Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Ikiwa Mkristo hawezi kuwa kwenye sherehe ya Chakula cha Jioni cha Bwana, anapaswa kufanya nini?
Ni jambo la maana kwamba Wakristo wahudhurie sherehe ya kila mwaka ya Chakula cha Jioni cha Bwana, kwa maana Yesu alisema hivi alipokuwa akiianzisha: “Endeleeni kufanya hivyo kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19, NW) Wakristo wa kwanza walifanya hivyo. Basi mtume Paulo angeweza kuandika juu ya ndugu za Korintho ambao kila mwaka ‘walikutana wakiwa kundi zima,’ au ‘wakakutanika,’ kwa ajili ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu cha dhabihu. (1 Wakorintho 11:20,The New English Bible; UV) Lakini wao wangalifanya nini juu ya Ukumbusho katika hali zenye magumu? Kwa mfano, Paulo mwenyewe alifanya nini wakati wa miaka ambayo alifungwa gerezani (akiwa chini ya ulinzi na labda akiwa ametiwa minyororo) katika Kaisaria?—Matendo 23:35; 24:26, 27.
Kulingana na amri ya wazi ya Yesu, hata kama Paulo angalikuwa peke yake mbali na wengine katika pindi ya Chakula cha Jioni cha Bwana, hakika angalirudia kujikumbusha mambo ya Kimaandiko juu ya tukio hilo. Kwa kuwa alikuwa Mkristo aliyepakwa mafuta kwa roho, angalifanya kila jitihada ashiriki vitu vyenye kufaa zaidi ambavyo angeweza kutumia viwe mifano. Siku hizo divai ilikuwa kinywaji chenye kutumiwa kwa kawaida, kwa hiyo ijapokuwa Paulo alikuwa mfungwa angaliweza kuwa na divai fulani na mkate wa namna fulani wa kutumia. Jambo hilo lingalielekea hata zaidi kuwa hivyo wakati alipozuiwa baadaye katika Rumi, ambako aliruhusiwa kuwa na wageni. Labda ndugu fulani kutoka Rumi walijaribu ‘kukutanika’ pamoja naye katika kikundi kidogo ili kusherehekea Chakula cha Jioni cha Bwana.—Matendo 28:30.
Katika sehemu zote za dunia leo, makundi ya Mashahidi wa Yehova yanakusanyika, katika tarehe inayolingana na Nisani 14, kwa ajili ya Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Lakini nyakati nyingine vipingamizi visivyo vya kawaida vinatokea. Pindi kwa pindi, mvua kali za mafuriko zimezuia kundi, au wengine wa washiriki walo, kukutana pamoja kama ilivyopangwa. Katika visa vichache sana, sheria ya kijeshi imefikilizwa huku askari wenye silaha wakizuia raia kutoka nje ya nyumba baada ya jua kushuka. Wakristo wengine wameshindwa kuwa kwenye sherehe ya kundi kwa sababu ya kuwa hospitalini au kuwa wagonjwa sana. Ni jambo gani linaloweza kufanywa katika visa vya namna hiyo?
Ingawa bado inafaa kundi zima liungane kwa ajili ya tukio hilo la maana, hali kama zilizotajwa juu huenda zikafanya hilo lisiwezekane. Wakati hali mbaya sana ya hewa, maafa ya kiasili, au mambo kama hayo, yanapozuia kabisa jamaa au kisehemu cha kundi kisikutane pamoja na kundi, wenye kuwa peke yao wanaweza kukutana na kuzungumza masimulizi ya Kimaandiko kama yale yanayopatikana katika Luka 22:7-23, 28-30 na 1 Wakorintho 11:20-31, na pia kuzungumza maana ya pindi hiyo. Vivyo hivyo, uzuizi uliofikilizwa na sheria (kafyu ili watu wasitoke nje baada ya wakati fulani ukifanya iwe haiwezekani kundi kukusanyika) katika usiku ule unaofaa, kukutana katika vikundi vya Funzo la Kitabu la Kundi au katika vikundi vya ujirani huenda kukawa ndiyo njia ya kutatulia jambo hilo. Hapo hesabu ya wahudhuriaji ingekuwa ndiyo ripoti ya hudhurio la kundi. Hotuba fupi hata inaweza kutolewa ikiwa ndugu mwenye uwezo aliye wakf yupo katika kikundi. Hakuna uhitaji wa hangaiko la kwamba mifano inayofaa haipatikani mradi hakuna mmoja katika hali hii ya dharura aliyeshiriki hapo zamani mkate na divai akiwa Mkristo aliyepakwa mafuta.
Sheria ya Mungu kwa Israeli ilikuwa na mpango wa pekee kwa ajili ya mtu ambaye hakuwa katika hali ya kuweza kushiriki chakula kile cha kawaida cha Kupitwa; mtu huyo angeweza kufanya hivyo mwezi mmoja (siku 30) baadaye. (Hesabu 9:10, 11; 2 Mambo ya Nyakati 30:1-3, 15) Kwa njia inayolingana na hiyo, katika hali ya kupita kiasi inayohusu Mwisraeli wa kiroho asiyeweza kabisa kuhudhuria au kupitishiwa mifano siku ya Nisani 14, mtu huyo wa kiume au kike angeweza kushiriki siku 30 baadaye. Hilo lingetumika katika kisa cha Mkristo aliyepakwa mafuta peke yake ambaye yuko chini ya amri ya kushiriki mkate na divai.—Wagalatia 6:16.
Siku ya Aprili 4, 1985, baada ya jua kushuka, makundi ya Wakristo wa kweli katika sehemu zote za dunia watakusanyika kwa kutii amri hii ya Yesu: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” Sisi tunakukaribisha ukusanyike pamoja nao.—1 Wakorintho 11:25, New English Bible.