Kuponya kwa Kutumia Imani Ni Nini Kinachofanya Kuvutie?
Kanisa linavuma kwa kupiga gitaa, tarumbeta, ngoma, matari, na patu za mgongano. Wanaume, wanawake, na watoto wanacheza dansi na kuimba wakiwa katika hali ya msisimuko kama wa kichaa. Hali hiyo imekuwa yenye kufaa ili yale maponyo yaanze.
Yule mponyaji-kwa-imani, akiwa amevaa kanzu ndefu zilizo nyeupe, anaanza kwa kuweka mikono yake juu ya mwanamume mmoja kilema anayetembea kwa kutumia mikono na miguu yake. Halafu, zamu ya mwanamume mmoja kipofu, ambaye miwani yake myeusi inafunika macho yake yasiyoona. “Ni muujiza!” watazamaji wanapaaza sauti wakati viwete wanapoanza kutembea na vipofu kuanza kuona . . .
TAMASHA kama hizo zinapatikana mara nyingi katika makanisa mengi ya Kiafrika yanayoponya kwa imani. Kwa kweli, waponyaji-kwa-imani wanafuatwa na watu wengi katika Afrika na nchi nyinginezo kwa sababu ya madai yao kwamba kupitia sala na imani katika Mungu, wao wanaweza kutatua matatizo ya namna zote. Watu fulani hivyo wanakuja kwenye waponyaji-kwa-imani wakiwa na matatizo ya kifedha. Na kwa kuwa katika jamii ya Kiafrika mara nyingi kutokuwa na mtoto kunakuwa na sifa mbaya, watu fulani wanakuja kwenye waponyaji-kwa-imani wakitumaini kupata ponyo la utasa.
Hata hivyo, matatizo ya kiafya yanashughulisha fikira za waponyaji-kwa-imani zaidi ya jambo jinginelo lote. Ingawa dawa za kulevya zenye mafaa ya kitibabu zimejaza sana soko la ulimwengu na jitihada kubwa zinafanywa katika mambo ya tiba ili kuletea wagonjwa kitulizo, bado mwanadamu yuko mbali na kupata jibu kwa tatizo la ugonjwa. Watu fulani wenye ugonjwa mzito wametumia pesa nyingi sana wakitafuta maponyo, wasipate yo yote. Basi, si ajabu kwamba watu wengi wanageukia waponyaji-kwa-imani kwa sababu ya kushindwa na la kufanya!
Watu fulani wanahisi kwamba kuponya kwa imani kumewasaidia watu hao na hawawezi kuona hitilafiano lo lote kati ya maponyo hayo na Ukristo. Kwa kweli, kwa kuwa mara nyingi waponyaji-kwa-imani wanadai kwamba wao wanafanya kazi katika jina la Yesu, si jambo lisilo la kawaida kwa wafuasi wao kuwa washiriki wa dini fulani kubwa na wa kanisa fulani linaloponya kwa imani. Lakini je! inaweza kufaa mwabudu wa kweli wa Mungu ajifaidi mwenyewe na mponyaji-kwa-imani? (Yohana 4:23) Na je! maponyo yo yote yenye kuletwa na mtu kama huyo yanaweza kwa kweli kuhesabiwa kuwa yameletwa na Mungu?