“Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya—Ndicho Kitu Tulichohitaji Hasa!
“MIOYO imefikiwa na mielekeo ya watu ikaguswa.” “Yehova aliandaa karamu kubwa ya milo mingi mizuri ajabu.” “Hotuba zilikuwa za kutoboa mambo na kuyasema wazi-wazi.” “Hicho ndicho hasa kitu tulichohitaji SASA!” “Hiki ndicho kitu tulichokihitaji hasa!”
Hiyo ni mifano halisi ya maneno mengi ya uthamini yaliyosikiwa kuhusu “Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova wa 1986. Maneno yote hayo yalionyesha kwamba wale waliohudhuria walikuwa wametii shauri zuri sana walilopewa na mwenyekiti na pia na ile hotuba ya kufungua: “Sikilizeni Mfahamu.”
Kwa kuwa kichwa cha amani kinatajwa kwa umashuhuri sana katika Neno la Mungu, neno hilo likiwa linaonekana mara zaidi ya 300 katika Biblia, ilifaa sana kwamba lifanywe kichwa cha mikusanyiko ya wilaya yetu ya 1986. Kwa kweli, 18 kati ya barua zilizoongozwa na Mungu kuanzia Warumi mpaka Ufunuo zinaanza kwa maneno kama “Fadhili zisizostahilika na amani na ziongezwe kwenu.” (NW) Na iangaliwe pia kwamba katika Maandiko ya Kiebrania neno linalotafsiriwa “amani” ni sha·lohmʹ, ambalo linamaanisha si kutokuwapo tu kwa vita na ugomvi bali pia linadokeza maana ya afya, ufanisi, na masilahi.—1 Petro 1:2.
Amani ilikaziwa tena na tena katika sehemu zote za programu. Kama vile msemaji wa hotuba ya msingi alivyokazia, Yehova ndiye “Mungu wa amani” na “Mungu apaye amani.” Mwanaye, yule “Mwana-Mfalme wa Amani,” aliwaahidi wafuasi wake amani. (Wafilipi 4:9, NW; Warumi 16:20; Isaya 9:6, NW; Yohana 14:27; 16:33) Msemaji wa hotuba ya msingi alionyesha pia kwamba amani ambayo sisi Mashahidi tunafurahia haina kifani katika maana ya kwamba hiyo haitegemei hali za kinje-nje. Inategemea kuheshimu kwetu mamlaka, ambayo ndiyo sababu inayofanya ulimwengu usiwe na amani—huo hauna heshima kwa Yehova Mungu, Mamlaka iliyo kubwa zaidi. Isaya alieleza jambo hilo vizuri sana: “Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji.”—Isaya 48:18.
Miongoni mwa madokezo yenye mafaa yaliyotolewa ili sisi tuweze kufurahia amani ya kimungu kwa ukamili zaidi ni kwamba tujitahidi kuchukua kutokana na kila mkutano shauri moja lenye mafaa la kutengeneza. Hotuba hiyo ilionyesha pia kwamba ili tuwe wafanya amani haitoshi tuwe wenye amani tu; ni lazima tufanye kazi ya kuleta amani, tuwe na nia ya kuachia upande wetu ili kuwe na amani.
Nyayo Zilizovishwa Vifaa vya Habari Njema za Amani
Ujumbe wetu umeitwa kwa kufaa “habari njema za amani.” (Waefeso 6:15) Sisi tulipokea mashauri mengi mazuri sana juu ya jinsi ya kuletea wengine habari njema hizi za amani. Mfululizo wenye sehemu tatu wa hotuba juu ya huduma yetu ulisaidia sana kuelekea kusudi hilo. Msemaji wa kwanza alionyesha jinsi huduma ya nyumba kwa nyumba imekuwa kitambulisho cha kazi ya Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa kazi hiyo si rahisi, sisi tunathibitishia Mungu na wanadamu upendo wetu kwa kujitia katika kazi hiyo. Ili tuwe wenye matokeo kweli kweli, ni lazima tuwe wenye kudhamiria mambo na wenye uelekevu wa kufanya mambo, tukitunza maandishi ya kumbukumbu zilizo sahihi na kutembelea watu nyakati tofauti-tofauti ili tufikie wote.
