‘Viumbe Vyote Vinaugua’—Kwa Sababu Gani?
MWANAMUME na mwanamke wa kwanza waligeuzia Mungu visogo vyao. Lakini kwa kuwa walipata “kukombolewa” walikotaka, sasa walilazimika kuelekeza mambo yao vizuri kama walivyoweza. Baada ya muda mfupi wakagundua kwamba kiwango kizuri kabisa ambacho wangeweza kujisimamia hakikuwa kizuri vya kutosha. Ukosefu wa ujuzi na wa maarifa ya kutosha uliwaongoza kwenye matatizo.
Hiyo ndiyo sababu wengi wetu tumetendwa ubaguzi au udhalimu. Hiyo ndiyo sababu sisi sote tumeingia katika utumwa wa hali za kutokukamilika kwa kibinadamu, ndiyo sababu tunakuwa wagonjwa, tunapatwa na maumivu yasio ya kiafya katika mwili na akili, na kumwaga machozi ya huzuni. Au, kama inavyoelezwa katika usemi wa Kibiblia, hiyo ndiyo sababu ‘viumbe vyote vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.’—Warumi 8:22.
Hivyo jaribio la kwanza la mwanadamu la kupata kukombolewa lilimtumikisha. Kwa muda wa karne 60 sasa yeye amekuwa akijaribu kujikomboa kwenye matokeo mabaya ya jaribio hilo. Lakini je, amefanikiwa kadiri gani?
Kukombolewa Kisiasa
Mwanadamu amefanya jaribio la kutumia serikali ya aina zote. Zile zilizofanya uonevu au udhalimu, au zilizoshindwa kutimiza mahitaji ya haraka ya watu, zimetupiliwa mbali au hata zikapinduliwa kwa jeuri na nafasi yazo ikachukuliwa na nyingine—lakini kukawa na mashaka-mashaka.
Mwandikaji wa habari za majarida, Lance Morrow, anatoa maoni haya akisema juu ya mapinduzi ya kisiasa: “Katika historia kumekuwa na tawala nyingi mno zilizodhaniwa zingekuwa nzuri sana kumbe zikageuka kuwa za kutumia mamlaka kamili ya chama kimoja, zikawa zenye mauaji mengi, kama zile serikali zilizofagiliwa mbali na tawala hizo—ukawa ni msisimuko tu wa kutumainia kutokeza kitu ambacho kimeshindikana tangu zamani.”
Kubadilisha serikali moja isiyo kamilifu na nyingine siyo njia bora ya kukombolewa kikweli. Kwa hiyo, Mfalmu Sulemani mwenye hekima aliongozwa na Mungu aandike hivi: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Mhubiri 8:9) Kwa wazi, ‘viumbe vyote vitaendelea kuugua pamoja na kuwa na utungu pamoja’ mpaka serikali kamilifu itakapovikomboa kwenye utawala usio mkamilifu.
Kukombolewa Kutoka kwa Ubaguzi wa Kikabila na Kitaifa
Maoni yasiyofaa ya kikabila au kitaifa yanapingana waziwazi na kweli za Biblia zinazosema kwamba Mungu “alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika [mtu] mmoja” na kwamba “Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Matendo 17:26; 10:34, 35) Lakini mara nyingi watu wenye kutafuta kuonyeshwa usawa hawakutendewa kwa njia hiyo, hata katika mataifa yanayodai kuwa ni ya Kikristo.
Kwa mfano, ifikirie jamii ya weusi. Watu fulani wanaoitwa Wakristo wanadai kwamba rangi ya ngozi nyeusi imetokana na laana ya kimungu iliyowekwa juu ya Kanaani na wazao wake, wakaachwa kwenye hali ya utumwa. Kwa kusema hivyo wanakosea. Jamii hii ya weusi haikutokana na Kanaani bali Kushi na labda Puti. Wala hakuna laana iliyowekwa juu ya ye yote kati ya hao wawili.—Mwanzo 9:24, 25; 10:6.
Ijapokuwa hivyo, mara nyingi weusi wamejikuta wakigandamizwa kijamii na kiuchumi hata na weusi wenzao. Wao wametamani sana kukombolewa. Lakini vyama vyao vya kutafuta kukombolewa, zijapokuwa jitihada za kupinga ubaguzi na maandamano ya kuteta, vimewaletea mafanikio ya kadiri fulani tu. Kwa sababu hawana uwezo wa kubadili mioyo kwa ukamili, wameshindwa kuondolea mbali maoni mabaya ya ubaguzi wa rangi, ukosefu wa maarifa ya kidini, na ukosefu wa kupenda jirani.
Kwa hiyo ‘viumbe vyote vitaendelea kuugua pamoja na kuwa na utungu pamoja’ mpaka ubaguzi wa rangi utakapofagiliwa mbali na Ufalme wa Mungu kupitia Kristo.
Kukombolewa kwa Wanawake
Muda wa karne zilizopita, wanawake wametendwa vibaya na mara nyingi wakahesabiwa kuwa ni wanadamu ovyo tu. Hilo si kosa la Muumba wao. Yeye hakuumba mwanamke ili mwanamume amwone yeye kuwa chombo cha kutoshelezea nyege zake tu. Wala mwanamume hakuagizwa amtende mwanamke kwa ukatili. Akiwa mke wa mwanamume, mwanamke alipaswa awe “msaidizi” wake, atumikie akiwa “kikamilisho chake,” awe “mwili mmoja” pamoja naye.—Mwanzo 1:26-28; 2:18-24, NW.
Tamaa ya Hawa ya kutaka ajitegemee bila kuwa chini ya mamlaka yenye upendo wa Mungu haikutokeza uhuru bali ilitokeza hali ya kutiishwa kwa ukali. Alitangulia kuona jambo hilo, Mungu alitabiri: “Tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala.” (Mwanzo 3:16) Kwa wanawake wengi, kutawalwa na mwanamume kwa njia isiyo na ukamilifu kumekuwa jambo la kuchukiza sana, na vyama kadha vya wanawake vimejaribu kuondolea mbali utawala huo.
Lakini ingawa Chama cha Kukomboa Wanawake kimetokeza mabadiliko fulani bora, kimeshindwa kufanikiwa kwa sababu kiko kinyume cha ukombozi uliosawazika ambao Mungu anaahidi. ‘Viumbe vyote vitaendelea kuugua pamoja na kuwa na utungu pamoja’ mpaka Ufalme wa Mungu utakapowafundisha wanaume wote “kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe” na kuwatendea “wanawake wazee kama mama; wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote.”—Waefeso 5:28; 1 Timotheo 5:2.
Kweli siku hiyo itafika? Kabla ya kueleza jinsi siku hiyo itakavyofika, ni lazima tushughulikie ulizo jingine la maana. Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani hasa juu ya vyama vya vya ukombozi vya siku hizi?
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Kubadilisha serikali moja isiyo kamilifu na kuweka nyingine isiyo kamilifu pia si suuhisho la kuleta ukombozi halisi
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Maasi ya kiraia, jitihada za kupinga ubaguzi, na maandamano ya kutete hayabadili mioyo
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Chama cha Kukomboa Wanawake kimeshindwa kwa sababu kiko kinyume cha ukombozi uliosawazika ambao Mungu anaahidi