Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Katika mfano wa Yesu juu ya tajiri ambaye hakuwa tajiri kuelekea Mungu, ni akina nani wale ‘waliotaka’ nafsi ya mtu yule?
Yesu hakuwa akimaanisha kikundi cho chote cha wanadamu au malaika. Katika Luka 12:20 alitumia kisehemu cha neno “wa” kama njia ya kuonyesha tu jambo ambalo lingempata mtu yule.
Mfano huo unapatikana kwenye Luka 12:16-21. Tajiri aliye katika mfano huo hakutosheka na vitu vya kimwili vya kutosha alivyokuwa navyo. Aliendelea kukaza fikira zake juu ya biashara ili aongeze utajiri wake. Yesu alimalizia hivi: “Lakini Mungu akamwambia [mtu yule tajiri], Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka [nafsi] yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”
Tafsiri nyingine zinatumia ufasiri wa kumtaja mtu mwenyewe peke yake, kama vile: “Usiku huu huu nafsi yako inatakwa kutoka kwako.” (New American Standard Bible) “Usiku huu huu dai litafanywa kwa ajili ya nafsi yako.” (The Jerusalem Bible) “Usiku huu huu uhai wako unadaiwa.” (The Twentieth Century New Testament) “Usiku huu nafsi yako itaitishwa.” (Byington) Lakini, Kiebrania (ambacho Yesu alitumia kusema) na Kigiriki (ambacho Luka alitumia kuandika) kinatumia namna ya kutaja mtu wa tatu asiyejulikana. Maandishi ya Kigiriki kwenye Luka 12:20 yanasema kwa uhalisi “kwa huu ule usiku ile nafsi ya wewe wao wamaomba kutoka wewe.” Kitenzi hicho kimo katika wingi wa mtu wa tatu. Kwa hiyo, badala ya kubadili kitenzi hicho bila sababu kiwe katika namna ya kumtaja mtu yule mwenyewe tu (kama vile katika mifano iliyotanguliwa kuonyeshwa), Biblia ya New World Translation na nyingine zinatumia fasiri kama vile “wao wanadai.”
Ingawa hivyo, ingefaa tusiruhusu vijambo vidogo-vidogo tu vya kisarufi visivyoonekana wazi vifunike onyo la upole ambalo Yesu alitoa juu ya ufuatiaji wa vitu vya kimwili. Yeye hakuwa akifafanua wazi ni jinsi gani tajiri huyo angekufa. Maana ilikuwa kwamba kwa njia fulani mtu huyo angepoteza nafsi au uhai wake usiku huo. Lakini alikuwa na msimamo gani na Mungu? Wo wote kati yetu wangeweza kujiingiza sana katika kufanya maendeleo ya vitu vyetu vya kimwili na vivyo hivyo wakose kuwa matajiri kuelekea Mungu. Ulimwengu wa biashara unakuza roho ya ‘kupata zaidi na zaidi.’ Hata watu ambao mashirika yao yanapata kutokana na mauzo faida kubwa sana za mamilioni ya dola, pauni, mafaranga, shilingi, na kadhalika, huenda wakashawishwa watafute vitu vingi zaidi—wafanya kazi wengi zaidi, mauzo mengi zaidi, faida nyingi zaidi, anasa nyingi zaidi, pesa nyingi zaidi katika benki. Ulizo la Yesu linafaa leo kama vile lilivyofaa alipoliuliza mara ya kwanza: “Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? ”—Luka 12:20.