Msemaji wa pili alieleza kwamba ili sisi tufanye wanafunzi ni lazima tuendelee kufanya ziara za kurudia juu ya watu wenye kupendezwa, tukifanya hivyo kwa mwelekeo wa kutazamia mazuri. Inatupasa tupendezwe kibinafsi na wale tunaotembelea, tuwe tumekwisha kuandika katika ziara ile ya kwanza ni mambo gani yanayopendeza mwenye nyumba. Hakikisha kwamba katika kila ziara ya kurudia mwenye nyumba anajifunza jambo fulani jipya.
Msemaji wa tatu alionyesha kwamba wanafunzi wetu wa Biblia watasaidiwa wawe Mashahidi ikiwa sisi tunafikia mioyo yao kwa maulizo ya maoni. Tunataka tuonyeshe tunapendezwa kikweli nao kwa kuwaelekeza kwenye tengenezo la Mungu, kuwasaidia wafike mikutanoni, kuwatembelea katika nyakati zile nyingine, na hata kuwaalika kwenye nyumba zetu. Katika muda wa miaka 35 iliyopita, mafunzo ya Biblia yameongezeka mara kumi.
Kufuata mfululizo wa hotuba hizo, tulikaziwa uhitaji wa kudhihirisha hamu nyingi ya kushiriki na wengine habari njema za amani ko kote inakowezekana na chini ya hali zote. Umri si kizuizi. Watoto wachanga na wale walio katika miaka yao ya tisini na kitu wanaendelea kuhubiri. Wengine ni mapainia, au wahubiri wa wakati wote, ingawa ni vipofu kabisa. Wengine wanapainia ingawa ni viziwi, na wengine pia wanafanya hivyo ingawa hawatoki katika viti-magurudumu vya wagonjwa. Mume na mke ambao ni mapainia wana watoto sita wanaoambatana nao katika utumishi wa shambani.
Lenye kufaa zaidi lilikuwa shauri lililosema “Jitahidi Sana kwa Kushiriki Katika Huduma ya Wakati Wote.” Utumishi wa wakati wote ni njia ya maisha yenye kuridhisha zaidi, ya kuthawabisha zaidi. Wakiisha kuanza, mapainia walihimizwa wafanye yote wawezayo wabaki katika utumishi wa wakati wote.
Kama ilivyokuwa kwenye mikusanyiko iliyotangulia, tulisikia mambo kutokana na watangazaji wa habari njema wa muda mrefu, wengine wao wakiwa wakitumikia kuanzia miaka 30 mpaka hata 70. Wao walieleza juu ya furaha yao katika kuzihubiri habari njema. Ilitia moyo kweli kweli kusikia jinsi wameshinda vipingamizi ili waendelee katika huduma. Kwa mfano, ndugu mmoja hakukosa kuhubiri hata mwezi mmoja katika miaka ya utumishi 43.
Shauri kwa Washiriki wa Jamaa
Shauri zuri sana kwa washiriki wa jamaa lilihitajiwa sana kwa sababu ya tisho ambalo mfumo mbovu wa mambo unatokezea wale walio katika jamaa ya Kikristo. Vijana waliulizwa: “Je! Mnaendelea Kiroho?” Leo vijana wengi wanatumikia wakati wote wakiwa mapainia na kwenye makao ya Betheli. Lakini je! wengi zaidi wangeweza kuwa wakifanya hivyo? Kuwa wenye maendeleo kiroho kunamaanisha kutanguliza mapenzi ya Mungu kwanza katika maisha zetu. Kunamaanisha pia kuwa na mazoea mazuri ya kujifunza na kushiriki kwa ukawaida katika utendaji mbalimbali wa kundi na katika utumishi wa shambani, na pia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na walio wazee-wazee. Na kunamaanisha kutofurahia jambo lo lote ambalo Neno la Mungu linakataza.
