Kwa Sababu Gani Kuna Watoto Wengi Sana Wanaotoroka?
Biblia na Maisha ya Kijamaa—Kichwa hiki kitakaziwa katika matoleo manne yenye kufuatana-fuatana ya Mnara wa Mlinzi
“Je! mtu ye yote anaweza kuwazia jinsi mama anavyoteseka wakati binti yake anapotoroka? Hilo ni jinamizi lenye kusumbua sana. Kwa sababu gani yeye akaondoka? Mimi siwezi kuelewa. Yeye alikuwa msichana mzuri sana mwenye furaha, tena kijana sana.
“Yeye yuko wapi usiku wa leo? Je! yuko mahali ambapo hapigwi na baridi? Je! ana njaa? Ni mpweke? Mimi nampenda sana. Sina mtu wa kuongea naye. Sina la kufanya ila kungojea.
“Kila wakati simu inapolia moyo wangu unadunda. Lakini yeye hapigi simu na hakuna habari juu yake. Mimi nimesali kuomba awe salama na kuomba imara ya kuvumilia mpaka jambo hili litakapomalizika. Ninaendelea kuwazia kwamba dakika yo yote yeye ataingia kupitia mlangoni.
“ . . . Nafikiria mambo mengi sana yasiyofaa nikijaribu kutuliza lile umivu. Ee, Mungu wangu, leta kisichana changu nyumbani.”
BARUA iliyoko juu ilipelekwa kwa mwandikaji mashuhuri wa safu za magazeti aliye mtoa-mashauri, mwanzoni-mwanzoni mwa ile miaka ya 1970. Huo ulikuwa wakati ambapo ilichukuliwa kwamba watoto walikuwa wanaondoka kwa sababu za kutafuta raha: utafutaji wa vituko, kujitahini waone kama wanaweza kujitegemea, kutoafikiana juu ya saa wanazopaswa kurudi nyumbani, kukata tumaini kwa sababu ya mahaba yaliyovunjika. Ingawa baadhi yao wangali wakiondoka kwa sababu hizo hizo, mambo yamebadilika katika miaka 15 iliyopita.
Mara nyingi vijana wa leo wanaondoka kwa sababu ya hali ambazo ni zenye kuhuzunisha zaidi—hali za kijamaa zilizomomonyoka sana ambamo wao wanahisi hawatakiwi na hawapendwi; huenda wao hata wakatendwa vibaya. Na badala ya kukimbia waende kwenye kitu fulani—kwenye mtindo wa maisha yenye kunasa tamaa na ya kuvutia —wao wanakimbia kutoka kwenye jambo fulani, maisha ya kinyumbani yenye kuzorota na yasiyo na furaha. “Watoto wanaotoroka wako tofauti sana sasa na vile walivyokuwa wakati habari nyingi sana zilipokuwa zikiandikwa juu yao” katika mwanzo-mwanzo wa ile miaka ya 1970, anasema Dakt. Douglas Huenergardt, msimamizi wa kao moja la Florida la watoto wanaotoroka. “Wakati huo sisi tulikuwa na watoto wenye kutafuta mitindo-maisha iliyo tofauti. Hilo silo linalotendeka leo. Mtoto ambaye anatoroka ni yule ambaye hawezi tena kuvumilia hali ya nyumbani.”
Uchunguzi mbalimbali wa hivi majuzi unashuhudiza jambo hilo. Na bado unaonyesha jambo jingine ambalo linagutusha. Si kwamba tu watoto wengi wanatoroka ili waepe maisha ya kijamaa yasiyovumilika, bali leo karibu nusu ya watoto wanatoroka katika United States wanaondoka nyumbani bila ya wao kujitolea kufanya hivyo —wanasukumwa nje au wanatiwa moyo waondoke nyumbani na wazazi wao wenyewe! “Kwa vijana wengi wabalehe kutoroka ni jibu kwa jamaa isiyo na afya, hali ya kikazi au kishule,” linataarifu jarida Family Relations. “Kwa kweli, watoto wengi wanaotoroka ni watupiliwa-mbali, wakupushwaji, au wasukumwa-nje. Vijana hao wanaambiwa waondoke au wanaachiliwa mbali na wazazi wao. Baadhi yao wanatendwa-tendwa vibaya sana na hawaoni njia yo yote nyingine isipokuwa kuondoka.”
Inahuzunisha kama nini! Inasikitisha kama nini kwa watoto hao! Kwa maana, mara wakiisha kuwa nje vichochoroni, wakiwa na pesa kidogo tu na bila njia ya kujiruzuku, mara nyingi vijana wanageukia kuombaomba, kuuza-uza dawa za kulevya, kufanya umalaya, na kuiba, au wanatumiwa vibaya na wengine. “Si wafanya kazi wa kijamii na wasaikolojia wanaowalaki watoto wanaotoroka katika vituo vya mabasi, bali ni manamba, wauzaji dawa za kulevya na wanapornografia,” linasema gazeti Psychology Today. “Asilimia themanini na sita [86] ya wastadi waliochunguzwa maoni walisema kwamba yanayofanywa ili kuzuia watoto wanaotoroka wasitumiwe vibaya na mbuai hao ni machache au hakuna linalofanywa. Si jambo la kushangaza kwamba afya ya watoto wanaotoroka inazidi kuwa mbaya kwa kadiri ambavyo wao wanakaa kule vichochoroni.”
Ni kweli, vibanda zaidi na zaidi vinasimamishwa ili kuwapa makao, kuwalisha, na kuwapa mwongozo watoto wasio na maskani. Lakini pana tofauti kati ya kuwapeleka huko watoto wanaotoroka na kuweza kuwasaidia kikweli, “Kazi yetu ni kukaza ndani yao kipimo fulani cha kujiheshimu, kuwafanya wajiangalie wenyewe,” anataarifu mshauri mmoja. “Na hiyo ndiyo kazi ngumu zaidi ya zote ambayo mimi nimepata kuwa nayo.” Kwa maana vijana wakiisha kufikia hapo, mara nyingi wao wanakuwa wakijihadhari na watu wazima na kutowaitibari, wanakuwa wameumizwa maoni, wamekasirika, au wamekata tumaini, na huenda hata wakawa wanataka kujiua.
Je! matatizo yangeweza kutatuliwa yakiwa kwenye chanzo chayo? “Kwa kadiri kubwa, hesabu iliyo kubwa zaidi ya visa vya watoto wanaotoroka itatokana na mambo ya namna fulani ya kijamaa,” yanasema Search, maandishi ya New Jersey ya usajili wa wenye kukosekana. “Mtu ambaye hasa ni mwenye furaha hatatoroka.” Basi, je! ni jambo gani litakalosaidia kuleta furaha katika jamaa? Je! vile vifungo kati ya mzazi na mtoto vinaweza kuimarishwa?