Je! kwa Kweli Ni “Ajali Tu”?
“Hata uwe nani au uwe unafanya nini si kitu,” mtu huyo mwenye huzuni akasema, “mambo kama hili yanaweza kutokea.” Vipande vikubwa vya mwamba vilikuwa vimeanguka kutoka juu ya jengo, vikamgonga rafiki yake na kumuua. “Ni ajali,” akamalizia kwa moyo mzito.
Lakini kwa kweli, je, sisi ni vinyangarika vilivyo hoi vya jambo fulani linaloitwa ajali? Ulizo hilo limevuruga wanadamu kwa karne nyingi. Na kuna sababu nzuri ya kuvurugika hivyo. Ni kama Mfalme Sulemani alivyosema wakati mmoja: “Wenye mbio hawashindi mashindano ya kukimbia, wala walio hodari kushinda vita, wala wenye hekima pia hawana chakula, wala wenye ufahamu pia hawana mali, wala hata wale walio na maarifa hawana kibali.’ (Mhubiri 9:11, NW) Ni nini kinachosababisha hali hizo zisizolingana?
Sulemani alieleza hivi: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (NW) Lakini wengi husadiki kwamba Mungu anaamua yatakayowapata. Kwa mfano, wengi wanaunga mkono nadharia ya mtaalamu wa mambo ya kidini wa karne ya 16, John Calvin, juu ya ‘kuandikiwa na Mungu mambo ambayo yatakupata.” Viongozi wengine wa kidini walikuwa wamedai kwamba Mungu anatangulia kuagiza rasmi watu mmoja mmoja waokolewe. Hata hivyo, Calvin alisema kwamba ikiwa ndivyo mambo yalivyo, basi ni jambo la akili kusema pia watu wanatangulia kuandikiwa mateso ya moto baada ya kufa! Aliita jambo hilo “amri yenye kuchukiza sana” ya Mungu.
Wengine walipinga kwamba fundisho hilo la kidini lilimfanya Mungu awe mwenye lawama la dhambi. Lakini akijaribu kumkanusha “mtu fulani asiyefaa kitu” aliyepinga nadharia yake, kwa dharau na hasira Calvin alijibu: “Jamaa huyu goigoi haelewi kwamba, kwa kutumia visababu vya uongo kukana haki ya Mungu, anapindua uwezo wa Mungu.” Lilikuwa jambo lisilowazika kwa Calvin kwamba Mungu aliye mweza yote angekuwa bila maarifa kamili ya kimbele.
Kwa lazima imani ya kwamba mtu ameandikiwa na Mungu mambo yatakayompata au katika ajali inakuwa na matokeo makubwa juu ya namna ya maisha ya mtu. Lakini je, kwa kweli Biblia inafundisha kwamba tumeandikiwa wakati ujao usioweza kuepukika, kwamba sisi tunapatwa na “ajali” tu?