Mfululizo mwingine wenye sehemu tatu za hotuba ulianza kwa ulizo lenye kuchunguza moyo, “Je! Nyumba Yenu ni Mahali pa Pumziko na Amani?” Msingi wa jambo hilo ni kuchagua mwenzi aliye shahidi wa Yehova anayetanguliza faida za Ufalme kwanza na anayedhihirisha tunda la roho ya Mungu. Ili nyumba iwe mahali pa pumziko na amani, ni lazima mume achukue uongozi katika mambo ya kiroho, na imempasa apende mke wake kama mwili wake. Mke anapaswa awe mwenye kuunga mkono na kuonyesha mumeye heshima yenye kina kirefu. Ni jambo la maana kabisa pia wasali pamoja na wasiruhusu nafasi ya Ibilisi kuingia. Watoto wanaweza kuchanga ili wafanye nyumbani kuwe mahali pa amani na pumziko kwa kuwa watiifu na wenye ushirikiano. Vifungo vya jamaa vinatiwa nguvu kwa kujifunza Biblia na vitabu vya Kibiblia pamoja.—Zaburi 34:11.
Iliyohitajiwa sana pia ni hotuba iliyofuata, “Je! Kutengana ni Njia ya Kuleta Amani Katika Ndoa?” Jibu lilikuwa nini? Labda kwa walimwengu lakini si kwa Mashahidi! Kwao, mtengano si njia ya urahisi ya kutoka katika ndoa yenye majaribu. Upatano wote wa shauri la Mungu juu ya ndoa ni kwamba watu waliofunga ndoa wabaki wakiwa na umoja. Karibu nyakati zote mtengano unakuwa na madhara juu ya watoto wanaohusika, na kuna matunda mengine mabaya. Ikisemwa kwa kutoboa mambo bila kuficha, mtengano ni kukiri kwamba mmoja wa wenzi wa ndoa au wote wawili hawadhihirishi tunda la roho maishani.—Wagalatia 5:22, 23, NW.
Wakristo waseja walipewa pia mashauri mazuri sana katika ile hotuba: “Je! Mseja Ahisi Kuwa Si Kamili?” Hata kidogo! Kwa kuwa huduma ndicho kitovu cha maisha zetu, sisi tunaweza kuwa kamili tuwe tu waseja au tumefunga ndoa. Kwa kweli, kama Paulo anavyoonyesha, Wakristo waseja wana mambo fulani ya kuwazidi waliofunga ndoa. Kwa kusitawisha uradhi, wanaweza kufurahia sana zawadi ya useja na kuutumia kwa faida iliyo kubwa zaidi.—1 Wakorintho 7:32-34.
Mashauri Yanayohitajiwa Juu ya Maisha Safi
Hali ya tabia za ulimwengu inayozidi kuharibika imefanya hesabu fulani ya Mashahidi wakaripiwe au hata watengwe kwa sababu ya mwenendo mbaya. Kwa hiyo yalifaa kama nini mashauri ya kutoboa wazi yaliyotolewa juu ya mambo ya mwenendo! Ili tufurahie amani ya kimungu, ni lazima tuchunge mwenendo wetu nyakati zote. Kwa mfano, jambo hilo lilionyeshwa wazi katika hotuba “Epuka Mitego ya Vitumbuizo vya Starehe.” Karamu za kujifurahisha zinaweza kupendeza sana, lakini tusipojiangalia, zinaweza kwa urahisi kuvuruga-vuruga utendaji wa kitheokrasi na kutuongoza kwenye uchafu. Moyo wa kibinadamu usio mkamilifu ni mdanganyifu na tayari kutumia nafasi yo yote ili kucheza-cheza na ukosefu wa adili. Hasa karamu za kujifurahisha zilizo kubwa-kubwa ndizo zinazotokeza hatari nzito-nzito. Ndivyo na muziki unaoshusha heshima.—1 Wakorintho 15:33, NW.
