Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Kwa sababu ya ripoti zinazosema kwamba huenda madaktari wakawa wanaweza kufungulia nguvu za uzazi za mtu ambaye alikuwa amefungwa kwa hiari yake mwenyewe, je! Wakristo fulani hawawezi kuichagua hiyo iwe namna moja ya kupanga uzazi?
Biblia inaonyesha kwamba Mungu anaheshimu sana nguvu za uzazi. Yeye alikusudia kwamba wanadamu waijaze dunia kwa kuzaa viumbe vya jinsi yao. (Mwanzo 1:28; 9:6, 7) Baadaye, Waisraeli waliziona jamaa kubwa-kubwa kuwa baraka kutoka kwa Yehova, na mtu alipoteza upendeleo wa Mungu alipocheza-cheza na nguvu za uzazi. (Zaburi 127:3-5; Kumbukumbu la Torati 1:11; 23:1; 25:11, 12) Mawazo hayo yaliyo katika Maandiko ya Kiebrania yamekuwa na nguvu zenye kuongoza kufikiri kwa wengi wa watumishi wa Mungu kwa habari ya zoea la kufunga nguvu za uzazi kwa hiari ya mtu.a
Ingawa hivyo, tunakuta nini katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo juu ya jambo hilo? Kwanza, tunajifunza kwamba Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa. (Wagalatia 3:24, 25) Tena, Yesu alihimiza Ukristo upanuliwe kwa kuhubiri habari njema, si kwa kuzaa. Kwa kuwa mavuno makubwa ya wanafunzi yangetokana na jambo hilo, Yesu aliwapa mauidha wawe matowashi kiroho wale ambao kati ya wanafunzi wangeweza kufanya hivyo, huku wakionyesha kujiweza wakiwa waseja. Kuhusiana na maana iyo hiyo, mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo wasioe au kuolewa na hivyo wawe na uhuru mkubwa zaidi wa kuhubiri na kufundisha. Kwa njia hiyo wangekusanya watoto wa kiroho na kuwaleta ndani. Hata wenzi waliooana walipaswa kukumbuka kwamba “muda ubakio si mwingi”; mradi wao unapasa uwe ‘kutokuwa na masumbufu’ ya maisha ya kijamaa.—1 Wakorintho 7:29-32, 35; Mathayo 9:37, 38; 19:12.
Safari ile iliyokuwa yetu ya mwisho kuzungumza katika safu hii* juu ya kufunga nguvu za uzazi kwa hiari ya mtu mwenyewe, matabibu walio wengi walikuwa na maoni ya kwamba zikiisha kufungwa haziwezi kufunguliwa na hivyo ni jambo la kudumu. Lakini, matukio ya kitiba katika miaka kumi iliyopita yamebadili kidogo hali hiyo, Kwa mfano, kichapo Population Reports (Novemba-Desemba 1983, Chuo Kikuu cha Johns Hopkins) kinasema hivi juu ya visa vya upasuaji wa kufunga katika wanaume sehemu fulani ya kile kifereji kinachovuta shahawa kutoka kwenye eneo la mapumbu: “Katika ripoti za hivi majuzi, kufunguliwa kwa sehemu hiyo kumeiacha wazi tena—yaani, mbegu za uzazi zimepatikana katika umajimaji wenye kutoka humo—katika asilimia 67 mpaka 100 ya wanaume. Mafanikio yanayohusu utendaji wa kiungo hicho—yaani, uchukuaji mimba kati ya wake za wanaume ambao wamefunguliwa tena kifereji hicho—umekuwa kati ya asilimia 16 na 85.” Njia mpya za upasuaji na za kuweka vizibo vinavyokifunga kwa muda kifereji hicho zinatajwa pia kuwa zinaonyesha kwamba bado kutakuwa na mafanikio zaidi ya kufungua tena kisehemu hicho kilichokuwa kimefungwa.
Kwa kuwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hayatoi mwongozo wa moja kwa moja juu ya mambo hayo, ni lazima Wakristo wafanye maamuzi ya kibinafsi juu ya kuzuia jamaa yao isiwe kubwa sana na juu ya kupanga uzazi. Kwa habari ya kufunga nguvu za uzazi, inawapasa wazingatie akilini kwamba ingawa sasa inafikiriwa kwa-mba uwezekano umeongezeka wa kufungulia tena nguvu za uzazi kuliko vile ilivyokuwa miaka kumi iliyopita, matabibu hawawezi kuhakikisha kabisa kwamba nguvu za uzazi zinaweza kurudishwa.
Juu ya yote, wenzi wa ndoa wanapaswa kuendeleza dhamiri safi mbele za Yehova na kuelekea Wakristo wenzao. Ikiwa wenzi wa ndoa wanafikiria kufunga nguvu za uzazi kuwa namna fulani ya kupanga uzazi, bado inawapasa wafikirie matokeo yo yote ambayo vitendo vyao vinaweza kuleta juu ya wengine. Ingawa kwa kawaida wenzi waliooana hawatangazi-tangazi uamuzi wao juu ya kupanga uzazi, ikijulikana na watu wengi kwamba wenzi wa ndoa walienda kufungwa nguvu za uzazi kwa hiari yao wenyewe, je! ingeweza kuwa kwamba kundi litaudhika sana na kuacha kuwaheshimu?(1 Timotheo 3:2,12,13) Hayo ni mambo ya kufikiria kwa uzito sana, hata katika jambo hilo la faragha na la kibinafsi. Mwisho kabisa, maneno haya ya Paulo yanafaa: “Kwa [Yehova] bwana wake mwenyewe yeye husimama au huanguka.”—Warumi 14:4,10-12.
[Maelezo ya Chini]
a Ona, kwa mfano, “Maswali Kutoka kwa Wasomaji,” Mnara wa Mlinzi wa Juni 1,1975.