Je, Wakati Ujao Wetu Umeandikwa Kimbele?
MKRISTO, Mwislamu, Myahudi, Mhindu, au mwamini wa dini nyingineyo—watu wa imani zote hupatwa na msiba na kuhuzunika juu yake.
Kwa mfano, Desemba 6, 1997, msiba mbaya sana ulitokea katika jiji la Siberia la Irkutsk. Ndege kubwa mno aina ya AN-124 ya usafirishaji ilikuwa imetoka tu kuruka wakati ambapo injini zake mbili zilishindwa kufanya kazi. Hiyo ndege, ikiwa imejazwa mafuta, iliangukia majengo ya makazi. Vyumba kadhaa vilifunikwa kwa moto, ukisababisha vifo na majeraha kwa wakaaji wengi wasioweza kujikinga, kutia na watoto wasio na hatia.
Katika hilo eneo la Siberia ambako aksidenti hiyo ilitokea, yaelekea kuna watu wenye maoni ya kidini yanayotofautiana. Huenda baadhi yao wakaonyesha itikadi katika Ukristo, lakini bado wangeweza kufikiri kwamba huo msiba ulitokana na ajali. Huenda wao na wengine wakahisi, ‘Yalikuwa mapenzi ya Mungu, na ikiwa waliouawa hawangekufa kwa njia hiyo, wangekufa kwa njia nyingine—hawangeiepuka ajali hiyo.’
Kufikiri kama huko, kuwe ni kwa kusema au kwa kimyakimya, hudhihirisha fikra ambayo ni ya kawaida katika dini nyingi tufeni pote—ajali. Watu wengi huamini kwamba, kwa njia fulani wakati ujao wetu umeandikwa kimbele, tangu siku ya kuzaliwa kwetu hadi siku ya kufa kwetu.
Itikadi katika ajali hutofautiana, ikifanya iwe vigumu kuwa na ufafanuzi wenye kutia ndani maana zote. Kimsingi ajali hutokeza wazo la kwamba kila kitu kitukiacho, kila tendo, kila tukio—liwe jema au baya—haliepukiki; limekusudiwa kutukia kwa sababu limeamuliwa kimbele na kani ya juu zaidi, ipitayo uwezo wa mwanadamu. Fikra kama hiyo yaweza kupatikana katika unajimu, Uhindu, na karma ya Ubudha, na vilevile katika fundisho la Jumuiya ya Wakristo la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu. Huko nyuma katika Babilonia ya kale, watu waliamini kwamba miungu walidhibiti ajali na wakati ujao kupitia hati iliyoandikwa. Yadhaniwa kwamba, mungu yeyote aliyedhibiti “mabamba [hayo] ya mambo yaliyokusudiwa kimbele” angeweza kuamua ajali ambazo zingepata wanadamu, falme, na hata hiyo miungu yenyewe.
Waumini wengi huamini kwamba, kupitia agizo la kimungu kabla ya kuzaliwa kwa wanadamu, Mungu huamua yote yatakayowapata watu, kutia na urefu wa maisha yao, iwe watakuwa wanaume au wanawake, tajiri au maskini, wenye furaha au wasio na furaha. Hayo yote husemekana kuwako katika akili ya Mungu au kuandikwa katika kitabu kabla ya tukio kutokea. Kwa hiyo afa litokeapo, ni jambo la kawaida kwa mwamini kusema “mektoub,”—imeandikwa! Yawaziwa kwamba kwa kuwa Mungu ajua kila kitu kimbele, lazima pia aamue ni nani atakayemtii na ni nani atakayekosa kumtii. Hivyo wafuasi wengi huamini kwamba hata kabla mtu hajazaliwa, Mungu tayari ameamua kama amekusudiwa raha idumuyo milele katika Paradiso au kama atapokea hukumu idumuyo milele.
Huenda ukahisi kwamba hilo lasikika kuwa sawa kabisa na lile fundisho la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu, ambalo hufundishwa katika makanisa fulani ya Jumuiya ya Wakristo. Mtetezi mashuhuri wa fundisho la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu alikuwa Mleta-Mabadiliko Mfaransa, John Calvin, aliyekuwa Mprotestanti. Alifasili fundisho hilo la kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu kuwa “agizo la milele la Mungu, ambalo kwalo Mungu aliamua kile alichotaka kufanyia kila mwanadamu. Si wote waumbwao katika hali moja, lakini uhai wa milele umeamuliwa kimbele kwa watu fulani na hukumu ya milele kwa wengine.” Calvin alisisitiza hivi: “Mungu aliona kimbele kutumbukia katika dhambi kwa mwanadamu wa kwanza, na ndani yake akaona kuangamizwa kwa wazao wake; lakini pia kwa kutaka, akapanga iwe hivyo.”
Hata hivyo, si washiriki wote wa dini ambazo hufundisha juu ya kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu au nadhariajali ambao kibinafsi, huamini hayo. Baadhi yao hutoa hoja kwa usahihi kwamba, maandishi ya kidini hutaja hiari ya mwanadamu. Kwa kweli, kumekuwa na ubishi mkubwa juu ya vitendo vya kibinadamu, viwe vyatokana na kuchagua kwa hiari kwa kibinadamu au vimeamuliwa kimbele na Mungu. Kwa mfano, wengine wamebisha kwamba ni lazima mwanadamu awe na hiari ya kuchagua na ya kutenda, kwa kuwa Mungu mwenye haki, humwajibisha mwanadamu kutoa hesabu kwa matendo yake. Wengine wamesema kwamba Mungu hutokeza matendo ya mwanadamu lakini kwa njia fulani mwanadamu “hujipatia” matendo hayo na kuwa mwenye daraka kuyahusu. Hata hivyo, kwa ujumla wengi huamini kwamba kila tukio katika maisha yetu ya kila siku, liwe kubwa au dogo, limeagizwa na Mungu.
Je, wewe waamini nini? Je, Mungu tayari ameamua wakati ujao wako utakuwaje? Je, wanadamu kwa kweli wana hiari, uwezo wa kuchagua kihalisi juu ya wakati ujao wao? Je, ni kwa kadiri gani mwisho wetu hutegemea matendo yetu? Makala inayofuata itajaribu kutoa majibu kwa maswali hayo.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
SEL/Sipa Press