Woga Unakupata Wewe?
“KUNA misiba yenye maafa makuu leo katika ulimwengu.” Ndivyo alivyoandika René Dubos, mwanasayansi na mwanafalsafa, katika kitabu chake cha hivi juzi kinachoitwa Celebrations of Life (Maadhimisho ya Uhai). Aliendelea kusema hivi: “Lakini, nyingi ya huzuni kubwa ya sasa haitokani na magumu yanayotupata hasa, bali inatokana na tazamio la maafa ambayo hayajatokea, ambayo huenda yasitokee kamwe.” Ndiyo kusema, mwanadamu anaogopa wakati ujao kwa sababu anaishi akitazamia kutokea kwa mambo yasiyo ya uhakika na yasiyoweza kuzuiwa.
Kulingana na Dubos, ni nini mengine ya maafa yanayoonekana kuwa yanaweza kutokea wakati ujao? “Sisi tunatiwa wasiwasi mwingi sana na uwezekano wa kutokea vita ya nyukilia na wa misiba mikubwa kweli kweli inayoweza kutokezwa na mipasuo ya chembe za nyukilia... Sisi kwa ujumla tuna wasiwasi kwa sababu tunatazamia kwamba hali za ulimwengu zitazidi kuwa mbaya ikiwa hesabu ya watu na mambo ya ufundi yataendelea kuongezeka kwa kiasi ambacho yanaongezeka sasa. Karibuni dunia itajawa na watu kupita kiasi kisha mali zake za asili zimalizike; kutakuwa na upungufu wa chakula wenye kuleta maafa makubwa.” Ingawa René Dubos mwenyewe ni mtu mwenye kutazamia mema wakati ujao, yeye anatambua kwamba sisi tunaishi katika “hali ya huzuni kubwa ambayo sasa imeenea katika sehemu kubwa ya ulimwengu.”
Alvin Toffler, mtu anayeshughulika na hali za kijamii aliye mwandikaji pia, alitumia miaka mitano akihoji watu wa namna nyingi juu ya matokeo yatakayoletwa na badiliko na wakati ujao katika maisha yao. “Washindi wa zawadi ya Nobeli, mahipi, madaktari wanaochunguza ugonjwa wa neva na akili, matabibu, wafanya biashara, wataalamu wanaochunguza mambo ya wakati ujao, wanafalsafa, na walimu walisema wana hangaiko kwa sababu ya badiliko, wana masumbuko juu ya kupata badiliko maishani, wana woga wa namna nyingi juu ya wakati ujao.” (Mwandiko wa italiki ni wetu.) Uchunguzi wake ulimthibitishia kwamba imekuwa kawaida ya watu kuwa na masumbuko na woga juu ya wakati ujao.
Hali hiyo ya kutazamia mabaya wakati ujao ambayo wanadamu kwa ujumla wamekuwa nayo wakati wa karne hii ilitabiriwa vizuri na Yesu Kristo karibu miaka 2,000 iliyopita. Yeye alikuwa ametabiri kwamba hekalu lililokuwa Yerusalemu lingeharibiwa, na wanafunzi wake walitaka sana kujua “mambo hayo yatakuwa lini nayo ni nini ishara ya kuwa mambo hayo ya karibu kutukia?”—Luka 21:7.
Katika kisehemu cha kwanza cha jibu lake, Yesu alisimulia matukio ambayo watu wengi wa kizazi hicho waliendelea kuwa hai wakayaona. Lakini alitumia ulizo lao kwa faida ili kutia ndani matukio ya ulimwenguni pote ambayo yangeshuhudiwa, si na kizazi hicho cha mwisho cha waabudu wa Kiyahudi waliofanya ibada yao hekaluni, lakini, kwa maana zaidi, na wale ambao wangeishi waupite umalizio wa mfumo huu wa sasa wa ulimwengu. Yeye alionya hivi: “Pia, kutakuwako ishara katika jua na katika mwezi na katika nyota, na duniani huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea kwa sababu ya uvumi wa bahari na msukosuko wake, huku wanadamu wakizimia moyo kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu; kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.”—Luka 21:25, 26, 32, NW.a
Kwa wazi, katika vizazi vilivyopita wanadamu wameishi pia katika woga—woga wa kupatwa na vita katika sehemu walizokaa, wa kupatwa na magonjwa ya mapigo, maangamizi makubwa na badiliko katika hali ya jamii ya watu. Lakini je! kile kizazi cha mwaka wa 1914 kiliona jambo tofauti? Ndivyo kwa uhakika, kwa sababu ‘dunia yote inayokaliwa na watu,’ mataifa yote, imepatwa na matokeo hayo tangu wakati huo ulioanzisha badiliko kubwa. (Luka 21:25, 26, NW) Mambo mengi sana yametukia katika muda wa miaka 69 iliyopita mpaka watu walio wazee-wazee ambao wamepatwa nayo wakawa na wasiwasi mwingi na woga. Na sasa, kwa sababu ya tisho la kuweza kutokea kwa vita ya nyukilia, watu wa umri wote, hata watoto, wanasumbuka kwa kutaka kujua wanaweza kutazamia kuishi muda mrefu namna gani. Kwa kufaa imesemwa kwamba jambo linalohangaisha moyo zaidi katika karne ya 20 ni WOGA.
Lakini labda wewe unafikiri tunatia chumvi. Je! woga unaohusu matukio ya sasa na ya wakati ujao umeenea vya kutosha hivi kwamba tunaweza kuamini unatimiza unabii wa Yesu? Je! kweli woga huo ni sehemu ya uthibitisho wa kwamba sisi tuko katika wakati wa mwisho? Je! hiki ndicho kipindi cha wakati ambao ‘wanadamu wanazimia moyo kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu’?
[Maelezo ya Chini]
a Biblia ya Kispania ya Kikatoliki inayoitwa Cantera-Iglesias inatoa maelezo ya chini juu ya masimulizi yanayolingana na hayo ambayo yamo katika sura ya 24 ya Mathayo. Inasema hivi: “Uzuri wa hekalu unampa Yesu nafasi ya kutabiri uharibifu wake; wanafunzi wanauliza uharibifu huo utakuwa wakati gani (mstari wa 3), halafu ulizo hilo linatokeza utangulizi wa habari inayohusu maangamizi makubwa ya mwisho ya ulimwengu, tarehe ya maangamizi yenyewe na ishara zenye kuyatangulia.”