Waheshimu Baba Yako na Mama Yako’’
Hivyo ndivyo ilivyosema ya tano kati zile Amri Kumi. (Kutoka 20:12) Maneno hayo yalikazwa juu ya akili za watoto wa Kiyahudi. (Kumbukumbu la Torati 5:16; 6:6, 7) Kutokutii wazazi wa mtu kulikuwa jambo lisilofikirika—katika visa vingine likiwa ni kosa lililostahili adhabu ya kifo’, (Kumbukumbu la Torati 21:18-21) Njia ya kale ya maisha ilisaidia wazazi kudumisha uongozi huo wenye upendo lakini wenye vizuizi thabiti. Akina baba walihusika sana katika mipango ya jamaa. Madaraka ya wazazi yalijulikana waziwazi kabisa. Watoto walionwa kuwa mali yenye faida, baraka, na kazi mbalimbali katika jamii yao yenye kufuata ukulima ziliwapa shughuli nyingi za kufanya.—Linganisha Zaburi 127:3.
Lakini, taifa hilo lilipoendelea kulegea kwa kuziacha njia za Yehova, maisha ya jamaa yalizorota. Karibu miaka 800 baada ya zile Amri Kumi kutolewa, nabii Mika alisema hivi: “Mwana humwaibisha babaye, na binti huondoka ashindane na mamaye . . . adui za mtu ni watu wa nyumbani mwake mwenyewe.” (Mika 7:6) Vivyo hivyo, Ezekieli alisema hivi juu ya mji wa Yerusalemu: Ndani yako wamedharau baba na mama.” (Ezekieli 22:7) Madharau makubwa hivyo kwa wazazi yalikuwa dalili ya kushuka kwa adili kulikokuwa kumeenea sana. Basi, Mungu alichukua hatua ya kulitolea taifa zima nidhamu kali.—Yeremia 1:15, 16.
Ukiangalia mambo kutokea upande huo, inaelekea utakubali kwamba sehemu kubwa ya mwenendo wa watoto wa karne ya 20 ungalionekana na Paulo kuwa wa kuchukiza sana huko nyuma katika karne ya kwanza. Maoni ya siku hizi ya kulea watoto kwa kuwapa uhuru mwingi sana hayakuwako siku hizo. Kwa hiyo, tunahitaji kukumbuka kwamba uchunguzi unaofanywa kisha baada ya hapo inasemwa kwamba maisha ya kisasa ya jamaa ni mazuri sana unakosa kujali viwango ambavyo Mungu amewekea watoto. (Waefeso 6:1-3) Wakati maoni na mwenendo ulio wa kawaida sana kati ya watoto wa leo yanapolinganishwa na viwango vya Mungu, tunaweza kufahamu sababu gani Biblia inaita kizazi cha sasa ‘kisichotii.’ Si kusema kwamba watoto wote ni waasi. Lakini kutokutii kumeenea sana kwa njia yenye kuonekana wazi na iliyokolea—yenye kuonekana wazi sana.
Lakini je! kweli ‘kutokutii wazazi’ ni jambo la ulimwenguni pote? Je! kuna ushuhuda wa kutosha wa kwamba wazazi na watoto hawapatani kuonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho”?—2 Timotheo 3:1, 2.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
‘Si watoto wote walio waasi lakini kutokutii kumeenea sana kwa njia yenye kuonekana wazi na iliyokolea’