Ili tuhifadhi amani yetu ya kimungu, ni lazima ‘Tuepuke “Hewa” Yenye Kuleta Kifo ya Ulimwengu Huu.’ Kama vile hewa tunayovuta, roho hiyo ya ubinafsi na kutokutii ya ulimwengu imetuzunguka pande zote. Hotuba hiyo ilishughulika na madhihirisho tisa ya hewa hiyo yenye kuleta kifo. Miongoni mwa hayo ni kucheza-cheza na ukosefu wa adili. Mitindo ya kupita kiasi ya mavazi na kujipamba, kukosa kiasi katika matumizi ya chakula na vinywaji, na kuwa na uzoevu wa michezo, na kujivunia kabila la mtu. Endelea tu kuvuta hewa hiyo nayo itakuua wewe kiroho.
Jambo hilo lilikaziwa hata zaidi na ile hotuba “Je! Wewe Unadumu Ukiwa Safi Katika Kila Jambo?” Uzembe unatufanya tuwe na hatia ya unafiki. Ili tuwe na dhamiri njema, ni lazima tuendelee kuwa safi kimwili, kiakili, kiadili, na kiroho. Kwa kusudi hilo ni lazima ‘tuchukie lililo baya, ‘tukirihi lililo ovu.’ Hii ni kutia ndani kukirihi propaganda za waasi-imani. —Zaburi 97:10; Warumi 12:9, NW.
Ile hotuba nzuri sana “Nidhamu ya Yehova Inazaa Tunda la Amani” ilifaa sana hapa pia. Yehova ndiye Mtia-Nidhamu Mkuu, naye anatutia nidhamu sisi kwa sababu anatupenda. Hakuna hata mmoja kati yetu asiyehitaji nidhamu. Hata Mwana wa Mungu alihitaji nidhamu! (Waebrania 5:8) Ndiyo, kwa msingi nidhamu inamaanisha mazoezi, si kutiwa adhabu sikuzote, na ili tunufaike na zile njia nyingi ambazo Mungu anatumia kuitoa, ni lazima sisi tuwe wanyofu kwa upande wetu wenyewe—na kuendelea kuwa wanyenyekevu!
Ile hotuba “Endeleeni Kujengana” ilitoa mashauri mazuri sana juu ya usemi wetu. Ni madhara mengi kama nini tunayoweza kufanya kwa maongezi yasiyofikiriwa vizuri, ya kuchambua-chambua watu, au ya kulalamika! Kwa kweli, ulimi ni mgumu kuongozwa. Kwa kufaa, tulikumbushwa kwamba inatupasa ‘tuache kunena dhidi ya mtu na mwenzake.’ (Yakobo 4:11, NW) Upendo wa kidugu utatufanya tuwe waangalifu. Na kabla hatujasema jambo fulani, upendo huo utatufanya tuulize hivi: “Je! kwa kweli jambo hili ni la kweli?” “Je! ni lazima niseme juu yalo?” “Je! litakuwa la kujenga?”
Kutumia Mambo ya Unabii
Hotuba baada ya hotuba zilitumia mambo ya unabii ulioongozwa na Mungu kwa kusudi la vikumbusho na onyo la upole. Hivyo, katika ile hotuba “Hukumu za Mungu—Hazipendwi na Ulimwengu,” msemaji alikazia kwamba habari njema tulizo nazo si za kuhubiri juu ya paradiso tu bali pia, kama Yeremia, tuna matangazo ya kutoa juu ya hukumu za Mungu zinazokuja. (Yeremia sura 6 na 7) Kama vile Yeremia alivyofunua kwa ujasiri mafundisho ya uwongo na mazoea yenye ufisadi ya viongozi wa kidini wa siku zake, ndivyo na sisi tunavyoonywa kwa upole tufanye.
Ile hotuba “Wakati wa Kujaribu na Kupepeta” ilionyesha matumizi ya kisasa ya Malaki 3:1-3. Kweli kweli, watu wa Yehova wamesafishwa mafundisho na mazoea ya uwongo ya Kibabuloni. Kuanzishwa kwa utaratibu wa kitheokrasi na ufahamu wa kwamba huduma ya nyumba kwa nyumba ndiyo ya maana kuu zaidi ni kati ya mambo yenye mwelekeo mzuri yaliyotajwa na msemaji.
