Mmoja Aliye Mchanga Amsifu Yehova
NAFASI nyingi za kutoa ushuhuda ziko wazi kwa walio wachanga wanapokuwa na tamaa yenye nguvu ya kumtumikia Yehova. Hilo lilionekana katika jambo lililoonwa na kivulana mwenye umri wa miaka mitano katika Magharibi mwa Kenya.—Mhubiri 12:1.
Mamaye alimuuliza: “Unataka kuwa nini utakapokuwa mtu mzima?” Kivulana huyo alikuwa amemwona painia wa pekee katika kundi naye akajibu: “Mimi nataka kuwa painia wa pekee kama Ndugu F .” Mamaye akajibu: “Lakini hilo haliwezekani; wewe huwezi hata kuwa painia wa kawaida kwa sababu wewe huna funzo la Biblia.” Yule kivulana akauliza: “Naweza kufanya nini basi?” Mama yake akamdokezea ajaribu kufundisha wenzake anaocheza nao akitumia nakala yake ya Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.
Kivulana huyo mwenye umri wa miaka mitano akachukua kitabu chake cha Hadithi za Biblia akaenda kuwaita rafiki zake, akiwaalika wajifunze Biblia pamoja naye. Matokeo yakawaje?
Yeye alifanyiza kikundi cha watoto kumi ambao angeweza kujifunza pamoja nao. Yeye alitumia vizuri zile picha, akauliza maswali mengi yenye kuchunguza mambo kindani na akauliza maswali ya kurudia mambo waliyojifunza mwisho wa funzo. Ikiwa wao hawakukumbuka, alirudia tena habari hiyo pamoja nao. Mamaye alieleza kwamba ilikuwa furaha kweli kweli kuona watoto hao wote wakiketi chini mbele ya nyumba yake wakijifunza pamoja! Mwanaye mwenye umri wa miaka mitano ndiye huyo akiuliza maswali, kisha mikono yote ingeinuliwa juu kujibu.
Ilikuwa furaha zaidi kwa mama huyo, na kwa kundi pia, kuona wanane wa watoto hao wakihudhuria mikutano ya kundi. Wale wengine wawili walikuwa wadogo mno. Yote hayo yalitokea kwa sababu kivulana mmoja mwenye umri wa miaka mitano alitaka kumsifu Yehova na kusaidia wengine.