Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 12/1 kur. 25-27
  • Utumishi wa Painia Ulichangamsha Maisha Yangu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Utumishi wa Painia Ulichangamsha Maisha Yangu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Badiliko la Utumwaji
  • Roho ya Upainia Katika Jamaa
  • 1914—Mwaka Usiosahaulika
  • Kusafiri-safiri na Habari Njema
  • Kushikamana na Utumishi wa Painia
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kusonga Kuelekea Ulimwengu Mpya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 12/1 kur. 25-27

Utumishi wa Painia Ulichangamsha Maisha Yangu

Kama ilivyosimuliwa na Arthur Gustavsson

KULE juu katika milima ya Himalaya iliyofunikwa na theluji, ukweli unaopatikana katika Neno la Mungu Biblia ulifikia wazazi wangu, Fred na Amanda Gustavsson. Ulikuwa mwaka 1903, na wakati huo mimi nilikuwa katika tumbo la uzazi la mama yangu. Wazazi wangu walikuwa wakifanya nini kule juu, mbali sana na nchi ya kwao ya Uswedi?

Katika mwaka 1880 wao walikuwa wamehama Uswedi kwenda United States. Wote wawili walikuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. Walijiunga na kanisa Scandinavian Mission Alliance katika Chicago. Baada ya kipindi fulani cha mazoezi, wao walitumwa wakawe wamisionari Baltistan, eneo ambalo sasa liko kaskazini kabisa mwa Pakistani. Lakini, baada ya muda mfupi walikuta kwamba ilikuwa vigumu sana kugeuza Waislamu wafuate mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo. Wao wenyewe walianza kutia shaka kama Mungu angeweza kweli kuwa mkatili sana hata awalaani watu hao wenye moyo mchangamfu, walio wakaribishaji, wapate adhabu ya milele ya moto wa mateso kama hawangegeuza dini yao. Wazazi wangu hawakutambua kwamba akili zao zilikuwa zikitayarishwa kwa ajili ya jambo lililo zuri zaidi.

Baada ya muda fulani walipokea kitabu kimoja kutoka kwa rafiki mmoja katika United States ambacho kilibadili kabisa kufikiri kwao. Kilikuwa The Divine Plan of the Ages, kilichotungwa na Charles T. Russell, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Sosaiti wa Mnara wa Mlinzi. Wao walikisoma, ikawa kana kwamba magamba yenye kufunika macho yao yalikuwa yameanguka. Waliona waziwazi kwamba mshahara wa dhambi ni mauti, wala si mateso ya milele. (Warumi 6:23) Sasa walikuwa na ujumbe wa tumaini wenye mambo mazuri ya kuwaambia watu​—kwamba Ufalme wa Mungu utageuza dunia iwe paradiso.

Badiliko la Utumwaji

Ni karibu na wakati huo mimi nilipozaliwa katika Shigar katika Baltistan. Kitambo kidogo baadaye dada yangu Mirjam akazaliwa. Wazazi wangu walikuwa wameamua kwamba walitaka kufanya kazi chini ya mwelekezo wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ili kuutangaza ukweli mpya waliokuwa wamepata. Ijapokuwa hivyo, hali ziliwalazimisha kurudi Uswedi katika 1908. Kule katika Goteborg walianza kuzihubiri ‘habari njema za Ufalme’ wakiwa makolpota, kama vile wahudumu wa wakati wote walivyoitwa wakati huo. (Mathayo 24:14) Wakati wa ile miaka kumi ya kwanza, walimaliza mara tatu kufanya kazi katika mji mzima katika huduma yao ya nyumba kwa nyumba. Watu wengi waliukubali ukweli.

Mimi nakumbuka alikuwako Bi. Hanna Gunnarsson aliyeona ghadhabu sana wakati baba aliposema kwamba Biblia haifundishi kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa. Mwanamke huyo alipaaza sauti hivi: “Ikiwa hatuna nafsi isiyoweza kufa, afadhali uende zako ukajizamishe ufe katika kile kijito!” Baba alitabasamu tu kwa fadhili na kumpa kijitabu What Say the Scriptures About Hell? (Maandiko Yanasema Nini Juu ya Hell?) Baadaye mwanamke huyo akawa Shahidi, pamoja na binti zake. Kisa hicho kilinifundisha kutokufadhaishwa kamwe​—hata watu waseme nini.

Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, Ndugu Rutherford alikuja Goteborg kutoa hotuba ya watu wote: “Wafu Wako Wapi?” Wakati wa utoaji wake, yeye alifanya toleo la kumpa dola 1,000 mtu ye yote katika wasikilizaji ambaye angeweza kuthibitisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa. Hakuna mtu aliyejitokeza kupambana na mwito huo wa ushindani.