Tulisikia pia hotuba nzuri sana ambamo msemaji alizungumza sura ya 11 na 12 za Danieli. Kichwa cha hotuba hiyo kilikuwa “Siri Takatifu Zifunuliwazo Hutoa Tumaini Hakika la Kuwa na Amani.” Ushindani baina ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini unaendeleza ulimwengu katika msukosuko. Kulingana na unabii wa Danieli, tunaweza kuona kwamba wafalme hao hawatakomesha kamwe mahitilafiano yao. Ni Mikaeli tu anayeweza ‘kusimama’ alete amani ya kudumu.
Hotuba nyingine yenye kutumia mambo ya unabii ulioongozwa na Mungu ilikuwa “Usalama wa Ulimwenguni Pote Chini ya ‘Mwana-Mfalme wa Amani.’ “Ilishughulika na Isaya 9:6, 7 na habari zinazozunguka andiko hilo, ikionyesha jinsi unabii huo ulivyotumiwa kwa kufaa kuhusu Yesu Kristo. Msemaji alisema katika umalizio wake kwamba Mikaeli “atafikia upeo wa kazi yake tukufu kwa ushindi huo penye Har–Magedoni ambao mshindo wao utaendelea bila kufifia kamwe wakati wa umilele wote . . . Haya basi, songeni mbele enyi Mashahidi wa Yehova wote, mpate kujulikana zaidi sana ulimwenguni kuliko hapo zamani, mkimtumainia kabisa Mungu wenu na mfalme wake anayetawala, ‘Mwana-Mfalme wa Amani’! Onyesheni ushujaa kabisa bila kuogopa shauri bovu la sasa la ulimwengu . . . ninyi nyote iweni ishara na miujiza kwa utukufu wa Yehova!” Kwa kweli hiyo ilikuwa moja za hotuba zenye kusisimua zaidi za mkusanyiko.
Wathamini Wale Wanaoongoza
Mfululizo wa hotuba yenye sehemu mbili yenye kichwa “Waangalizi Wanaotumikia Faida za Amani” ilitusaidia kikweli tuwathamini wale wanaoongoza. Msemaji wa kwanza alizungumza sehemu inayotimizwa na waangalizi wasafirio na akaonyesha kwamba wao, kweli kweli, wanastahili heshima maradufu kwa sababu ya wajibu wao mwingi. Huo ni kutia ndani kutoa hotuba, kusaidia watu katika matatizo yao, kuwazoeza akina ndugu katika kazi ya ushahidi, na kutembelea walio wagonjwa kimwili au kiroho. Kweli, waangalizi wanaosafiri wote wanastahili ushirikiano wetu kamili na ukaribishaji kama wa Lidia.—Matendo 16:15.
Msemaji wa pili aliendeleza mtajo wa wajibu mbalimbali wa wazee na sehemu wanaotimiza katika kuendeleza amani kundini. Wanaweza kufanya hivyo kwa kujitayarisha kwa ajili ya mikutano na kuiongoza, kufanya ziara za uchungaji, kushughulikia mambo ya hukumu, kuongoza katika utumishi wa shambani, na kuweka mfano mzuri katika mwenendo na maisha ya kijamaa. Kwa uhakika, sisi sote tunapasa tutake kuonyesha uthamini kwa wazee waliowekwa rasmi kwa kuwa watiifu na wenye kusikia maneno, hata kama tunavyoshauriwa kwenye Waebrania 13:17.
“Kufikia na Kujipatia Msimamo Mzuri” ilikuwa hotuba iliyokazia moyoni uhitaji wa wazee wanaostahili kwa sababu ya maongezeko makubwa ya Mashahidi. Ilionyesha ndugu wote walio wakfu ambao si wazee jinsi wanavyoweza kujitahidi kufikia mapendeleo makubwa zaidi. Hasa hotuba hiyo ilihimiza wale wanaostahili lakini wasioona uhitaji wa kutumikia kwa kadiri kubwa zaidi wajiulize wenyewe hivi, Mbona mimi nasita-sita?
