“Hazina za Nchi Takatifu”
MANHATTAN wenye shughuli nyingi ni kikao kisicho cha kawaida kwa mkusanyo wa sanaa zinazounga mkono historia ya Biblia. Hata hivyo, Metropolitan Museum of Art inayokaa kana kwamba inaegemea kwenye Central Park ya Mji wa New York, hivi karibuni ilikuwa na maonyesho yenye kichwa “Hazina za Nchi Takatifu: Sanaa za Kale Kutoka Nyumba ya Kuhifadhia Vitu vya Kale ya Israeli.” Maonyesho hayo yalikuwa na vitu karibu 200 vilivyokopwa kutoka Nyumba ya Kuhifadhia Vitu vya Kale ya Israeli katika Yerusalemu.
Wakaaji wa kale wa nchi ya Biblia husimulia hadithi yao kupitia sanaa hizo. Njoo, acha tutazame, tusikilize, na kujifunza. Kwanza, ingawa hivyo, ni lazima upande vipandio 28 vya ngazi vinavyoongoza kwenye kiingilio cha mnara wa Metropolitan Museum Ukiisha ingia ndani, uko tayari kuanza safari yako ya kutembea kati ya maelfu kadha ya miaka ya historia ya Biblia. Yafuatayo ndiyo ungeweza kuyaona:
Kitabu cha Maelezo cha Habakuki—kitabu cha kukunjwa cha urefu wa karibu meta 1.5, ambacho katika hicho jina la kimungu linaonekana mara kadha. Kunjo hilo ni mojapo la yale ya kwanza kugunduliwa na ndilo limehifadhiwa vizuri zaidi la yale Makunjo ya Bahari ya Chumvi, ambayo yameitwa “uvumbuzi ulio mkubwa zaidi wa kiuchimbuzi wa karne hii.” (Makunjo hayo yana sehemu za kila kitabu cha Biblia isipokuwa Esta na yana tarehe za kurudi nyuma mpaka karne ya pili K.W.K. Hivyo, isipokuwa vipande-vipande vya hati, yanapita kwa mileani tarehe yo yote ya nakala za kale zaidi za Kibiblia zinazojulikana.) Kitabu cha Maelezo cha Habakuki kina karibu theluthi mbili za kitabu cha Habukuki (1:4—2:20), kilinakiliwa kwa mwandiko wa herufi kubwa katika Kiaramu mwishoni mwa karne ya kwanza K.W.K., na kilichanganywa pamoja na maelezo “Lakini lile jina la Yehova la herufi nne, Tetragramatoni, kila mahali limeandikwa kwa mwandiko wa Kiebrania cha kale,” yasema kadi ya taarifa ya nyumba ya kuhifadhia vitu vya kale. Ndiyo, ungeweza kuona hizo Tetragramatoni!
Kigae cha “Nyumba ya Mungu”—kigae ambacho juu yacho jina la kimungu linaonekana mara mbili katika namna ya Tetragramatoni. Kigae hicho kilichopatikana katika kusini mwa Israeli kilikuwa na barua aliyoandikiwa mwanamume aliyeitwa Eliashibu na kina tarehe ya huko nyuma ya nusu ya pili ya karne ya saba K.W.K. “Kwa bwana wangu Eliashibu: Yehova na aulize amani yako,” yaanza barua hiyo. Inamalizia hivi: “Yeye anakaa katika nyumba ya Yehova.”—Ona ukurasa 12 wa broshua Jina la Mungu Litakaloendelea Milele, iliyochapishwa na Sosaiti yetu.
Mwandiko wa Pontio Pilato—maandishi ya kihistoria ya aina ya pekee sana kutoka karne ya kwanza, yaliyovumbuliwa katika Kaisaria. Kabla ya 1961, mtajo pekee wa Pontio Pilato ulikuwa katika kurasa za Biblia na maandishi ya karne ya kwanza ya wanahistoria wa Kirumi na Kiyahudi. Sasa, ingawa hivyo, ungeweza kuona yakiwa yameandikwa katika Kilatini kisichokamilika juu ya kipande cha jiwe la chokaa maneno “Pontio Pilato [Mtawala] wa Yudea.” Hiyo inaunga mkono kwamba kulikuwako mwanamume aliyetoa ruhusa Yesu Kristo auawe.
Mwandiko wa “Mahali pa Kupigia Tarumbeta”—wakati mmoja ulikuwa sehemu ya ukuta wa kusini-magharibi wa ua la hekalu katika Yerusalemu. Hekalu lilipoharibiwa katika 70 W.K., kisehemu hicho cha jiwe kilianguka kwenye barabara ya mji iliyokuwa chini. Maneno kwenye “mahali pa kupigia tarumbeta” yameandikwa katika Kiebrania juu ya jiwe hili ambalo kidogo ni la pembe nne za mraba, lenye urefu wa meta moja nalo linataja mahali ambapo mpiga tarumbeta alisimama, pengine wakati wa kupiga tarumbeta ya kuanza na kufunga Sabato. Kwa habari ya majengo yaliyokuwa katika wanja za hekalu, mwandiko huo ndio kitu pekee cha maana kinachobaki, hivyo kuthibitisha utimizo wa unabii wa Yesu kwenye Mathayo 24:1,2.
