Je! Vita Vitakuwako Sikuzote?
SIKU ya Julai 1, 1916, katika jimbo la Picardy lililo la kupendeza kwa ukulima katika Ufaransa Kaskazini, lilianza lile Pigano la Kwanza la Somme. Baada ya kurushiana-rushiana risasi za mizinga na kufanyiana mashambulizi ya kutoka angani, kani za Uingereza na Ufaransa zilitupa kitu ambacho wao walitumaini kingekuwa njia ya kufanikiwa kuyashinda kabisa kabisa majeshi ya Ujeremani yaliyokuwa ndani ya mahandaki na ambayo yalikabiliana nao uso kwa uso. Lakini njia hiyo haikupatikana. Badala ya hivyo, katika siku ya kwanza, askari 20,000 Waingereza waliuawa. Kadiri ambavyo majuma yalizidi kupita, pigano lile liliendelea kukiwa kungali hakujapatikana njia. Katika Oktoba mvua zenye kububujika sana ziligeuza uwanja wa pigano ukawa bahari ya matope. Kufikia katikati ya Novemba yale Mataifa-Mafungamani yalikuwa yamesonga mbele kilometa 8 tu. Kwa sasa, uhai wa Wajeremani 450,000, Wafaransa 200,000, na Waingereza 420,000 ulikuwa umepotezwa. Askari zaidi ya milioni moja, walio wengi wakiwa ni wanaume vijana, walipotelea mbali katika pigano hilo!
Hilo lilikuwa moja tu la matukio mengi katika ile vita ya ulimwengu ya kwanza. Nayo vita ya ulimwengu ilikuwa moja tu—ingawa ilikuwa ndiyo mbaya zaidi kufikia wakati huo—kati ya vita vile visivyohesabika ambavyo vimepiganwa muda wote wa historia. Lo, ni upotevu wa kijinga kama nini wa uhai wa kibinadamu!
Kwa nini wanadamu wanasisitiza juu ya kuuana kwa njia hiyo? Kuna mambo mengi ambayo yanahusika, na miongoni mwayo tungeweza kutaja ubinafsi, tamaa ya makuu, pupa, na pia ashiki ya kutaka mamlaka na fahari. Kisababishi kingine cha vita kimekuwa ni utukuzo wa taifa. Kweli kweli, vita inaonyesha usahihi wa oneleo linalohusu historia ya kibinadamu ambalo linapatikana katika Biblia: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9.
Mara nyingi dini pia imechochea vita. Krusedi za zile Enzi za Katikati zilipiganwa na mataifa ya kidini kwa kisingizio cha kwamba kusudi lilikuwa la kidini: ili kushinda Palestina irudie kuwa milki ya Jumuiya ya Wakristo. Katika vita vya ulimwengu vyote viwili vya karne hii, makasisi kutoka madhehebu tofauti-tofauti wamejaribu kutumia hisia za kidini za wale askari ili kuwafanya wazidi kuwa na nia ya kuua askari wenzao upande ule mwingine. Na mengine ya mapambano yanayowaka moto sasa hivi yanahusiana sana na sababu fulani ya kidini.
Dalili za Tumaini
Je! kuna tumaini lolote kwamba siku moja vita vitakoma? Ndiyo, kunalo. Yesu Kristo anaitwa “Mwana-Mfalme wa Amani.” Alipokuja duniani, yeye aliishi kulingana na jina hilo, akifundisha watu kupenda jirani zao kama wao wenyewe. Hata aliwaambia wapende adui zao. (Isaya 9:6, NW; Mathayo 5:44; 22:39) Tokeo ni kwamba, wale waliotii mafundisho yake katika karne ya kwanza walikuja kuwa udugu wa kimataifa, ulio na amani. Lilikuwa jambo lisilofikirika kwao kufanyiana vita mmoja na mwenzake. Hata hivyo, kwa kusikitisha, baadaye imani yenye kutakata ya Wakristo hao wa mapema ilichafuliwa. Baada ya muda, makanisa yalijiingiza-ingiza katika siasa na mikono yao ikaja kulowana katika damu ya vita vya mataifa.
Muda mwingi baadaye, pepo za mabadiliko zilianza kuvuma Ulaya. Ilionekana kana kwamba aina ya binadamu ilikuwa ikichoshwa na vita ya wakati wote. Katika 1899 na tena katika 1907, mikusanyiko ya kimataifa ilifanywa katika The Hague, Uholanzi. Kwenye mkusanyiko wa 1899, mwafaka ulipitishwa ili kuwe na “Utatuzi Wenye Amani wa Mizozo ya Kimataifa.” Kwa hiyo karne ya 20 ilipokuwa ikipambazuka, watu wengi walitumaini kwamba ulimwengu ungeendelea kusitawi pole kwa pole mpaka ukashinde tamaa yao ya kufanya vita. Hata hivyo, matumaini hayo yalivunjiliwa mbali na zile bunduki za vita ya ulimwengu ya kwanza. Je! hiyo ilimaanisha kwamba maneno ya Isaya hayangetimizwa kamwe?