Kitabu cha Imani Kamili
BIBLIA si kitabu cha mashaka bali kitabu cha imani. Haitokezi maulizo kama, Je! kuna Mungu? Au, Je! Biblia ni Neno lake? Tofauti na hayo, inaanza kwa usemi huu: ‘Hapo mwanzo Mungu aliumba.’ Na Biblia inasema waziwazi: ‘Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na roho takatifu.’—Mwanzo 1:1; 2 Petro 1:21.
Ni kweli masimulizi mengi ya Biblia yametolewa kwa ufupi. Kwa hiyo huenda Biblia isituambie sikuzote kila jambo ambalo huenda tukataka kujua. Lakini inatoa habari ambayo Mungu alijua tungeihitaji ili tuelewe hali yenye msukosuko ya ulimwengu, kupatanisha maisha zetu na mapenzi yake na kupata kibali yake na zawadi yake ya uzima wa milele. Ni nini kinachoweza kuwa chenye thamani kuliko hayo?
Mapema katika kurasa za Biblia tunajifunza kwamba zamani sana malaika mwasi alibisha juu ya haki ya utawala wa ulimwengu wote wa Mungu. Lakini pia ilifunuliwa kwamba “uzao” fulani mwishowe ungekuja kukomesha uasi huo na kuondolea lawama Yehova Mungu akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. (Mwanzo 3:1-15; Ayubu 1:6-12) Biblia inaeleza nasaba ambayo kupitia hiyo “uzao” huo ungekuja—kupitia wanaume wa imani kama Ibrahimu, Isaka, Yakobo na Daudi.—Mwanzo 26:4, 5; 2 Samweli 7:12, 13; Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-38.
Kitabu hicho cha ajabu kinaeleza juu ya kuzaliwa, kifo, na ufufuo wa mshiriki mkuu wa “uzao” huo, Yesu Kristo. Kinaeleza jinsi Yesu alivyojulisha jina la Babaye wa kimbingu, Yehova, na kutoa ukombozi kwa ajili ya wanadamu watiifu.—Wagalatia 3:16; Yohana 17:6-8, 26; Mathayo 20:28.
Pia Biblia inasema juu ya uzima wa milele, inaeleza juu ya ufufuo wa wafu na kutangaza “mbingu mpya na dunia mpya” zilizo nzuri ajabu ambamo katika hizo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13, NW; Yohana 3:36; 5:28, 29) Zaidi ya hayo, inadokeza kwamba baraka hizo nzuri ajabu zimekaribia sana, kwamba wengi wanaoishi sasa wataokoka ole za ulimwengu wa sasa na kuziona baraka hizo!—Mathayo 24:3-14, 32-34.
Matunda Bora Sana!
Yesu alisema kwamba “kila mti mwema huzaa matunda mazuri.” (Mathayo 7:15-20) Ndiyo, unaweza kutambua watu wanyofu kwa matunda yao. Mafundisho ya Biblia yanawezesha watu wanaofundishika wazae matunda bora sana. Kitabu hicho kinatoa maarifa, kinajenga imani na kutia hekima. (Yohana 17:3; Mithali 1:1-4) Kinatupa viwango bora zaidi vya kutegemeza maamuzi yanayohusu maisha zetu.—Warumi 12:2; Wakolosai 3:9, 10.
Zaidi ya hayo, Biblia inagusa mioyo. Inachochea watu wapatanishe maisha zao na njia za Mungu na wamtumikie. Mafundisho yayo yanatokeza uradhi, maisha yenye furaha zaidi, afya bora, adili za juu zaidi na wenzi wema zaidi wa ndoa, wazazi bora zaidi na watoto bora zaidi. Wote ambao wamejifunza njia za Kimaandiko na kuzifuata pia wamekuwa udugu wenye upendo wa ulimwenguni pote, kwa kupatana na usemi wa Yesu: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”—Yohana 13:35.
Thamani ya Biblia inaonekana wazi katika maisha za kila siku za wale ambao wanafuata kanuni zayo kabisa kabisa. Kwa sababu gani ye yote atilie shaka ahadi zayo? Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, inawezekana tukawa thabiti katika imani, bila kuwa na shaka hata kidogo.