Roho ya Upainia Katika Jamaa

Kwa sababu ya mfano mzuri sana wa wazazi wangu, baada ya muda mfupi mimi niliingiwa sana na roho ya upainia. Nilianza kushiriki katika huduma nikiwa na umri mdogo. Baba aliniagiza nitolee watu handibili zenye kutangaza hotuba za watu wote. Mimi nilifurahia kufanya hivyo na nikapata mambo yaliyoonwa yasiyo ya kawaida. Siku moja niliendea mwalimu wangu wa kike kumwalika kwenye hotuba moja. Yeye alikikataa kwa ukali kikaratasi kile. Mimi nilishangaa sana hata nikajikwaa na kuanguka kwenye ngazi ya nyumba ile. Hilo lilikuwa somo kwangu​—lilinifunza kuwa na maoni yanayolingana na matukio ya kweli. Si sikuzote watu wanapokuwa jinsi sisi tungependa wawe.

Nyumba yetu ikawa kama nyumba ya mapainia, huku kila mmoja akifanya upande wake. Mirjam dada yangu na mimi tuliujua umaana wa kazi ya kuhubiri ambayo Baba na Mama walikuwa wakiifanya. Basi, mara nyingi sisi wenyewe tulikuwa tukiisafisha nyumba nzima baada ya kuja nyumbani kutoka shuleni.

Nikiwa na umri wa miaka 16 nilijiweka wakfu nifanye mapenzi ya Yehova na kubatizwa katika 1919 kwenye mkusanyiko mmoja katika Orebro. Mwaka uliofuata nilialikwa nifanye kazi pamoja na kikundi kidogo cha ndugu wanane waliokuwa na shughuli nyingi kwenye afisi ya tawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika Uswedi. Miaka hiyo ya utumishi katika tawi iliweka msingi wa maisha yenye nidhamu na utaratibu mzuri katika utumishi wa Yehova.

1914—Mwaka Usiosahaulika

Kwa miaka mingi kabla ya 1914, Wanafunzi wa Biblia, kama sisi tulivyoitwa wakati huo, walikuwa wamekuwa wakitazamia mwaka huo kuwa kitu cha pekee. Kwa kuwa ulikuwa umetiwa alama katika unabii wa Biblia, sisi tulitazamia matukio yasiyo ya kawaida. Mimi ninaweza kukumbuka vizuri Jumapili, Agosti 2, 1914. Baba alikuwa akiongoza mkutano katika Goteborg tuliposikia kule nje mvulana mleta-habari akipaaza sauti: “Moto mkubwa wa ulimwengu umeanza!” Ndugu waliokuwa katika Jumba lile wakaanza kutazamana. Mengine ya mambo tuliyokuwa tukitangaza juu ya 1914 yalikuwa yakianza kutimia.

Mwaka 1914 pia ulimaanisha jambo fulani kwa Johan Severin Petersson. Ida dada yake alikuwa ametangulia kumwachia vitabu vitatu vilivyoandikwa na Ndugu Russell. Yeye alifikiri vilikuwa hatari, kwa hiyo akavichoma kwa moto. Ida alisikia juu ya tukio hilo, na akiendelea na jitihada yake, akamwazima vingine vitatu. Safari hii huyo ndugu yake alivifungia katika kitoto cha meza.

Ndipo ikaja ile Vita Kuu ya 1914. Johan alikuwa amesikia kwamba vitabu hivyo vilinena juu ya tarehe hiyo. Kwa kufanya udadisi, yeye alifungua kile kitoto cha meza, akavitoa humo, na kuvisoma. Macho yake yalifunguliwa kuuona ukweli wa Biblia, naye pia akawa Mwanafunzi wa Biblia. Alibatizwa katika 1917, na Rosa binti yake akafuata mfano wake katika 1918. Katika 1928 Rosa akawa mke wangu mpendwa na mwenzi wa maisha yote katika utumishi wa Yehova.

Kusafiri-safiri na Habari Njema

Nilipooa, niliondoka katika afisi ya tawi, na Rosa na mimi tukatumia tafrija ya ndoa yetu tukipainia! Wakati wa mwezi wetu wa kwanza wa maisha ya ndoa, sisi tuliangusha nakala 4,000 za kijitabu Freedom for the Peoples.

Baada ya miezi michache tu, mimi niliulizwa kama ningefikiria kusafiri nikiwa mkurugenzi wa utumishi wa mkoa, ambaye leo anajulikana kuwa mwangalizi wa mzunguko. Hiyo ingemaanisha kutembelea makundi katika sehemu zote za Uswedi na baadaye Norwei. Siku hizo hakukuwa na mipango yo yote kwamba uambatane na mke wako katika safari hizo. Ilinilazimu niwe mbali na nyumbani majuma sita-sita au saba-saba kwa safari moja, nikiwa na siku chache za kuacha kidogo kati ya kila safari. Tulikuwa na nia ya kufanya dhabihu hiyo na tulifanya hivyo miaka 14.

