“Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1986
KINAFAA kama nini kichwa cha mikusanyiko ya wilaya yetu ya 1986 kiwe “Amani ya Kimungu”! Ndiyo, Yehova Mungu wetu “si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” Yeye yuko tofauti sana na “mungu wa huu mfumo wa mambo,” Shetani Ibilisi, ambaye ni mungu wa machafuko, ugomvi, na mvurugo.—1 Wakorintho 14:33, UV; 2 Wakorintho 4:4, NW.
Kwa kufaa sana, Yehova katika Neno lake anatajwa-tajwa kuwa “Mungu wa amani.” (Wafilipi 4:9; 1 Wathesalonike 5:23; Waebrania 13:20) Katika Neno lake, amani imeahidiwa, imeshauriwa ifuatwe, na kukaziwa tangu mwanzo mpaka mwisho, nayo inatajwa karibu mara 250. Kwa kweli, Yehova ndiye “Mungu apaye amani” watu wake.—Warumi 15:33; 16:20, NW.
Basi, ni jambo la maana kama nini watumishi wake wote, ndiyo, kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova, awe mtu wa amani! Hiyo haimaanishi kuwa mwenye amani tu, bali ‘kutafuta amani na kuifanya iwe jambo letu la kufuatia,’ kama vile mtume Petro anavyotushauri tufanye. (1 Petro 3:10, 11, NW) Hiyo maana yake ni kwamba lazima tuwe “wafanya amani,” kama vile tafsiri yetu ya Kingdom Interlinear inavyofasiri Mathayo 5:9.
Si jambo jepesi kuwa wafanya amani, kujitahidi kuleta amani, kujaribu kuhifadhi amani hiyo. Kuna udhaifu mbalimbali wa hali ya mwanadamu asiye mkamilifu ambao unaleta mahitilafiano ya nyutu. Ni kama vile wimbo wetu wa Ufalme (Na. 213, katika kitabu cha Kiingereza) unavyoeleza: “Kukosana huwa pia; si wakamilifu sisi.” Wimbo huo unaendelea kushauri hivi: “Na tupatane haraka. Umoja udumu.” Pia kuna mikazo ya ulimwengu ya Shetani, pamoja na vyambo vyao vyote vyenye kushawishi, vinavyoelekea kuharibu ‘amani ya Mungu ipitayo akili zote’ ambayo tunayo. (Wafilipi 4:7) Na, bila shaka, kuna Shetani na mashetani wake, wanaofanya yote wawezayo ili kuchafua amani yetu; ni lazima tushindane nao.—Waefeso 6:12.
Katika nyakati za kale, Mungu alipanga kwamba watu wake waje pamoja kwenye pindi za pekee ili wajengwe kiroho na kutiwa nguvu waendelee kupiga moyo konde wazitii amri za Yehova. Vivyo hivyo leo, kati ya misaada mingi ambayo ameandaa kutusaidia tuwe wafanya amani ni mikusanyiko yetu ya wilaya kila mwaka. Tunasikia Neno la Mungu likielezwa kwenye makusanyiko hayo. Kwa muda wa siku nne tunafundishwa na Baba yetu wa kimbingu kupitia hotuba, mahoji, mawonyesho, na michezo ya kuigizwa. Ndiyo, hata nyimbo zetu zinatuhimiza juu ya amani kwa njia iliyo au isiyo ya moja kwa moja.
Mwaka huu kwenye “Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya tutaihisi roho ya udugu tunapokaribishana mtu na mwenzake. Kwa kuona jinsi idara zote mbalimbali za kusanyiko zitakavyofanya kazi kwa upatano, tutaipata kweli kweli roho ya mkusanyiko.
Kwa hiyo na tuje tukiwa tunaujua kikweli uhitaji wetu wa kiroho na kwa kujitayarisha kujifaidi kikamili kutokana na programu yote, tufike mapema kukitwaa kipindi kile cha kwanza kabisa alasiri ya Alhamisi na kubaki mpaka mwisho kabisa kwenye wimbo na sala alasiri ya Jumapili.
Zaidi ya hilo, je, haitupasi kujitahidi kuwa watu wenye upatani? Kwa njia zipi? Kwa kuthamini kweli kweli chakula cha kiroho kilichoandaliwa. Wengi wetu tutakuwa tumefika baada ya kugharimia wakati na pesa nyingi. Kwa hiyo na tuhakikishe kwamba tunafika bila kuchelewa na tu katika hali nzuri kimwili. Hiyo inamaanisha tusile wala kunywa kupita kiasi na tusikae sana usiku kabla ya kulala. Bali, na tuhakikishe kwamba tunatumia vitu kwa kiasi na kulala mapema ili tuwe na miili iliyoburudika na yenye nguvu kuweza kutwaa chakula cha kiroho chote kinachoandaliwa. Programu inapoendelea, na tuwe tumeketi tukisikiliza, si kutanga-tanga, si kuongea-ongea na rafiki fulani mpendwa ambaye hatujaonana naye kwa muda. Wakati wa kusema na rafiki zetu ni kabla na baada ya vipindi. Ndiyo, na tuwe tumepiga moyo konde kweli kweli kwamba tumekuja ili tujengwe sana kiroho.
Katika nyakati za kale Mungu alipanga kwamba watu wake waje pamoja kwa ukawaida katika pindi za pekee ili wajengwe kiroho. Na kwa kweli leo, mikusanyiko ya wilaya tunayokuwa nayo kila mwaka imo kati ya misaada mingi ambayo ametuandalia ili tuwe wafanya amani.
Ili mjitayarishe, zinazofuata ni tarehe zisizothibitishwa na mahali pa makusanyiko:
Nairobi (Kiingereza): Desemba 18-21, 1986
Machakos (Kiswahili): Desemba 18-21, 1986
Nairobi (Kiswahili): Desemba 25-28, 1986
Kericho (Kiswahili): Desemba 25-28, 1986
Eldoret (Kiswahili): Januari 1-4, 1987
Mombasa (Kiswahili): Januari 1-4, 1987
Ushelisheli (Kiingereza, Creole): Januari 23-25, 1987