Je! Dini Imetosheleza Mahitaji Yetu?
MARIA alikuwa mtawa wa kike wa Katoliki ya Roma kwa miaka 21. Yeye alikua katika mazingira ya kidini sana. Kwani, hata akiwa mtoto, yeye angeamka usiku na kusali kwa ajili ya wengine! Hata hivyo, hatimaye, umaskini, kuteseka, na udhalimu uliondelea ijapokuwa maelfu ya miaka ya uvutano wa kidini ulimfanya ajiulize: ‘Je! kweli dini imetosheleza mahitaji yetu?’
Dini zilizo nyingi zinatetea mawazio na kanuni za adili za juu. Lakini mara nyingi dini inaonwa kuwa kisababishi cha matatizo, ikiongezea kwenye magumu yetu, badala ya kutosheleza mahitaji yetu. Kwa mfano, ebu yafikirie maelezo haya yanayotolewa na watazamaji wa tamasha ya kidini: “Sababu ya ndani kabisa ya ukatili wa kinyama ni dini.” (National Review) “Msukumo ulio mkubwa sana wa vita si pupa tena bali ni dini.” (Toronto Star) “Yale Maangamizi Makuu ‘yote yalifanywa na Wakristo waliobatizwa.’”—The Tampa Tribune.
Je! ni jambo la kushangaza kwamba watu wanayatupilia mbali madai ya dini kwamba hiyo ndiyo kitoshelezaji cha mahitaji yetu? Wao wameona mazao yayo. Mathalani, “Ilikuwa Shinto, dini ya asili ya Japani, ambayo haikutegemeza tu kwa moyo wote matengenezo ya vita bali ilitoa sababu za kuyategemeza,” kikasema kichapo The Christian Century. Ni dini ngapi ambazo zimefanya vivyo hivyo—‘zikategemeza kwa moyo wote matengenezo ya vita’! Ebu yafikirie yale machinjo na visasi vilivyolipizwa na Wahudha na Wahindu wa Sri Lanka, yale mauaji na ukatili unaohusu Wakatoliki na Waprotestanti wa Ailandi—kwani, orodha hiyo inaonekana kuwa haina mwisho! “Wahindu, Waislamu, Wasiki, na mafarakano mengine yamekuwa yakimwaga damu ya mmoja na mwenzake kwa kame nyingi katika India,” likaomboleza U.S.News & World Report.
Huenda wengine wasione kwamba dini ni kani ya kuleta mabaya, lakini kwa hakika wao hawaioni kuwa kani yenye nguvu ya kuleta mema. Kichapo National Catholic Reporter kilizungumza juu ya “ukosefu wa makanisa ya kimapokea kujishughulisha ifaavyo na matakwa na mahitaji ya binadamu.” Na lile jarida Liberty lilisema kwamba jamii ya watu inamwona kasisi kuwa “mbariki-mtakasaji-mfadhili” anayeonekana katika pindi za kisherehe tu. Liliongeza hivi: “Katika akili za watu wengi yeye ni mhudumu katika hadhi tu.” Je! wewe umeiona dini katika njia hiyo—isiyoelekea sana kutufanyia madhara lakini pia isiyoelekea kutufanyia sisi mema mengi?
Leo dini inafanana sana na ilivyokuwa wakati Yesu Kristo alipokuwa duniani. Yeye alisema kwamba viongozi wa kidini wa siku zake walimheshimu Mungu kwa vinywa vyao tu. Matokeo ya mazoea yao ni kwamba wao waliongezea mizigo ya watu badala ya kutosheleza mahitaji yao. “Wao hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao,” akasema. (Mathayo 23:4) Leo, dini inaahidi mengi sana lakini inaonekana kutoa machache sana. Kwa hiyo je! kuna sababu yo yote ya kuitikadi kwamba dini inaweza kutosheleza mahitaji yetu?