Maandishi ya Maziko ya Uzia, Mfalme wa Yuda—kipande cha jiwe cha ukubwa wa meta 0.3 za mraba kikiwa na maandishi haya ya Kiaramu: “Hapa ililetwa mifupa ya Uzia Mfalme wa Yuda. Usifungue.” Onyo hilo huenda likadokeza ukoma wake, au huenda likaelekeza kwenye katazo la ujumla dhidi ya kufungua makaburi. (2 Nyakati 26:16-23) Kipande hiki, ambacho tarehe yacho ni karibu na karne ya kwanza K.W.K., kilipatikana karibu na Yerusalemu na kilionyesha kuzikwa mara ya pili kwa mifupa ya mfalme huyo karne nyingi baada ya kifo chake, kwa kuwa hapo mwanzoni hakuzikwa katika uwanja wa maziko ya kifalme wa mji huo.
Kinara cha Madhehebu Kikiwa na Wapiga-muzika—kinara cha udongo kisicho cha ukawaida chenye kimo cha karibu meta 0.3 kikionyesha kwa dhahiri sana sherehe za kimadhehebu. Kiweko kina wapiga-muziki watano, kila mmoja akipiga chombo cha muziki—patu, paipu maradufu, chombo chenye uzi, na tari. Kinara hiki kinapatikana katika Ashdodi na ni cha tarehe ya kuanzia mwisho-mwisho wa karne ya 11 kufika mwanzo-mwanzo wa karne ya 10 K.W.K.
Kinara cha Madhehebu cha Kikanaani—kinara cha udongo cha miraba, chenye shimo katikati kilichopambwa kwa picha za wanadamu na wanyama. Kinatia ndani ile miungu mikuu ya Kikanaani Ashera, ikiwa na umbo la namna ya mti mtakatifu au kigingi, na Baali, katika umbo la ndama akikaliwa na kisahani cha jua chenye mabawa. (Kutoka 34:12-14; 2 Wafalme 23:4, 5) Kinara hicho cha kimo cha karibu meta 0.6, ambacho pengine kilikusudiwa kuwa cha matoleo au sadaka za kumiminwa, kilipatikana karibu na Megido na ni cha tarehe ya kuanzia mwisho wa karne ya 10 K.W.K.—Linganisha 2 Nyakati 34:4.
Pembe kutoka Samaria—vitu vilivyochongwa kutoka Samaria vyenye tarehe ya kuanzia karne ya 9 mpaka ya 8 K.W.K vinamkumbusha mtu juu ya “nyumba ya pembe” aliyoijenga Ahabu katika Samaria au juu ya mapambo ya “vitanda vya pembe” vilivyoonyesha tabia ya mtindo wa maisha ya anasa iliyolaumiwa na nabii Amosi. (1 Wafalme 22:39, Amosi 3:15; 6:4) Kwa kuwa wachongaji wa sanaa Wafoinike sana sana walitumia pembe, nyingine za sanaa hizi za sanamu ndogo-ndogo zaonyesha ibada ya kipagani ya Baali, ambayo labda ilianzishwa na mke wa Ahabu Mfoinike, Yezebeli.
Vingi vya vitu vinavyoonyeshwa ni vizuri katika umbo na rangi Lakini baadhi yavyo, kama vile sanamu za miungu ya kike ya nguvu za uzazi, vinaonyesha mazoea machafu ya kidini ya nchi hiyo. Vingine vinaonyesha jinsi mavutano ya kigeni yalivyofanyiza tabia zayo. Maonyesho hayo ya “Hazina za Nchi Takatifu” na mengineyo kama hayo yanaongezea ufahamu wa mtu juu ya watu, siasa, dini, na ufundi-sanaa wa nchi ya Biblia.
[Pichas katika ukurasa wa 24, 25]
Kitabu cha Maelezo cha Habakuki
[Credit Line]
Shrine of the Book, Israel Museum, Jerusalem
Kigae cha “Nyumba ya Mungu”
[Credit Line]
Israel Museum, Jerusalem
Mwandiko wa Pontio Pilato
[Credit Line]
Israel Museum, Jerusalem
Mwandiko wa “Mahali pa Kupigia Tarumbeta”
[Credit Line]
Israel Museum, Jerusalem
Mwandiko wa Maziko ya Uzia
[Credit Line]
Israel Museum, Jerusalem
Kinara cha Madhehebu Kikiwa na Wapiga-muziki
[Credit Line]
Israel Museum, Jerusalem