Rosa alifanya nini wakati wa kipindi hicho? Yeye alipainia pamoja na dada yangu katika Halsingborg, Uswedi. Siku hizo iliwalazimu waendeshe sana baiskeli ili kulimaliza lile eneo pana. Lakini acheni asimulie hadithi yake.

“Kupainia katika miaka ya 1930 kulikuwa tofauti sana na kutumikia leo. Mirjam na mimi tulikuwa tukikodi chumba kidogo kwa juma moja au mawili hivi tulipokuwa tukihama mtaa mmoja kwenda mtaa mwingine. Wakati huo tulikuwa tukihama kwa kurundika mizigo yetu katika baiskeli zetu​—mavazi, sufuria zenye mikono, na masanduku ya vitabu. Ilikuwa tamasha!

“Haikuwa rahisi sikuzote kupata mahali pa kulala. Siku moja baada ya kufanya kazi kila mtu pekee yake, Mirjam na mimi tulikutana karibu saa mbili za jioni.

“Tuliendelea kuendesha baiskeli mpaka kwenye shamba lililokuwa mbele nasi tukaona taa. Ndipo tulipoitambua nyumba ile. Mioyo yetu ilizimia. Watu wa hapo walikuwa wamekuwa wakipinga sana wakati tulipowatembelea hapo kwanza. Kwa kusita-sita, Mirjam akaenda mlangoni na kuomba mahali pa kulala. Tulishangaa na kutulia mioyo yule bibi alipotuambia tuingie tuketi. Baada ya kitambo fulani tukaombwa tuingie katika chumba kizuri kabisa, ambamo meza ilikuwa imepangwa chakula kingi. Tulishangaa ajabu! Tulipokwisha kula, tukaonyeshwa chumba cha kulala ambamo vitanda vilikuwa vimetandikwa shuka nzuri kabisa za kitani. Tuliduwazwa na badiliko hilo la mwelekeo.

“Asubuhi yake tukapewa kiamsha-kinywa. Tulipotaka kulipa, wao wakakataa pesa zetu. Tukawauliza kama tungeweza kuwapa kitabu kinachoitwa Deliverance kiwe zawadi. ‘Oh, ndiyo, tunakitaka kitabu hicho,’ wakasema. ‘Mwanamke aliye jirani yetu alituambia mlimpa kimoja mlipokaa naye. Alituambia alikifurahia sana.’

“Jambo hilo lililoonwa lilitufunza kwamba huwezi kujua ni matunda gani yatakayotokana na kuangusha mara moja tu vitabu vya Biblia.”

Kushikamana na Utumishi wa Painia

Katika 1942 kazi ya kusafiri ilisimamishwa kwa kitambo fulani, kwa hiyo Rosa na mimi tukaweza kurudia upainia tukiwa pamoja tena. Baadaye baba akawa mgonjwa, nasi tukaacha huduma yetu ya wakati wote ili tumtunze. Ijapokuwa hivyo, mara tu hali ziliporuhusu, tulirudia utendaji wetu tulioupenda​—utumishi wa wakati wote. Tulihisi tumerudia kazi inayotufaa kabisa. Tukiisha kurudi nyumbani baada ya siku ya kutumia nguvu nyingi katika kuhubiri, mara nyingi tumesema hivi: “Utumishi wa painia unazistahili dhabihu zote na jitihada zinazohusika humo.”

Kwa miaka mingi sasa sisi tumekuwa tukipainia katika sehemu ya magharibi ya Uswedi, tukifanya kazi pamoja na Kundi la Svenljunga la Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu sasa umri wetu umesonga sana, hatuna zile nguvu za siku za ujana wetu, lakini tuna furaha kuweza kuendelea katika upainia. Sasa mimi nimemaliza miaka 55 katika utumishi wa wakati wote, na mke wangu miaka 48. Lakini, sisi hatutegemei tu mambo ya zamani, ingawa yanatufanya tuhisi vizuri. Hata uwe una umri gani, ni lazima sikuzote utazame mbele. Tamaa yetu ya moyo mweupe ni kwamba tupate kutembea kwa uaminifu na kiasi pamoja na Mungu wetu, Yehova, na hatimaye tuzipate baraka nzuri ajabu za Ufalme wake ambao tumeuhubiri katika utumishi wa wakati wote kwa miaka mingi sana.​—Mika 6:8, NW.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mke wangu na mimi tumefanya kazi pamoja katika utumishi wa Yehova kwa miaka 58

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki