Unaweza Kupata Hazina za Bei Isiyohesabika!
“E! UNAWEZA kuona chochote?” Mwingereza tajiri akauliza. “Ndiyo, vitu vya ajabu,” akajibu mtaalamu mwenye kuchunguza vitu vya kale katika Misri. Mwaka ulikuwa 1922, na Howard Carter alikuwa ndiyo sasa tu ametupa jicho ndani ya kaburi la Farao Tutankhamen katika Bonde la Misri la Wafalme. Maneno ya Carter yajawa na msisimuko:
“Macho yangu yalipozoelea ile nuru, pole kwa pole yalizidi kupenya ndani ya ukungu ule, yakaona wanyama wa ajabu, sanamu, na dhahabu—dhahabu ikimeta-meta kila mahali. Muda huo mfupi—lazima uwe ulionekana kama umilele kwa wengine waliosimama kando—niliduwaa kwa kustaajabu . . . Tulikuwa hatujawahi kuwazia kitu kama hiki, chumba cha utele—kilionekana kama jumba lenye utele wa vitu vya makumbusho—kilichojaa vitu.” Mara hiyo Carter alihisi lile “tazamio kubwa sana . . . la mtafuta-hazina.”
Ugunduzi huo ulitokeza wazi hazina za ajabu zilizofichika kwa miaka zaidi ya 3,000 iliyopita. Lakini Mungu anatutaka tujitie katika utafutaji wa hazina kubwa zaidi. Ni utafutaji wenye kuthawabisha zaidi ya utafutaji mwingine wowote wa vito, dhahabu, au fedha. Huo ni utafutaji wa hazina ya hekima ya kimungu, na moja ya mali zenye thamani kubwa zaidi ni uhai wa milele.—Yohana 17:3.
Jitihada Inahitajiwa Sana
Jitihada kubwa inatakwa ili kuchimbua mahali penye vitu vya kale. Si rahisi kuchimba mwituni au kushuka ndani ya maji hatari kwa kutafuta hazina iliyofichika, iliyozikwa, au iliyozama. Lakini watafuta-hazina wenye bidii hufurahi kufanya jitihada hizo. Mara nyingi wao huvumilia magumu makali na kushinda vipingamizi vinavyoonekana kuwa haviwezekani. Basi, je! utafutaji wa hekima ya kimungu haustahili jitihada kubwa hata zaidi?
Tunaweza kupata hazina za bei isiyohesabika tukifanya jitihada inayohitajiwa ili kujifunza Biblia na vichapo vya Ukristo wa kweli ambavyo vimetungwa kwa njia ya kutusaidia tupate vito vya hekima iliyomo. Ni muhimu kuendelea kujitahidi. Hatungekuwa matajiri tukianza kuchimba hazina za kimwili lakini tuchoke na kuacha baada ya kukwaruza juujuu. Ingekuwa ivyo hivyo kama tungeanza kuchimba tutafute hazina za kiroho na upesi tuache kwa sababu tumefikiri kuendelea kunachosha sana. “Hekima itokayo juu” ni kwa ajili ya wale wanaojitahidi kuipata. (Yakobo 3:17) Je! haikupasi ufanye jitihada inayohitajiwa ili kupata hazina zisizohesabika bei za hekima ya kimungu?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]
Jalada na picha ya ukurasa 3 K. Scholz/H. Armstrong Roberts