Mambo Mazuri Mengine ya Kiroho
Iliyothaminiwa sana ilikuwa hotuba “Je! Unaridhika na Maandalizi ya Yehova?” Tulisikia mifano ya Kibiblia ya wale waliothamini maandalizi ya kiroho yaliyotolewa na Mungu na wale wasioyathamini. Kwa kadiri ambayo sisi tunauona uhitaji wetu wa kiroho, sisi tutaridhika na maandalizi ya Yehova na kuonyesha tunafanya hivyo. Jinsi gani? Kwa kukomboa wakati wa funzo la kibinafsi la Kibiblia na kujitia nidhamu tunapokuwa mikutanoni ili tupate faida zilizo kubwa zaidi kutokana nayo.
Jambo ambalo lingeweza kusemwa kuwa lilitutokezea mwito wa ushindani kwa hali yetu ya kiroho lilitajwa katika hotuba “Sala Zako Ni Zenye Kujaa Maana Kadiri Gani?” Ilidokezwa kwamba tujiulize wenyewe: Je! sisi tumeacha sala zetu ziwe za kurudia-rudia, za kusema-sema mambo bila kubadilikana, au za haraka-haraka, kama kwamba sisi ni wenye shughuli mno tusiweze kuyafanya maongezi yetu na Mungu kama inavyostahili? Katika sala, sisi tunakuja kwenye Mtu Mashuhuri na aliye mkubwa kuliko wote katika ulimwengu mzima wote. Ili sala zetu ziwe zenye kujaa maana, ni lazima tumchukue Mungu kuwa mtu wa kikweli kabisa. Ni lazima sala zetu zitoke moyoni na zitaje mambo waziwazi, na lazima tuzifikirie kwa uangalifu.
Jambo jingine zuri lililotufurahisha lilikuwa hotuba ya ubatizo “Kupata Amani Pamoja na Mungu Kupitia Wakfu na Ubatizo.” Msemaji alionyesha kwamba ubatizo wetu ni pindi nzito sana na ya furaha sana wakati ule ule mmoja. Kupitia hiyo, sisi tunaweza kupata amani pamoja na Mungu na kuwa wahudumu walioagizwa rasmi wa Mashahidi wa Yehova. Na wakfu wetu si wajibu tu wa kufanya jambo fulani, kwa maana tunaweza kupata na kutunza hesabu fulani ya wajibu mbalimbali kwa wakati ule ule mmoja. Badala ya hivyo, kuwa wakfu kunamaanisha tuwe tumejitoa tufanye utumishi kwa Mwenye Umungu peke yake kabisa, Yehova Mungu.
Ile michezo ya kuigiza miwili ya Kibiblia ilikuwa miongoni mwa mambo ya mkusanyiko yaliyopendwa zaidi na wengi. “Kuhifadhi Uhai Wakati wa Njaa” ni mchezo ulioshughulika na hadithi yenye kugusa moyo ya Yusufu na ndugu zake, nao ulitosha wengi machozi. Roho ya Yusufu ya kuwa na moyo mkuu wa kusamehe ni mfano mzuri sana wa kuigwa na sisi sote. Usimulizi huo una maana ya kiunabii pia. Ule mchezo wa kuigiza wa pili, “Tafuteni Uadilifu wa Mungu Mkaokolewe,” ulitoa mashauri yenye mkazo mwingi na ya kutazamisha kuhusu matatizo ya vijana wetu. Ulikazia uhitaji wa kulinda mwenendo wetu, kuweka faida za Ufalme kwanza, na kutokuwa wepesi wa kuhukumu makusudio ya wengine.
