Ukombozi—Unatamanika Kama Nini!
“NIPE uhuru au unipe kifo!” akapaza sauti Mwamerika mwenye roho ya uzalendo Patrick Henry miaka zaidi ya 200 iliyopita. Kwa maoni yake, kukombolewa kulikuwa jambo lenye thamani kubwa kuliko uhai wenyewe. Katika muda wote wa karne zilizopita, mamilioni ya watu wamekuwa na maoni kama hayo.
Lakini, katika muda wa nusu-karne iliyopita, tamaa ya kukombolewa imeongezeka. Serikali za kikoloni zimenyang’anywa mamilioni ya raia wakati hao walipotafuta na kupata uhuru wa kisiasa. Vyama vya kijamii, kiuchumi, na hata vya kidini vimeanzishwa vitafute kukombolewa kwenye uonevu na ubaguzi, iwe ni kwa njia ya kweli au ya kuwazia tu. Hatujapata kuwa na wakati mwingine kama huo ambapo watu wengi sana wametaka kukombolewa kwenye mamlaka ya waajiri-kazi na serikali, wanawake wengi sana wakataka kukombolewa kwenye mamlaka ya waume na baba zao, na watoto wengi sana wakataka kukombolewa kwenye mamlaka ya wazazi na walimu. Hata hivyo, vyama vya kutaka kukombolewa si jambo jipya. Kwa kweli, muda ambao vimekuwapo unakaribia kulingana na ule ambao mwanadamu mwenyewe amekuwapo. Kitabu cha historia kilicho cha zamani zaidi ulimwenguni, Biblia Takatifu, kinatueleza mengi zaidi. Wazo kuu la hadithi yenyewe, kama inavyopatikana kwenye Mwanzo 3:1-7, ni hili:
Muda mfupi baada ya mwanamume na mwanamke kuumbwa, mwanamke aliendewa na kiumbe wa kimalaika. Vitendo vya kiumbe huyo vilionyesha alitamani kujiondoa kwenye mamlaka ya Muumba wake. Kwa hiyo si ajabu kwamba alikazana ya kuwa mwanamke huyo na mumeye walihitaji kukombolewa. Kwani haikuwa kweli, yeye akabisha, kwamba Mungu alikuwa ameweka vizuizi juu yao? Lakini mbona, yeye akauliza, wao wasile kutokana na “matunda ya mti ulio katikati ya bustani”? Ingawaje, ule mti ulipendeza macho, sivyo? Ndivyo!
Jiondoeni katika wajibu, akahimiza, na “mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Jambo la kutamanika kama nini! Ndiyo, kukombolewa kwenye “utawala wenye uonevu” wa Mungu kulifanywa kuonekane kuwa jambo lenye thamani kubwa kama uhai wenyewe.
“Nipe uhuru au unipe kifo!” Adamu na Hawa walipata mambo yote hayo mawili—wakajiletea huzuni wao wenyewe na sisi pia! Jinsi gani?