Sababu Gani Yatamalizika Pasipo Shaka
MFALME wa kale Sulemani aliona hivi juu ya matumizi mabaya ya uwezo katika siku zake: “Kisha nikarudi na kuona madhalimu [matumizi mabaya ya uwezo] yote yanayotendeka chini ya jua; na tazama, machozi yao waliodhulumiwa, ambao walikuwa hawana mfariji; na upande wa wale waliowadhulumu kulikuwa na uwezo.”—Mhubiri 4:1.
Huenda wewe ukauliza, ‘Kwa kuwa matumizi mabaya ya uwezo yamekuwapo kwa muda mrefu sana, je! yatakuwa pamoja nasi milele?’ Hapana. Kwa sababu, kama vile Sulemani mwenyewe alivyoandika kwa uongozi wa Mungu, kuna anayeona yote hayo: “ikiwa [u]naona katika jimbo kuonewa kwa maskini na kuondolewa kijeuri kwa haki na uadilifu usistaajabishwe na jambo hilo, kwa maana mmoja aliye juu ya walio juu zaidi anatazama, naam Aliye Juu Zaidi Sana yuko juu yao.”—Mhubiri 5:8, Rotherham.
Neno la Mungu, Biblia Takatifu, linaonyesha kwamba Yehova, Aliye Juu Zaidi Sana ana uwezo na hekima isiyo na mipaka, na pia ni mkamilifu katika haki na ndiye umbo la upendo. Kwa sababu yeye ni Mungu wa namna hiyo, hatavumilia milele hali hizi zenye udhalimu. Daudi mtunga zaburi aliandika hivi: “Usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya. Maana watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao [Yehova] ndio watakaoirithi nchi.”—Zaburi 37:8, 9.
Tunapata uhakikisho zaidi kutokana na maneno ya nabii Isaya: “Nami nitaadhibu . . . wenye dhambi kwa sababu ya hatia yao; nami nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao walio wakali [wenye kutumia uwezo vibaya].”—Isaya 13:11.
Lakini karne nyingi zimepita tangu maneno hayo yalipoandikwa, kwa hiyo mbona tuwe na uhakika kwamba Yehova Mungu bado atatimiza ahadi yake ya kumaliza matumizi yote mabaya ya uwezo? Ni kwa sababu yeye ameonyesha nyakati zilizopita azimio lake la kufanya hivyo. Kabla ya Gharika ya siku za Noa, kulikuwa na matumizi mabaya mengi ya uwezo. Tunasoma kwamba “dunia ikajaa dhuluma.” (Mwanzo 6:5, 11) Na je! dhuluma si matumizi mabaya ya uwezo? Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya miji miovu ya Sodoma na Gomora siku za Loti. (Mwanzo 18:20, 21; 19:4-29) Katika visa vyote viwili Yehova alikomesha matumizi hayo mabaya. Kwa hiyo tunaona kwamba Yehova Mungu si Mtu wa kuvumilia matumizi mabaya ya uwezo kwa wakati usiojulikana.
Msingi zaidi wa sisi kuwa na hakika kwamba Yehova atachukua hatua ni uhakika wa kwamba yeye anaonea jina lake wivu, na matumizi yote mabaya ya uwezo ni kutusi adhama yake. Angalia jinsi jambo hilo linavyohusiana na maandiko haya: “Amwoneaye maskini humsuta Muumba wake.” “Amdhihakiye maskini humsuta Muumba wake.”—Mithali 14:31; 17:5.
Basi, tunaweza kubaki tukiwa na uhakika wa kwamba Aliye Juu Zaidi Sana hatavumilia kusutwa kwa muda wote. Jambo hilo linabakisha ulizo moja tu: Ni wakati gani matumizi mabaya ya uwezo yatakapomalizika?
Ni Wakati Wakati Gani Yatakapomalizika?
Neno la Mungu linatujulisha kwamba “kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati wa kila kusudi chini ya mbingu.” (Mhubiri 3:1) Huenda wengine wakakosa subira kwa orodha ya wakati ya Mungu, lakini tunaambiwa: “[Yehova] hakawii kuitimiza ahadi yake, . . . bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee.”—2 Petro 3:9.
Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kamba tunaishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu mbovu, au mfumo wa mambo. Kizazi hiki kimeona utimizo wa unabii mkuu wa Yesu kuhusu kuwapo kwake na umalizio wa mfumo huu wa mambo: vita, matetemeko ya ardhi, njaa kubwa, magonjwa ya kipuku, ongezeko la kutokutii sheria, na kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:1-35; Luka 21:10, 11) Mambo hayo yanauonyesha barabara wakati wetu kuwa ndio siku za mwisho za ulimwengu huu mbovu.
Kwa sababu hizi ndizo siku za mwisho, tunaweza kutumainia kuona karibuni unabii ulio kwenye Sefania 3:8 ukitimizwa: “Basi ningojeni, asema [Yehova], hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.”
Hakika maneno hayo ni uhakikisho wa kwamba Yehova Mungu atamaliza matumizi mabaya ya uwezo.