Yenye kupatana kabisa na kichwa cha mkusanyiko ilikuwa hotuba ya watu wote, “Hatimaye Amani!—Mungu Asemapo.” Kwanza, tulisikia ukifunuliwa wazi upumbavu wa matayarisho yote ya kinyukilia na ukosefu wa tumaini wa hali ya ulimwengu kwa kutegemea maoni yo yote ya kibinadamu. Ni Ufalme wa Mungu tu unaotolea watu tumaini lo lote halisi. Inamaanisha nini kusikiliza Mungu asemapo? Inamaanisha si kwamba tusikilize kwa makini tu na kuelewa anayosema Mungu bali pia kwamba tuchukue hatua fulani kuhusiana na anayosema. Hapo ndipo sisi hatutadanganywa na tangazo la udanganyifu la “Amani na Usalama.”
Hotuba ya kumalizia, “Mungu wa Amani Ametupa Vifaa Tufanye Mapenzi Yake,” iliwasindikiza nyumbani wakusanyikaji wote wakihisi vizuri moyoni kwa ajili ya karamu yote ya kiroho waliyofurahia wakati wa siku zile nne. Kwa kweli, mkusanyiko huo umetupa sisi vifaa vya kufanyia mapenzi ya Mungu kama isivyopata kuwa tena wakati uliotangulia. Kwa hiyo “acheni sisi tusonge mbele tukiwa tumeazimia kwa ukamili kufanya nini? Kusonga mbele katika ile kazi kubwa ya kuuhubiri Ufalme, tukiwa tumethamini kweli kweli amani ya kimungu yetu na mambo yote inayomaanisha kwetu.”
Katika United States, kulikuwa na mikusanyiko 135 iliyofanywa mahali 65 mbalimbali na katika lugha 11. Hudhurio lililo kilele lilikuwa 1,276,578, na watu 12,603 wakabatizwa. Mikusanyiko ile mitatu kwenye Yankee Stadium Mjini New York ilikuwa na hudhurio la kilele cha watu 95,091, na 1,110 wakabatizwa.
[Sanduku katika ukurasa wa 30]
Vitolewaji vya Mkusanyiko “Amani ya Kimungu”
Kitolewaji cha kwanza kilikuwa chapa iliyosahihishwa ya kile kijitabu “Tazama! Nayafanya Yote Kuwa Mapya,” kwenye umalizio wa hotuba iliyohusu habari hiyo. Sasa hiyo ni broshua yenye rangi nne, iliyopigwa chapa kubwakubwa na yenye habari za ziada. Inapasa iwe yenye kufaa sana kuanzishia mafunzo ya nyumbani ya Biblia.
“Mashahidi wa Yehova — Wanafanya kwa Umoja Mapenzi ya Mungu Ulimwenguni Pote” ambayo pia ni broshua yenye rangi nne ya ukubwa wa gazeti, ndiyo iliyokuwa kitolewaji cha pili. Hicho ni chombo kizuri sana cha kufanya wengine wazoeleane na utendaji wetu mbalimbali na pia kinatoa habari nyingi za kihistoria juu ya Mashahidi wa Yehova.
Kitolewaji cha tatu kilikuwa msaada wa kujifunza Biblia wenye kurasa 192 ambao kwanza utatumiwa kwenye Mafunzo ya Kitabu ya Kundi. Una kichwa kinachosema Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani.”
Kingdom Melodies Namba 7 ndicho kitolewaji cha nne, na kisehemu cha muziki uliopigwa kutokana nayo kilifurahisha sana wakusanyikaji wote.
Walipokuwa wakisikiliza maelezo ya kumalizia, wote walifurahi sana kusikia kwamba Watch Tower Publications lndex ya 1930-1985 ingepatikana kufikia Septemba 1. Hiyo ni baraka kama nini kwa wanafunzi wote wa Biblia walio na bidii nyingi!
[Picha katika ukurasa wa 31]
1. Yusufu aliuzwa na ndugu zake, hilo lilionyeshwa katika mchezo wa kuigiza kwenye mkusanyiko mmoja wa Kikorea katika United States
2. Msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, F.W. Franz, akihutubia wasikilizaji wa mkusanyiko mmoja
3. Sehemu ya wasikilizaji wenye kutega masikio katika Yankee Stadium, Mjini New York
4. Maelfu walibatizwa kuonyesha wakfu wao kwa Yehova Mungu